Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waliozeeka Ni Baraka Kwa Vijana

Waliozeeka Ni Baraka Kwa Vijana

Waliozeeka Ni Baraka Kwa Vijana

“Mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache, mpaka nikitangazie kizazi habari za mkono wako, habari za nguvu zako, kwa wale wote watakaokuja.”— ZABURI 71:18.

1, 2. Watumishi wa Mungu waliozeeka wanapaswa kuthamini nini, na sasa tutachunguza nini?

MZEE mmoja Mkristo katika Afrika Magharibi alimtembelea ndugu mmoja mtiwa-mafuta na kumuuliza, “Habari gani?” Ndugu huyo alijibu hivi: “Ninaweza kukimbia na ninaweza kuruka-ruka,” huku akijaribu kutenda kupatana na maneno yake. Na akaongeza hivi: “Lakini, siwezi kupaa angani.” Mzee huyo alielewa hivi maneno hayo: ‘Kile ninachoweza kufanya, ninafurahi kukifanya, lakini kile ambacho siwezi kufanya, sikifanyi.’ Mzee aliyemtembelea ndugu huyo, kwa sasa ana umri wa miaka 80 na kitu, na bado anakumbuka kwa shangwe jinsi ndugu huyo alivyokuwa mshikamanifu na mwenye kuchekesha.

2 Sifa za kimungu ambazo zinaonyeshwa na mtu aliyezeeka zinaweza kuwa na uvutano wa kudumu juu ya wengine. Bila shaka, umri peke yake haumfanyi mtu awe mwenye hekima na kuwa na sifa kama za Kristo. (Mhubiri 4:13) Biblia inasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Methali 16:31) Ikiwa una umri mkubwa, je, unatambua jinsi maneno na matendo yako yanavyoweza kuwa na uvutano mzuri juu ya wengine? Chunguza mifano fulani inayotajwa katika Biblia ambayo inaonyesha jinsi watu waliozeeka walivyokuwa baraka kwelikweli kwa vijana.

Imani Yenye Matokeo ya Kudumu

3. Uaminifu wa Noa umewafaidi jinsi gani watu wote wanaoishi leo?

3 Imani ya Noa na kubaki kwake imara kulitokeza faida ambazo zinatunufaisha hata leo. Noa alikuwa akikaribia umri wa miaka 600 alipojenga safina, kukusanya wanyama, na kuwahubiria majirani wake. (Mwanzo 7:6; 2 Petro 2:5) Kwa sababu ya kumwogopa na kumheshimu Mungu, Noa pamoja na familia yake, waliokoka ile Gharika kubwa, naye akawa babu ya watu wote wanaoishi duniani leo. Kwa kweli, Noa aliishi wakati ambapo watu wengi walikuwa wakiishi miaka mingi. Lakini, hata akiwa mwenye umri mkubwa, Noa alibaki mwaminifu, na hilo lilitokeza baraka nyingi sana. Jinsi gani?

4. Kubaki imara kwa Noa kumewafaidi jinsi gani watumishi wa Mungu leo?

4 Noa alikuwa na umri wa karibu miaka 800 Nimrodi alipowachochea watu kujenga Mnara wa Babeli ili kuasi amri ya Yehova ya ‘kujaza dunia.’ (Mwanzo 9:1; 11:1-9) Hata hivyo, Noa hakushiriki katika uasi wa Nimrodi. Hivyo, inaelekea kwamba lugha yake haikubadilishwa wakati lugha ya waasi ilipovurugwa. Imani ya Noa na kubaki kwake imara, kulikoonekana si tu wakati wa uzee wake bali pia katika maisha yake yote marefu, kunastahili kwa kweli kuigwa na watumishi wa Mungu walio na umri wowote ule.—Waebrania 11:7.

Uvutano Katika Familia

5, 6. (a) Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 75, Yehova alimwambia afanye nini? (b) Abrahamu aliitikia jinsi gani amri ya Mungu?

