Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwaka Mmoja Katika “Nchi Nzuri”

Mwaka Mmoja Katika “Nchi Nzuri”

Mwaka Mmoja Katika “Nchi Nzuri”

MWAKA wa 1908, kitu fulani chenye kuvutia kiligunduliwa katika eneo la jiji la Gezeri linalotajwa katika Biblia ambalo liko karibu na eneo tambarare la pwani magharibi ya Yerusalemu. Kitu kilichogunduliwa katika eneo hilo ni bamba dogo la jiwe la chokaa ambalo linaaminika kuwa la karne ya kumi K.W.K. Kwenye bamba hilo, kuna maandishi ya kale ya Kiebrania, ambayo yana kile kinachofikiriwa kuwa chati ya mwaka au mzunguko wa kilimo ambayo haina maelezo mengi, lakini inaonyesha shughuli zote za kilimo. Baadaye, bamba hilo liliitwa Kalenda ya Gezeri.

Bamba hilo lina jina: Abiya. Wataalamu wengi wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa wanaliona bamba hilo kuwa kitabu cha mvulana wa shule kilichoandikwa kama shairi. Lakini wataalamu wengine hawakubaliani na jambo hilo. * Je, ungependa kuchunguza jinsi mvulana aliyeishi nyakati hizo za zamani alivyoona majira yakibadilika? Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kukumbuka matukio fulani yanayosimuliwa katika Biblia.

Miezi Miwili ya Kukusanya

Mwandikaji wa kalenda hiyo ya zamani alianza na kipindi cha ujumla cha kukusanya. Ingawa kipindi hicho kinaorodheshwa kwanza katika kalenda hiyo, unaweza kuelewa kwa nini Waisraeli waliona kukusanya kuwa kilele au mwisho wa sehemu kubwa ya mwaka wa kilimo. Mwezi wa Ethanimu (baadaye uliitwa Tishri) unalingana na Septemba/Oktoba (Mwezi wa 9/10) kwenye kalenda tunayotumia leo. Kwa kuwa kazi kubwa ya kuvuna ilikuwa imekwisha, hicho kilikuwa hasa kipindi cha sherehe yenye shangwe ambacho kingemhusu kijana Abiya. Wazia jinsi alivyosisimka alipokuwa akimsaidia baba yake kujenga kibanda ambamo wangekaa kwa muda wa juma moja huku wakimshukuru Yehova kwa shangwe kwa sababu ya mavuno ya mashamba yao!—Kumbukumbu la Torati 16:13-15.

Karibu na wakati huo, zeituni zilikuwa zikikaribia kuiva na kuvunwa. Familia ya Abiya ilivuna zeituni kwa kupiga matawi ya miti, kazi ambayo ingekuwa ngumu sana kwa kijana Abiya lakini ambayo angefurahia kuona ikifanywa. (Kumbukumbu la Torati 24:20) Kisha, waliokota zeituni na kuzipeleka mahali pa kusagia zeituni ili kutengeneza mafuta. Au familia ingepata kiasi fulani cha mafuta kwa kutumia njia rahisi, yaani, kutia zeituni zilizopigwa-pigwa au zilizopasuliwa katika maji na kuchota mafuta yaliyoelea juu ya maji. Kwa vyovyote vile, mafuta hayo yenye thamani hayakutumiwa tu kama chakula. Yalitumiwa pia kama mafuta ya taa na ya kutibu vidonda na majeraha, ambayo mvulana kama Abiya angepata alipokuwa akicheza.

