Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamwiga Yehova Katika Kuwajali Wengine?

Je, Unamwiga Yehova Katika Kuwajali Wengine?

Je, Unamwiga Yehova Katika Kuwajali Wengine?

‘TUPENI mahangaiko yenu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ (1 Petro 5:7) Huo ni mwaliko wenye upendo kama nini! Yehova Mungu anamjali kila mmoja wa watu wake. Tunaweza kujihisi salama mikononi mwake.

Tunapaswa kusitawisha na kuonyesha mtazamo kama huo wa kuwajali wengine. Kwa kuwa sisi si wakamilifu, tunapaswa kujihadhari na mitego fulani tunapoonyesha sifa ya kuwajali wengine. Kabla ya kuzungumzia mitego fulani kati ya hiyo, acheni tuchunguze baadhi ya njia za Yehova za kuwajali watu wake.

Akitumia mfano wa mchungaji, mtunga-zaburi Daudi alieleza jinsi Mungu anavyojali: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha. Anaiburudisha nafsi yangu. . . . Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya.”—Zaburi 23:1-4.

Kwa kuwa yeye mwenyewe alikuwa mchungaji, Daudi alijua mambo yanayohusika katika kuchunga kundi la kondoo. Mchungaji anawalinda kondoo wake kutokana na wanyama wanaowinda kama vile simba, mbwa-mwitu, na dubu. Anawazuia kondoo wasitawanyike, anawatafuta waliopotea, anabeba kifuani pake wana-kondoo waliochoka, na kuwatunza walio wagonjwa na waliojeruhiwa. Anawanywesha kondoo kila siku. Hilo halimaanishi kwamba mchungaji anaongoza kila hatua ya kondoo. Kondoo wana uhuru ijapokuwa wanalindwa.

Hivyo ndivyo Yehova anavyowajali watu wake. Mtume Petro alieleza hivi: ‘Mnalindwa na nguvu za Mungu.’ Hapa, neno ‘kulindwa’ linamaanisha kihalisi “kuwekwa chini ya uangalizi.” (1 Petro 1:5) Kwa sababu anatujali kikweli, Yehova anatutazama daima, akiwa tayari wakati wowote kutusaidia tunapomwomba msaada. Lakini, Yehova alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua, hivyo haingilii matendo na maamuzi yetu yote. Tunaweza kumwiga Yehova jinsi gani katika jambo hilo?

Mwige Mungu Katika Kuwatunza Watoto Wako

“Wana ni urithi kutoka kwa Yehova.” Hivyo, wazazi wanapaswa kuwalinda na kuwatunza watoto wao. (Zaburi 127:3) Huenda hilo likamaanisha kuwatia moyo watoto watoe maoni yao na kufunua hisia zao na kisha kufikiria maoni na hisia hizo unaposhughulika nao. Wazazi wakijaribu kuongoza kila hatua ya watoto wao, huku wakipuuza kabisa mapendezi ya watoto, watakuwa kama mchungaji anayejaribu kuongoza kondoo wake kwa mnyororo. Hakuna mchungaji ambaye angechunga kundi lake kwa njia kama hiyo; wala Yehova hatuchungi kwa njia hiyo.

Mariko * anakubali hivi: “Kwa miaka mingi nilikuwa nikiwaambia watoto wangu, ‘Fanyeni hivi’ na ‘Msifanye vile.’ Niliamini kwamba huo ndio uliokuwa wajibu wangu nikiwa mzazi. Sikuwapongeza wala sikuzungumza kwa undani pamoja nao.” Ingawa binti ya Mariko angezungumza na marafiki wake kwa saa nyingi kwenye simu, hangezungumza kwa muda mrefu na mama yake. “Ndipo nilipotambua tofauti iliyokuwako,” anaendelea Mariko. “Binti yangu alipokuwa akizungumza na marafiki wake, alitumia maneno yanayoonyesha huruma, kama vile ‘Ndiyo, nakubali,’ au ‘Hata mimi pia.’ Nilianza kutumia maneno kama hayo ili kumchochea binti yangu atoe maoni yake, na muda si muda mazungumzo yetu yakawa marefu na yenye kupendeza.” Hilo linaonyesha umuhimu wa kuwa na mazungumzo mazuri, ambayo kwa kawaida yanahusisha pande zote mbili wala si upande mmoja tu.

Wazazi wanapaswa kuwachochea watoto wao watoe maoni yao, na watoto wanapaswa kuelewa kwa nini utunzaji wa wazazi wao ni ulinzi. Biblia inawashauri watoto wawatii wazazi wao; kisha inatoa sababu: “Ili mambo yakuendee vema nawe ukae muda mrefu duniani.” (Waefeso 6:1, 3) Watoto ambao wamesadikishwa kwamba kuna faida za kujitiisha, wanatii kwa urahisi.

Katika Kutunza Kundi la Yehova

Hangaiko la upendo la Yehova linaonekana katika kutaniko la Kikristo. Akiwa Kichwa cha kutaniko, Yesu Kristo anawaagiza wazee walitunze kundi lake. (Yohana 21:15-17) Katika Kigiriki, neno mwangalizi linahusiana na kitenzi kinachomaanisha “tazama kwa uangalifu.” Akikazia jinsi jambo hilo linavyopaswa kufanywa, Petro anawaagiza wazee hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.”—1 Petro 5:2, 3.