5 Uvutano ambao watu waliozeeka wanaweza kuwa nao juu ya imani ya watu wa familia zao unaweza kuonwa katika maisha ya wazee wa ukoo walioishi baada ya Noa. Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75 hivi Mungu alipomwambia: “Nenda zako kutoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na kutoka kwa nyumba ya baba yako mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha; nami nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki.”—Mwanzo 12:1, 2.

6 Wazia ukiambiwa uache nyumba yako, marafiki wako, nchi ulikozaliwa, na usalama wa watu wako wa ukoo ili uende katika nchi usiyoijua. Abrahamu aliambiwa afanye hivyo. ‘Alienda kama vile Yehova alivyokuwa amemwambia,’ na kwa muda wote uliobaki wa maisha yake, aliishi katika mahema akiwa mgeni na mkaaji wa kuhama-hama katika nchi ya Kanaani. (Mwanzo 12:4; Waebrania 11:8, 9) Ingawa Yehova alimwambia kwamba angekuwa “taifa kubwa,” Abrahamu alikufa muda mrefu kabla ya wazao wake kuwa wengi. Sara, mke wake, alimzalia mwana mmoja tu, Isaka, baada ya Abrahamu kukaa katika Nchi ya Ahadi kwa miaka 25. (Mwanzo 21:2, 5) Hata hivyo, Abrahamu hakuchoka wala hakurudi Uru, jiji alikotoka. Ni mfano mzuri kama nini wa imani na uvumilivu!

7. Uvumilivu wa Abrahamu ulikuwa na matokeo gani juu ya mwana wake Isaka, na kwa wanadamu?

7 Uvumilivu wa Abrahamu ulikuwa na matokeo yenye nguvu juu ya mwana wake Isaka, ambaye aliishi maisha yake yote, yaani, miaka 180, akiwa mkaaji mgeni katika nchi ya Kanaani. Uvumilivu wa Isaka ulitegemea imani katika ahadi ya Mungu, imani ambayo ilijengwa ndani yake na wazazi wake waliozeeka, na baadaye ikatiwa nguvu na neno ambalo Yehova mwenyewe alimpa. (Mwanzo 26:2-5) Kubaki imara kwa Isaka kulitimiza jambo la maana sana katika utimizo wa ahadi ya Yehova kwamba “uzao” ambao kupitia huo wanadamu wote wangejibariki ungetokana na familia ya Abrahamu. Mamia ya miaka baadaye, Yesu Kristo, sehemu kuu ya “uzao” huo, aliwafungulia njia wote ambao wangemwamini ili wapatanishwe na Mungu na kupata uzima wa milele.—Wagalatia 3:16; Yohana 3:16.

8. Yakobo alionyesha jinsi gani imani yenye nguvu, na matokeo yakawa nini?

8 Naye Isaka alimsaidia mwana wake Yakobo kusitawisha imani yenye nguvu ambayo ilimwimarisha hata alipozeeka. Yakobo alikuwa na umri wa miaka 97 alipopigana mieleka usiku mzima na malaika ili abarikiwe. (Mwanzo 32:24-28) Kabla ya kifo chake akiwa na umri wa miaka 147, Yakobo alitumia nguvu zake zote zilizobaki ili kumbariki kila mmoja wa wanawe 12. (Mwanzo 47:28) Maneno ya unabii aliyosema, yanayopatikana sasa kwenye Mwanzo 49:1-28, yalithibitika kuwa ya kweli na bado yanatimizwa.

9. Tunaweza kusema nini kuhusu uvutano ambao watu wazee na wakomavu kiroho wanaweza kuwa nao juu ya familia zao?

9 Kwa wazi, watumishi washikamanifu wa Mungu waliozeeka wanaweza kuwa na uvutano mzuri sana juu ya watu wa familia zao. Mafundisho ya Maandiko, mashauri yenye hekima, na mfano mzuri wa uvumilivu, unaweza kumsaidia sana kijana kukua akiwa na imani yenye nguvu. (Methali 22:6) Watu wazee hawapaswi kamwe kupuuza uvutano mzuri ambao wanaweza kuwa nao juu ya familia zao.