Miezi Miwili ya Kupanda

Mvua za mapema zilipoanza, huenda Abiya alifurahi wakati maji baridi ya mvua yalipoanguka juu ya ngozi yake. Inawezekana kwamba baba yake alimweleza jinsi mvua ilivyokuwa muhimu kwa nchi. (Kumbukumbu la Torati 11:14) Udongo, uliochomwa na jua kwa miezi mingi ungekuwa laini na tayari kwa ajili ya kulimwa. Mkulima wa zamani aliyetumia jembe la ng’ombe alielekeza kwa ustadi jembe ambalo huenda lilikuwa na kichwa cha chuma, huku mnyama akilivuta jembe hilo. Alifanya hivyo ili kukata mitaro au mifereji iliyonyooka juu ya udongo. Mashamba yalikuwa yenye thamani, hivyo wakulima Waisraeli walikuwa na mashamba madogo hata kwenye vilima. Lakini huenda walilazimika kulima sehemu hizo kwa mkono.

Baada ya udongo huo laini kulimwa, ngano na shayiri zingepandwa. Inapendeza kwamba katika Kalenda ya Gezeri miezi miwili inayofuata ni ya kupanda nafaka. Huenda mpandaji akabeba mbegu katika mfuko wa nguo zake na kutawanya mbegu hizo kwa kuzirusha kwa mkono wake.

Miezi Mingine Miwili ya Kupanda

Sikuzote ile “nchi nzuri” iliendelea kutoa chakula. (Kumbukumbu la Torati 3:25) Katika mwezi wa Desemba (Mwezi wa 12), mvua kubwa ilinyesha na nchi ikawa na mimea mingi. Huo ulikuwa wakati wa kupanda mboga kama vile njegere za aina mbalimbali, na pia mboga nyinginezo. (Amosi 7:1, 2) Kwenye bamba hilo, Abiya anakiita kipindi hicho “malisho ya masika” au, tafsiri nyingine inakiita “majira ya baadaye ya kupanda,” kipindi ambapo kulikuwa na chakula kingi kitamu cha mboga za majira hayo.

Majira ya joto yalipoanza, mti wa mlozi, ambao unatia alama majira ya kuchipua, ulichanua maua ya rangi nyeupe na ya waridi. Hilo lingetukia wakati tu joto lilipoanza kutokea, mapema mnamo Januari (Mwezi wa 1) katika kalenda yetu.—Yeremia 1:11, 12.

Mwezi Mmoja wa Kuvuna Kitani

Kisha Abiya anataja kitani. Pengine hilo litakufanya ukumbuke jambo lililotukia karne nyingi kabla ya siku za Abiya katika upande wa mashariki wa vilima vya Yudea. Katika jiji la Yeriko, Rahabu aliwaficha wapelelezi wawili “kati ya majani ya kitani yaliyokuwa yametandikwa kwa mistari” ili yakauke yakiwa juu ya dari ya nyumba. (Yoshua 2:6) Mmea wa kitani ulikuwa muhimu sana katika maisha ya Waisraeli. Ili kutokeza nyuzi za kitani, majani yake yalipaswa kuachwa yaoze. Majani hayo yangeoza polepole ikiwa yangeachwa kwenye umande na yangeoza haraka ikiwa yangewekwa kwenye kidimbwi, ama katika mfereji au mtaro. Nyuzi hizo zilitumiwa kutengeneza kitani ambacho kilitumiwa kutengeneza matanga, mahema, na nguo. Kitani kilitumiwa pia kutengeneza tambi za taa.

Watu fulani wanapinga wazo la kwamba mmea wa kitani ulikuzwa katika eneo la Gezeri, ambalo halikuwa na maji mengi. Wengine wanasisitiza kwamba kitani kilipandwa baadaye katika mwaka. Hiyo ndiyo sababu baadhi yao wanaamini kwamba neno “kitani” lililo katika Kalenda ya Gezeri lilimaanisha “majani.”

