Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hekima Ni Ulinzi”

“Hekima Ni Ulinzi”

“Hekima Ni Ulinzi”

“KUPATA hekima ni bora kama nini kuliko dhahabu! Na kupata uelewaji kunapasa kuchaguliwa kuliko fedha,” inasema Methali 16:16. Kwa nini hekima ni yenye thamani sana? Kwa sababu “hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi; lakini faida ya ujuzi ni kwamba hekima huwahifadhi hai waliyo nayo.” (Mhubiri 7:12) Hata hivyo, hekima inahifadhi hai waliyo nayo jinsi gani?

Kupata hekima kutoka kwa Mungu, yaani, kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu Biblia, na kutenda kulingana nao, kunatusaidia kutembea katika njia ambayo Yehova anakubali. (Methali 2:10-12) Mfalme Sulemani wa Israeli la kale anasema: “Njia kuu ya wanyoofu ni kuepuka ubaya. Anayeilinda njia yake anaitunza nafsi yake.” (Methali 16:17) Ndiyo, hekima inawakomboa waliyo nayo kutoka katika njia mbaya na kuwahifadhi hai! Maneno machache na yenye hekima yaliyo katika Methali 16:16-33 yanaonyesha matokeo mazuri ambayo hekima kutoka kwa Mungu inaweza kuwa nayo juu ya mtazamo, usemi, na matendo yetu. *

‘Uwe na Roho ya Unyenyekevu’

Hekima inayofananishwa na mtu inaonyeshwa ikisema hivi: “Nimechukia kujiinua na kiburi.” (Methali 8:13) Kiburi na hekima ni sifa zinazotofautiana sana. Tunahitaji kutenda kwa hekima na kuwa waangalifu tusisitawishe mtazamo wa kiburi au wa majivuno. Tunapaswa kujihadhari hasa ikiwa tumefanikiwa katika sehemu fulani za maisha au ikiwa tumepewa mapendeleo fulani katika kutaniko la Kikristo.

“Kiburi hutangulia kuanguka,” inaonya Methali 16:18, “na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” Fikiria tukio kubwa zaidi katika ulimwengu wote la kuanguka, kule kuanguka kwa mwana mkamilifu wa roho wa Mungu ambaye alijifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:1-5; Ufunuo 12:9) Je, hakuonyesha roho ya kiburi kabla ya kuanguka kwake? Biblia inaonyesha hilo inaposema kwamba Mkristo mpya hapaswi kuwekwa kuwa mwangalizi katika kutaniko la Kikristo ili “asije akajivuna kwa kiburi na kuanguka katika hukumu iliyopitishwa juu ya Ibilisi.” (1 Timotheo 3:1, 2, 6) Ni muhimu kama nini tujihadhari tusisitawishe kiburi au kuwachochea wengine wawe nacho!

“Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na wapole kuliko kugawanya nyara pamoja na watu wanaojiinua,” inasema Methali 16:19. Kisa cha Mfalme Nebukadneza wa Babiloni la kale kinaonyesha kwamba hilo ni shauri lenye hekima. Mfalme huyo alisimamisha kwa kiburi sanamu kubwa sana katika nchi tambarare ya Dura. Huenda sanamu hiyo ilimwakilisha Nebukadneza. Pengine sanamu hiyo ilisimamishwa juu ya jukwaa refu sana hivi kwamba ikafikia urefu wa mita 27 kwenda juu. (Danieli 3:1) Sanamu hiyo kubwa ilipaswa kuwa ishara yenye kustaajabisha ya milki ya Nebukadneza. Ingawa vitu vilivyo juu na vilivyoinuka kama sanamu hiyo, nguzo, minara, na majengo marefu sana, yanaweza kuwastaajabisha wanadamu, vitu hivyo haviwezi kumstaajabisha Mungu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova yuko juu, hata hivyo yeye humwona mnyenyekevu; lakini yeye anamjua mwenye kiburi kutoka mbali tu.” (Zaburi 138:6) Kwa kweli, “kilichoinuka sana kati ya wanadamu ni chukizo machoni pa Mungu.” (Luka 16:15) Ni afadhali ‘tuongozwe na mambo ya hali ya chini’ kuliko “kukaza akili zetu juu ya mambo makuu.”—Waroma 12:16.

