Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—I

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—I

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—I

NI MWAKA wa 613 K.W.K. Nabii Yeremia yuko Yuda, akitangaza bila woga kuharibiwa kwa Yerusalemu kunakokaribia na kufanywa ukiwa kwa nchi ya Yuda. Mfalme Nebukadneza wa Babiloni tayari amewachukua mateka Wayahudi wengi. Baadhi ya Wayahudi hao ni kijana Danieli na waandamani wake watatu ambao wanafanya kazi katika makao ya mfalme wa Wakaldayo. Wengi wa Wayahudi waliohamishwa wako kando ya mto Kebari “katika nchi ya Wakaldayo.” (Ezekieli 1:1-3) Yehova anawapa watu hao waliotekwa mjumbe. Anamweka rasmi Ezekieli aliye na umri wa miaka 30 awe nabii.

Kitabu cha Ezekieli ambacho kilikamilishwa mwaka wa 591 K.W.K., kinazungumzia kipindi cha miaka 22. Ezekieli anaandika kwa uangalifu na kwa makini. Anaonyesha tarehe za unabii mbalimbali anaotoa, hata anataja siku na mwezi na mwaka. Sehemu ya kwanza ya ujumbe wa Ezekieli inakazia kuanguka na kuharibiwa kwa Yerusalemu. Sehemu ya pili ina matangazo ya hukumu juu ya mataifa jirani, na sehemu ya mwisho inahusu kurudishwa kwa ibada ya Yehova. Makala hii inazungumzia Ezekieli 1:1–24:27, ambayo ina maono, unabii mbalimbali, na maigizo ya mambo ambayo yangelipata jiji la Yerusalemu.

“NIMEKUFANYA KUWA MLINZI”

(Ezekieli 1:1–19:14)

Baada ya kupewa maono ya ajabu ya kiti cha ufalme cha Yehova, Ezekieli anapokea utume wake. “Nimekufanya kuwa mlinzi katika nyumba ya Israeli,” Yehova anamwambia, “nawe utasikia maneno kutoka katika kinywa changu nawe lazima utawapa maonyo kutoka kwangu.” (Ezekieli 3:17) Ili kutoa unabii kuhusu kuzingirwa kwa Yerusalemu na matokeo yake, Ezekieli anaamriwa aigize matukio mawili. Akizungumza kuhusu nchi ya Yuda, Yehova anasema hivi kupitia Ezekieli: “Tazama mimi! Ninaleta upanga juu yenu, nami hakika nitaharibu mahali penu pa juu.” (Ezekieli 6:3) Anawaambia hivi wakaaji wa nchi hiyo: “Lazima shada [la msiba] likujie wewe.”—Ezekieli 7:7.

Mnamo 612 K.W.K., katika maono, Ezekieli anapelekwa mpaka Yerusalemu. Anaona mambo yenye kuchukiza kama nini yakitendwa ndani ya hekalu la Mungu! Yehova anapotuma vikosi vyake vya mbinguni vya kutekeleza hukumu (vinavyowakilishwa na “wanaume sita”) ili kuonyesha hasira yake juu ya waasi-imani, wale tu waliotiwa “alama kwenye mapaji ya uso” ndio watakaookolewa. (Ezekieli 9:2-6) Lakini kwanza, ni lazima “makaa ya moto,” yaani, ujumbe mkali wa uharibifu kutoka kwa Mungu, utangazwe jijini. (Ezekieli 10:2) Ingawa ‘Yehova ataleta njia ya waovu wenyewe juu ya vichwa vyao,’ anaahidi kuwakusanya Waisraeli waliotawanywa.—Ezekieli 11:17-21.

Roho ya Mungu inamrudisha Ezekieli huko Ukaldayo. Igizo fulani linaonyesha jinsi Mfalme Sedekia na watu wengine watakavyokimbia kutoka Yerusalemu. Manabii wa uwongo wa kiume na wa kike wanashutumiwa. Waabudu-sanamu wanakataliwa. Yuda inalinganishwa na mzabibu usio na thamani. Fumbo la tai na mzabibu linaonyesha matokeo machungu ya Yerusalemu kuigeukia Misri ili kupata msaada. Fumbo hilo linamalizia kwa ahadi ya kwamba ‘Yehova atapandikiza kitawi kichanga juu ya mlima mrefu.’ (Ezekieli 17:22) Hata hivyo, huko Yuda, hakutakuwa na “fimbo yoyote ya enzi ya kutawalia.”—Ezekieli 19:14.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:4-28—Gari la kimbingu linafananisha nini? Gari hilo linafananisha sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova ambalo limefanyizwa na viumbe waaminifu wa roho. Roho takatifu ya Yehova ndicho chanzo cha nguvu zake. Mwenye Kupanda gari hilo, ambaye anamwakilisha Yehova, ana utukufu usio na kifani. Upinde maridadi wa mvua unaonyesha utulivu alio nao.

