Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barzilai—Mtu Aliyetambua Udhaifu Wake

Barzilai—Mtu Aliyetambua Udhaifu Wake

Barzilai—Mtu Aliyetambua Udhaifu Wake

‘KWA nini niwe mzigo kwako?’ Mzee mwenye umri wa miaka 80 aliyeitwa Barzilai ndiye aliyemwambia Mfalme Daudi wa Israeli maneno hayo. Biblia inasema kwamba alikuwa “mwanamume mkuu sana,” bila shaka aliitwa hivyo kwa sababu alikuwa tajiri. (2 Samweli 19:32, 35) Barzilai aliishi katika nchi ya Gileadi, katika eneo lenye milima upande wa mashariki wa Mto Yordani.—2 Samweli 17:27; 19:31.

Barzilai alikuwa katika hali gani alipomwambia Daudi maneno hayo? Kwa nini mzee huyo alisema hivyo?

Kumwasi Mfalme

Daudi alikuwa hatarini. Absalomu, mwana wake, alikuwa amenyakua kiti cha ufalme baada ya “kuiba mioyo ya watu wa Israeli.” Ilikuwa wazi kwamba Absalomu alikusudia kumdhuru mtu yeyote ambaye alikuwa mshikamanifu kwa baba yake. Kwa hiyo, Daudi na watumishi wake walikimbia kutoka Yerusalemu. (2 Samweli 15:6, 13, 14) Daudi alipofika Mahanaimu, eneo ambalo liko mashariki ya Yordani, Barzilai alimsaidia.

Barzilai na wanaume wengine wawili walimpa Daudi vyakula vingi sana. Watu hao watatu washikamanifu walionyesha kwamba walielewa hali ngumu ya Daudi waliposema hivi kumhusu yeye na wanaume wake: “Watu wana njaa nao wamechoka na wana kiu nyikani.” Barzilai, Shobi, na Makiri walifanya yote waliyoweza ili kutosheleza mahitaji hayo kwa kumpa Daudi na wanaume wake vitanda, ngano, shayiri, unga, nafaka iliyochomwa, maharagwe mapana, dengu, nafaka iliyokauka, asali, siagi, kondoo, na vitu vingine.—2 Samweli 17:27-29.

Kumsaidia Daudi kulikuwa hatari. Inaelekea kwamba Absalomu hangekosa kumwadhibu mtu yeyote aliyemuunga mkono mfalme aliyekuwa na haki ya kutawala. Kwa hivyo, Barzilai alitenda kwa ujasiri alipomwonyesha Daudi ushikamanifu.

Hali Inabadilika

Muda mfupi baadaye, wanajeshi waasi wa Absalomu walikutana na wanaume wa Daudi. Vita vikatokea katika msitu wa Efraimu, labda karibu na Mahanaimu. Jeshi la Absalomu lilishindwa, “na mauaji hapo yakawa makubwa siku hiyo.” Ingawa Absalomu alijaribu kukimbia, muda si muda aliuawa.—2 Samweli 18:7-15.

Kwa mara nyingine tena, Daudi akawa mfalme wa Israeli bila kupingwa. Wafuasi wake hawakuhitaji tena kuishi kama wakimbizi. Zaidi ya hayo, Daudi aliwaheshimu na kuwathamini kwa sababu walikuwa washikamanifu kwake.

Daudi alipokuwa karibu kurudi Yerusalemu, “Barzilai Mgileadi akashuka kutoka Rogelimu ili apite mpaka Yordani pamoja na mfalme, apate kumsindikiza mpaka Yordani.” Wakati huo, Daudi alimtolea Barzilai aliyezeeka mwaliko huu: “Wewe vuka pamoja nami, nami nitakuandalia chakula wewe pamoja nami katika Yerusalemu.”—2 Samweli 19:15, 31, 33.

Bila shaka, Daudi alithamini sana msaada wa Barzilai. Haionekani kwamba mfalme alitaka tu kuonyesha shukrani kwa kumwandalia vyakula. Barzilai aliyekuwa tajiri hakuhitaji msaada wa aina hiyo. Huenda Daudi alitaka aishi katika makao ya mfalme kwa sababu ya sifa zenye kuvutia za mzee huyo. Lingekuwa jambo la heshima kwa Barzilai kukaa katika makao hayo muda wote, kwa kuwa angeweza kufaidika kwa sababu ya pendeleo la kuwa rafiki ya mfalme.