Ndiyo, kazi ya wazee ni kama ile ya wachungaji. Wazee Wakristo wanapaswa kuwatunza wale walio wagonjwa kiroho na kuwarekebisha ili waishi kupatana na viwango vya uadilifu. Wazee wana wajibu wa kupanga shughuli za kutaniko, kufanya mipango kwa ajili ya mikutano, na kudumisha utaratibu kutanikoni.—1 Wakorintho 14:33.

Hata hivyo, maneno hayo ya Petro yanafunua hatari fulani, yaani, hatari ya wazee “kupiga ubwana juu ya” kutaniko. Jambo moja linaloonyesha kwamba mzee anapiga ubwana juu ya kutaniko ni kutunga sheria zisizo za lazima. Akihisi kwamba ana wajibu mkubwa wa kulinda kundi, mzee anaweza kupita mipaka. Katika kutaniko moja huko Mashariki, wazee waliweka sheria kuhusu jinsi ya kuwasalimu wengine katika Jumba la Ufalme—kama vile ni nani anayepaswa kuwa wa kwanza kutoa salamu—wakiamini kwamba kufuata sheria hizo kungeleta amani kutanikoni. Hapana shaka kwamba walikuwa na nia njema, hata hivyo, je, wazee hao walikuwa wakiiga mfano wa Yehova wa kuwajali watu wake? Ni muhimu kwamba mtazamo wa akilini wa mtume Paulo ulionyeshwa na maneno yake yafuatayo: “Si kwamba sisi ndio mabwana juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba ninyi mnasimama.” (2 Wakorintho 1:24) Yehova anawatumaini watu wake.

Mbali na kuepuka kuweka sheria zisizotegemea Maandiko, wazee wanaojali wanaonyesha kwamba wanahangaikia kundi kikweli kwa kutofunua mambo ya siri ya watu. Wanatii onyo hili kutoka kwa Mungu: “Usifunue mazungumzo ya siri ya mwingine.”—Methali 25:9.

Mtume Paulo alilinganisha kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta na mwili wa mwanadamu: “Mungu aliuungamanisha mwili . . . ili kusiwe na mgawanyiko katika mwili, bali ili viungo vyake vitunzane kwa njia ileile.” (1 Wakorintho 12:12, 24-26) Maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “vitunzane kwa njia ileile” yanamaanisha kihalisi ‘vihangaikiane sana.’ Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanapaswa kuhangaikiana sana.—Wafilipi 2:4.

Wakristo wa kweli wanaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba ‘wanahangaikiana sana’? Wanaweza kuonyesha kwamba wanawahangaikia washiriki wengine wa kutaniko kupitia sala zao na kwa kuwasaidia wenye uhitaji. Hilo linasaidia kutokeza sifa njema za wengine. Fikiria jinsi Tadataka alivyosaidiwa kwa kuhangaikiwa kwa upendo. Alipobatizwa akiwa na umri wa miaka 17, ni yeye tu katika familia yao aliyekuwa akimtumikia Yehova. Anasema hivi: “Familia fulani kutanikoni ilinikaribisha kwa ukawaida kwa ajili ya chakula na ushirika. Karibu kila siku asubuhi nilipokuwa nikienda shuleni nilipitia kwao ili tuzungumzie andiko la siku la Biblia pamoja. Nilipewa mashauri kuhusu njia ya kukabiliana na matatizo shuleni na tulisali kuhusu matatizo hayo pamoja. Familia hiyo ilinifundisha kuwa na roho ya kutoa.” Sasa Tadataka anatumia mambo aliyojifunza katika maisha yake kwa kutumikia katika mojawapo ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova.

Mtume Paulo alionya kuhusu mtego fulani wa pekee kuhusiana na kuwahangaikia wengine. Alitaja wanawake fulani ambao walikuwa “wenye kupiga porojo na wenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine wakiongea juu ya mambo ambayo hawapaswi.” (1 Timotheo 5:13) Ingawa ni vema kuwahangaikia wengine, tunapaswa kujihadhari tusipite mipaka na kujiingiza katika mambo yao ya kibinafsi. Kuwahangaikia wengine kwa njia isiyofaa kunaweza kuonekana kwa ‘kuongea juu ya mambo ambayo hatupaswi,’ kama vile kuwachambua wengine.

Ni vyema tukumbuke kwamba Wakristo wanaweza kuwa na maoni tofauti kuhusu vile ambavyo watashughulikia mambo yao ya kibinafsi, chakula watakachokula, na burudani wanayopenda. Kila mmoja ana uhuru wa kuchagua atakachofanya akitegemea kanuni za Biblia. Paulo aliwahimiza hivi Wakristo Waroma: “Na tusiwe tukihukumiana tena. . . . Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Waroma 14:13, 19) Tunapaswa kuonyesha kwamba tunahangaikiana kikweli kutanikoni, si kwa kujiingiza katika mambo ya watu wengine bali kwa kuwa tayari kusaidia. Tunapowajali wengine kwa njia hiyo, upendo na umoja unasitawi katika familia na kutanikoni.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wachochee watoto wako watoe maoni yao kwa kuwapongeza na kujali hisia zao