Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Maombolezo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Maombolezo

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Maombolezo

NABII Yeremia anaona ujumbe wa hukumu ambao amekuwa akitangaza kwa miaka 40 ukitimizwa. Nabii huyo anahisi namna gani anapojionea mwenyewe kuharibiwa kwa jiji lake analolipenda? “Yeremia aliketi chini akalia na kuomboleza kwa maombolezo haya kuelekea Yerusalemu,” inasema Septuajinti ya Kigiriki katika maelezo ya utangulizi ya kitabu cha Maombolezo. Kitabu cha Maombolezo kiliandikwa mwaka wa 607 K.W.K., nabii Yeremia akiwa bado anakumbuka kuzingirwa kwa Yerusalemu kwa muda wa miezi 18 na kuteketezwa kwa jiji hilo. Kitabu hicho kinaeleza kwa undani huzuni kubwa ya Yeremia. (Yeremia 52:3-5, 12-14) Hakuna jiji lingine katika historia ambalo limeombolezewa kwa maneno yenye kuhuzunisha na yenye kugusa moyo kama hayo.

Kitabu cha Maombolezo kina nyimbo tano za mashairi. Nyimbo nne za kwanza ni maombolezo; wimbo wa tano ni ombi, au sala. Nyimbo nne za kwanza zimepangwa kialfabeti, kila mstari ukianza na herufi tofauti kupatana na mpangilio wa herufi 22 za alfabeti ya Kiebrania. Ingawa wimbo wa tano una mistari 22 inayolingana na idadi ya herufi za alfabeti ya Kiebrania, wimbo huo haujapangwa kialfabeti.—Maombolezo 5:1.

‘MACHO YANGU YAMECHOKA KWA MACHOZI’

(Maombolezo 1:1–2:22)

“Lo! jinsi ameketi akiwa mpweke, jiji lililokuwa limejaa watu! Jinsi amekuwa kama mjane, yule aliyekuwa na hesabu kubwa ya watu kati ya mataifa! Jinsi yule aliyekuwa binti ya kifalme kati ya wilaya za utawala amekuja kufanya kazi ya kulazimishwa!” Hivyo ndivyo maombolezo ya nabii Yeremia kuhusu Yerusalemu yanavyoanza. Akieleza sababu ya msiba huo, nabii huyo anasema hivi: “Yehova mwenyewe amemletea huzuni kwa sababu ya wingi wa makosa yake.”—Maombolezo 1:1, 5.

Likifananishwa na mjane aliyefiwa na mume na watoto, jiji la Yerusalemu linauliza: “Je, kuna uchungu wowote ulio kama uchungu wangu?” Jiji hilo linasali hivi kwa Mungu kuhusu maadui wake: “Ubaya wao wote na uje mbele zako, nawe uwatendee vikali, kama vile ulivyonitendea vikali kwa sababu ya makosa yangu yote. Kwa maana ninaugua sana, na moyo wangu ni mgonjwa.”—Maombolezo 1:12, 22.

Akiwa mwenye kutaabika sana, Yeremia anasema: “Katika joto kali la hasira [Yehova] amekata kila pembe ya Israeli. Amerudisha mkono wake wa kuume kutoka mbele ya adui; naye huendelea kuwaka katika Yakobo kama moto unaowaka ambao umeteketeza kuzunguka pande zote.” Akielezea huzuni kubwa aliyo nayo, nabii huyo anaomboleza hivi: “Macho yangu yamechoka kabisa kwa machozi matupu. Matumbo yangu yako katika msukosuko. Ini langu limemwagwa chini kabisa.” Hata wale wanaopita hapo wameonyesha mshangao, na kusema: “Je, hili ndilo lile jiji ambalo walikuwa wakisema hivi kwa habari zake, ‘Hili ndilo ukamilifu wa uzuri, furaha ya dunia yote’?”—Maombolezo 2:3, 11, 15.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:15—Yehova alikuwa “amekanyaga shinikizo la divai la binti Yuda aliye bikira” jinsi gani? Kwa kuliharibu jiji hilo lililosemwa kuwa bikira, Wababiloni walimwaga damu nyingi sana hivi kwamba ilifanana na kukanyaga zabibu katika shinikizo la divai. Yehova alitabiri jambo hilo na akaruhusu litukie, hivyo inaweza kusemwa kwamba ‘alikanyaga shinikizo la divai.’

