Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tumegawanywa na Lugha Lakini Tumeunganishwa na Upendo”

“Tumegawanywa na Lugha Lakini Tumeunganishwa na Upendo”

“Tumegawanywa na Lugha Lakini Tumeunganishwa na Upendo”

Ukombozi. Uhuru. Wokovu. Kwa karne nyingi, watu wametamani kukombolewa kutokana na mizigo na mahangaiko. Tunaweza kupambana jinsi gani na matatizo ya maisha? Je, wanadamu watapata kukombolewa? Ikiwa ndivyo, watakombolewa namna gani?

HILO ndilo jambo lililozungumziwa katika mfululizo wa makusanyiko ya wilaya ya siku tatu yaliyopangwa na Mashahidi wa Yehova na kufanywa kuanzia Mei (Mwezi wa 5) 2006. Kichwa cha makusanyiko hayo ya wilaya kilikuwa “Ukombozi Unakaribia!”

Makusanyiko tisa kati ya hayo yalihudhuriwa na maelfu ya wajumbe kutoka nchi mbalimbali. Yalifanywa katika Julai na Agosti (Mwezi wa 7 na wa 8) 2006, huko Prague, mji mkuu wa Jamhuri ya Cheki; Bratislava, mji mkuu wa Slovakia; Chorzow na Poznan, huko Poland; * na katika majiji matano huko Ujerumani—Dortmund, Frankfurt, Hamburg, Leipzig, na Munich. Kwa ujumla, watu zaidi ya 313,000 walihudhuria makusanyiko hayo.

Ni roho gani iliyoenea katika makusanyiko hayo? Vyombo vya habari viliripoti nini kuyahusu? Na wahudhuriaji walihisi namna gani baada ya kuyahudhuria?

Matayarisho

Wageni na Mashahidi wenyeji walitazamia kwa hamu sana pindi hiyo ya kiroho ambayo walijua ingekuwa ya pekee. Kufanya mipango ya kutosha ya mahali pa kulala kwa ajili ya wageni ilikuwa kazi kubwa sana. Kwa mfano, wakati wa kusanyiko la Chorzow, Mashahidi wa Poland waliwakaribisha nyumbani mwao wageni 13,000 hivi kutoka Ulaya Mashariki. Wajumbe wa kusanyiko hilo walitoka Armenia, Belarus, Estonia, Georgia, Kazakhstan, Kyrgyzstan, Latvia, Lithuania, Marekani, Moldova, Tajikistan, Turkmenistan, Ukrainia, Urusi, na Uzbekistan.

Wajumbe wengi walihitaji kufanya mipango ya kusafiri miezi mingi mapema. Tatiana, ambaye ni mweneza-injili wa wakati wote huko Kamchatka, rasi ya Urusi iliyo kaskazini mashariki ya Japani, alianza kuweka pesa za safari hiyo mwaka mmoja mapema. Alihitaji kusafiri kilomita 10,500. Kwanza, alisafiri muda wa saa 5 kwa ndege; kisha akasafiri kwa gari la moshi kwa siku tatu hivi; na mwishowe akasafiri kwa saa 30 kwa basi ili afike Chorzow.

Maelfu walijitolea kufanya kazi kabla ya kusanyiko ili mahali pa kusanyiko na mazingira yake pafae kwa ajili ya ibada. (Kumbukumbu la Torati 23:14) Kwa mfano, huko Leipzig, Mashahidi wenyeji walifanya kazi nzuri sana ya kusafisha uwanja, na wakaahidi kufanya kazi hiyo tena baada ya kusanyiko. Kwa sababu hiyo, maofisa wa uwanja huo walifuta sheria fulani katika mkataba wa kukodi uwanja iliyodai kiasi kikubwa cha pesa ili kulipia gharama za kusafisha uwanja.

Kuwaalika Watu

Makutaniko ulimwenguni pote yaliwajulisha watu wengi kuhusu Makusanyiko hayo ya “Ukombozi Unakaribia!” Wale ambao wangehudhuria makusanyiko hayo ya pekee walishiriki kwa bidii katika kampeni hiyo. Waliendelea kuwaalika watu mpaka usiku uliotangulia kusanyiko. Je, bidii yao ilikuwa na matokeo yoyote mazuri?