Mwezi Mmoja wa Kuvuna Shayiri

Kila mwaka baada ya mwezi wa kukata kitani, Abiya aliona masuke ya kijani ya shayiri, mmea ambao anataja sasa katika kalenda yake. Mwezi wa Kiebrania unaolingana nao ni mwezi wa Abibu, neno linalomaanisha “Masuke ya Kijani.” Huenda neno hilo linarejelea wakati ambapo masuke yanaiva lakini bado ni mororo. Yehova aliamuru hivi: “Mwezi wa Abibu na uadhimishwe, nawe utasherehekea pasaka kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 16:1) Abibu (baadaye uliitwa Nisani) unalingana na sehemu ya Machi na Aprili (Mwezi wa 3/4). Labda wakati wa kuiva kwa shayiri ulionyesha mwanzo wa mwezi huo. Hata leo, mwaka mpya wa Wayahudi wa Karaite unaanza wakati wa kuiva kwa shayiri. Kwa vyovyote vile, matunda ya kwanza ya shayiri yalipaswa kutikiswa mbele za Yehova katika siku ya 16 ya Abibu.—Mambo ya Walawi 23:10, 11.

Shayiri ilikuwa muhimu sana katika maisha ya kila siku ya Wayahudi wengi. Mara nyingi, watu maskini walipendelea hasa shayiri ili kuoka mikate kwa kuwa ilikuwa na bei nafuu.—Ezekieli 4:12.

Mwezi Mmoja wa Kuvuna na Kupima

Ukifikiria siku za Abiya, unaweza kuwazia kwamba huenda siku moja asubuhi aliona mawingu ya mvua yakitoweka. Mvua haingenyesha tena kwa muda fulani. Sasa mimea ya nchi nzuri ilitegemea umande. (Mwanzo 27:28; Zekaria 8:12) Wakulima Waisraeli walijua kwamba mazao mbalimbali ambayo yalivunwa wakati wa miezi yenye jua kali zaidi yalihitaji kiwango kinachofaa cha upepo hadi Pentekoste. Upepo baridi wenye umajimaji kutoka kaskazini huenda ulisaidia nafaka kukua, lakini uliharibu miti ya matunda mara tu ilipochanua maua. Upepo mkavu na wenye joto kutoka kusini ulisaidia miti kuchanua maua na kuyachavusha.—Methali 25:23; Wimbo wa Sulemani 4:16.

Yehova, Mtengenezaji wa vitu vyote, alianzisha utaratibu mzuri katika mazingira. Katika siku za Abiya, Israeli ilikuwa “nchi ya ngano na shayiri na mizabibu na tini na makomamanga, nchi ya mizeituni ya mafuta na asali.” (Kumbukumbu la Torati 8:8) Huenda babu ya Abiya alimwambia kuhusu kipindi fulani cha wingi wa chakula wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani mwenye hekima, jambo ambalo lilionyesha wazi baraka za Yehova.—1 Wafalme 4:20.

Baada ya kutaja kipindi cha mavuno, kalenda ilikuwa na neno ambalo watu fulani wanasema linamaanisha “kupima.” Pengine hilo linamaanisha kupima mavuno ili kuwapa wenye shamba na wafanyakazi sehemu fulani au hata kuitoa kama kodi. Hata hivyo, kulingana na wasomi fulani neno hilo la Kiebrania linamaanisha “karamu” na wanafikiri kwamba neno hilo linarejelea Sherehe ya Majuma ambayo ilifanywa mwezi wa Sivani, yaani, Mei/Juni (Mwezi wa 5/6).—Kutoka 34:22.

Miezi Miwili ya Kukata Matawi

Halafu Abiya aliandika kuhusu miezi miwili ya kutunza mizabibu. Je, inawezekana kwamba alisaidia kukata matawi mengi ya mizabibu ili kuruhusu jua lifikie zabibu? (Isaya 18:5) Kisha ukafika wakati wa kukusanya zabibu, ambacho kilikuwa kipindi chenye kusisimua sana kwa kijana aliyeishi wakati huo. Zabibu za kwanza zilizoiva zilikuwa tamu kama nini! Inaelekea kwamba Abiya alisikia habari kuhusu wale wapelelezi 12 waliotumwa na Musa katika Nchi ya Ahadi. Walienda huko katika kipindi cha zabibu za kwanza zilizoiva ili wachunguze jinsi nchi hiyo ilivyokuwa nzuri. Wakati huo, kishada kimoja cha zabibu kilikuwa kikubwa sana hivi kwamba ilihitaji wanaume wawili kukibeba!—Hesabu 13:20, 23.

