Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?

Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?

Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?

“Kuna dhambi ambayo huleta kifo.”—1 YOHANA 5:16.

1, 2. Tunajua jinsi gani kwamba inawezekana kuitendea dhambi roho takatifu ya Mungu?

“NIMESUMBULIWA sana na wazo la kwamba nimeitendea dhambi roho takatifu.” Hivyo ndivyo alivyoandika mwanamke mmoja huko Ujerumani, ingawa alikuwa akimtumikia Mungu. Je, Mkristo anaweza kwa kweli kuitendea dhambi roho takatifu, au nguvu ya utendaji ya Mungu?

2 Ndiyo, inawezekana kuitendea dhambi roho takatifu ya Yehova. Yesu Kristo alisema hivi: “Watu watasamehewa kila namna ya dhambi na kufuru, lakini hawatasamehewa kufuru juu ya roho.” (Mathayo 12:31) Tunaonywa hivi: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi, lakini kuna tarajio hakika lenye kuogopesha la hukumu.” (Waebrania 10:26, 27) Naye mtume Yohana aliandika: “Kuna dhambi ambayo huleta kifo.” (1 Yohana 5:16) Lakini je, mtu aliyetenda dhambi nzito ndiye anayeamua mwenyewe ikiwa ametenda “dhambi ambayo huleta kifo”?

Kutubu Kunaleta Msamaha

3. Inaelekea kuna uhakika gani ikiwa tunahuzunika sana kwa sababu ya dhambi ambayo tumetenda?

3 Yehova ndiye Mwamuzi mkuu wa wakosaji. Kwa kweli, ni lazima sote tutoe hesabu kwake, na sikuzote yeye anafanya yaliyo sawa. (Mwanzo 18:25; Waroma 14:12) Yehova ndiye anayeamua ikiwa tumetenda dhambi isiyoweza kusamehewa, naye ndiye anayeweza kuiondoa roho yake juu yetu. (Zaburi 51:11) Hata hivyo, ikiwa tunahuzunika sana kwa sababu ya dhambi ambayo tumetenda, inaelekea kwamba tumetubu kikweli. Lakini toba ya kweli ni nini?

4. (a) Kutubu kunamaanisha nini? (b) Kwa nini maneno ya Zaburi 103:10-14 yanafariji?

4 Kutubu kunamaanisha kwamba tumebadili mtazamo wetu kuelekea makosa tuliyotenda au tuliyokusudia kutenda. Kunamaanisha kwamba tunahuzunika au tunasikitika na kuachana na dhambi. Ikiwa tumetenda dhambi nzito lakini tumechukua hatua za lazima ili kuonyesha kwamba tumetubu kikweli, tunaweza kufarijiwa na maneno yafuatayo ya mtunga-zaburi: “[Yehova] hakututendea kulingana na dhambi zetu; wala kuleta juu yetu kile tunachostahili kulingana na makosa yetu. Kwa maana kama mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo fadhili zake zenye upendo zilivyo kuu kuwaelekea wale wanaomwogopa. Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi. Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:10-14.

5, 6. Taja wazo kuu la 1 Yohana 3:19-22, na eleza maana ya maneno hayo ya mtume.

5 Pia, maneno yafuatayo ya mtume Yohana yanafariji: “Kwa jambo hili tutajua kwamba sisi tunatokana na kweli, nasi tutaihakikishia mioyo yetu mbele zake kwa habari ya lolote ambalo huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote. Wapendwa, ikiwa mioyo yetu haituhukumu kuwa na hatia, tuna uhuru wa kusema kwa Mungu; na chochote kile tunachoomba tunapokea kutoka kwake, kwa sababu tunazishika amri zake na tunafanya mambo yanayopendeza machoni pake.”—1 Yohana 3:19-22.

6 ‘Tunajua kwamba sisi tunatokana na kweli’ kwa kuwa tunaonyesha upendo wa kindugu na hatuzoei kutenda dhambi. (Zaburi 119:11) Tukihisi tunajihukumu kwa sababu fulani, tunapaswa kukumbuka kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” Yehova anatuonyesha rehema kwa sababu anajua ‘upendo wetu wa kindugu usio na unafiki,’ pambano letu juu ya dhambi, na jitihada zetu za kufanya mapenzi yake. (1 Petro 1:22) Moyo wetu ‘hautatuhukumu’ tukimtegemea Yehova, tukionyesha upendo wa kindugu, na ikiwa hatuna hatia ya kutenda dhambi kimakusudi. Tutakuwa na “uhuru wa kusema kwa Mungu” katika sala, naye atatujibu kwa sababu tunashika amri zake.

