Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Msimlipe Yeyote Uovu Kwa Uovu”

“Msimlipe Yeyote Uovu Kwa Uovu”

“Msimlipe Yeyote Uovu Kwa Uovu”

“Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote.”—WAROMA 12:17.

1. Watu wengi wana tabia gani?

MTOTO anaposukumwa na mtoto mwenzake, kwa kawaida jambo la kwanza analofanya ni kumsukuma pia. Inasikitisha kwamba si watoto tu walio na tabia hiyo ya kulipiza kisasi. Watu wengi wazima wanatenda vivyo hivyo. Mtu fulani anapowaudhi, wako tayari kulipiza kisasi. Ni kweli kwamba watu wengi wazima hawawasukumi wenzao kihalisi, lakini wengi wanalipiza kisasi kwa njia za werevu. Labda wanaeneza porojo yenye kuumiza kuhusu yule aliyewakosea au wanatafuta njia za kumzuia asifanikiwe maishani. Hata watumie njia gani, nia yao ni moja, kulipiza kisasi.

2. (a) Kwa nini Wakristo wa kweli wanapambana na tamaa ya kulipiza kisasi? (b) Tutazungumzia maswali gani na sura gani ya Biblia?

2 Ijapokuwa tamaa ya kulipiza kisasi ina nguvu sana, Wakristo wa kweli wanapambana ili isiwashinde. Wanajitahidi kufuata himizo hili la mtume Paulo: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.” (Waroma 12:17) Ni nini kitatuchochea tuishi kupatana na kiwango hicho cha juu? Ni nani hasa ambaye hatupaswi kumlipa uovu? Tutapata faida gani tusipolipiza kisasi? Ili kujibu maswali hayo, acheni tuchunguze kwa undani maneno ya Paulo ili tuone jinsi sura ya 12 ya Waroma inavyoonyesha kwamba kutolipiza kisasi ni jambo linalofaa, la kiasi, na la upendo. Tutazungumzia mambo hayo matatu, jambo moja baada ya lingine.

“Kwa Sababu Hiyo Nawasihi Ninyi”

3, 4. (a) Paulo anazungumzia nini kuanzia Waroma sura ya 12, na kwa nini anatumia maneno “kwa sababu hiyo”? (b) Huruma za Mungu zilipaswa kuwa na matokeo gani kwa Wakristo huko Roma?

3 Kuanzia sura ya 12, Paulo anazungumzia mambo manne yanayohusiana ambayo yanagusa maisha ya Mkristo. Anazungumzia uhusiano wetu pamoja na Yehova, pamoja na waamini wenzetu, pamoja na wasio waamini, na pamoja na mamlaka za kiserikali. Paulo anaonyesha kwamba kuna sababu muhimu ya kuepuka mielekeo isiyofaa, kutia ndani tamaa ya kulipiza kisasi. Anasema hivi: “Kwa sababu hiyo nawasihi ninyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu.” (Waroma 12:1) Angalia maneno “kwa sababu hiyo,” ambayo yanamaanisha “kupatana na mambo yaliyotangulia.” Ni kana kwamba Paulo anasema, ‘Kwa sababu ya mambo ambayo nimekwisha kuwaeleza, ninawasihi mfanye jambo ambalo sasa nitawaambia.’ Paulo alikuwa amewaeleza nini Wakristo hao wa Roma?

4 Katika sura 11 za kwanza za barua yake, Paulo alizungumzia pendeleo la pekee ambalo Wayahudi na Watu wa Mataifa wanalo la kutawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa Mungu, tumaini ambalo Waisraeli wa asili walikataa. (Waroma 11:13-36) Pendeleo hilo lenye thamani liliwezekana tu “kwa huruma za Mungu.” Wakristo wanapaswa kuitikia jinsi gani fadhili hizo kubwa zisizostahiliwa kutoka kwa Mungu? Wanapaswa kuchochewa na shukrani nyingi sana za kutoka moyoni kufanya jambo ambalo Paulo anasema: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.” (Waroma 12:1) Lakini, kwa kweli Wakristo hao wangeweza kujitoa wenyewe jinsi gani wakiwa “dhabihu” kwa Mungu?

5. (a) Mtu anaweza kujitoa mwenyewe namna gani kuwa “dhabihu” kwa Mungu? (b) Ni kanuni gani inayopaswa kuongoza mwenendo wa Mkristo?

5 Paulo anaendelea kueleza hivi: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Badala ya kuruhusu roho ya ulimwengu ifinyange fikira zao, walihitaji kufanya upya akili zao ili zipatane na njia ya Kristo ya kufikiri. (1 Wakorintho 2:16; Wafilipi 2:5) Kanuni hiyo inapaswa kuongoza mwenendo wa Wakristo wote wa kweli kila siku, kutia ndani sisi leo.