2:1—‘Uzuri wa Israeli ulitupwa chini kutoka mbinguni mpaka duniani’ jinsi gani? Kwa kuwa ‘mbingu ziko juu kuliko dunia,’ nyakati nyingine kushushwa kwa vitu ambavyo vimeinuliwa kunaweza kulinganishwa na ‘kutupwa chini kutoka mbinguni mpaka duniani.’ “Uzuri wa Israeli,” yaani, utukufu na nguvu ambazo taifa hilo lilikuwa nazo Yehova alipokuwa akilibariki, zilitupwa chini Yerusalemu lilipoharibiwa, na pia Yuda lilipoachwa ukiwa.—Isaya 55:9.

2:1, 6—“Kiti cha miguu” cha Yehova ni nini na “kibanda” chake ni nini? Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Na tuingie katika maskani yake kuu; na tuiname kwenye kiti chake cha miguu.” (Zaburi 132:7) Hivyo, “kiti cha miguu” katika Maombolezo 2:1 kinamaanisha nyumba ya Yehova ya ibada, au hekalu lake. Wababiloni ‘waliiteketeza nyumba ya Yehova’ kana kwamba ilikuwa kibanda, au nyumba ya msonge tu katika bustani.—Yeremia 52:12, 13.

2:16, 17—Kulingana na mpangilio wa alfabeti ya Kiebrania, je, mstari wa 16 haupaswi kuanza na herufi ayin ya Kiebrania na mstari wa 17 ambao unafuata uanze na herufi pe? Walipokuwa wakitunga mashairi kwa kufuata utaratibu huu, kwa kawaida waandishi walioongozwa na roho walifuata mpangilio wa alfabeti. Hata hivyo, hawakufuata mpangilio huo ikiwa hilo lingeharibu mtiririko wa kawaida wa mawazo. Maana ya mawazo ilionwa kuwa muhimu kuliko kushikamana na mbinu ya kuandika iliyokusudiwa tu kuwasaidia watu kuikumbuka habari. Mpangilio wa herufi hizo mbili unakosa tena kufuatwa katika wimbo wa 3 na 4 wa Maombolezo.—Maombolezo 3:46, 49; 4:16, 17.

2:17—Ni “neno” gani hasa ambalo Yehova alitimiza kuhusiana na Yerusalemu? Inaelekea neno hilo lilihusiana na andiko la Mambo ya Walawi 26:17 linalosema: “Hakika mimi nitauweka uso wangu juu yenu, nanyi hakika mtashindwa mbele ya adui zenu; nao wale wanaowachukia ninyi watawakanyagia chini, nanyi kwa kweli mtakimbia wakati ambapo hakuna mtu yeyote anayewafuatilia.”

Mambo Tunayojifunza:

1:1-9. Jiji la Yerusalemu linalia sana usiku, na machozi yake yako kwenye mashavu yake. Malango yake yameachwa ukiwa, na makuhani wake wanaugua. Mabikira wake wamepata huzuni, naye mwenyewe ana uchungu. Kwa nini? Kwa sababu Yerusalemu amefanya dhambi waziwazi. Uchafu wake umo ndani ya nguo zake. Dhambi zake hazimletei shangwe; zinamletea machozi, kuugua, huzuni, na uchungu.

1:18. Nyakati zote Yehova anatenda kwa haki na kwa uadilifu anapowaadhibu wakosaji.

2:20. Waisraeli walionywa kwamba ikiwa hawangeisikiliza sauti ya Yehova, wangepata laana ambayo ilitia ndani kula ‘nyama ya wana wao na binti zao.’ (Kumbukumbu la Torati 28:15, 45, 53) Ni jambo lisilo la hekima kama nini kuchagua kutomtii Mungu!