Waliitendea Dhambi Roho

7. Ni nini kinachoamua kama dhambi inaweza kusamehewa au hapana?

7 Ni dhambi gani zisizoweza kusamehewa? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze mifano fulani katika Biblia. Hilo linapaswa kutufariji ikiwa tumetubu lakini bado tunahuzunika sana kwa sababu ya makosa yetu mazito. Tutaona kwamba jambo linaloamua kama dhambi inaweza kusamehewa au hapana, si aina ya dhambi ambayo mtu ametenda; bali ni nia, hali ya moyo, na ni kwa kadiri gani alikusudia kufanya dhambi.

8. Viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza waliitendea dhambi roho takatifu jinsi gani?

8 Viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza ambao walimpinga Yesu Kristo kwa hila walikuwa wakiitendea dhambi roho takatifu. Waliona roho ya Mungu ikitenda kazi kupitia Yesu alipofanya miujiza ambayo ilimletea Yehova heshima. Hata hivyo, maadui hao wa Kristo walisema kwamba nguvu hizo zilitokana na Shetani Ibilisi. Hivyo, kulingana na Yesu, wale waliokufuru roho takatifu ya Mungu walikuwa wakitenda dhambi ambayo haingesamehewa katika “mfumo huu wa mambo wala katika ule utakaokuja.”—Mathayo 12:22-32.

9. Kukufuru ni nini, na Yesu alisema nini kuhusu tendo hilo?

9 Kukufuru ni kuchongea, kusema maneno yenye kuumiza au matukano. Kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo cha roho takatifu, kusema mambo mabaya juu ya roho yake ni kusema vibaya juu ya Yehova. Mtu anayesema maneno ya aina hiyo bila kutubu hawezi kusamehewa. Maneno ya Yesu kuhusu dhambi kama hiyo yanaonyesha kwamba Yesu anazungumza kuhusu wale wanaopinga kimakusudi utendaji wa roho takatifu ya Mungu. Kwa kuwa roho ya Yehova ilikuwa ikitenda kazi kupitia Yesu lakini wapinzani wake walidai kwamba nguvu hizo zilitoka kwa Ibilisi, walikufuru na kuitendea dhambi roho hiyo. Hivyo, Yesu alisema: “Yeyote yule anayekufuru roho takatifu hatapata msamaha milele, bali ana hatia ya dhambi ya milele.”—Marko 3:20-29.

10. Kwa nini Yesu alimwita Yuda “yule mwana wa maangamizi”?

10 Pia, fikiria kisa cha Yuda Iskariote. Hakuwa mnyoofu, na alikuwa akiiba pesa zilizowekwa ndani ya sanduku alilokabidhiwa. (Yohana 12:5, 6) Baadaye, Yuda aliwaendea watawala wa Kiyahudi akapanga kumsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. Ndiyo, baada ya kumsaliti Yesu, Yuda alijihisi kuwa mwenye hatia, lakini hakutubu kamwe dhambi yake aliyotenda kimakusudi. Kwa sababu hiyo, Yuda hastahili kufufuliwa, hivyo Yesu alimwita “yule mwana wa maangamizi.”—Yohana 17:12; Mathayo 26:14-16.

Hawakuitendea Dhambi Roho

11-13. Mfalme Daudi alitenda dhambi jinsi gani pamoja na Bath-sheba, na tunaweza kupata faraja gani kutokana na jinsi Mungu alivyowashughulikia?

11 Mara kwa mara, Wakristo ambao wameungama dhambi zao nzito na ambao wamepokea msaada wa kiroho kutoka kwa wazee wa kutaniko, huenda wakawa bado wanafadhaika kwa sababu walivunja sheria ya Mungu wakati uliopita. (Yakobo 5:14) Ikiwa sisi binafsi tunavurugika kwa njia hiyo, inaelekea sana kwamba tutafaidika tukichunguza yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu wale ambao dhambi zao zilisamehewa.