Sema kwa “Ufahamu” na “Ushawishi”

Kuwa na hekima kuna uvutano gani juu ya usemi wetu? Mfalme mwenye hekima anatuambia hivi: “Anayetumia ufahamu katika jambo atapata mema, naye anayemtegemea Yehova ni mwenye furaha. Mtu mwenye hekima moyoni itasemwa kwamba ana uelewaji, naye mwenye midomo mitamu huongeza ushawishi. Ufahamu ni kisima cha uzima kwa hao walio nao; nayo nidhamu ya wapumbavu ni upumbavu. Moyo wa mtu mwenye hekima hukifanya kinywa chake kionyeshe ufahamu, na kwenye midomo yake huongeza ushawishi.”Methali 16:20-23.

Hekima inatusaidia kuzungumza kwa ufahamu na ushawishi. Kwa nini? Kwa sababu mtu mwenye hekima moyoni anajaribu ‘kupata mema’ katika jambo, naye ‘anamtegemea Yehova.’ Tunapojitahidi kuona sifa njema za wengine, inaelekea sana tutasema mambo mema kuwahusu. Badala ya kuwa wakali au wenye kushindana, maneno yetu yanakuwa matamu na yenye kushawishi. Kufahamu hali za wengine kutatusaidia kuelewa matatizo ambayo huenda wanakabili na jinsi wanavyopambana nayo.

Usemi unaoongozwa na hekima ni muhimu pia katika kazi yetu ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Tunapowafundisha wengine Neno la Mungu, kusudi letu si kuwapa tu ujumbe wa Kimaandiko. Kusudi letu ni kufikia mioyo ya watu. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na midomo yenye ushawishi. Mtume Paulo alimhimiza mshiriki wake Timotheo aendelee katika mambo ‘aliyoshawishiwa kuamini.’—2 Timotheo 3:14, 15.

Kamusi ya W. E. Vine (An Expository Dictionary of New Testament Words) inasema kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “shawishi” linamaanisha “kutokeza badiliko la akili kupitia kujadiliana au kufikiria mambo mema.” Ili tutoe hoja zenye kusadikisha ambazo zitabadili akili ya msikilizaji wetu ni lazima tufahamu jinsi anavyofikiri, mapendezi yake, hali zake, na malezi yake. Tunaweza kupata ufahamu huo jinsi gani? Mwanafunzi Yakobo anajibu hivi: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Kwa kumtia moyo msikilizaji wetu atoe maoni yake na kumsikiliza kwa makini, tunaweza kujua yaliyo moyoni mwake.

Mtume Paulo alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kuwashawishi wengine. (Matendo 18:4) Hata Demetrio, fundi mmoja wa fedha ambaye alikuwa mpinzani wake, alisema hivi: “Si katika Efeso tu, bali pia katika karibu wilaya yote ya Asia, Paulo huyu ameshawishi umati mkubwa na kuwageuza kwenye kauli nyingine.” (Matendo 19:26) Je, Paulo alidai kwamba ustadi wake ndio uliofanya awe na matokeo katika kazi ya kuhubiri? Sivyo hata kidogo. Aliona kazi yake ya kuhubiri kuwa ‘wonyesho wa roho na nguvu za Mungu.’ (1 Wakorintho 2:4, 5) Leo sisi pia tunasaidiwa na roho takatifu ya Yehova. Kwa sababu tunamtegemea Yehova, tuna hakika kwamba atatusaidia tunapojitahidi kusema kwa ufahamu na ushawishi katika huduma yetu.

Haishangazi kwamba “mtu mwenye hekima moyoni” anaitwa “mwenye akili” au “mwenye utambuzi”! (Methali 16:21, An American Translation; New International Version) Ndiyo, ufahamu ni “kisima cha uzima” kwa wale walio nao. Lakini namna gani wapumbavu? ‘Wanadharau hekima na nidhamu.’ (Methali 1:7) Wanapata matokeo gani wanapokataa nidhamu ya Yehova? Kama ilivyoonyeshwa hapo juu, Sulemani anasema: “nidhamu ya wapumbavu ni upumbavu.” (Methali 16:22) Kwa kawaida wanapata nidhamu zaidi, wanapoadhibiwa vikali. Wapumbavu wanaweza pia kujiletea matatizo, aibu, magonjwa, na hata kifo cha mapema.

