Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Tumeumbwa Kwa Njia ya Ajabu’

‘Tumeumbwa Kwa Njia ya Ajabu’

‘Tumeumbwa Kwa Njia ya Ajabu’

“Nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—ZABURI 139:14.

1. Kwa nini watu wengi wenye akili wanaamini kwamba Mungu ndiye aliyeumba viumbe vya ajabu vilivyo duniani?

ULIMWENGU wa asili umejaa viumbe vya ajabu. Vilitoka wapi? Watu fulani wanafikiri kwamba jibu linaweza kupatikana bila kumhusisha Muumba mwenye akili. Wengine wanaamini kwamba mtu asipomfikiria Muumba hatauelewa ulimwengu. Wanaamini kwamba viumbe vilivyo duniani vinatatanisha sana, ni tofauti sana, na unaweza kuongeza kwamba ni vya ajabu sana visiweze kutokea vyenyewe tu. Watu wengi, kutia ndani wanasayansi fulani, wanaona ushuhuda wa kwamba ulimwengu uliumbwa na Mtengenezaji mwenye hekima, mwenye nguvu, na mkarimu. *

2. Ni nini kilichomchochea Daudi amsifu Yehova?

2 Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliamini kabisa kwamba Mtengenezaji anastahili kusifiwa kwa sababu ya uumbaji Wake wa ajabu. Ingawa Daudi aliishi muda mrefu kabla ya enzi ya leo ya kisayansi, alitambua kwamba alikuwa amezungukwa na kazi za ajabu za uumbaji wa Mungu. Daudi alihitaji tu kuchunguza mwili wake ili aogope na kuuheshimu uwezo wa Mungu wa kuumba. Aliandika hivi: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.”—Zaburi 139:14.

3, 4. Kwa nini ni jambo la maana kwa kila mmoja wetu kutafakari kwa uzito kuhusu kazi za Yehova?

3 Daudi alikuwa na usadikisho huo kwa sababu alitafakari kwa uzito. Leo, shule nyingi na vyombo vya habari vinafundisha mawazo yanayovunja imani kuhusu mwanzo wa mwanadamu. Ili tuwe na imani kama ya Daudi, tunapaswa pia kutafakari kwa uzito. Hatupaswi kufuata tu mawazo ya wengine, hasa kuhusiana na mambo ya maana sana kama vile kuwapo kwa Muumba na daraka lake.

4 Zaidi ya hayo, kufikiria kwa uzito kuhusu kazi za Yehova kunatufanya tumthamini zaidi na tuwe na uhakika katika ahadi zake za wakati ujao. Na hilo linaweza kutuchochea tumjue Yehova vizuri zaidi na kumtumikia. Kwa hiyo, acheni tuone jinsi ambavyo sayansi ya leo imethibitisha kauli ya Daudi ya kwamba ‘tumeumbwa kwa njia ya ajabu.’

Jinsi Mwili Wetu Unavyokua kwa Njia ya Ajabu

5, 6. (a) Uhai wetu sote ulianza namna gani? (b) Figo zetu zinafanya kazi gani?

5 “Wewe mwenyewe uliumba figo zangu; wewe uliniweka nikiwa nimekingwa katika tumbo la mama yangu.” (Zaburi 139:13) Uhai wa kila mmoja wetu ulianzia katika tumbo la mama ukiwa chembe moja ndogo kuliko nukta iliyo mwishoni mwa sentensi hii. Chembe hiyo ndogo sana ilikuwa tata kabisa, ni kama maabara ndogo ya kemikali. Ilikua haraka sana. Kufikia mwisho wa mwezi wako wa pili katika tumbo la uzazi, tayari ulikuwa na viungo muhimu, kutia ndani figo. Ulipozaliwa, figo zako zilikuwa tayari kusafisha damu yako, kuondoa sumu na maji ya ziada mwilini, na kuhifadhi vitu muhimu. Figo zako mbili, ikiwa hazina tatizo lolote, zinasafisha maji yaliyo katika damu yako. Zinasafisha lita 5 hivi za maji kwa kila dakika 45 katika mwili wa mtu mzima!

