Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nguvu za Ulimi

Nguvu za Ulimi

Nguvu za Ulimi

ULIMI wa twiga una urefu wa sentimita 45, unanyumbulika, na una nguvu za kutosha kung’oa majani katika matawi ya miti. Ulimi wa nyangumi mwenye rangi ya bluu-kijivu una uzito kama wa tembo. Wazia nguvu zinazohitajiwa ili kuusogeza tu ulimi huo!

Ulimi wa mwanadamu hauwezi kamwe kulinganishwa na ukubwa, uzito, na uwezo wa ndimi hizo. Hata hivyo, una nguvu zaidi. “Kifo na uzima viko katika nguvu za ulimi,” inasema Biblia kuhusu kiungo hicho kidogo cha mwili wa mwanadamu. (Methali 18:21) Kwa kweli, ni mara ngapi tumesikia nguvu za kifo za ulimi wa mwanadamu zikitumiwa kutunga uwongo na ushahidi wa uwongo ambao umesababisha uharibifu, hata kifo cha watu wasio na hatia?

Vivyo hivyo, urafiki wa muda mrefu umevunjwa na maneno yenye kuumiza. Watu wameumizwa kihisia na maneno makali. “Ninyi mtaendelea kunikasirisha nafsi yangu mpaka wakati gani na kuendelea kuniponda kwa maneno?” akalia Ayubu aliyeshutumiwa sana. (Ayubu 19:2) Mwanafunzi Yakobo alieleza kwa njia nzuri nguvu za kuharibu za ulimi usiozuiwa: “Ulimi ni kiungo kidogo na bado hujigamba kwa njia kubwa. Tazameni! Ni moto mdogo tu unaohitajika ili kuuwasha mwitu mkubwa! Basi, ulimi ni moto.”—Yakobo 3:5, 6.

Kwa upande mwingine, nguvu za ulimi zinaweza pia kuleta uzima. Maneno ya huruma na yenye kufariji yamewaokoa watu fulani walioshuka moyo na kuwazuia wasijiue. Kufuata mashauri mazuri kumewaokoa watu wengi waliokuwa wakitumia dawa za kulevya na wahalifu wa mitaani kutokana na kifo cha mapema. Kwa kweli, matunda ya ulimi wa mwadilifu ni “mti wa uzima,” na “neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.”—Methali 15:4; 25:11.

Hata hivyo, njia nzuri zaidi ya kutumia ulimi ni katika kumsifu Yehova Mungu, kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, na kuwafundisha wengine kweli zenye thamani za Biblia. Kwa nini? Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3; Mathayo 24:14; 28:19, 20.