Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, nyoka aliyezungumza na Hawa alikuwa na miguu?

Kama ilivyoandikwa katika Mwanzo 3:14, Yehova Mungu alizungumza na yule nyoka aliyemdanganya Hawa katika bustani ya Edeni. Mungu alisema: “Kwa sababu umefanya jambo hili, umelaaniwa kati ya wanyama wote wa kufugwa na kati ya wanyama wote wa mwituni. Utakwenda kwa tumbo lako na utakula mavumbi siku zote za maisha yako.” Biblia haisemi waziwazi kwamba mnyama aliyetumiwa kumdanganya Hawa mwanzoni alikuwa na miguu na baadaye akaipoteza. Ingawa maneno ya Mwanzo 3:14 yanaweza kuwafanya wengine wafikiri hivyo, si lazima tukate kauli kwamba kabla ya kulaaniwa nyoka walikuwa na miguu. Kwa nini?

Sababu kuu zaidi ni kwamba Shetani, yule roho asiyeonekana ambaye alimtumia kiumbe huyo wa hali ya chini, hasa ndiye aliyehukumiwa na Yehova. Biblia inaeleza kwamba Shetani ni “baba ya uwongo” na “nyoka wa zamani.” Inaelekea kwamba taarifa hizo mbili zinazungumzia wakati ambapo Shetani alimshawishi Hawa asitii amri ya Mungu, akimtumia nyoka, ambaye ni mnyama anayeonekana, kama njia yake ya kuwasiliana na Hawa.—Yohana 8:44; Ufunuo 20:2.

Mungu aliumba nyoka, na inaelekea kwamba kabla Shetani hajamdanganya Hawa, tayari Adamu alikuwa amewapa nyoka jina. Nyoka asiye na akili ambaye alizungumza na Hawa hakupaswa kulaumiwa. Nyoka huyo hangeweza kujua kwamba Shetani alikuwa akimtumia, na hangeweza kuelewa hukumu ya Mungu juu ya watu hao wasiotii.

Kwa nini basi Mungu alimwambia nyoka kwamba angetembea kwa tumbo? Kwa kufaa, tabia ya nyoka akiwa katika mazingira yake ya asili, yaani, kutembea kwa tumbo na kuchomoa-chomoa ulimi wake kana kwamba analamba mavumbi, inafananisha vizuri hali ya kushushwa ya Shetani. Mwanzoni Shetani alikuwa na cheo kikubwa akiwa mmoja wa malaika wa Mungu, lakini alishushwa kwenye hali ya chini ambayo inatajwa na Biblia kuwa Tartaro.—2 Petro 2:4.

Zaidi ya hilo, kama vile nyoka halisi anavyoweza kuumiza kisigino cha mtu, Shetani akiwa katika hali yake ya kushushwa ‘angetia jeraha kisigino’ cha “uzao” wa Mungu. (Mwanzo 3:15) Yesu Kristo ndiye sehemu kuu ya uzao huo, naye aliteseka kwa muda mfupi mikononi mwa watumishi wa Shetani. Lakini mwishowe, Kristo na waandamani wake Wakristo watiwa-mafuta ambao wamefufuliwa, wataponda kabisa kichwa cha nyoka huyo wa mfano. (Waroma 16:20) Hivyo, laana ya Mungu kuelekea nyoka anayeonekana ilifananisha hali ya kushushwa na kuharibiwa kabisa kwa “nyoka wa zamani” asiyeonekana, Shetani Ibilisi.