6 Figo zako pia zinasaidia kudhibiti kiwango cha madini katika damu yako, asidi, na msukumo wa damu. Figo zinafanya mambo mengine mengi yaliyo ya maana sana, kama vile kubadili vitamini D ili iweze kutumika kukuza mifupa kwa njia inayofaa na kutokeza homoni (erythropoietin) inayochochea mwili kutengeneza chembe nyekundu za damu ndani ya mifupa yako. Ndiyo sababu figo zimeitwa “wanakemia hodari wa mwili”! *

7, 8. (a) Eleza ukuzi wa mapema wa mtoto mchanga katika tumbo la uzazi. (b) Mtoto anayekua ‘anaungwa katika sehemu za chini kabisa za dunia’ katika maana gani?

7 “Mifupa yangu haikufichwa kwako nilipofanyizwa katika siri, nilipoungwa katika sehemu za chini kabisa za dunia.” (Zaburi 139:15) Chembe ya kwanza kabisa iligawanyika, na chembe mpya zilizotokezwa ziliendelea kugawanyika. Baada ya muda, chembe ziligawanyika katika makundi ya pekee, zikawa chembe za neva, chembe za misuli, chembe za ngozi, na kadhalika. Chembe za aina moja zilikusanyika pamoja na kutengeneza tishu na kisha viungo. Kwa mfano, katika juma la tatu la mimba, mifupa ilianza kukua katika mwili wako. Ulipokuwa na majuma saba tu ulikuwa na urefu wa sentimita 2.5, lakini ulikuwa na mifupa yote 206 uliyo nayo sasa ukiwa mtu mzima, hata hivyo haikuwa imekomaa na ilikuwa laini, na bado haikuwa migumu.

8 Ukuzi huo wa ajabu ulitukia ndani ya tumbo la uzazi la mama yako. Ni kana kwamba ulifichwa katika sehemu za chini za dunia ambamo mwanadamu hangeweza kuona. Kwa kweli, wanadamu bado hawajui mengi kuhusu jinsi tunavyokua. Kwa mfano, ni nini kilichofanya chembe fulani za urithi zichochee chembe kugawanyika na kufanyiza viungo mbalimbali vya mwili? Huenda mwishowe wanasayansi wakapata jibu, lakini kama Daudi anavyosema katika mstari unaofuata, Muumba wetu, Yehova, amekuwa akielewa vizuri jambo hilo.

9, 10. Ukuzi wa sehemu za kiini-tete ‘umeandikwa’ katika “kitabu” cha Mungu jinsi gani?

9 Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa, kuhusiana na siku ambazo zilifanyizwa na hakukuwako hata moja kati ya hizo.” (Zaburi 139:16) Chembe yako ya kwanza ilikuwa na ramani kamili ya mwili wako wote. Ramani hiyo iliongoza ukuzi wako kwa miezi tisa ambayo ulikuwa katika tumbo la uzazi kabla hujazaliwa na kisha ukuzi wako kwa zaidi ya miaka 20 kufikia kuwa mtu mzima. Wakati huo, mwili wako ulipitia hatua nyingi, na hatua hizo zote ziliongozwa na habari iliyohifadhiwa katika chembe hiyo ya kwanza.

10 Daudi hakuwa na ujuzi kuhusu chembe za urithi na chembe nyingine, kwa sababu hakuwa na darubini. Lakini alitambua kwa usahihi kwamba ukuzi wa mwili wake mwenyewe ulithibitisha kwamba ulipangwa mapema. Huenda Daudi alijua kidogo jinsi viini-tete vinavyokua, kwa hiyo angeweza kufikiri kwamba ni lazima kila hatua ifuate ramani na programu iliyotayarishwa mapema. Akitumia lugha ya kishairi, aliifafanua ramani hiyo kana kwamba ‘ilikuwa imeandikwa’ katika “kitabu” cha Mungu.

