Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Suluhisho la Chuki ya Kijamii?

Ni Nini Suluhisho la Chuki ya Kijamii?

Ni Nini Suluhisho la Chuki ya Kijamii?

HUKO Hispania refa fulani anasimamisha mchezo wa kandanda. Kwa nini? Kwa sababu mashabiki wengi wanamtusi mchezaji mmoja anayetoka Kamerun hivi kwamba mchezaji huyo anatishia kuondoka uwanjani. Huko Urusi limekuwa jambo la kawaida kuwashambulia kijeuri watu kutoka Afrika, Asia, na Amerika Kusini; katika mwaka wa 2004, mashambulizi ya kibaguzi yaliongezeka kwa asilimia 55 na kufikia visa 394 katika 2005. Huko Uingereza, sehemu moja kwa tatu ya Waasia na watu weusi ambao walihojiwa katika uchunguzi fulani walihisi kwamba walifutwa kazi kwa sababu ya ubaguzi wa rangi. Mifano hiyo inaonyesha jinsi hali zilivyo ulimwenguni pote.

Chuki ya kijamii inaonyeshwa kwa viwango tofauti-tofauti. Inaweza kuonyeshwa kwa matusi au maneno yenye kuumiza hisia au kwa jitihada za kitaifa za kuangamiza jamii nzima-nzima. * Ni nini chanzo cha chuki ya kijamii? Tunaweza kuepuka jinsi gani kuonyesha chuki hiyo? Je, ni jambo linalopatana na akili kutumaini kwamba siku moja familia zote za kibinadamu zitaishi pamoja kwa amani? Biblia inatoa habari yenye kupendeza kuhusu jambo hilo.

Ukandamizaji na Chuki

“Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea,” inasema Biblia. (Mwanzo 8:21) Hivyo, watu fulani wanafurahia kuwakandamiza wengine. Biblia inasema hivi pia: “Tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji; nao wakandamizaji walikuwa na nguvu.”—Mhubiri 4:1.

Biblia inaonyesha pia kwamba chuki ya kijamii ilianza zamani sana. Kwa mfano, zaidi ya miaka 3,700 iliyopita, Farao wa Misri alimkaribisha Yakobo Mwebrania na familia yake kubwa waishi Misri. Hata hivyo, baadaye Farao mwingine aliona kundi hilo kubwa la wahamiaji kuwa tisho. Kwa sababu hiyo, simulizi linasema: “Akawaambia watu wake: ‘Tazama! Watu wa wana wa Israeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa werevu, wasije wakaongezeka.’ . . . Basi wakaweka juu yao wakuu wa kazi ya kulazimishwa kusudi wawakandamize katika kazi yao ya kubeba mizigo.” (Kutoka 1:9-11) Wamisri hata waliagiza watoto wote wa kiume wachanga wa wazao wa Yakobo wauawe.—Kutoka 1:15, 16.

Ni Nini Chanzo cha Tatizo Hilo?

Dini za ulimwengu hazijasaidia sana kupinga chuki ya kijamii. Ingawa ni kweli kwamba watu fulani wamekuwa mashuhuri kwa sababu ya kupinga ukandamizaji, kwa ujumla dini zimewaunga mkono wakandamizaji. Hivyo ndivyo ilivyokuwa huko Marekani, ambako ubaguzi kuelekea watu weusi uliungwa mkono kisheria. Watu waliteketezwa kwa sababu ya ubaguzi nazo sheria za kupiga marufuku ndoa kati ya weusi na weupe zikaendelea kufuatwa hadi 1967. Ilikuwa hivyo pia huko Afrika Kusini wakati wa ubaguzi wa rangi, watu wachache walipokuwa wakidumisha mamlaka yao kwa kutumia sheria ambazo pia zilipiga marufuku ndoa kati ya watu wa rangi tofauti. Katika nchi hizo mbili, baadhi ya watu waliounga mkono ubaguzi huo walikuwa watu wanaoshikilia sana dini.

Hata hivyo, Biblia inafunua chanzo cha chuki ya kijamii. Inaeleza kwa nini jamii fulani zinakandamiza jamii nyinginezo. Inasema hivi: “Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo. Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yohana 4:8, 20) Taarifa hiyo inafunua chanzo hasa cha chuki ya kijamii. Wanadini na watu wasio wanadini, wanaonyesha chuki ya kijamii kwa sababu hawajamjua Mungu na hawampendi.

