Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Methali 22:6 inatoa uhakikisho kamili wa kwamba ikiwa watoto Wakristo wanazoezwa kwa njia inayofaa, hawataacha njia ya Yehova?

Andiko hilo linasema hivi: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” Kama vile tu kukunja tawi changa kunavyousaidia mti kukua kwa njia inayofaa, watoto wanaozoezwa kwa njia inayofaa wanakuwa na mwelekeo mkubwa zaidi wa kuendelea kumtumikia Yehova wanapokuwa watu wazima. Kama kila mzazi anavyojua, mazoezi hayo yanahitaji wakati na jitihada. Ili watoto wao wawe wanafunzi Wakristo, ni lazima wazazi wawafundishe watoto, wawashauri, wawahimize, na kuwatia nidhamu kwa uangalifu na vilevile kuwawekea mfano mzuri. Ni lazima wafanye hivyo kwa kuendelea na kwa upendo kwa miaka mingi.

Lakini je, hilo linamaanisha kwamba ikiwa mtoto ataacha kumtumikia Yehova, wazazi hawakumzoeza kwa njia inayofaa? Katika visa fulani, huenda wazazi hawakujitahidi vya kutosha kuwalea watoto wao katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova. (Waefeso 6:4) Kwa upande mwingine, methali hiyo si uhakikisho kamili wa kwamba mazoezi mazuri yatawafanya watoto wawe waaminifu kwa Mungu. Wazazi hawawezi kufanya watoto wao wawe vile wanavyopenda. Watoto wana uhuru wa kuchagua kama vile tu watu wazima, na ni lazima wachague njia watakayofuata katika maisha yao. (Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19) Hata wazazi wakijitahidi sana, watoto fulani wanakosa uaminifu, kama Sulemani ambaye aliandika andiko tunalozungumzia. Hata Yehova alikuwa na wana ambao hawakuendelea kuwa waaminifu.

Kwa hiyo, andiko hilo halimaanishi kwamba katika kila kisa mtoto “hatageuka kando na kuiacha” njia, lakini linamaanisha kwamba kwa kawaida matokeo yatakuwa hayo. Hilo ni jambo lenye kuwatia moyo sana wazazi! Wazazi wanapaswa kutiwa moyo kujua kwamba jitihada zao nyingi za kuwazoeza watoto wao kufuata njia ya Yehova zitafanikiwa. Kwa kuwa daraka lao ni la maana na uvutano wao ni mkubwa, wazazi wanahimizwa wachukue daraka lao kwa uzito.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Hata watoto wanapogeuka na kuacha kumtumikia Yehova, wazazi ambao wamekuwa wakiwazoeza watoto wao kwa bidii wanaweza kutumaini kwamba watoto wao watarudiwa na fahamu. Kweli ya Biblia ina nguvu, na mazoezi ya wazazi hayasahauliki kwa urahisi.—Zaburi 19:7.