Mwezi Mmoja wa Matunda ya Kiangazi

Mwezi wa mwisho katika kalenda ya Abiya unarejelea matunda ya wakati wa kiangazi. Nyakati za zamani huko Mashariki ya Kati, majira ya kiangazi yalikuwa sehemu ya mwaka wa kilimo iliyohusu matunda. Baada ya siku za Abiya, Yehova alitumia maneno “kikapu cha matunda ya wakati wa kiangazi” ili kuonyesha kwamba ‘mwisho ulikuwa umewafikia watu wake Israeli,’ akitumia maneno “matunda ya wakati wa kiangazi” na “mwisho” katika Kiebrania. (Amosi 8:2) Hilo lilipaswa kuwakumbusha Waisraeli wasio waaminifu kwamba taifa lao lilikuwa limefikia mwisho wake na kwamba hukumu ya Yehova ilikuwa imefika. Hapana shaka kwamba tini zilikuwa kati ya matunda ya kiangazi ambayo Abiya alitaja. Huenda tini za kiangazi zilishinikizwa ili kutengeneza keki za kula au za kutumiwa kuponya majipu.—2 Wafalme 20:7.

Jinsi Kalenda ya Gezeri Inavyokuhusu Wewe

Inaelekea kwamba kijana Abiya alihusika katika shughuli za kilimo za nchi yake. Katika nyakati hizo, Waisraeli wengi walijishughulisha na mambo ya kilimo. Hata kama hujishughulishi sana na mambo ya kilimo, maelezo yaliyo kwenye bamba la Gezeri yanaweza kukusaidia kuwazia mambo unayosoma katika Biblia, na hivyo kuyafanya yawe yenye kueleweka na yenye maana zaidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kalenda ya Gezeri haipatani kabisa na miezi ambayo kwa ujumla ilifuatwa katika Biblia. Zaidi ya hilo, shughuli fulani za kilimo zilitukia nyakati tofauti kidogo katika maeneo mbalimbali ya Nchi ya Ahadi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

TAFSIRI YA KALENDA YA GEZERI:

“Miezi ya zabibu na mavuno ya zeituni;

miezi ya kupanda;

miezi ya majani kuchipuka;

mwezi wa kukata kitani;

mwezi wa kuvuna shayiri;

mwezi wa kuvuna ngano na kupima;

mwezi wa kukata matawi;

mwezi wa matunda ya kiangazi.”

[jina:] Abiya *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 41 Inategemea buku la kwanza la kitabu cha John C. L. Gibson, (Textbook of Syrian Semitic Inscriptions) cha mwaka wa 1971.

[Picha zimeandalewa na]

Archaeological Museum of Istanbul

[Chati/Picha katika ukurasa wa 9]

 

NISANI (ABIBU)

Machi—Aprili

IYARI (ZIVU)

Aprili—Mei

SIVANI

Mei—Juni

TAMUZI

Juni—Julai

ABI

Julai—Agosti

ELULI

Agosti—Septemba

TISHRI (ETHANIMU)

Septemba—Octoba

HESHVANI (BULI)

Oktoba—Novemba

KISLEVU

Novemba—Desemba

TEBETHI

Desemba—Januari

SHEBATI

Januari—Februari

ADARI

Februari—Machi

VEADARI

Machi

[Hisani]

Farmer: Garo Nalbandian

[Picha katika ukurasa wa 8]

Eneo lililochimbuliwa huko Gezeri

[Hisani]

© 2003 BiblePlaces.com

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mlozi

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mmea wa kitani

[Hisani]

Dr. David Darom

[Picha katika ukurasa wa 10]

Shayiri

[Hisani]

U.S. Department of Agriculture