Uvutano Juu ya Waabudu Wenzao

10. Yosefu alitoa ‘amri gani kuhusu mifupa yake,’ na matokeo yalikuwa nini?

10 Pia, waliozeeka wanaweza kuwa na uvutano mzuri juu ya waamini wenzao. Yosefu, mwana wa Yakobo, alifanya tendo moja rahisi la imani katika uzee wake ambalo lilikuwa na matokeo makubwa juu ya mamilioni ya waabudu wa kweli walioishi baada yake. Yosefu alikuwa na umri wa miaka 110 ‘alipotoa amri kuhusu mifupa yake,’ kwamba wakati Waisraeli wangetoka Misri, wangepaswa kubeba mifupa yake. (Waebrania 11:22; Mwanzo 50:25) Amri hiyo ilitoa tumaini na uhakikisho wa kwamba baada ya kifo cha Yosefu, Waisraeli wangekombolewa kutoka katika maisha magumu ya utumwa wa miaka mingi.

11. Inaelekea Musa aliyezeeka alikuwa na uvutano gani juu ya Yoshua?

11 Musa ni mmoja wa wale ambao walitiwa moyo na maneno ya imani ya Yosefu. Musa alipokuwa na umri wa miaka 80, alipewa pendeleo la kuichukua mifupa ya Yosefu kutoka Misri. (Kutoka 13:19) Karibu na wakati huo, alikutana na Yoshua ambaye alikuwa kijana sana. Kwa miaka 40 iliyofuata, Yoshua alitumikia akiwa mhudumu wa Musa. (Hesabu 11:28) Alipanda pamoja na Musa kwenye Mlima Sinai na alikuwepo Musa alipoteremka kutoka mlimani akiwa na mabamba ya Ushuhuda. (Kutoka 24:12-18; 32:15-17) Ni wazi kwamba Musa aliyezeeka alimpa Yoshua mashauri bora na hekima nyingi kama nini!

12. Yoshua alithibitisha jinsi gani kwamba alikuwa na uvutano mzuri juu ya taifa la Israeli kwa muda wote alioishi?

12 Naye Yoshua alilitia moyo taifa la Israeli muda wote wa maisha yake. Andiko la Waamuzi 2:7 linatuambia hivi: “Watu wakaendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na siku zote za wale wanaume wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua na ambao walikuwa wameona kazi yote kubwa ya Yehova ambayo aliwafanyia Israeli.” Hata hivyo, baada ya kifo cha Yoshua na wanaume wengine wazee, kipindi cha miaka 300 cha kuyumba-yumba kati ya ibada ya kweli na ya uwongo kilianza na kuendelea mpaka siku za nabii Samweli.

Samweli ‘Alitenda Uadilifu’

13. Samweli alifanya nini ili ‘kutenda uadilifu?’

13 Biblia haisemi Samweli alikuwa na umri gani alipokufa, lakini matukio katika Kitabu cha Kwanza cha Samweli yanahusu kipindi cha miaka 102 hivi, na Samweli aliona mengi ya matukio hayo. Kwenye Waebrania 11:32, 33, tunasoma kwamba waamuzi na manabii wanyoofu ‘walitenda uadilifu.’ Ndiyo, Samweli aliwashawishi baadhi ya watu wa siku zake kuepuka au kuacha matendo maovu. (1 Samweli 7:2-4) Alifanya hivyo kwa njia gani? Alikuwa mshikamanifu kwa Yehova katika maisha yake yote. (1 Samweli 12:2-5) Hakuogopa kutoa mashauri mazito hata kwa mfalme. (1 Samweli 15:16-29) Zaidi ya hayo, Samweli, akiwa ‘amezeeka na mwenye mvi,’ aliweka mfano mzuri wa kusali kwa ajili ya wengine. Alisema ‘lilikuwa jambo lisilowaziwa amtendee Yehova dhambi kwa kuacha kusali’ kwa ajili ya Waisraeli wenzake.—1 Samweli 12:2, 23.