6. Kulingana na hoja za Paulo katika Waroma 12:1, 2, ni nini kinachotuchochea tusilipize kisasi?

6 Hoja anazotoa Paulo katika Waroma 12:1, 2 zinatusaidia jinsi gani? Kama Wakristo hao wa Roma waliotiwa mafuta, tunashukuru sana kwa sababu Mungu anaendelea kutuonyesha huruma nyingi naye anafanya hivyo kila siku ya maisha yetu. Kwa sababu hiyo, moyo uliojaa shukrani unatuchochea kumtumikia Mungu kwa nguvu, mali, na uwezo wetu wote. Tamaa hiyo ya kutoka moyoni inatuchochea pia kufanya yote tunayoweza ili kufikiri kama Kristo wala si kama ulimwengu. Kuwa na akili ya Kristo kunaongoza jinsi tunavyowatendea wengine, yaani, waamini wenzetu na watu ambao si waamini. (Wagalatia 5:25) Kwa mfano: Ikiwa tunafikiri kama Kristo, tunachochewa kupinga mwelekeo wa kulipiza kisasi.—1 Petro 2:21-23.

“Upendo Wenu na Uwe Bila Unafiki”

7. Ni upendo wa aina gani unaozungumziwa katika Waroma sura ya 12?

7 Hatuepuki kulipa uovu kwa uovu kwa sababu tu hilo si jambo zuri bali pia kwa sababu kutofanya hivyo ni kuonyesha upendo. Ona sasa jinsi mtume Paulo anavyozungumzia nia ya upendo. Katika kitabu cha Waroma, Paulo anatumia neno “upendo” (a·gaʹpe katika Kigiriki) mara nyingi anapozungumzia upendo wa Mungu na wa Kristo. (Waroma 5:5, 8; 8:35, 39) Hata hivyo, katika sura ya 12, Paulo anatumia neno a·gaʹpe kwa njia tofauti anapozungumza kuhusu upendo kuelekea wanadamu wengine. Baada ya kusema kwamba zawadi za kiroho zinatofautiana na kwamba waamini fulani wana zawadi hizo, Paulo anataja sifa ambayo inapaswa kusitawishwa na Wakristo wote. Anasema hivi: “Upendo wenu na uwe bila unafiki.” (Waroma 12:4-9) Kuwapenda wengine ni sifa kuu inayowatambulisha Wakristo wa kweli. (Marko 12:28-31) Paulo anatutia moyo tuhakikishe kwamba upendo wetu tukiwa Wakristo ni wa kweli.

8. Tunaweza kuonyesha jinsi gani upendo bila unafiki?

8 Kwa kuongezea, Paulo anaeleza jinsi upendo bila unafiki unavyoonyeshwa. Anasema: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.” (Waroma 12:9) Maneno “chukieni” na “shikamaneni” ni maneno yenye nguvu. Neno ‘chukia’ linaweza kutafsiriwa kuwa kukirihi, yaani, “kuchukia kabisa.” Ni lazima tuchukie si matokeo tu ya uovu bali pia uovu wenyewe. (Zaburi 97:10) Neno “shikamaneni” limetafsiriwa kutokana na kitenzi cha Kigiriki kinachomaanisha kihalisi “kushikanisha kwa gundi (colle).” Mkristo ambaye ana upendo wa kweli anashikamana kwa nguvu sana au kwa uthabiti na sifa ya wema hivi kwamba haiwezi kutenganishwa na utu wake.

9. Paulo anatoa himizo gani tena na tena?

9 Paulo anataja tena na tena njia moja hasa ya kuonyesha upendo. Anasema hivi: “Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa; muwe mkibariki wala msiwe mkilaani.” “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.” “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe.” “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:14, 17-19, 21) Bila shaka, maneno ya Paulo yanaonyesha wazi jinsi tunavyopaswa kuwatendea wasio waamini, hata wale wanaotupinga.

“Endeleeni Kuwabariki Wale Wanaowatesa”

10. Tunaweza jinsi gani kuwabariki wale wanaotutesa?

10 Tunaweza kutii namna gani himizo hili la Paulo: “Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa”? (Waroma 12:14) Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mathayo 5:44; Luka 6:27, 28) Hivyo, njia moja ya kuwabariki wale wanaotutesa ni kusali kwa ajili yao, na kumsihi Mungu kwamba ikiwa kuna wowote wanaotupinga kwa sababu ya kutojua, Yehova awafungue macho ili waone kweli. (2 Wakorintho 4:4) Ni kweli kwamba huenda likaonekana kuwa jambo la kushangaza kumwomba Mungu ambariki mtu anayetutesa. Hata hivyo, kadiri tunavyopatanisha njia yetu ya kufikiri na njia ya Kristo, ndivyo tutakavyoweza kuwapenda adui zetu. (Luka 23:34) Kuonyesha upendo kama huo kunaweza kuwa na matokeo gani?

11. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Stefano? (b) Watesaji fulani wanaweza kufanya mabadiliko gani kama maisha ya Paulo yanavyoonyesha?

11 Stefano alisali kwa ajili ya wale waliomtesa, na sala yake haikuwa ya bure. Muda mfupi baada ya Pentekoste ya 33 W.K., Stefano alikamatwa na wapinzani wa kutaniko la Kikristo, wakamburuta nje ya Yerusalemu na kumpiga kwa mawe. Kabla ya kufa, alipaaza sauti hivi: “Yehova, usiwahesabie dhambi hii.” (Matendo 7:58–8:1) Sauli alikuwa mmoja wa wanaume ambao Stefano alisali kwa ajili yao siku hiyo. Sauli alishuhudia na kukubali Stefano auawe. Baadaye, Yesu aliyefufuliwa alimtokea Sauli. Mtu huyo ambaye alikuwa akiwatesa Wakristo akawa mfuasi wa Kristo na kisha akawa mtume Paulo, ambaye aliandika ile barua kwa Waroma. (Matendo 26:12-18) Kupatana na sala ya Stefano, inaonekana kwamba Yehova alimsamehe Paulo dhambi ya kuwatesa Wakristo. (1 Timotheo 1:12-16) Haishangazi kwamba Paulo aliwatia moyo hivi Wakristo: “Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa”! Alijua kutokana na maisha yake kwamba watesaji fulani wanaweza mwishowe kuwa watumishi wa Mungu. Leo, watesaji fulani wamekuwa waamini kwa sababu watumishi wa Yehova wanafuatia amani.

“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

12. Maneno ya himizo katika Waroma 12:9, 17 yanahusiana namna gani?

12 Kisha, Paulo anatoa himizo hili kuhusu jinsi ya kuwatendea waamini na wasio waamini: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.” Maneno hayo yanapatana kabisa na yale aliyotangulia kusema, yaani, “Chukieni maovu.” Kwa kweli, mtu anaweza kusema namna gani kwamba anachukia kabisa yaliyo maovu ikiwa anawalipa wengine uovu? Kufanya hivyo ni kinyume kabisa cha kuwa na upendo “bila unafiki.” Kisha Paulo anasema hivi: “Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote.” (Waroma 12:9, 17) Tunafanya hivyo jinsi gani?

13. Tunajiendesha jinsi gani “machoni pa watu wote”?

13 Mwanzoni, katika barua yake kwa Wakorintho, Paulo aliandika kuhusu mateso ambayo mitume walipata. Alisema hivi: “Tumekuwa tamasha kwa ulimwengu, na kwa malaika, na kwa wanadamu. . . . Tunapotukanwa, tunabariki; tunapoteswa, tunavumilia; tunapoharibiwa sifa, tunasihi.” (1 Wakorintho 4:9-13) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli leo wanatazamwa na watu wa ulimwengu huu. Wale walio karibu nasi wanapoona mambo mazuri tunayofanya hata tunapotendewa kwa njia isiyo ya haki, huenda wakawa na mwelekeo wa kukubali ujumbe wetu wa Kikristo.—1 Petro 2:12.

14. Tunapaswa kujitahidi kadiri gani ili kufanya amani?

14 Hata hivyo, tunapaswa kujitahidi kadiri gani ili kufanya amani? Tunapaswa kujitahidi kadiri tunavyoweza. Paulo anawaambia hivi ndugu zake Wakristo: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:18) Maneno “ikiwezekana” na “kadiri inavyowategemea” yanaonyesha kwamba huenda sikuzote haitawezekana kufanya amani na wengine. Kwa mfano, hatutakosa kutii amri ya Mungu ili tu kufanya amani na mwanadamu. (Mathayo 10:34-36; Waebrania 12:14) Hata hivyo, tunajitahidi kadiri tunavyoweza ili kufanya amani “na watu wote” bila kulegeza msimamo wetu kuelekea kanuni za uadilifu.