11. Tulipata umbo la mwili wetu jinsi gani?

11 Leo, tunajua kwamba umbo ambalo ulirithi kutoka kwa wazazi wako na mababu, kama vile urefu, umbo la uso, rangi ya macho na ya nywele, na maelfu ya sifa nyingine, zilitegemea chembe zako za urithi. Kila moja ya chembe zako ina makumi ya maelfu ya chembe za urithi, na kila chembe ya urithi ni sehemu ya mnyororo mrefu unaofanyizwa na DNA au ADN (deoxyribonucleic acid). Maagizo ya kuujenga mwili wako ‘yameandikwa’ katika kemikali zilizo katika DNA ya mwili wako. Kila mara chembe zako zinapogawanyika ili kutengeneza chembe mpya au kuchukua mahali pa chembe zilizozeeka, DNA yako inatoa maagizo hayo, na hivyo kukufanya uendelee kuwa hai ukiwa na umbo lilelile. Huo ni mfano mzuri kama nini ambao unaonyesha nguvu na hekima ya Mtengenezaji wetu wa kimbingu!

Akili Yetu ya Pekee

12. Ni nini kinachofanya wanadamu wawe tofauti kabisa na wanyama?

12 “Kwa hiyo, jinsi mawazo yako yalivyo yenye thamani kwangu! Ee Mungu, jinsi jumla yake yote ilivyo kuu! Kama ningejaribu kuyahesabu, ni mengi kuliko hata chembe za mchanga.” (Zaburi 139:17, 18a) Wanyama pia wameumbwa kwa njia ya ajabu, na wanyama fulani wana uwezo na hisi fulani ambazo zinapita zile za wanadamu. Lakini Mungu aliwapa wanadamu akili inayopita akili ya mnyama yeyote yule. Kitabu kimoja cha sayansi kinasema hivi: “Ni kweli kwamba sisi wanadamu tunalingana na viumbe wengine kwa njia nyingi, lakini uwezo wetu wa kuzungumza lugha na kufikiri ni wa pekee sana miongoni mwa viumbe walio duniani. Pia, tuna hamu ya pekee sana ya kujua jinsi tulivyo: Mwili wetu umefanywa jinsi gani? Tuliumbwa jinsi gani?” Hayo ni maswali ambayo Daudi pia alifikiria.

13. (a) Daudi angeweza jinsi gani kutafakari kuhusu mawazo ya Mungu? (b) Tunaweza kufuata mfano wa Daudi jinsi gani?

13 Jambo la maana zaidi ni kwamba tofauti na wanyama, tuna uwezo wa pekee sana wa kutafakari kuhusu mawazo ya Mungu. * Zawadi hiyo ya pekee ni moja ya mambo yanayoonyesha tumeumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:27) Daudi alitumia zawadi hiyo vizuri. Alitafakari kuhusu mambo yanayothibitisha kwamba kuna Mungu na akatafakari pia kuhusu sifa nzuri zinazoonekana katika dunia. Daudi alikuwa pia na vitabu vya zamani vya Maandiko Matakatifu ambamo Mungu anafunua habari na kazi zake. Maandiko hayo yaliyoongozwa na roho yalimsaidia Daudi kuelewa mawazo, utu, na kusudi la Mungu. Kutafakari kuhusu Maandiko, uumbaji, na jinsi Mungu alivyoshughulika naye kulimchochea Daudi amsifu Mtengenezaji wake.

Imani Inatia Ndani Nini?

