Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anathamini Utii Wako

Yehova Anathamini Utii Wako

Yehova Anathamini Utii Wako

“Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie.” —METHALI 27:11.

1. Ni roho gani imeenea katika ulimwengu wa leo?

ROHO ya kujitegemea na kutotii imeenea katika ulimwengu wa leo. Katika barua yake kwa Wakristo Waefeso, mtume Paulo anaeleza kwa nini roho hiyo imeenea: ‘Wakati fulani mlitembea kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.’ (Waefeso 2:1, 2) Ndiyo, unaweza kusema kwamba Shetani Ibilisi, “mtawala wa mamlaka ya hewa,” ameambukiza ulimwengu wote roho ya kutotii. Alikuwa akifanya hivyo katika karne ya kwanza, na amekuwa akifanya hivyo hata zaidi tangu alipotupwa kutoka mbinguni karibu na wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.—Ufunuo 12:9.

2, 3. Tuna sababu gani za kumtii Yehova?

2 Hata hivyo, tukiwa Wakristo, tunajua kwamba Yehova Mungu anastahili utii wetu wa kutoka moyoni kwa sababu yeye ndiye Muumba wetu, Mtegemezaji wa uhai wetu, Mwenye Enzi Kuu aliye na upendo, na Mkombozi wetu. (Zaburi 148:5, 6; Matendo 4:24; Wakolosai 1:13; Ufunuo 4:11) Waisraeli wa siku za Musa walijua kwamba Yehova alikuwa Mpaji-uhai na Mwokozi wao. Kwa hiyo, Musa aliwaambia hivi: “Nanyi mtakuwa waangalifu kufanya kama vile ambavyo Yehova Mungu wenu amewaamuru ninyi.” (Kumbukumbu la Torati 5:32) Ndiyo, Yehova alistahili utii wao. Hata hivyo, muda si muda, waliacha kumtii Mwenye Enzi Kuu wao.

3 Utii wetu ni wa maana kadiri gani kwa Muumba wa ulimwengu wote mzima? Wakati fulani, Mungu alimwongoza nabii Samweli amwambie hivi Mfalme Sauli: “Kutii ni bora kuliko dhabihu.” (1 Samweli 15:22, 23) Kwa nini?

Jinsi Kutii ‘Kulivyo Bora Kuliko Dhabihu’

4. Tunaweza kumpa Yehova kitu fulani katika njia gani?

4 Akiwa Muumba, tayari Yehova anamiliki vitu vyote vya kimwili tulivyo navyo. Kwa kuwa ndivyo ilivyo, je, kuna kitu chochote ambacho tunaweza kumpa? Ndiyo, tunaweza kumpa kitu fulani chenye thamani sana. Ni kitu gani hicho? Tunaweza kupata jibu katika himizo lifuatalo: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Tunaweza kumpa Mungu utii wetu. Hata ingawa tuna hali na malezi tofauti, kila mmoja wetu anapotii anaweza kujibu shtaka lenye uovu la Shetani Ibilisi anayedai kwamba wanadamu hawawezi kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wakijaribiwa. Hilo ni pendeleo kubwa kama nini!

5. Kutotii kunamfanya Muumba ahisi namna gani? Toa mfano.

5 Mungu anapendezwa na maamuzi tunayofanya. Tusipomtii tunamhuzunisha. Jinsi gani? Anatiwa uchungu anapoona mtu fulani akifanya uamuzi usio wa hekima. (Zaburi 78:40, 41) Tuseme kwamba mtu mwenye ugonjwa wa sukari anakosa kula vyakula vinavyofaa ambavyo aliagizwa ale kwa ajili ya afya yake, naye anaendelea kula vyakula vinavyoharibu afya yake. Daktari wake mwenye kujali angehisi namna gani? Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anahisi uchungu wakati wanadamu wanapokosa kumtii, kwa kuwa anajua matokeo ya kupuuza maagizo yake yanayookoa uhai.

6. Ni nini kitakachotusaidia kuwa watiifu kwa Mungu?

6 Ni nini kitakachomsaidia kila mmoja wetu awe mtiifu? Kila mmoja wetu anapaswa kumwomba Mungu ampe “moyo mtiifu,” kama Mfalme Sulemani alivyoomba. Aliomba apewe moyo wa aina hiyo ili “atambue kati ya mema na mabaya” na hivyo aweze kuwahukumu Waisraeli wenzake. (1 Wafalme 3:9) Tunahitaji “moyo mtiifu” ili tutofautishe kati ya mema na mabaya katika ulimwengu uliojaa roho ya kutotii. Mungu ametupa Neno lake, vifaa vya kutusaidia kujifunza Biblia, mikutano ya Kikristo, na wazee wenye kujali wa kutaniko ili tuweze kukuza “moyo mtiifu.” Je, unatumia vizuri maandalizi hayo ya upendo?