Akizungumzia zaidi kuhusu matokeo mazuri ya hekima juu ya usemi wetu, mfalme wa Israeli anasema: “Maneno yenye kupendeza ni sega la asali, ni matamu kwa nafsi na maponyo mifupani.” (Methali 16:24) Kama asali tamu inayomburudisha haraka mtu mwenye njaa, maneno yenye kupendeza ni yenye kutia moyo na yenye kuburudisha. Pia, asali ina uwezo wa kuboresha afya na kumponya mtu. Maneno yapendezayo yako vivyo hivyo; ni yenye afya kiroho.—Methali 24:13, 14.

Jihadhari na ‘Njia Inayoonekana Kuwa Imenyooka’

“Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu,” anasema Sulemani, “lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Methali 16:25) Hilo ni onyo juu ya kujidanganya na kufuata njia inayopingana na sheria ya Mungu. Mtu ambaye si mkamilifu anaweza kuona njia fulani kuwa imenyooka lakini huenda njia hiyo inapingana na kanuni za uadilifu za Neno la Mungu. Zaidi ya hilo, Shetani anaweza kumfanya mtu azidi kujidanganya na hivyo aendelee kufuata njia anayoamini kuwa sawa, lakini ambayo kwa kweli inaongoza kwenye kifo.

Hakuna ulinzi bora zaidi dhidi ya moyo mdanganyifu kuliko kuwa na moyo wenye hekima na uelewaji na kuwa na dhamiri inayoongozwa na ujuzi wa Neno la Mungu. Tunapohitaji kufanya maamuzi iwe yanahusu maadili, ibada, au jambo lingine lolote, njia bora ya kujilinda tusijidanganye wenyewe ni kuongozwa na viwango vya Mungu kuhusu mema na mabaya.

“Hamu ya Kula ya Mfanyakazi Inamfanyia Kazi”

“Nafsi ya mfanyakazi mwenye bidii imemfanyia kazi kwa bidii,” anaendelea kusema mfalme mwenye hekima, “kwa sababu kinywa chake kimemkaza sana.” (Methali 16:26) Sulemani anasema kwamba hamu ya kula ya mfanyakazi ‘inaweza kumfanyia kazi kwa bidii’ kwa sababu njaa yake ‘inamsukuma,’ au inamchochea. Tafsiri moja (An American Translation) inasema hivi: “Hamu ya kula ya mfanyakazi inamfanyia kazi; kwa kuwa njaa yake inamsukuma.” Tamaa ya kawaida, kama vile hamu ya kula, inaweza kutuchochea kufanya kazi kwa bidii. Tamaa kama hiyo ni yenye faida. Hata hivyo, namna gani tamaa nzuri ikiachwa iwe na nguvu sana na kutokeza pupa? Matokeo yanakuwa sawa na wakati moto wa kupikia unapoongezeka na kuteketeza msitu. Pupa ni tamaa isiyozuiliwa na inasababisha uharibifu. Akitambua hatari, mtu mwenye hekima anazuia au kudhibiti hata tamaa zake nzuri.

Usiende “Katika Njia Isiyo Njema”

Maneno yanayotoka katika midomo yetu yanaweza kuleta uharibifu mkubwa kama moto mkali. Akieleza jinsi kutafuta-tafuta kasoro za wengine na kuzieneza kunavyoweza kusababisha uharibifu mkubwa, Sulemani anasema: “Mtu asiyefaa kitu anachimbua lililo baya, na katika midomo yake ni kana kwamba kuna moto unaounguza. Mtu mwenye hila huendelea kutokeza ugomvi nyakati zote, na mchongezi anawatenganisha wale wanaofahamiana.”Methali 16:27, 28.