14. Ili tuweze kuwa na imani katika Mungu kwa nini hatuhitaji kujua kila jambo kumhusu?

14 Kadiri Daudi alivyotafakari kuhusu uumbaji na Maandiko, ndivyo alivyotambua kwamba hangeweza kamwe kufahamu ujuzi kamili wa Mungu na uwezo wake. (Zaburi 139:6) Hali yetu ni kama ya Daudi. Hatutaweza kamwe kuelewa kila jambo kuhusu kazi zote za uumbaji za Mungu. (Mhubiri 3:11; 8:17) Lakini Mungu ‘amefunua’ ujuzi wa kutosha kupitia Maandiko na uumbaji ili kuwasaidia watu wanaotafuta kweli ambao wanaishi wakati wowote ule, kuwa na imani ambayo inategemea uthibitisho.—Waroma 1:19, 20; Waebrania 11:1, 3.

15. Onyesha jinsi imani na uhusiano wetu pamoja na Mungu zinavyohusiana.

15 Kuwa na imani kunatia ndani mambo mengi zaidi ya kukubali tu kwamba uhai na ulimwengu umetokana na Chanzo chenye akili. Kunatia ndani kumtegemea Yehova Mungu akiwa mtu, na kutambua kwamba anataka tumjue na kudumisha uhusiano mzuri pamoja naye. (Yakobo 4:8) Tunaweza kufikiria jinsi mtoto anavyomtegemea na kumwamini baba mwenye upendo. Mtu mwenye mashaka akikuuliza ikiwa baba yako anaweza kweli kukusaidia wakati wa taabu, huenda usiweze kumsadikisha kwamba baba yako anategemeka. Hata hivyo, ikiwa umeona mambo yanayothibitisha kwamba baba yako anategemeka, unaweza kuwa na hakika kwamba hatakosa kukusaidia. Vivyo hivyo, kupata kumjua Yehova kwa kujifunza Maandiko, kutafakari kuhusu uumbaji, na kuona akitusaidia kwa kujibu sala zetu kunatuchochea tumtegemee. Pia kunatufanya tutake kujifunza mengi zaidi kumhusu na kumsifu milele kwa sababu tunampenda bila ubinafsi na tumejitoa kwake. Hilo ndilo kusudi bora zaidi ambalo mtu anaweza kufuatia.—Waefeso 5:1, 2.

Tafuta Mwongozo wa Mtengenezaji Wetu

16. Tunajifunza nini tunapochunguza uhusiano wa karibu ambao Daudi alikuwa nao pamoja na Yehova?

16 “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.” (Zaburi 139:23, 24) Daudi alijua kwamba tayari Yehova alimjua kabisa. Mtengenezaji wake aliona kila jambo alilofikiria, alilosema, au alilofanya. (Zaburi 139:1-12; Waebrania 4:13) Ujuzi wa ndani sana ambao Mungu alikuwa nao ulimfanya Daudi ajisikie akiwa salama, kama vile mtoto mdogo anavyojisikia akiwa salama anapokuwa mikononi mwa wazazi wake wenye upendo. Daudi alithamini uhusiano huo wa karibu pamoja na Yehova, naye alijitahidi kuudumisha kwa kufikiria kwa undani kuhusu kazi za Yehova na kwa kusali Kwake. Kwa kweli, zaburi nyingi za Daudi, kutia ndani Zaburi ya 139, ni sala ambazo zimetungwa kama muziki. Kutafakari na kusali kunaweza kutusaidia vivyo hivyo kumkaribia Yehova.

17. (a) Kwa nini Daudi alitaka Yehova auchunguze moyo wake? (b) Njia yetu ya kutumia uhuru wetu wa kuchagua ina matokeo gani juu ya maisha yetu?