14, 15. Leo, waliozeeka wanaweza kumwiga Samweli jinsi gani kuhusiana na sala?

14 Yote hayo yanaonyesha njia muhimu ambayo watu waliozeeka wanaweza kuwa na uvutano mzuri juu ya watumishi wenzao wa Yehova. Ingawa wana udhaifu unaosababishwa na afya mbaya au hali nyingine, wale wenye umri mkubwa wanaweza kusali kwa ajili ya wengine. Enyi mliozeeka, je, mnatambua jinsi sala zenu zinavyolifaidi sana kutaniko? Kwa sababu ya imani yenu katika damu ya Kristo iliyomwagwa, mna msimamo unaokubalika machoni pa Yehova, na kwa sababu ya uvumilivu wenu wa miaka mingi, imani yenu imepata “sifa iliyojaribiwa.” (Yakobo 1:3; 1 Petro 1:7) Msisahau kamwe hili: “Dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi.”—Yakobo 5:16.

15 Sala zenu za kutegemeza kazi ya Ufalme wa Yehova zinahitajiwa. Baadhi ya ndugu zetu wamo gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo. Wengine wamepatwa na misiba ya asili, vita, na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. Kwa kuongezea, kuna wengine katika makutaniko yetu ambao wanakabiliana na vishawishi au upinzani. (Mathayo 10:35, 36) Mnahitaji pia kusali kwa ukawaida kwa ajili ya wale wanaoongoza katika kazi ya kuhubiri na kusimamia makutaniko. (Waefeso 6:18, 19; Wakolosai 4:2, 3) Inatia moyo sana mnapotaja waamini wenzenu katika sala zenu, kama alivyofanya Epafra!—Wakolosai 4:12.

Kufundisha Kizazi Kinachokuja

16, 17. Ni nini kilichotabiriwa kwenye Zaburi 71:18, na hilo limetimia jinsi gani?

16 “Kondoo wengine” ambao wana tumaini la kuishi milele duniani, wamepata mazoezi mazuri sana kwa sababu ya kushirikiana na watumishi waaminifu wa “kundi dogo,” yaani, wale walio na tumaini la kwenda mbinguni. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Hilo lilitabiriwa kwenye Zaburi 71:18, ambapo tunasoma hivi: “Mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache, mpaka nikitangazie kizazi habari za mkono wako, habari za nguvu zako, kwa wale wote watakaokuja.” Kabla ya kwenda mbinguni ili kutukuzwa pamoja na Yesu Kristo, watiwa-mafuta wamekuwa wenye bidii ya kuwazoeza washiriki wenzao wa kondoo wengine ili watimize madaraka mengi ambayo yanazidi kuongezeka.

17 Kanuni ya Zaburi 71:18 kuhusu kuwafundisha “wale wote watakaokuja” inaweza pia kuwahusu kondoo wengine ambao wamefundishwa na watiwa-mafuta wa Mungu. Yehova amewapa washiriki waliozeeka wa kondoo wengine pendeleo la kutoa ushuhuda kuhusu jina lake kwa wale ambao sasa wanakubali ibada ya kweli. (Yoeli 1:2, 3) Kondoo wengine wanahisi kwamba wamebarikiwa kwa sababu ya yale ambayo wamejifunza kutoka kwa watiwa-mafuta, nao wanachochewa kushiriki elimu yao ya Biblia pamoja na wengine wanaotamani kumtumikia Yehova.—Ufunuo 7:9, 10.

18, 19. (a) Watumishi wengi wa Yehova waliozeeka wanaweza kueleza habari gani zenye thamani? (b) Wakristo waliozeeka wanaweza kuwa na uhakika gani?