7. Kwa nini Yehova anakazia utii kuliko dhabihu?

7 Kuhusiana na jambo hilo, kumbuka kwamba wakati uliopita Yehova aliwaambia watu wake wa zamani kwamba utii ulikuwa wa maana sana hata kuliko dhabihu za wanyama. (Methali 21:3, 27; Hosea 6:6; Mathayo 12:7) Kwa kuwa Yehova ndiye aliyewaamuru watu wake watoe dhabihu kama hizo, kwa nini aliwaambia hivyo. Hata hivyo, yule anayetoa dhabihu ana nia gani? Je, anafanya hivyo ili ampendeze Mungu? Au anafuata tu desturi fulani? Ikiwa kwa kweli mwabudu fulani anataka kumpendeza Mungu, atakuwa mwangalifu katika kutii amri zote za Mungu. Mungu hahitaji dhabihu za wanyama, lakini utii wetu ni kitu chenye thamani ambacho tunaweza kumpa.

Mfano wa Kuonya

8. Kwa nini Mungu alimkataa Sauli asiwe mfalme?

8 Maelezo ya Biblia kuhusu Mfalme Sauli yanakazia umuhimu wa utii. Sauli alikuwa mtawala mnyenyekevu na mwenye kiasi alipoanza, alikuwa ‘mdogo machoni pake mwenyewe.’ Hata hivyo, baada ya muda, alianza kufanya maamuzi kwa kiburi na kwa kutegemea mawazo yasiyofaa. (1 Samweli 10:21, 22; 15:17) Wakati mmoja, Sauli alipaswa kupigana na Wafilisti. Samweli alimwambia mfalme Sauli amngoje ili aje kumtolea Yehova dhabihu kisha ampe mwongozo zaidi. Hata hivyo, Samweli hakuja haraka kama ilivyotazamiwa, nao watu wakaanza kutawanyika. Sauli alipoona hivyo, “akaitoa dhabihu ya kuteketezwa.” Jambo hilo halikumpendeza Yehova. Mwishowe Samweli alipofika, mfalme alitoa kisingizio cha kutotii kwake. Alisema kwamba kwa sababu Samweli alichelewa, ‘alijilazimisha’ kutoa dhabihu ya kuteketezwa ili kuutuliza uso wa Yehova. Mfalme Sauli aliona kwamba kutoa dhabihu hiyo ni jambo la maana sana kuliko kutii maagizo aliyopewa ya kumngojea Samweli ili atoe dhabihu hiyo. Samweli alimwambia hivi: “Umetenda kipumbavu. Hukuishika amri ya Yehova Mungu wako ambayo alikuamuru.” Sauli alipoteza cheo chake cha kuwa mfalme kwa sababu hakumtii Yehova.—1 Samweli 10:8; 13:5-13.

9. Sauli alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa na zoea la kutomtii Mungu?

9 Je, mfalme huyo alijifunza somo kutokana na jambo hilo? Hapana! Baadaye, Yehova alimwamuru Sauli aliangamize taifa la Amaleki, ambalo wakati uliopita lilishambulia Israeli bila kuchokozwa. Sauli alipaswa kuwaua hata wanyama wa kufugwa. Alimtii Yehova kwa ‘kupiga Amaleki kutoka Havila mpaka Shuri.’ Samweli alipokuja kukutana naye, mfalme alifurahi kwa sababu ya ushindi huo akasema hivi: “Umebarikiwa na Yehova. Nimelitimiza neno la Yehova.” Hata hivyo, kinyume kabisa na maagizo ya wazi ambayo alikuwa amepewa, Sauli hakumwangamiza Mfalme Agagi na “wanyama bora zaidi wa kundi na mifugo na walio wanono na kondoo-dume na vyote vilivyokuwa bora.” Mfalme Sauli alitetea kutotii kwake kwa kusema hivi: “Watu waliwahurumia wanyama walio bora zaidi wa kundi na mifugo, kwa kusudi la kutoa dhabihu kwa Yehova, Mungu wako.”—1 Samweli 15:1-15.