17 Kwa kuwa tumefanywa kwa mfano wa Mungu, tumepewa uhuru wa kuchagua. Tunaweza kuchagua kufanya mema au mabaya. Kwa kuwa tuna uhuru huo tuna wajibu wa kiadili. Daudi hakutaka kuhesabiwa pamoja na waovu. (Zaburi 139:19-22) Alitaka kuepuka kufanya makosa yenye kuumiza. Hivyo, alipotafakari kuhusu ujuzi wa Yehova wa mambo yote, Daudi alimwomba Mungu kwa unyenyekevu achunguze utu wake wa ndani na kumwongoza katika njia ya uzima. Viwango vya Mungu vya maadili vya uadilifu vinamhusu kila mtu; kwa hiyo sisi pia tunahitaji kufanya maamuzi yanayofaa. Yehova anatuhimiza sote tumtii. Tukifanya hivyo atatukubali na tutapata faida nyingi. (Yohana 12:50; 1 Timotheo 4:8) Kutembea pamoja na Yehova siku kwa siku kunatusaidia kusitawisha amani ya akili, hata tunapopata matatizo yenye kuhuzunisha.—Wafilipi 4:6, 7.

Mfuate Mtengenezaji Wetu wa Ajabu!

18. Daudi alikata kauli gani alipotafakari kuhusu uumbaji?

18 Akiwa kijana, mara nyingi Daudi alikuwa nje, akichunga makundi ya kondoo. Kondoo waliinamisha vichwa vyao ili kulisha, lakini yeye aliinua macho yake mbinguni. Katika giza la usiku, alitafakari kuhusu fahari ya ulimwengu mzima na maana yake. Daudi aliandika hivi: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake. Siku moja baada ya siku nyingine hufanya maneno yabubujike, na usiku mmoja baada ya usiku mwingine huonyesha ujuzi.” (Zaburi 19:1, 2) Daudi alielewa kwamba alihitaji kumtafuta na kumfuata Yule ambaye alitengeneza vitu vyote kwa njia ya ajabu. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo.

19. Vijana na wazee wanaweza kujifunza nini kuhusu jinsi ‘tulivyoumbwa kwa njia ya ajabu’?

19 Daudi aliweka mfano mzuri wa kufuata shauri ambalo baadaye mwana wake Sulemani aliwapa vijana: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako . . . Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:1, 13) Akiwa kijana, tayari Daudi alitambua kwamba ‘aliumbwa kwa njia ya ajabu.’ Kuishi kupatana na ujuzi huo kulimletea faida kubwa katika maisha yake yote. Ikiwa sisi, vijana kwa wazee, tutamsifu na kumtumikia Muumba wetu Mkuu, maisha yetu ya sasa na ya wakati ujao yatakuwa yenye kupendeza. Biblia inaahidi hivi kuhusu wale ambao wanadumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kuishi kupatana na njia zake za uadilifu: “Wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi, wataendelea kuwa wanono na wabichi, ili kutangaza kwamba Yehova ni mnyoofu.” (Zaburi 92:14, 15) Nasi tutakuwa na tumaini la kufurahia milele kazi za ajabu za Mtengenezaji wetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Ona gazeti la Amkeni! la Juni 22, 2004 (22/6/2004), lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 6 Ona pia makala “Mafigo Yako—Chujio la Kutegemeza Uhai,” katika gazeti la Amkeni! la Agosti 8, 1997 (8/8/1997).

^ fu. 13 Inaonekana maneno ya Daudi katika Zaburi 139:18b yanamaanisha kwamba ikiwa angehesabu mawazo ya Yehova siku nzima mpaka alipolala usiku, bado angekuwa na mawazo mengi ya kuhesabu wakati angeamka asubuhi.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ukuzi wa kiini-tete unaonyesha jinsi gani kwamba ‘tumeumbwa kwa njia ya ajabu’?

• Kwa nini tunapaswa kutafakari kuhusu mawazo ya Yehova?

• Kuna uhusiano gani kati ya imani na uhusiano wetu pamoja na Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ukuzi wa mtoto katika tumbo la uzazi unafuata ramani iliyotayarishwa mapema

DNA

[Hisani]

Unborn fetus: Lennart Nilsson

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tuna uhakika katika Yehova kama watoto wanaomtegemea baba mwenye upendo

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kutafakari kuhusu kazi za mikono za Yehova kulimchochea Daudi amsifu Mungu