Ujuzi Juu ya Mungu —Msingi wa Amani ya Kijamii

Kumjua Mungu na kumpenda kunaleta amani kati ya jamii mbalimbali jinsi gani? Neno la Mungu linafunua ujuzi gani ambao unawazuia watu wasiwadhuru wale wanaoonekana kuwa tofauti nao? Biblia inafunua kwamba Yehova ni Baba ya watu wote. Inasema: “Kwa kweli kwetu sisi kuna Mungu mmoja aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake.” (1 Wakorintho 8:6) Inasema hivi pia: “Alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Matendo 17:26) Hivyo, kwa kweli, watu wote ni ndugu.

Jamii zote zinaweza kushukuru kwa kuwa zimepata uhai kutoka kwa Mungu, lakini zote zina jambo lenye kuhuzunisha kuhusu chanzo cha ukoo wao. Paulo, mwandikaji wa Biblia alisema hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu.” Hivyo, “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23; 5:12) Yehova ni Mungu anayependa vitu vya aina mbalimbali—hakuna viumbe viwili vinavyofanana kabisa. Hata hivyo, hajaipa jamii yoyote ile msingi wa kujiona kuwa bora kuliko jamii nyingine. Maoni yaliyoenea sana ya kwamba jamii moja ni bora kuliko jamii nyinginezo yanapingana na mafundisho ya Maandiko. Bila shaka, ujuzi kutoka kwa Mungu unachangia amani ya kijamii.

Mungu Anajali Mataifa Yote

Watu fulani wanajiuliza ikiwa Mungu alichangia chuki ya kijamii kwa kupendelea Waisraeli na kuwafundisha wajitenge na mataifa mengine. (Kutoka 34:12) Wakati mmoja, Mungu alichagua taifa la Israeli kuwa mali yake ya pekee kwa sababu ya imani ya pekee ya Abrahamu, babu ya Waisraeli. Mungu mwenyewe aliwaongoza Waisraeli wa kale, akawachagulia watawala, na kuwapa mfumo wa sheria. Wakati ambapo Waisraeli walikubali mpango huo, watu wengine wangeweza kuona jinsi matokeo ya utawala ulioongozwa na Mungu yalivyotofautiana na ya utawala wa wanadamu ambao waliongoza mataifa mengine. Yehova pia aliwafundisha Waisraeli walioishi wakati huo kuhusu uhitaji wa kutoa dhabihu ili kuwawezesha wanadamu kuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Hivyo, shughuli za Yehova na Waisraeli zililetea mataifa yote faida. Hilo lilipatana na yale ambayo Mungu alimwambia Abrahamu: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.

Kwa kuongezea, Wayahudi walipata pendeleo la kupokea maneno matakatifu ya Mungu na kuwa taifa ambamo Masihi alizaliwa. Lakini ilikuwa hivyo ili mataifa yote yafaidike. Maandiko ya Kiebrania ambayo Wayahudi walipewa yanaeleza kwa njia yenye kuchangamsha kuhusu wakati ambapo jamii zote zitapokea baraka nyingi: “Mataifa mengi hakika yatakwenda na kusema: ‘Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova na kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake’ . . . Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena. Nao wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.”—Mika 4:2-4.

Ingawa Yesu Kristo mwenyewe aliwahubiria Wayahudi, alisema hivi pia: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hakuna taifa ambalo lingekosa kusikia habari njema. Hivyo, Yehova aliweka mfano bora kwa kushughulika na jamii zote bila ubaguzi. “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Sheria ambazo Mungu alilipa taifa la kale la Israeli zinafunua pia kwamba anayajali mataifa yote. Ona kwamba Sheria haikutaka tu Waisraeli wawavumilie watu wasio Waisraeli ambao waliishi katika nchi hiyo, bali pia ilitaka wafanye mengi zaidi. Ilisema hivi: “Yule mkaaji mgeni anayekaa akiwa mgeni pamoja nanyi atakuwa kwenu kama mwenyeji wenu; nawe utampenda kama wewe mwenyewe, kwa maana mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.” (Mambo ya Walawi 19:34) Nyingi kati ya sheria za Mungu ziliwafundisha Waisraeli wawe wenye fadhili kwa wahamiaji. Hivyo, Boazi, babu wa kale wa Yesu, alipomwona mwanamke maskini akiokota masalio, alitenda kupatana na yale aliyojifunza kutoka kwa Mungu alipowaagiza wavunaji wake waache masalio mengi ya nafaka kwa ajili ya mwanamke huyo.—Ruthu 2:1, 10, 16.