18 Watumishi wa Yehova ambao wamezeeka, watiwa-mafuta na wale wa kondoo wengine, wanaishi wakati wa matukio ya maana sana ya kihistoria. Wachache wao ambao bado wako hai walikuwepo wakati sinema ya kwanza ya “Photo-Drama of Creation” ilipoonyeshwa. Mashahidi fulani waliozeeka waliwajua kibinafsi ndugu waliokuwa wakiongoza ambao walifungwa gerezani mwaka wa 1918. Wengine walishiriki kutangaza habari kwenye kituo cha redio cha WBBR cha Watchtower. Wengi wanaweza kueleza kuhusu wakati ambapo mapambano ya kisheria ya kesi zilizohusu uhuru wa kidini wa Mashahidi wa Yehova yalipofanywa katika mahakama zilizo kuu zaidi. Wengine walibaki imara kwa ajili ya ibada ya kweli huku wakiendelea kuishi chini ya serikali za kidikteta. Ndiyo, waliozeeka wanaweza kusimulia jinsi ambavyo uelewaji wa kweli za Biblia umefunuliwa hatua kwa hatua. Biblia inatutia moyo tufaidike na ujuzi wao mwingi.—Kumbukumbu la Torati 32:7.

19 Wakristo waliozeeka wanahimizwa wawe mifano mizuri kwa vijana. (Tito 2:2-4) Kwa sasa, pengine huoni jinsi uvumilivu, sala, na mashauri yako yanavyowafaidi wengine. Ni wazi kwamba Noa, Abrahamu, Yosefu, Musa, na wengine hawangeweza kujua jinsi uaminifu wao ungevifaidi vizazi vilivyofuata. Hata hivyo, imani na utimilifu wao uliwafaidi sana wengine. Mfano wako unaweza pia kuwa na matokeo kama hayo kwa vijana.

20. Wale wanaodumisha tumaini lao likiwa imara mpaka mwisho watapata baraka gani?

20 Iwe utalindwa na kuokoka “dhiki kuu” au utafufuliwa, itakuwa shangwe kama nini kufurahia “uzima ulio wa kweli”! (Mathayo 24:21; 1 Timotheo 6:19) Fikiria kipindi cha Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo wakati ambapo Yehova ataondoa madhara ya kuzeeka. Badala ya miili yetu kuendelea kudhoofika, kila siku na hatua kwa hatua, tutaamka miili yetu ikiwa yenye nguvu zaidi, tukiwa na uwezo mzuri zaidi wa kuona, wa kusikia, na tukiwa na umbo zuri zaidi! (Ayubu 33:25; Isaya 35:5, 6) Wale watakaobarikiwa kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu watakuwa vijana sikuzote kwa sababu wataishi milele. (Isaya 65:22) Hivyo basi, sisi sote na tudumishe tumaini letu likiwa imara mpaka mwisho na kuendelea kumtumikia Yehova kwa nafsi yetu yote. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza yote ambayo ameahidi na kwamba yale atakayofanya yatazidi kwa mbali matarajio yoyote ambayo huenda tukawa nayo.—Zaburi 37:4; 145:16.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kubaki imara kwa Noa aliyezeeka kuliwaletea wanadamu wote baraka jinsi gani?

• Imani ya wazee wa ukoo ilikuwa na matokeo gani juu ya wazao wao?

• Wakiwa katika umri wao wa uzee, Yosefu, Musa, Yoshua, na Samweli waliwatia waabudu wenzao nguvu jinsi gani?

• Watu waliozeeka wanaweza kuwawekea wengine mfano gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Uvumilivu wa Abrahamu ulikuwa na matokeo yenye nguvu juu ya Isaka

[Picha katika ukurasa wa 28]

Shauri la ukomavu la Musa lilimtia Yoshua moyo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Sala zako kwa ajili ya wengine zinaweza kutimiza mambo mengi mazuri

[Picha katika ukurasa wa 30]

Vijana wanafaidika kwa kuwasikiliza watu waaminifu waliozeeka