Shahidi Mpolandi anayeitwa Bogdan alikutana na mwanamume mzee ambaye alitaka kuhudhuria kusanyiko lakini akasema kwamba kiasi kidogo cha pesa zake za uzeeni hakingemwezesha kusafiri kilomita 120 kwenda Chorzow. Basi lililokuwa limekodiwa na kutaniko la eneo hilo lilikuwa na nafasi ya mtu mmoja zaidi. Bogdan anasema hivi: “Tulimwambia mwanamume huyo kwamba tungesafiri naye bila malipo iwapo angekuja mahali ambapo tungekutania ili kuanza safari saa 11:30 asubuhi.” Mwanamume huyo alikubali mwaliko huo naye akahudhuria kusanyiko. Baadaye, aliwaandikia hivi akina ndugu: “Baada ya kuhudhuria kusanyiko hilo, nimeazimia kuwa mtu bora.”

Huko Prague mwanamume mmoja alikuwa akikaa katika mojawapo ya hoteli ambamo wajumbe wa kusanyiko waliotoka Uingereza walikuwa wakikaa. Jioni moja aliwaambia wajumbe hao kwamba yeye pia alihudhuria kusanyiko siku hiyo. Ni nini kilichomsukuma aende kusanyikoni? Mwanamume huyo alisema kwamba alilazimika kwenda kusanyikoni baada ya kupokea mialiko kutoka kwa wahubiri kumi tofauti-tofauti mitaani! Alivutiwa sana na alikuwa na hamu ya kujifunza mengi zaidi.—1 Timotheo 2:3, 4.

Programu ya Kiroho Yenye Kujenga

Programu ilizungumzia jinsi ya kushughulikia matatizo mbalimbali. Mashauri ya wazi ya Kimaandiko yalionyesha jinsi matatizo hayo yanavyoweza kutatuliwa ama kuvumiliwa.

Watu mmoja-mmoja wanaotaabika kwa sababu ya uzee, afya mbaya, kifo cha wapendwa, au matatizo mengine ya kibinafsi, walitiwa moyo kupitia Biblia ili wawe na mtazamo unaofaa kuhusu maisha. (Zaburi 72:12-14) Wenzi wa ndoa na wazazi walipewa mashauri ya Biblia kuhusu jinsi ya kuwa na furaha katika ndoa na jinsi ya kuwalea watoto wao kwa mafanikio. (Mhubiri 4:12; Waefeso 5:22, 25; Wakolosai 3:21) Vijana Wakristo—ambao wanashawishiwa na vijana wenzao wafanye mambo mabaya shuleni na ambao pia wanapewa mashauri mazuri kutoka katika Neno la Mungu nyumbani na kutanikoni—walipewa mashauri mazuri juu ya kushughulika na vishawishi kutoka kwa marafiki wao na jinsi ya “kuzikimbia tamaa zinazotukia ujanani.”—2 Timotheo 2:22.

Undugu wa Kweli wa Kimataifa

Nyakati zote Mashahidi wa Yehova wanapokea mwongozo mzuri wa Kimaandiko katika makusanyiko yao. (2 Timotheo 3:16) Hata hivyo, kilichofanya makusanyiko hayo yawe tofauti ni watu wa mataifa mbalimbali waliohudhuria. Katika makusanyiko hayo yote ya pekee, programu ileile ya kiroho ilitolewa katika lugha kadhaa. Kila siku, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova walitoa hotuba, nazo ripoti kutoka nchi mbalimbali zilifanya programu ivutie sana. Hotuba na ripoti hizo zilitafsiriwa kwa ajili ya wahudhuriaji wanaozungumza lugha mbalimbali.