10. Sauli alikosa kujifunza somo gani?

10 Basi, Samweli akamwambia Sauli: “Je, Yehova hupendezwa sana na matoleo ya kuteketezwa na dhabihu kuliko kuitii sauti ya Yehova? Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikiliza kuliko mafuta ya kondoo-dume.” (1 Samweli 15:22) Kwa kuwa Yehova alikuwa amesema kwamba wanyama hao walipaswa kuangamizwa, hangekubali watolewe dhabihu.

Uwe Mtiifu Katika Mambo Yote

11, 12. (a) Yehova ana maoni gani kuhusu jitihada zetu za kumpendeza katika ibada yetu? (b) Mtu anaweza kujidanganya namna gani na kufikiri kwamba anafanya mapenzi ya Mungu huku kwa kweli akikosa kutii?

11 Yehova anafurahi sana anapoona watumishi wake washikamanifu wakibaki imara wanapoteswa, wakitangaza Ufalme hata ingawa watu wengi hawapendi ujumbe huo, na wakihudhuria mikutano ya Kikristo hata ingawa si rahisi kupata riziki! Moyo wake unashangilia anapoona tukitii katika mambo hayo muhimu ya maisha yetu ya kiroho! Jitihada zetu za kumwabudu Yehova ni zenye thamani kwake zinapochochewa na upendo. Huenda wanadamu wakapuuza kazi yetu ngumu, lakini Mungu anaona na kukumbuka matoleo yetu tunayotoa kwa moyo wote.—Mathayo 6:4.

12 Hata hivyo, ili tumpendeze kabisa Mungu wetu, ni lazima tuwe watiifu katika kila sehemu ya maisha yetu. Hatupaswi kamwe kujidanganya kwa kufikiri kwamba tunaweza kuvunja matakwa fulani ya Mungu maadamu tunamtolea ibada katika sehemu nyingine za maisha. Kwa mfano, huenda mtu akajidanganya kwa kufikiri kwamba akifanya kidesturi tu mambo fulani ya ibada, anaweza kuepuka nidhamu akihusika katika mwenendo mchafu au akifanya dhambi nyingine nzito. Ni kosa kama nini kufikiri hivyo!—Wagalatia 6:7, 8.

13. Utii wetu kwa Yehova unaweza kujaribiwa jinsi gani tunapokuwa mahali pa siri?

13 Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninamtii Yehova katika shughuli zangu za kila siku, hata katika mambo yanayoonekana kuwa ya kibinafsi?’ Yesu alisema: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu ambaye si mwaminifu katika lililo dogo zaidi si mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Je, ‘tunatembea katika utimilifu wa moyo wetu’ hata ‘ndani ya nyumba yetu,’ ambamo wengine hawawezi kutuona? (Zaburi 101:2) Kwa kweli, utimilifu wetu unaweza kujaribiwa tukiwa ndani ya nyumba yetu. Katika nchi nyingi ambako kompyuta zinatumiwa kwa ukawaida nyumbani, watu wanaweza kupata kwa urahisi sana picha chafu kwenye kompyuta. Miaka michache iliyopita, mtu hangeweza kuona picha hizo chafu isipokuwa katika sehemu zenye burudani chafu za ngono. Je, tutatii kutoka moyoni maneno haya ya Yesu: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake”? Je, tutakataa hata kutazama picha chafu? (Mathayo 5:28; Ayubu 31:1, 9, 10; Zaburi 119:37; Methali 6:24, 25; Waefeso 5:3-5) Namna gani kuhusu vipindi vya televisheni ambavyo vinaonyesha jeuri? Je, sisi ni kama Mungu wetu, ambaye nafsi yake ‘hakika inamchukia mtu yeyote anayependa jeuri’? (Zaburi 11:5) Au namna gani kunywa kileo kupita kiasi kwa siri? Biblia haishutumu ulevi tu bali pia inawaonya Wakristo wasiwe na zoea la kunywa “divai nyingi sana.”—Tito 2:3; Luka 21:34, 35; 1 Timotheo 3:3.

14. Tunaweza kuonyesha tunamtii Mungu katika masuala kama gani yanayohusisha pesa?

14 Pia tunahitaji kuwa waangalifu sana kuhusu masuala ya pesa. Kwa mfano, je, tungeshiriki katika miradi ya kujitajirisha upesi ambayo inaelekea kuhusisha upunjaji? Je, tunashawishiwa kutumia njia zisizo halali kuepuka kulipa kodi? Au badala yake, dhamiri yetu inatusukuma tutii amri ya ‘kuwapa wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi’?—Waroma 13:7.