12 Mfalme Daudi alitenda dhambi nzito na Bath-sheba, mke wa Uria. Daudi akiwa kwenye paa alimwona mwanamke huyo mrembo akioga. Aliagiza mwanamke huyo aletwe kwenye jumba lake la kifalme na akafanya ngono naye. Baadaye, alipojulishwa kwamba mwanamke huyo ana mimba, Daudi alipanga njama ili Uria, mume wa mwanamke huyo, alale na mke wake na hivyo kufunika uzinzi huo. Njama hiyo ilipokosa kufanikiwa, mfalme huyo alipanga Uria auawe vitani. Baadaye, Bath-sheba akawa mke wa Daudi naye akamzalia mtoto ambaye alikufa.—2 Samweli 11:1-27.

13 Yehova alishughulikia mambo ya Daudi na Bath-sheba. Mungu alimsamehe Daudi, inaelekea alitilia maanani mambo kama vile toba ya Daudi na agano la Ufalme ambalo alikuwa amefanya pamoja naye. (2 Samweli 7:11-16; 12:7-14) Kwa kuwa alipata pendeleo la kuwa mama ya Mfalme Sulemani na nyanya ya Yesu Kristo, ni wazi kwamba Bath-sheba alitubu. (Mathayo 1:1, 6, 16) Ikiwa tumetenda dhambi, ni vizuri kukumbuka kwamba Yehova anatilia maanani mtazamo wetu wa kutubu.

14. Kisa cha Mfalme Manase kinaonyesha Mungu anasamehe kadiri gani?

14 Kisa cha Mfalme Manase wa Yuda kinaonyesha kadiri ambavyo Yehova anasamehe. Alifanya mambo yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova. Manase alisimamisha madhabahu kwa ajili ya Baali, akaabudu “jeshi lote la mbinguni,” na hata akajenga madhabahu kwa ajili ya miungu ya uwongo katika nyua mbili za hekalu. Alipitisha wanawe katika moto, akawatia watu moyo wajiingize katika mazoea ya kuwasiliana na pepo, na akasababisha wakaaji wa Yuda na Yerusalemu “wafanye mabaya zaidi kuliko yale mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyaangamiza kutoka mbele ya wana wa Israeli.” Watu hawakutii maonyo yaliyotolewa na manabii wa Mungu. Mwishowe, mfalme wa Ashuru akamchukua Manase mateka. Akiwa utekwani, Manase alitubu na kwa unyenyekevu akaendelea kusali kwa Mungu, naye akamsamehe na kumrudisha tena kuwa mfalme huko Yerusalemu, ambako aliendeleza ibada ya kweli.—2 Mambo ya Nyakati 33:2-17.

15. Ni tukio gani katika maisha ya Petro linaloonyesha kwamba Yehova anasamehe “kwa njia kubwa”?

15 Karne nyingi baadaye, mtume Petro alitenda dhambi nzito kwa kumkana Yesu. (Marko 14:30, 66-72) Hata hivyo, Yehova alimsamehe Petro “kwa njia kubwa.” (Isaya 55:7) Kwa nini? Kwa sababu Petro alitubu kikweli. (Luka 22:62) Uthibitisho ulio wazi wa kwamba Mungu alimsamehe ulionekana siku 50 baadaye katika siku ya Pentekoste, wakati Petro alipopewa pendeleo la kutoa kwa ujasiri ushuhuda kumhusu Yesu. (Matendo 2:14-36) Tuna sababu ya kuamini kwamba Mungu anawasamehe vivyo hivyo Wakristo wanaotubu kikweli leo. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama? Kwa maana kwako wewe kuna msamaha wa kweli.”—Zaburi 130:3, 4.

Kutuliza Wasiwasi wa Kwamba Umeitendea Dhambi Roho

16. Mungu anasamehe kwa msingi gani?

16 Mifano tuliyozungumzia inapaswa kutuliza wasiwasi wetu kwamba tumeitendea dhambi roho takatifu. Mifano hiyo inaonyesha kwamba Yehova anawasamehe watenda-dhambi wanaotubu. Ni jambo la maana kusali kwa bidii kwa Mungu. Ikiwa tumetenda dhambi, tunaweza kusihi tusamehewe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu, rehema za Yehova, kutokamilika kwetu tulikorithi, na utumishi wetu mwaminifu wa miaka mingi. Tukijua fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tunaweza kuomba msamaha tukiwa na hakika kwamba tutasamehewa.—Waefeso 1:7.

17. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tumetenda dhambi na tunahitaji msaada wa kiroho?