Kiasi na Kuona Mambo Jinsi Yalivyo

Barzilai alimjibu hivi Mfalme Daudi kuhusu mwaliko huo: “Siku za miaka ya maisha yangu ni ngapi, ili kwamba niende Yerusalemu pamoja na mfalme? Mimi leo nina umri wa miaka 80. Je, ninaweza kutambua kati ya jema na baya, au je, mtumishi wako anaweza kuonja ladha ya kile ninachokula na kile ninachokunywa, au je, ninaweza kusikiliza tena sauti za waimbaji wa kiume na wa kike?” (2 Samweli 19:34, 35) Kwa hiyo, Barzilai alikataa kwa heshima mwaliko huo na pendeleo hilo zuri. Lakini kwa nini?

Huenda sababu moja iliyomfanya Barzilai aamue hivyo ni umri wake wa uzee na udhaifu wa kimwili. Labda Barzilai alihisi kwamba hangeishi muda mrefu zaidi. (Zaburi 90:10) Alikuwa amefanya yale aliyoweza ili kumsaidia Daudi, lakini pia alitambua udhaifu aliokuwa nao kwa sababu ya umri wake wa uzee. Barzilai hakuruhusu fahari na umaarufu umzuie kuchanganua kihalisi mambo ambayo angeweza kufanya. Tofauti na Absalomu mwenye tamaa ya makubwa, kwa hekima Barzilai alionyesha kiasi.—Methali 11:2.

Huenda sababu nyingine iliyomfanya Barzilai afanye uamuzi huo ni kwamba hakutaka udhaifu wake uzuie utendaji wa mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu. Barzilai aliuliza hivi: “Kwa nini basi mtumishi wako awe mzigo tena kwa bwana wangu mfalme?” (2 Samweli 19:35) Ingawa bado alimuunga mkono Daudi, inaelekea kwamba Barzilai aliamini kwamba mwanamume kijana angeweza kutimiza migawo vizuri zaidi. Labda akizungumza kuhusu mwana wake mwenyewe, Barzilai alisema: “Tazama, mtumishi wako Kimhamu. Acha avuke pamoja na bwana wangu mfalme; nawe umfanyie yaliyo mema machoni pako.” Badala ya kuudhika, Daudi alikubali pendekezo hilo. Kwa kweli, kabla ya kuvuka Yordani, Daudi “akambusu Barzilai na kumbariki.”—2 Samweli 19:37-39.

Usawaziko Unahitajiwa

Simulizi la Barzilai linakazia uhitaji wa usawaziko. Kwa upande mmoja, hatupaswi kukataa mapendeleo ya utumishi au kukataa kujitahidi kuyafikia kwa sababu tunataka kuishi maisha ya starehe au tunahisi hatuwezi kuyatimiza. Tukimtegemea Mungu atupe nguvu na hekima, yeye anaweza kujazia upungufu wetu.—Wafilipi 4:13; Yakobo 4:17; 1 Petro 4:11.

Kwa upande mwingine, tunahitaji kutambua udhaifu wetu. Kwa mfano, huenda Mkristo tayari ni mwenye bidii katika utendaji wa kiroho. Anatambua kwamba akikubali migawo zaidi, anaweza kupuuza madaraka fulani ya Kimaandiko kama vile kuiandalia familia yake. Katika hali kama hiyo, je, hangekuwa akionyesha kiasi na usawaziko kwa kukataa mapendeleo zaidi wakati huu?—Wafilipi 4:5; 1 Timotheo 5:8.

Barzilai anaweka mfano mzuri, na ni vyema tutafakari mfano wake. Alikuwa mshikamanifu, mkarimu, mwenye ujasiri, na mwenye kiasi. Zaidi ya yote, Barzilai aliazimia kutanguliza mambo ya Mungu wala si mambo yake mwenyewe.—Mathayo 6:33.

[Ramani katika ukurasa wa 15]

 

Barzilai aliyekuwa na miaka 80, alifunga safari ya kuchosha ili amsaidie Daudi

GILEADI

Rogelimu

Sukothi

Mahanaimu

Mto Yordani

Gilgali

Yeriko

Yerusalemu

EFRAIMU

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kwa nini Barzilai alikataa mwaliko wa Daudi?