Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sauli Akutana na Marafiki na Maadui wa Zamani

Sauli Akutana na Marafiki na Maadui wa Zamani

Sauli Akutana na Marafiki na Maadui wa Zamani

INAELEKEA kwamba Sauli, ambaye alijulikana baadaye kuwa mtume Paulo, alikuwa na wasiwasi aliporudi Yerusalemu kwa mara ya kwanza tangu ageuzwe imani na kuwa Mkristo. * Miaka mitatu mapema alitoka katika jiji hilo akiwatisha wanafunzi wa Yesu na kutaka kuwaua. Aliamriwa kumkamata Mkristo yeyote wa Yesu huko Damasko.—Matendo 9:1, 2; Wagalatia 1:18.

Wakati alipogeuka na kuwa Mkristo, Sauli alitangaza kwa ujasiri kwamba anamwamini Masihi aliyefufuliwa. Kwa sababu hiyo, Wayahudi huko Damasko walitaka kumuua. (Matendo 9:19-25) Je, kweli angetarajia akaribishwe kwa uchangamfu na marafiki wake wa zamani Wayahudi huko Yerusalemu? Hata hivyo, jambo lililokuwa la muhimu zaidi kwa Sauli lilikuwa kukutana na wafuasi wa Kristo huko Yerusalemu. Hilo halingekuwa jambo rahisi.

“Alipofika Yerusalemu akafanya jitihada za kujiunga na wanafunzi; lakini wote walikuwa wakimwogopa, kwa sababu hawakuamini alikuwa mwanafunzi.” (Matendo 9:26) Hilo linaeleweka. Habari za karibuni walizojua kumhusu ni kwamba Sauli alikuwa mtesaji asiye na huruma. Kudai kwake kwamba yeye ni Mkristo kulionekana kuwa ni mbinu yake ya kujipenyeza katika kutaniko. Hivyo, Wakristo wa Yerusalemu walijiepusha naye.

Hata hivyo, mmoja wao alimsaidia Sauli. Biblia inasema kwamba Barnaba alimwongoza mtesaji huyo wa zamani “kwa mitume.” Inaelekea alikuwa akizungumza kuhusu Petro (Kefa) na Yakobo, ndugu ya Bwana, akiwaeleza jinsi Sauli alivyogeuzwa imani na pia kuhusu mahubiri yake huko Damasko. (Matendo 9:27; Wagalatia 1:18, 19) Biblia haisemi ni nini kilichomfanya Barnaba asiwe na shaka kumwelekea Sauli. Je, wanaume hao wawili walifahamiana, na hivyo kumchochea Barnaba kumchunguza Sauli kwa makini na kuwahakikishia mitume kwamba alikuwa mnyoofu? Je, Barnaba aliwajua Wakristo fulani huko Damasko na hivyo akapata habari ya jinsi Sauli alivyogeuka? Kwa vyovyote vile, Barnaba aliondoa mashaka ya wengine kumhusu Sauli. Kwa hiyo, Sauli akakaa na mtume Petro kwa muda wa siku 15.

Siku Kumi na Tano Pamoja na Petro

Sauli alipewa utume wake moja kwa moja na Yesu. Hivyo, hakuhitaji kupewa ruhusa na mwanadamu yeyote, kama inavyoonyeshwa katika barua yake kwa Wagalatia. (Wagalatia 1:11, 12) Lakini bila shaka Sauli alitambua umuhimu wa kujulishwa vizuri kuhusu huduma ya Yesu. Kukaa na Petro kungempa nafasi nzuri ya kujifunza kuhusu huduma hiyo. (Luka 24:12; 1 Wakorintho 15:3-8) Sauli angekuwa na mambo mengi ya kuwauliza Petro na Yakobo, nao wangemuuliza kuhusu maono yake na utume wake.

Jinsi Alivyookolewa Kutokana na Marafiki wa Zamani

Inasemekana kuwa Stefano ndiye Mkristo wa kwanza kuuawa kwa ajili ya imani. Wale ambao Stefano alikuwa amebishana nao mapema walikuwa wa “lile lililoitwa Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru, na kati ya Wakirene na Waaleksandria na kati ya wale wa kutoka Kilikia na Asia.” Sasa Sauli alikuwa ‘akibishana na Wayahudi wenye kusema Kigiriki,’ akiwatolea ushuhuda kwa ujasiri. Matokeo yalikuwa nini? Walitaka kumuua.—Matendo 6:9; 9:28, 29.