Wajumbe walikuwa na hamu ya kukutana na ndugu na dada zao kutoka nchi mbalimbali. “Tofauti za lugha hazikuwatatiza sana,” alisema mjumbe mmoja. “Badala yake, tofauti hizo zilichangia shangwe ya tukio hilo. Wageni walitoka katika malezi mbalimbali ya kijamii, lakini wote waliunganishwa na imani ileile.” Wale waliohudhuria kusanyiko la Munich walisema hivi: “Tumegawanywa na lugha lakini tumeunganishwa na upendo.” Iwe walitoka wapi au walizungumza lugha gani, wahudhuriaji walihisi kwamba walikuwa kati ya marafiki wa kweli, ndugu na dada wa kiroho.—Zekaria 8:23.

Kutoa Shukrani

Mtazamo na uvumilivu wa wajumbe wa makusanyiko huko Poland ulijaribiwa na hali ya hewa. Mvua ilinyesha karibu muda wote na pia kulikuwa na baridi kali. Ndugu mmoja kutoka Marekani alisema hivi: “Ilikuwa hali mbaya ya hewa na baridi kali zaidi niliyowahi kuhisi katika kusanyiko, na nilielewa mambo machache tu yaliyokuwa kwenye programu. Lakini ushirika wa ajabu wa kimataifa, roho nzuri, na ukaribishaji wa pekee sana ulifunika matatizo yote hayo. Kusanyiko hilo haliwezi kusahaulika!”

Jambo ambalo halitasahauliwa na wahudhuriaji Wapolandi ni tangazo la kutolewa kwa Insight on the Scriptures katika Kipolishi, thawabu nzuri ajabu ya kuvumilia baridi na mvua. Wahudhuriaji walishangilia sana kitabu kipya Izingatie Siku ya Yehova Maishani kilipotolewa katika Makusanyiko ya “Ukombozi Unakaribia!”

Wahudhuriaji wengi watakumbuka kusanyiko hilo kwa sababu nyingine. Kristina, dada Mcheki ambaye alijitolea kwenda pamoja na kikundi cha wajumbe kutoka ng’ambo waliosafiri kwa basi, anakumbuka hivi: “Tulipokuwa tukiagana, dada mmoja alinivuta kando, akanikumbatia na kusema: ‘Nilijisikia nimetunzwa vizuri sana! Ulituletea chakula kwenye viti vyetu na hata kutupa maji ya kunywa. Nakushukuru sana kwa upendo wako wa kujidhabihu.’” Alikuwa akizungumzia mpango wa chakula cha mchana kwa ajili ya wajumbe kutoka ng’ambo. Ndugu mmoja alieleza hivi: “Ilikuwa kazi ambayo hatukuwa tumewahi kufanya. Kazi hiyo ilihusisha kupeleka vifurushi 6,500 hivi vya chakula cha mchana kila siku. Tuliguswa moyo kuona wengi, kutia ndani watoto, wakijitolea kusaidia.”

Dada mmoja aliyesafiri kutoka Ukrainia kwenda Chorzow kwa ajili ya kusanyiko alisema: “Tumeguswa sana na upendo, hangaiko, na ukarimu wa waamini wenzetu. Tunashukuru sana hata hatujui tuseme nini.” Naye Annika, kutoka Ufini, mwenye umri wa miaka minane aliiandikia hivi ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Poland: “Kusanyiko hilo lilikuwa lenye kupendeza kuliko nilivyowazia. Ni jambo bora kuwa katika tengenezo la Yehova, kwa kuwa mtu anakuwa na marafiki ulimwenguni pote!”—Zaburi 133:1.

Maelezo ya Watazamaji

Kabla ya makusanyiko, mipango ilifanywa ili baadhi ya wajumbe watembelee maeneo mbalimbali. Katika maeneo ya mashambani ya Bavaria, wageni hao walisimama mahali penye Majumba ya Ufalme, na wakakaribishwa na Mashahidi wenyeji. Kiongozi wa kikundi kimoja ambaye si Shahidi alivutiwa sana na upendo huo wa kindugu. “Tulipokuwa katika basi tukirudi hotelini,” anaripoti mjumbe mmoja, “kiongozi wetu alisema kwamba sisi ni tofauti sana na vikundi vingine vya watalii. Tulikuwa tumevalia vizuri, na wote walishirikiana na wale waliokuwa wakituelekeza. Hakuna aliyetumia lugha chafu wala hapakuwa na mvurugo. Hakuamini jinsi ambavyo watu wasiofahamiana wangeweza mara moja kuwa marafiki wakubwa.”