Mtu anayejaribu kuteketeza au kuharibu sifa njema ya mwenzake ni mtu “asiyefaa kitu.” Tunapaswa kujitahidi kutafuta sifa njema za watu wengine na kusema mambo yatakayowafanya waheshimiwe. Namna gani kuwasikiliza wale wanaoeneza porojo yenye kuumiza? Maneno yao yanaweza kwa urahisi kutokeza mashaka yasiyo na msingi, kuwatenganisha marafiki, na kusababisha mgawanyiko kutanikoni. Hekima itatuchochea tukatae kuwasikiliza.

Akionya juu ya nguvu yenye kushawishi inayoweza kumfanya mtu afuate njia mbaya, Sulemani anasema: “Mtu wa jeuri atamshawishi mwenzake, naye hakika humfanya aende katika njia isiyo njema. Anakonyeza-konyeza macho yake ili kupanga hila. Akikaza midomo yake, hakika yeye hukamilisha madhara.”Methali 16:29, 30.

Je, jeuri inaweza kuwashawishi waabudu wa kweli? Watu wengi leo, wameshawishiwa “kupanga hila.” Wanaunga mkono au kutenda jeuri. Huenda isiwe vigumu kwetu kuepuka kushiriki moja kwa moja katika jeuri. Lakini namna gani kushawishiwa kwa werevu tujihusishe na jeuri? Je, mamilioni ya watu hawajashawishiwa kutazama vipindi au sinema na michezo inayotukuza jeuri? Maandiko yanaonya hivi waziwazi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Hekima ya kimungu inatoa ulinzi mkubwa kama nini!

Tunaweza kusema nini kumhusu mtu ambaye amekuwa na hekima na uelewaji maisha yake yote, na ‘hajaenda katika njia isiyo njema’? Mtu ambaye ametumia maisha yake katika njia ya uadilifu ni mwenye kupendeza machoni pa Mungu na anastahili kuheshimiwa. “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu,” inasema Methali 16:31.

Kwa upande mwingine, hasira isiyozuiliwa haipendezi hata kidogo. Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa, ‘alimwakia kwa hasira’ Abeli ndugu yake na ‘akamshambulia na kumuua.’ (Mwanzo 4:1, 2, 5, 8) Ingawa huenda nyakati nyingine tukawa na sababu ya kukasirika, tunapaswa kujihadhari tusishindwe kuzuia hasira yetu. Methali 16:32 inasema hivi waziwazi: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.” Hasira isiyozuiliwa si sifa njema, nayo haionyeshi kwamba mtu ana uwezo. Huo ni udhaifu unaoweza ‘kumfanya mtu aende katika njia isiyo njema.’

Wakati Ambapo ‘Kila Uamuzi Unatoka kwa Yehova’

“Watu hutupa kura ndani ya mkunjo wa nguo,” anasema mfalme wa Israeli, “lakini kila uamuzi unaofanywa kupitia kura hiyo hutoka kwa Yehova.” (Methali 16:33) Katika Israeli la kale, nyakati fulani Yehova alitumia kura ili kujulisha mapenzi yake. Kura hizo zilikuwa mawe madogo ya mviringo au mabamba ya mbao au mawe. Kwanza, Yehova aliombwa aamue jambo fulani. Kisha, kura hizo zilitupwa ndani ya mkunjo wa nguo halafu zikatolewa. Matokeo ya kura hizo yalikubaliwa kuwa uamuzi wa Mungu.

Yehova hatumii tena kura ili kuwajulisha watu wake maoni yake. Amefunua mapenzi yake katika Neno lake Biblia. Ujuzi sahihi wa Biblia ni wa muhimu sana ili kuwa na hekima ya kimungu. Hivyo, tusiache hata siku moja ipite bila kusoma Maandiko yaliyoongozwa na roho.—Zaburi 1:1, 2; Mathayo 4:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa habari zaidi kuhusu Methali 16:1-15, ona ukurasa wa 17-20 wa toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2007 (15/5/2007).

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kwa nini hekima ni bora kuliko dhahabu?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni nini kinachoongeza ushawishi kwenye midomo yako unapokuwa katika huduma?

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Mtu asiyefaa kitu anachimbua lililo baya”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Hasira isiyozuiliwa inaweza kumfanya mtu “aende katika njia isiyo njema”

[Picha katika ukurasa wa 12]

Jeuri ina nguvu ya kushawishi