“USIFICHE SIKIO LAKO KWA OMBI LANGU LA KITULIZO”

(Maombolezo 3:1–5:22)

Katika Maombolezo sura ya 3, taifa la Israeli linaitwa “mwanamume.” Ingawa amepatwa na taabu, mwanamume huyo anaimba hivi: “Yehova ni mwema kwa yule anayemtumaini, kwa nafsi inayoendelea kumtafuta.” Anamwomba Mungu wa kweli hivi: “Uisikilize sauti yangu. Usifiche sikio lako kwa ombi langu la kitulizo, kwa kilio changu cha kuomba msaada.” Anasema hivi akimwomba Yehova atazame shutuma za adui: “Utawalipa tendo fulani, kulingana na kazi ya mikono yao, Ee Yehova.”—Maombolezo 3:1, 25, 56, 64.

Yeremia anamwaga hisia zake na kuomboleza hivi kuhusu matokeo mabaya ya kuzingirwa kwa Yerusalemu kwa miezi 18: “Adhabu kwa kosa la binti ya watu wangu pia inakuwa kubwa kuliko adhabu kwa kosa la dhambi ya Sodoma, lililoangamizwa kama kwa dakika moja, na ambalo hakuna mikono iliyojitokeza kulisaidia.” Yeremia anaendelea kusema: “Wale waliouawa kwa upanga wamekuwa bora kuliko wale waliouawa kwa njaa, kwa sababu hao hudhoofika, wakichomwa kwa sababu ya ukosefu wa mazao ya shambani.”—Maombolezo 4:6, 9.

Katika shairi la tano, wakaaji wa jiji la Yerusalemu ndio wanaozungumza. Wanasema: “Ee Yehova, ukumbuke yale yaliyotupata. Utazame, uone shutuma zetu.” Wanaomba hivi wanaposimulia jinsi walivyotaabika: “Ee Yehova, utaketi mpaka wakati usio na kipimo. Kiti chako cha ufalme ni cha kizazi baada ya kizazi. Uturudishe kwako, Ee Yehova, nasi tutarudi bila kukawia. Utuletee siku zilizo mpya kama katika zamani za kale.”—Maombolezo 5:1, 19, 21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:16—Ni nini kinachodokezwa na maneno haya: “Naye huvunja meno yangu kwa changarawe”? Chanzo kimoja cha marejeo kinasema: “Wayahudi, wakiwa njiani kwenda uhamishoni, walilazimika kuoka mikate yao katika mashimo yaliyochimbwa ardhini, hivyo, mkate wao ulichanganyika na changarawe.” Kula mkate kama huo kungeweza kuvunja sehemu fulani ya meno ya mtu.

4:3, 10—Kwa nini Yeremia analinganisha “binti ya watu [wake]” na “mbuni nyikani”? Mbuni “huwatendea wanawe kwa ukali, kana kwamba si wake,” linasema andiko la Ayubu 39:16. Kwa mfano, baada ya mayai kutotoa au kuangua vifaranga, mbuni wa kike anaenda zake pamoja na mbuni wengine wa kike na kumwachia mbuni wa kiume kazi ya kuwatunza vifaranga. Na ni nini kinachotukia wanapokabiliana uso kwa uso na hatari? Mbuni wa kike na wa kiume wanakimbia kutoka kwenye kiota na kuwaacha vifaranga wao. Wakati Wababiloni walipozingira Yerusalemu, kulikuwa na njaa kali katika jiji hilo hivi kwamba akina mama ambao kwa kawaida wanawahurumia watoto wao walikuwa wakatili kwa watoto wao, kama mbuni nyikani. Hilo linatofautiana sana na jinsi mbweha anavyowatunza watoto wake.

5:7—Je, Yehova anawatoza watu hesabu kwa sababu ya makosa ya mababu zao? Hapana, Yehova hawaadhibu watu hasa kwa sababu ya dhambi za mababu zao. “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe,” inasema Biblia. (Waroma 14:12) Hata hivyo, matokeo ya makosa yanaweza kuendelea katika vizazi vitakavyofuata. Kwa mfano, Waisraeli wa kale walipogeukia ibada ya sanamu walifanya iwe vigumu hata kwa Waisraeli waaminifu walioishi baadaye kushikamana na njia ya uadilifu.—Kutoka 20:5.

Mambo Tunayojifunza:

3:8, 43, 44. Wakati wa msiba uliokumba Yerusalemu, Yehova alikataa kusikiliza vilio vya kuomba msaada vya wakaaji wa jiji hilo. Kwa nini? Kwa sababu watu hao walikuwa wasiotii, na walikataa kutubu. Tukitaka Yehova ajibu sala zetu, ni lazima tumtii.—Methali 28:9.