Ndugu aliyefanya kazi katika Idara ya Upashaji wa Habari katika kusanyiko la Prague anasema: “Jumapili asubuhi (Siku ya Yenga), ofisa aliyewasimamia polisi waliotumwa kwenye kusanyiko alitutembelea. Aliona amani imetanda na akasema hawakuwa na kazi ya kufanya. Pia, alisema watu fulani wanaoishi karibu na uwanja huo walikuwa wameuliza kuhusu programu. Ofisa huyo alipotaja Mashahidi wa Yehova, kwa kawaida watu hao waliudhika, naye akawaambia: ‘Iwapo watu wangejiendesha kwa kadiri fulani kama Mashahidi wa Yehova, polisi hawangehitajiwa tena kamwe.’”

Wengi Tayari Wamekombolewa!

Neno la Mungu, Biblia, linaunganisha jamii mbalimbali, na kuwawezesha watu kuwa Wakristo wenye amani na umoja. (Waroma 14:19; Waefeso 4:22-24; Wafilipi 4:7) Makusanyiko ya pekee ya wilaya ya “Ukombozi Unakaribia!” yalithibitisha jambo hilo. Tayari Mashahidi wa Yehova wamekombolewa kutoka katika taabu nyingi zinazokumba ulimwengu huu. Uadui, chuki, na ubaguzi ni baadhi ya matatizo yanayokumba jamii, lakini Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kuyashinda, nao wanatazamia wakati ambapo matatizo kama hayo hayatakuwapo tena ulimwengu pote.

Wale waliohudhuria makusanyiko hayo walijionea jinsi Mashahidi kutoka nchi na jamii mbalimbali walivyo na umoja. Umoja huo ulionekana waziwazi mwishoni mwa makusanyiko hayo. Wote walipiga makofi, wakawakumbatia marafiki wapya, na kupiga picha zao za mwisho. (1 Wakorintho 1:10; 1 Petro 2:17) Wakiwa na furaha na wakiwa wamesadikishwa kwamba ukombozi kutoka katika matatizo na mahangaiko yote unakaribia, wajumbe walirudi nyumbani kwao na kwenye makutaniko yao wakiwa wameazimia upya kushika sana ‘neno la Mungu la uzima.’—Wafilipi 2:15, 16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Makusanyiko mengine sita kotekote nchini Poland na kusanyiko moja huko Slovakia yaliunganishwa kwa simu wakati wa sehemu za kimataifa za programu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Lugha 25 Zinaunganishwa

Katika makusanyiko yote tisa, programu ilitolewa katika lugha ya nchi. Wakati wa makusanyiko ya Kijerumani, hotuba zilitolewa pia katika lugha nyingine 18. Huko Dortmund hotuba zilitolewa katika Kiarabu, Kifarsi, Kihispania, Kireno, na Kirusi; huko Frankfurt zilitolewa katika Kifaransa, Kiingereza, na Kiserbia/Kikroatia; huko Hamburg zilitolewa katika Kidenishi, Kiholanzi, Kiswedi, na Kitamili; huko Leipzig zilitolewa katika Kichina, Kipolishi, na Kituruki; na huko Munich zilitolewa katika Kigiriki, Kiitaliano, na katika Lugha ya Ishara ya Kijerumani. Katika kusanyiko la Prague hotuba zote zilitolewa katika Kicheki, Kiingereza, na Kirusi. Huko Bratislava programu ilitolewa katika Kiingereza, Kihungaria, Kislovaki, na Lugha ya Ishara ya Kislovaki. Huko Chorzow ilitolewa katika Kipolishi, Kirusi, Kiukrainia, na Lugha ya Ishara ya Poland. Na huko Poznan, ilitolewa katika Kipolishi na Kifini.

Hiyo ni jumla ya lugha 26! Kwa kweli, wale waliohudhuria makusanyiko hayo waligawanywa na lugha, lakini wakaunganishwa na upendo.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wajumbe Wakroatia huko Frankfurt walifurahi kupokea “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” katika lugha yao wenyewe