1:5-11—Wale viumbe hai wanne ni nani? Katika maono yake ya pili yanayohusu gari hilo, Ezekieli anawatambulisha viumbe hai wanne kuwa makerubi. (Ezekieli 10:1-11; 11:22) Katika maelezo haya ya baadaye, Ezekieli anauita uso wa ng’ombe-dume “uso wa kerubi.” (Ezekieli 10:14) Hilo linafaa kwa sababu ng’ombe-dume anafananisha nguvu na uwezo, na makerubi ni viumbe wa roho wenye nguvu.

2:6—Kwa nini Ezekieli anaitwa tena na tena “mwana wa binadamu”? Yehova anamwita Ezekieli mwana wa binadamu ili kumkumbusha nabii huyo kwamba ameumbwa kwa nyama na damu, na hivyo kuonyesha tofauti kubwa kati ya mjumbe wa kibinadamu na Mungu aliye Chanzo cha ujumbe huo. Katika Injili, Yesu Kristo pia anaitwa mwana wa binadamu mara 80 hivi ili kuonyesha wazi kwamba Mwana wa Mungu alikuja akiwa mwanadamu wala si kiumbe wa roho aliyevaa mwili wa kibinadamu.

2:9–3:3—Kwa nini kitabu cha kukunjwa chenye nyimbo za huzuni na maombolezo kilikuwa kitamu kwa Ezekieli? Mtazamo wa Ezekieli kuhusu utume wake ndio uliofanya kitabu hicho cha kukunjwa kiwe kitamu kwake. Ezekieli alithamini kumtumikia Yehova akiwa nabii.

4:1-17—Je, kweli Ezekieli aliigiza kuzingirwa kwa Yerusalemu ambako kulikuwa kumekariba? Kwa kuwa Ezekieli aliomba abadilishiwe kile ambacho angetumia kuoka keki naye Yehova akakubali ombi lake, inaonekana kwamba kwa kweli nabii huyo aliigiza kuzingirwa kwa Yerusalemu. Alilala kwa upande wake wa kushoto kwa ajili ya kipindi cha miaka 390 cha makosa ya ufalme wa makabila kumi, yaani, kuanzia mwaka wa 997 K.W.K. mpaka uharibifu wa Yerusalemu mnamo 607 K.W.K. Alilala kwa upande wake wa kuume kwa ajili ya kipindi cha miaka 40 cha dhambi za Yuda, kilichoanza Yeremia alipowekwa rasmi kuwa nabii mnamo 647 K.W.K. mpaka 607 K.W.K. Katika kipindi chote hicho cha siku 430, Ezekieli alikuwa na kiasi kidogo sana cha chakula na maji, akionyesha kinabii kwamba kungekuwa na njaa kali wakati wa kuzingirwa kwa Yerusalemu.

5:1-3—Tendo la Ezekieli la kuchukua hesabu ndogo katika nywele alizotawanya kwenye upepo na kuzifunga katika pindo za nguo yake lilimaanisha nini? Tendo hilo lilionyesha kwamba mabaki fulani wangerudi Yuda na kuanzisha upya ibada ya kweli baada ya miaka 70 ya ukiwa.—Ezekieli 11:17-20.

17:1-24—Wale tai wawili wakubwa ni nani, kilele cha machipukizi ya mwerezi kinang’olewa jinsi gani, na ni nani kile “kitawi kichanga” kinachopandikizwa na Yehova? Wale tai wawili wanawakilisha watawala wa Babiloni na Misri. Tai wa kwanza anakuja kwenye kilele cha mwerezi, yaani, juu ya mtawala wa serikali ya ukoo wa kifalme wa Daudi. Tai huyo anang’oa kilele cha machipukizi kwa kumwondoa Mfalme Yehoyakini wa Yuda na kumweka Sedekia. Ingawa alikula kiapo cha ushikamanifu, Sedekia anatafuta msaada wa yule tai mwingine, mtawala wa Misri, lakini hafanikiwi. Atachukuliwa mateka na kufia Babiloni. Yehova pia anang’oa “kitawi kichanga,” yaani, Mfalme wa Kimasihi. Mfalme huyo anapandikizwa juu ya “mlima mrefu na ulio juu sana,” yaani, juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu, ambapo atakuwa “mwerezi mkubwa,” chanzo cha baraka hakika kwa ajili ya dunia.—Ufunuo 14:1.