Ni jambo linaloeleweka kwamba Sauli alitaka kueleza kuhusu mabadiliko makubwa katika maisha yake na kujaribu kufundisha marafiki wake wa zamani kumhusu Masihi. Hata hivyo, Wayahudi hao wenye kusema Kigiriki walimtendea Sauli kwa ukatili na kumwona kuwa msaliti.

Je, Sauli alitambua hatari kubwa aliyokabili? Tunasoma kwamba alipokuwa akisali katika hekalu, alipata njozi na akamwona Yesu ambaye alimwambia hivi: “Fanya upesi uondoke Yerusalemu haraka, kwa sababu hawatakubali ushahidi wako kunihusu.” Sauli alijibu hivi: “Bwana, wao wenyewe wanajua vema kwamba nilikuwa nikiwatia gerezani na kuwapiga viboko katika sinagogi moja baada ya lingine wale wenye kukuamini; na wakati damu ya Stefano shahidi wako ilipokuwa ikimwagwa, mimi mwenyewe nilikuwa pia nimesimama kando nikikubaliana na jambo hilo.”—Matendo 22:17-20.

Watu fulani wanafikiri kuwa jibu la Sauli linamaanisha kwamba alitambua hatari iliyomkabili. Wengine wanafikiri kwamba alikuwa akisema: ‘Nilikuwa mtesaji kama wao, na wanajua hilo. Bila shaka, watachukua kwa uzito kugeuzwa kwangu imani. Labda ninaweza kuwasaidia kuelewa kweli.’ Hata hivyo, Yesu alijua kwamba Wayahudi hao hawatakubali ushuhuda wa “mwasi-imani.” Alimwambia Sauli hivi: “Ondoka uende, kwa sababu nitakutuma mbali sana kwa mataifa.”—Matendo 22:21, 22.

Wakristo wenzake walipotambua hatari aliyokabili, walimpeleka Sauli haraka katika bandari ya Kaisaria na kumtuma aende Tarso, mji wake wa nyumbani uliokuwa umbali wa kilomita 500. (Matendo 9:30) Miaka kadhaa ilipita kabla ya Sauli kurudi Yerusalemu.

Huenda kuondoka kwake haraka kulilinda kutaniko la Kikristo. Kuwapo kwa mtesaji huyo wa zamani kungetokeza hatari kubwa sana. Baada ya Sauli kuondoka, “kutaniko kotekote katika Yudea na Galilaya na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu likaendelea kuongezeka.”—Matendo 9:31.

Somo Kuhusu Kuwa Waangalifu

Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo tunaweza kukabili hali zinazotaka tuwe waangalifu. Hatuna sababu ya kuwa na mashaka isivyo lazima kuelekea watu tusiowajua. Hata hivyo, nyakati nyingine, watu wajanja wamejaribu kuwatumia vibaya watu wa Yehova ili wapate faida au wakiwa na nia ya kulidhuru kutaniko. Hivyo, tunatumia utambuzi ili tusipotoshwe na udanganyifu wa watu hao wajanja.—Methali 3:27; 2 Timotheo 3:13.

Jinsi Sauli alivyoondoka katika eneo alilokuwa akihubiri huko Yerusalemu inaonyesha njia nyingine ambayo Wakristo wanaweza kuwa waangalifu. Kuhubiri katika maeneo fulani au kuwahubiria watu fulani, kutia ndani marafiki wa zamani, kunaweza kuwa hatari kimwili, kiroho, au hata kiadili. Ni lazima tuwe waangalifu kuhusu mambo kama vile wakati na mahali tunapokuwa na watu hao.—Methali 22:3; Mathayo 10:16.

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba habari njema ya Ufalme wa Mungu itahubiriwa kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu. Sauli aliweka mfano mzuri sana kuhusu ‘kusema kwa ujasiri katika jina la Bwana’ hata kwa marafiki na maadui wa zamani!—Matendo 9:28.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Leo, Sauli anajulikana vizuri zaidi kuwa mtume Paulo. Hata hivyo, katika mistari mingi ya Biblia inayotajwa katika habari hii, Paulo anatajwa kwa jina lake la Kiyahudi, Sauli.—Matendo 13:9.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Sauli alipofika Yerusalemu aliwahubiria kwa ujasiri Wayahudi waliozungumza Kigiriki