Yesu Anafundisha Fadhili

Yesu alifunua ujuzi juu ya Mungu kuliko mtu mwingine yeyote. Aliwaonyesha wafuasi wake jinsi ya kuwatendea kwa fadhili watu wa jamii tofauti. Pindi moja alianzisha mazungumzo na mwanamke Msamaria. Mwanamke huyo alishangaa kwa kuwa Wayahudi wengi waliwadharau Wasamaria. Katika mazungumzo hayo, Yesu alimsaidia kwa fadhili kuelewa jinsi ambavyo angeweza kupata uzima wa milele.—Yohana 4:7-14.

Yesu pia alitufundisha jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu wa jamii nyingine alipotoa mfano wa Msamaria mwema. Msamaria huyo alimpata Myahudi aliyeumizwa vibaya na wanyang’anyi. Msamaria huyo angeweza tu kusema hivi: ‘Kwa nini nimsaidie Myahudi? Wayahudi wanawadharau watu wetu.’ Lakini Yesu alionyesha kwamba Msamaria huyo alikuwa na maoni tofauti kuelekea watu wa jamii nyingine. Hata ingawa wasafiri fulani walikuwa wamepitia hapo na kumwona mtu huyo aliyejeruhiwa, Msamaria huyo ‘alimsikitikia’ na kumsaidia sana. Yesu alimalizia mfano huo kwa kusema kwamba yeyote anayetaka kibali cha Mungu anapaswa kufanya vivyo hivyo.—Luka 10:30-37.

Mtume Paulo alifundisha kwamba wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanapaswa kubadili utu wao na kuiga jinsi Mungu anavyowatendea watu. Paulo aliandika: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba, ambapo hakuna Mgiriki wala Myahudi, tohara wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe . . . Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:9-14.

Je, Ujuzi Juu ya Mungu Unawabadili Watu?

Je, kwa kweli kumjua Yehova Mungu kunabadili jinsi watu wanavyowatendea watu wa jamii nyinginezo? Fikiria kisa cha mwanamke fulani kutoka Asia aliyehamia Kanada. Alivunjika moyo alipobaguliwa huko Kanada. Alikutana na Mashahidi wa Yehova na wakaanza kujifunza Biblia pamoja naye. Baadaye aliwaandikia barua ya shukrani akisema hivi: ‘Ninyi ni watu weupe wazuri sana na wenye fadhili. Nilipogundua kwamba mko tofauti na watu wengine weupe, nilijiuliza ni kwa nini. Niliwaza na kuwazua kisha nikakata kauli kwamba ninyi ni Mashahidi wa Mungu. Lazima kuwe na jambo fulani katika Biblia. Katika mikutano yenu niliona watu wengi weupe, weusi, wa kahawia, na wa manjano, lakini mioyo yao ilikuwa yenye rangi ileile moja, ilikuwa minyoofu, kwa kuwa walikuwa ndugu na dada. Sasa ninajua ni nani aliyewafanya wawe hivyo. Ni Mungu wenu.’

Neno la Mungu linatabiri wakati ambapo “dunia hakika itajawa na kumjua Yehova.” (Isaya 11:9) Hata sasa, unabii wa Biblia unatimizwa kwa kuwa umati mkubwa wa mamilioni ya watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” wanaunganishwa katika ibada ya kweli. (Ufunuo 7:9) Wanatazamia kuona upendo badala ya chuki katika jamii ya ulimwenguni pote ambayo hivi karibuni itatimiza kusudi la Yehova alilomwambia Abrahamu: “Familia zote za dunia zitabarikiwa.”—Matendo 3:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno “jamii” linarejelea kikundi cha watu wanaotofautishwa na wengine kwa sababu ya rangi, taifa, dini, lugha, au utamaduni.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Sheria ya Mungu iliwafundisha Waisraeli kuwapenda wakaaji wageni

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Msamaria mwema?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mungu hajaipa jamii yoyote ile msingi wa kujiona kuwa bora kuliko jamii nyingine