Mambo Tunayojifunza:

2:6-8; 3:8, 9, 18-21. Hatupaswi kuogopeshwa na waovu au kuacha kutangaza ujumbe wa Mungu, ambao unatia ndani onyo kwa waovu. Tunapokabili ubaridi au upinzani, tunahitaji kuwa wagumu kama almasi. Hata hivyo, tunapaswa kujihadhari tusiwe wenye mioyo migumu, sugu, au wakatili. Yesu aliwasikitikia watu aliowahubiria, nasi pia tunapaswa kuwahubiria watu kwa sababu tunawasikitikia.—Mathayo 9:36.

3:15. Baada ya kupokea utume wake, Ezekieli aliishi Tel-abibu, ‘kwa siku saba, akiwa amepigwa na bumbuazi,’ akitafakari ujumbe aliopaswa kutangaza. Je, hatupaswi kutenga wakati wa kujifunza kwa bidii na kutafakari ili tuelewe kweli nzito za kiroho?

4:1–5:4. Ilimbidi Ezekieli awe mnyenyekevu na mjasiri ili aweze kuigiza jumbe hizo mbili za kinabii. Sisi pia tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wajasiri katika kutimiza migawo yoyote tuliyopewa na Mungu.

7:4, 9; 8:18; 9:5, 10. Hatuhitaji kuacha macho yetu yawasikitikie au kuwahurumia watu ambao wamehukumiwa vikali na Mungu.

7:19. Yehova anapotekeleza hukumu yake juu ya mfumo huu wa mambo, pesa hazitakuwa na thamani yoyote ile.

8:5-18. Uasi-imani ni jambo hatari sana kiroho. “Mwasi-imani humletea mwenzake uharibifu kwa kinywa chake.” (Methali 11:9) Tunatenda kwa hekima tunapokataa hata wazo la kuwasikiliza waasi-imani.

9:3-6. Ili tuokoke “dhiki kuu” ni lazima tuwe na alama, yaani, uthibitisho wa kwamba sisi ni watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu na kubatizwa, na kwamba tuna utu wa Kikristo. (Mathayo 24:21) Wakristo watiwa-mafuta, ambao wanawakilishwa na mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi, wanaongoza katika kazi ya kuwatia watu alama, yaani, kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Ikiwa tunataka kudumisha alama yetu, ni lazima tuwasaidie kwa bidii watiwa-mafuta katika kazi hiyo.

12:26-28. Ezekieli alipaswa kuwaambia hivi hata wale waliodhihaki ujumbe wake: ‘Hakutakuwa na kucheleweshwa tena kwa yoyote ya maneno ya Yehova.’ Tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wengine kuweka uhakika wao katika Yehova kabla hajaleta mwisho wa mfumo huu wa mambo.

14:12-23. Kupata wokovu ni daraka letu wenyewe. Hakuna mtu mwingine anayeweza kututimizia daraka hilo.—Waroma 14:12.

18:1-29. Tutatozwa hesabu kwa matendo yetu wenyewe.

“NITALIHARIBU, NITALIHARIBU, NITALIHARIBU”

(Ezekieli 20:1–24:27)

Katika mwaka wa saba wa uhamisho, yaani, 611 K.W.K., wazee wa Israeli wanakuja kwa Ezekieli ili “kuuliza juu ya Yehova.” Wanasikiliza masimulizi marefu ya historia ya uasi wa Israeli na onyo la kwamba ‘Yehova atauchomoa upanga wake’ na kuwakatilia mbali. (Ezekieli 20:1; 21:3) Akizungumza na mkuu wa Israeli (Sedekia), Yehova anasema: “Kiondoe kilemba, na kulivua taji. Hili halitakuwa tena kama lilivyo. Kiinue kilicho chini, na ukishushe kilicho juu. Nitaliharibu, nitaliharibu, nitaliharibu. Nalo hili pia, hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, [Yesu Kristo] nami nitampa yeye.”—Ezekieli 21:26, 27.