17 Namna gani ikiwa tumetenda dhambi lakini tunashindwa kusali kwa sababu dhambi yetu imetufanya tuwe wagonjwa kiroho? Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi kuhusu hilo: “Na [mtu huyo] awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yakobo 5:14, 15.

18. Kwa nini si lazima mtu awe ametenda dhambi isiyoweza kusamehewa hata ikiwa ametengwa na ushirika wa kutaniko?

18 Hata ikiwa mkosaji hatubu naye anatengwa na ushirika wa kutaniko, si lazima dhambi yake iwe isiyoweza kusamehewa. Kuhusu mkosaji mtiwa-mafuta aliyetengwa na ushirika huko Korintho, Paulo aliandika hivi: “Kemeo hili linalotolewa na walio wengi linamtosha mtu wa namna hiyo, ili kwamba, kinyume chake sasa, mnapaswa kumsamehe kwa fadhili na kumfariji, ili kwa njia fulani mtu huyo asimezwe na huzuni yake ya kupita kiasi.” (2 Wakorintho 2:6-8; 1 Wakorintho 5:1-5) Hata hivyo, ili wakosaji wawe tena na uhusiano pamoja na Yehova, wanahitaji kukubali msaada wa kiroho unaotegemea vichapo vya Biblia na ambao unatolewa na wazee Wakristo, na hivyo kuonyesha kwamba wametubu kikweli. Wanapaswa ‘kuzaa matunda yanayofaa toba.’—Luka 3:8.

19. Ni nini kinachoweza kutusaidia tubaki “wenye afya katika imani”?

19 Ni nini kinachoweza kutufanya tuhisi kwamba tumeitendea dhambi roho takatifu? Kujilaumu kupita kiasi au kuwa dhaifu sana kimwili kunaweza kuchangia hali hiyo. Katika hali kama hizo, kusali na kupumzika zaidi kunaweza kusaidia sana. Hatupaswi hasa kumwacha Shetani atuvunje moyo, na hivyo kuacha kumtumikia Mungu. Kwa kuwa Yehova hafurahi mtu mwovu anapokufa, bila shaka hafurahi kumpoteza mtumishi wake yeyote. Kwa hiyo, ikiwa tunaogopa kwamba tumeitendea dhambi roho takatifu, tunapaswa kuendelea kujilisha Neno la Mungu, kutia ndani sehemu zenye kufariji kama vile Zaburi. Tunahitaji kuendelea kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Kufanya hivyo kutatusaidia kuwa “wenye afya katika imani,” nasi hatutakuwa na wasiwasi kwamba huenda tumetenda dhambi isiyoweza kusamehewa.—Tito 2:2.

20. Ni sababu gani zinazoweza kumsaidia mtu kuona kwamba hajaitendea dhambi roho takatifu?

20 Yeyote anayeogopa kwamba ameitendea dhambi roho takatifu anaweza kujiuliza hivi: ‘Je, nimeikufuru roho takatifu? Je, nilitubu kikweli dhambi yangu? Je, ninaamini kwamba Mungu anasamehe? Je, mimi ni mwasi-imani ambaye amekataa nuru ya kiroho?’ Inaelekea sana kwamba watu kama hao watatambua kuwa hawajaikufuru roho takatifu ya Mungu, wala si waasi-imani. Wametubu, nao wanaendelea kuwa na imani katika msamaha wa Yehova. Ikiwa ndivyo ilivyo, hawajaitendea dhambi roho takatifu ya Yehova.

21. Habari inayofuata itazungumzia maswali gani?

21 Ni baraka kama nini kuwa na uhakika wa kwamba hatujaitendea dhambi roho takatifu! Hata hivyo, maswali yanayohusiana na roho takatifu yatazungumziwa katika habari inayofuata. Kwa mfano, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, kweli ninaongozwa na roho takatifu ya Mungu? Je, matunda ya roho hiyo yanaonekana wazi katika maisha yangu?’

Utatoa Jubu Gani?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba mtu anaweza kuitendea dhambi roho takatifu?

• Kutubu kunamaanisha nini?

• Ni nani walioitendea dhambi roho takatifu Yesu alipokuwa duniani?

• Tunaweza kushinda jinsi gani wasiwasi kuhusu kutenda dhambi isiyoweza kusamehewa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wale waliosema kwamba Yesu alifanya miujiza kwa nguvu za Shetani waliitendea dhambi roho takatifu ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ingawa alimkana Yesu, Petro hakutenda dhambi isiyoweza kusamehewa