“Msijilipizie Kisasi Wenyewe”

15. Andiko la Waroma 12:19 linaonyesha sababu gani ya kutolipiza kisasi?

15 Paulo anatoa sababu nyingine nzuri ya kutolipiza kisasi; mwenendo huo unaonyesha kwamba tuna sifa ya kiasi. Anasema hivi: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Waroma 12:19) Mkristo ambaye anajaribu kulipiza kisasi ana kimbelembele. Anajichukulia daraka ambalo ni la Mungu. (Mathayo 7:1) Kwa kuongezea, anapojichukulia mambo mikononi mwake, anaonyesha kwamba hana imani katika uhakikisho huu wa Yehova: “Mimi nitalipa.” Kinyume cha hilo, Wakristo wa kweli wanasadiki kwamba Yehova “atasababisha haki ifanywe kwa ajili ya watu wake waliochaguliwa.” (Luka 18:7, 8; 2 Wathesalonike 1:6-8) Wanaonyesha sifa ya kiasi kwa kumwachia Mungu daraka la kulipiza uovu.—Yeremia 30:23, 24; Waroma 1:18.

16, 17. (a) Ni nini maana ya ‘kukusanya makaa yenye moto’ juu ya kichwa cha mtu? (b) Je, wewe binafsi umeona fadhili ikiondoa chuki katika moyo wa mtu ambaye si mwamini? Ikiwa umeona, toa mfano.

16 Inaelekea kwamba kumlipiza adui kisasi kunaweza kufanya moyo wake uwe mgumu, lakini kumtendea kwa fadhili kunaweza kuondoa chuki yake. Kwa nini? Angalia maneno ambayo Paulo anawaambia Wakristo huko Roma. Anasema hivi: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe; kwa maana kwa kufanya hivyo utakusanya makaa yenye moto juu ya kichwa chake.” (Waroma 12:20; Methali 25:21, 22) Hilo linamaanisha nini?

17 ‘Kukusanya makaa yenye moto juu ya kichwa chake’ ni usemi wa mfano ambao unatokana na njia iliyotumiwa kuyeyusha vyuma katika nyakati za Biblia. Mawe yenye chuma yalitiwa katika tanuru ya moto, na makaa yakawekwa juu na pia chini ya mawe hayo. Makaa yenye moto yaliyokusanywa juu ya vyuma yaliongeza joto ambalo liliyeyusha vyuma vigumu na kuvitenganisha na uchafu uliokuwa ndani ya mawe hayo. Vivyo hivyo, tunapomtendea mpinzani kwa fadhili, tunaweza “kuyeyusha” ugumu wake na kumfanya aonyeshe sifa zake nzuri. (2 Wafalme 6:14-23) Kwa kweli, washiriki wengi wa kutaniko la Kikristo walivutiwa na ibada ya kweli kwa sababu ya kutendewa kwa fadhili na watumishi wa Yehova.

Kwa Nini Hatulipizi Kisasi

18. Kwa nini kutolipiza kisasi ni jambo linalofaa, la upendo, na la kiasi?

18 Katika mazungumzo haya mafupi ya Waroma sura ya 12, tumeona sababu fulani muhimu zinazofanya ‘tusimlipe yeyote uovu kwa uovu.’ Kwanza, kutolipiza kisasi ni jambo linalofaa. Kwa sababu ya huruma ambazo Mungu ametuonyesha, ni jambo zuri na linalofaa kujitoa wenyewe kwa Yehova na kutii amri zake kwa kupenda, kutia ndani amri ya kuwapenda adui zetu. Pili, kutolipa uovu kwa uovu ni kuonyesha upendo. Tunapofanya amani na kutolipiza kisasi, tunatumaini kwa upendo kwamba tutawasaidia hata wapinzani fulani wakali wawe waabudu wa Yehova. Tatu, tunaonyesha sifa ya kiasi kwa kutolipa uovu kwa uovu. Kujilipizia kisasi ni kuwa na kimbelembele, kwa kuwa Yehova anasema: “Kisasi ni changu.” Neno la Mungu linatuonya hivi pia: “Je, kimbelembele kimekuja? Basi aibu itakuja; lakini wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2) Tunaonyesha sifa ya kiasi tunapomwachia Mungu daraka la kulipiza uovu.

19. Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

19 Paulo anatoa muhtasari wa mazungumzo yake kuhusu jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. Anawahimiza hivi Wakristo: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:21) Tunapambana na majeshi gani ya uovu leo? Tunaweza kuyashinda jinsi gani? Majibu ya maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo yatazungumziwa katika habari inayofuata.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni himizo gani linalorudiwa tena na tena katika Waroma sura ya 12?

• Ni nini kitakachotuchochea tusilipize kisasi?

• Ni faida gani ambazo sisi na watu wengine tutapata ‘tusipolipa uovu kwa uovu’?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

Andiko la Waroma sura ya 12 linaeleza uhusiano wa Mkristo pamoja na

• Yehova

• waamini wenzake

• wasio waamini

[Picha katika ukurasa wa 23]

Barua ya Paulo kwa Waroma inawatolea Wakristo mashauri yanayofaa maishani

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mwanafunzi Stefano?