3:20. Yehova, ‘Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote,’ amekwezwa sana hivi kwamba ni lazima ajishushe ili aweze “kutazama mbingu na dunia.” (Zaburi 83:18; 113:6) Lakini, Yeremia alijua vizuri kwamba Mweza-Yote yuko tayari kujishusha juu ya watu, yaani, kushuka kufikia kiwango chao ili kuwatia moyo. Tunaweza kufurahi kama nini kwamba Mungu wa kweli si tu mwenye nguvu zote na mwenye hekima yote bali pia ni mnyenyekevu!

3:21-26, 28-33. Tunaweza jinsi gani kuvumilia hata mateso makali sana? Yeremia anatueleza. Hatupaswi kamwe kusahau kwamba Yehova amejaa matendo ya fadhili zenye upendo na kwamba rehema zake ni nyingi. Tunapaswa pia kukumbuka kwamba kuwa hai kunatupa sababu nzuri ya kutokata tumaini na kwamba tunahitaji kuwa wenye subira na kumngojea Yehova, kimya-kimya na bila kulalamika, kwa ajili ya wokovu. Zaidi ya hayo, tunapaswa ‘kutia kinywa chetu mavumbini,’ yaani, kukubali majaribu kwa unyenyekevu, tukitambua kwamba Mungu anaacha mambo yatokee kwa sababu nzuri.

3:27. Huenda kupatwa na majaribu ya imani wakati wa ujana kukahusisha hali ngumu na dhihaka. Lakini ni ‘jambo jema kwa mwanamume kuchukua nira wakati wa ujana wake.’ Kwa nini? Kwa sababu kujifunza kuchukua nira ya mateso wakati wa ujana kunamtayarisha mtu kupambana na matatizo katika miaka yake ya baadaye.

3:39-42. Si jambo la hekima ‘kuzoea kulalamika’ tunapopatwa na mateso kwa sababu ya dhambi zetu. Badala ya kulalamika kwa sababu ya kuvuna matokeo ya kutenda dhambi, “na tutafute njia zetu na kuzichunguza, nasi turudi kabisa kwa Yehova.” Tunakuwa wenye hekima tunapotubu na kurekebisha njia zetu.

Mfanye Yehova Awe Uhakika Wako

Kitabu cha Biblia cha Maombolezo kinafunua jinsi Yehova alivyoliona jiji la Yerusalemu na nchi ya Yuda baada ya Wababiloni kuliteketeza jiji hilo na kufanya nchi hiyo kuwa ukiwa. Maneno ya kukiri dhambi yaliyo katika kitabu hicho yanaonyesha wazi kwamba kwa maoni ya Yehova, msiba huo ulitukia kwa sababu ya makosa ya watu. Nyimbo za kitabu hiki ambazo ziliongozwa na roho zina maneno yanayoonyesha tumaini katika Yehova na tamaa ya kugeukia njia iliyo sawa. Watu wengi walioishi siku za Yeremia hawakuwa na maoni hayo. Hata hivyo, Yeremia na mabaki waliotubu walikuwa na maoni kama hayo.

Hatua ya Yehova ya kuchanganua hali ya Yerusalemu kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Maombolezo inatufundisha mambo mawili ya maana sana. Kwanza, kuharibiwa kwa Yerusalemu na kufanywa ukiwa kwa Yuda kunakazia umuhimu wa kumtii Yehova na kutuonya tusipuuze mapenzi yake. (1 Wakorintho 10:11) Jambo la pili tunalojifunza linatokana na mfano wa Yeremia. (Waroma 15:4) Hata katika hali iliyoonekana kuwa haina tumaini, nabii huyo ambaye alikuwa na huzuni nyingi sana alimtegemea Yehova ili amwokoe. Ni muhimu kama nini kwamba tumtegemee kabisa Yehova na Neno lake na kumfanya awe uhakika wetu!—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nabii Yeremia aliona ujumbe wake wa hukumu ukitimizwa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Imani ya Mashahidi hawa wa Korea ilijaribiwa kuhusiana na suala la kutokuwamo kwa Kikristo