Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Nafsi Isiyoweza Kufa?

Je, Una Nafsi Isiyoweza Kufa?

Je, Una Nafsi Isiyoweza Kufa?

Je, sisi ni damu na nyama tu? Au je, tumefanyizwa kwa kitu kingine zaidi ya damu na nyama? Je, tutaishi kwa muda mfupi tu kisha tutoweke? Au kuna kitu fulani kisichoonekana ambacho kinaendelea kuishi tunapokufa?

INGAWA dini za ulimwengu zimetunga mafundisho mengi yanayowavuruga watu kuhusu maisha baada ya kifo, dini nyingi zinakubaliana juu ya jambo moja la msingi: Kuna kitu fulani ndani ya mtu ambacho hakiwezi kufa nacho kinaendelea kuishi baada ya kifo. Watu wengi wanaamini kwamba “kitu” hicho ni nafsi. Wewe unaamini nini? Je, sisi tumefanyizwa kwa nyama na nafsi? Nafsi ni nini? Je, wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa? Bila shaka ni muhimu tujue ukweli kuhusu jinsi ambavyo tumefanyizwa.

“Mtu Akawa Nafsi Hai”

Je, “nafsi” ni sehemu ya mtu inayojitenga na mwili na kuendelea kuishi mtu anapokufa? Kulingana na kamusi moja (Holman Illustrated Bible Dictionary), “kwa kawaida nafsi inamaanisha mtu mzima.” Kwa mfano, Mwanzo 2:7 linasema: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” Mtu wa kwanza, Adamu, alikuwa nafsi.

Wazo la kwamba neno “nafsi” linaweza kumaanisha mtu mzima linaungwa mkono na Maandiko mengine. Kwa mfano, Biblia inazungumza kuhusu nafsi inayofanya kazi. (Mambo ya Walawi 23:30) Nafsi inasemwa kuwa imekosa subira, imekasirika, imekosa usingizi, ina woga, na imehuzunika. (Waamuzi 16:16; Ayubu 19:2; Zaburi 119:28; Matendo 2:43; 1 Wathesalonike 5:14) Likionyesha nafsi kuwa mtu, Waroma 13:1 linasema: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa.” Na katika 1 Petro 3:20, tunasoma hivi: “Katika siku za Noa, . . . watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” Hakuna jambo lolote katika maandiko hayo linalodokeza kwamba nafsi ni sehemu isiyoonekana ya mtu ambayo inaendelea kuishi baada ya mtu kufa.

Namna gani wanyama na mimea? Je, wanyama na mimea ni nafsi? Fikiria jinsi Biblia inavyoeleza kuhusu kuumbwa kwa wanyama. “Maji na yajawe na nafsi hai,” Mungu akaamuru. Katika siku ya uumbaji iliyofuata, Mungu alisema: “Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake, mnyama wa kufugwa na mnyama anayetambaa na mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake.” (Mwanzo 1:20, 24) Hivyo, viumbe wote walio hai—wanadamu au wanyama—ni nafsi. Maandiko hayasemi kwamba mimea ni nafsi.

Neno “nafsi” linatumiwa katika maana nyingine pia. Katika Ayubu 33:22, tunasoma hivi: “Nafsi yake inakaribia shimoni, na uhai wake unakaribia waangamizi.” (Union Version) Hapa, maneno “nafsi” na “uhai” yanatumiwa kumaanisha kitu kimoja, na neno “nafsi” linapanua maana ya neno “uhai.” Kwa hiyo, neno “nafsi” linaweza pia kumaanisha uhai wa mtu, akiwa nafsi hai. Hivyo, Maandiko yanasema hivi kuhusu maadui wa Musa waliotaka kumuua: ‘Watu wote waliokuwa wakiiwinda nafsi yake wamekufa.’ (Kutoka 4:19) Na kumhusu Yesu Kristo, Biblia inasema hivi: ‘Mwana wa binadamu alikuja, kutoa nafsi yake, yaani, uhai wake kuwa fidia badala ya wengi.’—Mathayo 20:28.

Biblia inatoa ufafanuzi unaopatana na ulio rahisi wa neno “nafsi.” Neno hilo linaweza kumaanisha mwanadamu au mnyama au uhai wa kiumbe akiwa nafsi hai. Kama tutakavyoona, uelewaji huo unapatana na yale ambayo Biblia inasema kuwa yanaipata nafsi mtu anapokufa.

‘Nafsi Inayotenda Dhambi Itakufa’

Biblia inasema: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4) Nabii Eliya aliyetaabika ‘alianza kuomba kwamba nafsi yake ife.’ (1 Wafalme 19:4) Vivyo hivyo, Yona ‘aliendelea kuomba kwamba nafsi yake ife.’ (Yona 4:8) Ndiyo, nafsi inakufa mtu anapokufa; nafsi inaweza kufa. Kwa kuwa mtu ni nafsi, kusema kwamba mtu alikufa ni kusema kwamba nafsi yake ilikufa.

Lakini namna gani mistari ya Biblia inayosema kuhusu kutoka na kurudi kwa nafsi? Biblia inasema hivi kuhusu kile kilichompata Raheli alipomzaa mwana: “Nafsi yake ilipokuwa ikitoka (kwa sababu alikufa) akamwita jina lake Ben-oni; lakini baba yake akamwita Benyamini.” (Mwanzo 35:18) Na kuhusu ufufuo wa mwana wa mjane, 1 Wafalme 17:22 linasema: “Yehova akaisikiliza sauti ya Eliya [katika sala], hivi kwamba nafsi ya yule mtoto ikarudi ndani yake, akawa hai.” Je, mistari hiyo inaonyesha kwamba nafsi ni kitu fulani kisichoonekana, kisichoweza kuguswa, ambacho kinaondoka au kuingia mwilini?

Kumbuka kwamba maana moja ya neno “nafsi” ni “uhai.” Hivyo, nafsi ya Raheli ilikuwa ikitoka katika maana ya kwamba uhai wake ulikuwa ukifikia mwisho wake. Kwa kweli, katika Biblia fulani maneno “nafsi yake ilipokuwa ikitoka” yametafsiriwa hivi, “uhai wake ulipokuwa unafifia” (Knox) na “alipokuwa akivuta pumzi yake ya mwisho” (Jerusalem Bible). Vivyo hivyo, katika kisa cha mwana wa mjane, uhai ndio uliomrudia mtoto huyo.—1 Wafalme 17:23.

Mtu Ni Nini?

Kwa wazi, Biblia inaonyesha jinsi mtu amefanyizwa. Mtu hana nafsi; yeye ni nafsi. Kwa sababu mwanadamu amefanyizwa kwa njia hiyo, matumaini yoyote ya wafu kuwa hai tena yanategemea ufufuo. Biblia inaahidi hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Ahadi hiyo ya ufufuo iliyo hakika ndiyo msingi wa tumaini hakika kwa ajili ya wafu wala si fundisho la kutokufa kwa nafsi.

Ni jambo la maana kama nini kupata ujuzi sahihi kuhusu ufufuo na umuhimu wake kwa wanadamu! Pia ni muhimu kupata ujuzi juu ya Mungu na Kristo, kwa sababu Yesu alisema hivi katika sala: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kujifunza Biblia ili uongeze ujuzi wako kumhusu Mungu, Mwana wake, na ahadi za Mungu. Tunakualika uzungumze na Mashahidi au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Hawa wote ni nafsi

[Hisani]

Goat: CNPC—Centro Nacional de Pesquisa de Caprinos (Sobral, CE, Brasil)