Utii Unaochochewa na Upendo

15. Kwa nini unatii amri za Yehova?

15 Kutii kanuni za Mungu kunaleta baraka. Kwa mfano, tukiepuka kuvuta sigara, tukiishi maisha safi kiadili, na tukiheshimu utakatifu wa damu, tunaweza kuepuka magonjwa fulani. Kwa kuongezea, tukiishi kupatana na kweli ya Biblia katika sehemu nyingine za maisha yetu, tunaweza kufaidika kiuchumi, kijamii, au katika maisha yetu ya jamaa. (Isaya 48:17) Kwa kufaa, faida zozote za kimwili kama hizo zinaweza kuonwa kuwa baraka ambazo zinathibitisha kwamba sheria za Mungu zinaleta faida. Hata hivyo, tunamtii Yehova hasa kwa sababu tunampenda. Hatumtumikii Mungu kwa sababu za kichoyo. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Mungu alitupa uhuru wa kuchagua kumtii yeyote tunayetaka. Sisi tunachagua kumtii Yehova kwa sababu tunataka kumpendeza na kwa sababu tunataka kufanya yaliyo sawa.—Waroma 6:16, 17; 1 Yohana 5:3.

16, 17. (a) Yesu alimtii Mungu jinsi gani kwa sababu ya kumpenda kutoka moyoni? (b) Tunaweza kumwiga Yesu namna gani?

16 Yesu aliweka mfano mkamilifu wa kumtii Yehova kwa sababu ya kumpenda sana kutoka moyoni. (Yohana 8:28, 29) Alipokuwa duniani, Yesu “alijifunza kutii kutokana na mambo aliyoteseka.” (Waebrania 5:8, 9) Jinsi gani? Yesu “alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” (Wafilipi 2:7, 8) Ingawa tayari Yesu alikuwa mtiifu akiwa mbinguni, utii wake ulijaribiwa zaidi duniani. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu anastahili kabisa kutumika akiwa Kuhani Mkuu kwa ajili ya ndugu zake wa kiroho na pia kwa ajili ya wanadamu wengine wenye imani.—Waebrania 4:15; 1 Yohana 2:1, 2.

17 Namna gani sisi? Tunaweza kumwiga Yesu kwa kutanguliza utii kwa mapenzi ya Mungu. (1 Petro 2:21) Kila mmoja wetu anaweza kupata uradhi wakati upendo wake kwa Mungu unapomchochea kufanya yale ambayo Yehova anaamuru, hata tunaposukumwa au kushawishiwa tufanye kinyume. (Waroma 7:18-20) Hilo linatia ndani kuwa tayari kutii miongozo kutoka kwa wale wanaoongoza katika ibada ya kweli, ingawa wao si wakamilifu. (Waebrania 13:17) Yehova anathamini sana tunapotii amri zake katika maisha yetu ya faraghani.

18, 19. Tunapata faida gani tunapomtii Mungu kutoka moyoni?

18 Leo, huenda tukahitaji kumtii Yehova kwa kuvumilia mateso ili kudumisha utimilifu wetu. (Matendo 5:29) Pia, ili tutii amri ya Yehova ya kuhubiri na kufundisha ni lazima tuvumilie mpaka mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 24:13, 14; 28:19, 20) Tunahitaji kuvumilia ili kuendelea kukusanyika pamoja na ndugu zetu, hata ingawa huenda tukahisi tunalemewa na matatizo ya ulimwengu. Mungu wetu mwenye upendo anajua kabisa jitihada tunazofanya ili kumtii katika mambo hayo. Hata hivyo, ili tumtii kikamili, ni lazima tupambane na mwili wetu wenye dhambi, tuepuke mambo mabaya huku tukijitahidi kuthamini mambo mema.—Waroma 12:9.

19 Tunapomtumikia Yehova kwa sababu tunampenda na tuna moyo wenye uthamini, ‘anakuwa kwetu mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.’ (Waebrania 11:6) Dhabihu zinazofaa ni za maana na zinapendeza, lakini Yehova anapendezwa kabisa na utii kamili unaochochewa na upendo kumwelekea.—Methali 3:1, 2.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba tuna kitu ambacho tunapaswa kumpa Yehova?

• Sauli alifanya makosa gani?

• Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unaamini utii ni bora kuliko dhabihu?

• Ni nini ambacho kinakuchochea umtii Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Daktari mwenye kujali angehisi namna gani kumhusu mgonjwa anayepuuza maagizo yake?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kwa nini Mfalme Sauli alipoteza kibali cha Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Je, unatii amri za Mungu ukiwa ndani ya nyumba yako?