Yerusalemu linahukumiwa. Hatia ya Ohola (Israeli) na ya Oholiba (Yuda) inafunuliwa. Tayari Ohola ametiwa “mkononi mwa wale wanaompenda kwa tamaa, mkononi mwa wana wa Ashuru.” (Ezekieli 23:9) Kufanywa ukiwa kwa Oholiba kumekaribia sana. Katika mwaka wa 609 K.W.K., kuzingirwa kwa Yerusalemu kwa miezi 18 kunaanza. Mwishowe jiji hilo litakapoanguka, Wayahudi watapigwa na bumbuazi wasiweze kuonyesha huzuni yao. Ezekieli hapaswi kuwapa wahamishwa hao ujumbe wa Mungu mpaka “yeye aliyeponyoka” atakapompa habari kuhusu kuharibiwa kwa jiji hilo.—Ezekieli 24:26, 27.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

21:3—Ni nini ule “upanga” ambao Yehova anauchomoa kutoka katika ala yake? “Upanga” ambao Yehova anatumia kutekeleza hukumu yake juu ya Yerusalemu na Yuda ni Mfalme Nebukadneza wa Babiloni pamoja na jeshi lake. Pia, unaweza kutia ndani sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu lenye viumbe wa roho wenye nguvu.

24:6-14—Kutu ya chungu cha kupikia inafananisha nini? Yerusalemu lililozingirwa linafananishwa na chungu cha kupikia chenye mdomo mpana. Kutu yake inafananisha uchafu wa maadili wa jiji hilo, yaani, hatia yake ya uchafu, mwenendo mpotovu, na umwagaji wa damu. Lina uchafu mwingi sana hivi kwamba hata kusimamisha chungu hicho kisicho na kitu juu ya makaa na kukiacha kiwe na moto sana, hakuondoi kutu yake.

Mambo Tunayojifunza:

20:1, 49. Itikio la wanaume wazee Waisraeli linaonyesha kwamba walikuwa na mashaka kuhusu maneno ya Ezekieli. Tusisitawishe hata kidogo mtazamo wa kuwa na mashaka kuhusu maonyo ya Mungu.

21:18-22. Hata ingawa Nebukadneza alitumia uaguzi, ni Yehova aliyehakikisha kwamba mtawala mpagani angeshambulia Yerusalemu. Hilo linaonyesha kwamba hata roho waovu hawawezi kuzuia watekelezaji wa hukumu ya Yehova wasitimize kusudi lake.

22:6-16. Yehova anachukia uchongezi, mwenendo mpotovu, matumizi mabaya ya mamlaka, na kula rushwa. Tunapaswa kuazimia kabisa kuepuka maovu kama hayo.

23:5-49. Kufanya mapatano ya kisiasa kuliongoza Israeli na Yuda kwenye ibada ya uwongo ya washiriki wao. Acheni tujilinde tusiwe na ushirika wowote wa karibu pamoja na walimwengu, ushirika ambao unaweza kuharibu imani yetu.—Yakobo 4:4.

Ujumbe Ulio Hai na Ulio na Nguvu

Tunajifunza mambo yenye kupendeza kama nini katika sura 24 za kwanza za kitabu cha Biblia cha Ezekieli! Kanuni zilizo katika sura hizo zinaonyesha mambo yanayomfanya mtu apoteze kibali cha Mungu, jinsi tunavyoweza kupata rehema zake, na kwa nini tunapaswa kuwaonya waovu. Unabii kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu unaonyesha wazi kwamba Yehova ni Mungu ambaye ‘huwafanya watu wake wasikie mambo mapya kabla hayajaanza kutokea.’—Isaya 42:9.

Unabii kama huu ulioandikwa katika Ezekieli 17:22-24 na 21:26, 27 ulihusu kusimamishwa kwa Ufalme wa Kimasihi mbinguni. Hivi karibuni, utawala huo utatimiza mapenzi ya Mungu hapa duniani. (Mathayo 6:9, 10) Tukiwa na imani na usadikisho wenye nguvu, tunaweza kutarajia baraka za Ufalme. Ndiyo, “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Gari la kimbingu linafananisha nini?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kunatusaidia kudumisha “alama” yetu