Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Utaendelea Kutembea Kwa Roho’?

Je, ‘Utaendelea Kutembea Kwa Roho’?

Je, ‘Utaendelea Kutembea Kwa Roho’?

“Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.”—WAGALATIA 5:16.

1. Tunaweza kuondoa jinsi gani wasiwasi kwamba tumeitendea dhambi roho takatifu?

KUNA njia ya kuondoa wasiwasi wa kwamba tumeitendea dhambi roho takatifu ya Yehova. Ni kwa kufanya yale yaliyosemwa na mtume Paulo: “Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.” (Wagalatia 5:16) Tukiacha roho ya Mungu ituongoze, hatutashindwa na tamaa za mwili zisizofaa.—Waroma 8:2-10.

2, 3. Tukiendelea kutembea kwa roho, maisha yetu yatakuwa mazuri katika njia gani?

2 ‘Tunapoendelea kutembea kwa roho,’ nguvu ya utendaji ya Mungu itatuchochea kumtii Yehova. Tutaonyesha sifa za Mungu katika huduma yetu, kutanikoni, nyumbani, na mahali pengine. Matunda ya roho yataonekana wazi tunaposhughulika na mwenzi wetu wa ndoa, watoto wetu, waamini wenzetu, na watu wengine.

3 Kuishi “kuhusiana na roho kwa maoni ya Mungu” kunatuwezesha kuacha dhambi. (1 Petro 4:1-6) Tukiongozwa na roho, bila shaka hatutatenda dhambi isiyoweza kusamehewa. Lakini maisha yetu yatakuwa mazuri katika njia gani nyingine tukiendelea kutembea kwa roho?

Baki Karibu na Mungu na Kristo

4, 5. Kutembea kwa roho kuna matokeo gani juu ya maoni yetu kumhusu Yesu?

4 Kwa sababu tunatembea kwa roho takatifu, tunaweza kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na Mwana wake. Akiandika kuhusu zawadi za kiroho, Paulo aliwaambia hivi waamini wenzake huko Korintho: “Ningetaka [watu walioabudu sanamu zamani] mjue kwamba hakuna mtu yeyote ambaye anaposema kwa roho ya Mungu, husema: ‘Yesu amelaaniwa!’ na hakuna mtu anayeweza kusema: ‘Yesu ni Bwana!’ isipokuwa kwa roho takatifu.” (1 Wakorintho 12:1-3) Roho yoyote inayowachochea watu kumlaani Yesu lazima iwe imetoka kwa Shetani Ibilisi. Hata hivyo, tukiwa Wakristo ambao wanatembea kwa roho takatifu, tunasadiki kabisa kwamba Yehova alimfufua Yesu kutoka kwa wafu na akamweka juu zaidi ya uumbaji mwingine wote. (Wafilipi 2:5-11) Tuna imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo na tunamkubali Yesu kuwa Bwana aliyewekwa rasmi na Mungu juu yetu.

5 Watu fulani waliodai kuwa Wakristo katika karne ya kwanza W.K. walikana kwamba Yesu alikuja katika mwili. (2 Yohana 7-11) Kukubali maoni hayo ya uwongo kuliwafanya wengine wakatae mafundisho ya kweli kumhusu Yesu, yule Masihi. (Marko 1:9-11; Yohana 1:1, 14) Kutembea kwa roho takatifu kunatuzuia tusianguke katika uasi-imani kama huo. Lakini ni kwa kubaki macho kiroho tu ndipo tunaweza kuendelea kupokea fadhili zisizostahiliwa za Yehova na ‘kuendelea kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3, 4) Acheni basi tuazimie kukataa uasi-imani wote ili tuweze kudumisha uhusiano wenye nguvu pamoja na Baba yetu wa mbinguni.

6. Roho ya Mungu inatokeza sifa gani ndani ya wale wanaotembea kwa roho?

6 Paulo alitaja ibada ya sanamu ya uasi-imani na madhehebu kati ya “matendo ya mwili” kama vile uasherati na mwenendo mpotovu. Lakini alieleza hivi: “Wale walio wa Kristo Yesu waliutundika mwili mtini pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Ikiwa tunaishi kwa roho, na tuendelee kutembea kwa utaratibu pia kwa roho.” (Wagalatia 5:19-21, 24, 25) Ni sifa gani ambazo nguvu ya utendaji ya Mungu inatokeza ndani ya wale wanaoishi na kutembea kwa roho? Paulo aliandika hivi: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Wagalatia 5:22, 23) Acheni tuchunguze sifa hizo za matunda ya roho.

“Tuwe Tukipendana”

7. Upendo ni nini, na ni nini baadhi ya sifa zake?

7 Upendo ni moja ya sifa za matunda ya roho. Mara nyingi, sifa hiyo inatia ndani kuwapenda sana wengine, kuwahangaikia bila uchoyo, na kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja nao. Maandiko yanasema kwamba “Mungu ni upendo” kwa sababu yeye ndiye mfano bora zaidi wa sifa hiyo. Upendo mwingi wa Mungu na Mwana wake kwa wanadamu unaonekana wazi katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (1 Yohana 4:8; Yohana 3:16; 15:13; Waroma 5:8) Tukiwa wafuasi wa Yesu, tunatambuliwa kwa upendo tulio nao kati yetu. (Yohana 13:34, 35) Kwa kweli, tunaamriwa “tuwe tukipendana.” (1 Yohana 3:23) Na Paulo anasema kwamba upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Hauna wivu, na haujigambi, haujiendeshi bila adabu, au hautafuti faida zake wenyewe. Upendo hauchokozeki au hauweki hesabu ya ubaya. Unashangilia pamoja na kweli, wala si juu ya ukosefu wa uadilifu. Upendo unahimili, unaamini, na unavumilia mambo yote. Zaidi ya hayo, upendo haushindwi kamwe.—1 Wakorintho 13:4-8.

8. Kwa nini tunapaswa kuwaonyesha upendo waabudu wenzetu wa Yehova?

8 Tukiruhusu roho ya Mungu itokeze upendo ndani yetu, sifa hiyo itaonekana katika uhusiano wetu pamoja na Mungu na jirani. (Mathayo 22:37-39) Mtume Yohana aliandika hivi: “Yeye ambaye hapendi hukaa katika kifo. Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji, nanyi mnajua kwamba hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ukikaa ndani yake.” (1 Yohana 3:14, 15) Muuaji angekuwa salama katika jiji la makimbilio la Israeli ikiwa tu hakumchukia mtu aliyeuawa. (Kumbukumbu la Torati 19:4, 11-13) Tukiongozwa na roho takatifu, tutaonyesha upendo kwa Mungu, waabudu wenzetu, na watu wengine.

“Shangwe ya Yehova Ndiyo Ngome Yenu”

9, 10. Shangwe ni nini, na ni sababu gani mbalimbali zinazofanya tuwe wenye shangwe?

9 Shangwe ni hali ya kuwa na furaha kubwa. Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11; Zaburi 104:31) Mwana wake anafurahia kufanya mapenzi ya Baba yake. (Zaburi 40:8; Waebrania 10:7-9) Na “shangwe ya Yehova ndiyo ngome [yetu].”—Nehemia 8:10.

10 Shangwe inayotoka kwa Mungu inatuletea uradhi mkubwa tunapofanya mapenzi ya Mungu hata katika nyakati za magumu, huzuni, au mateso. “Kumjua Mungu” kunatuletea furaha kama nini! (Methali 2:1-5) Uhusiano wetu wenye shangwe pamoja na Mungu unategemea ujuzi sahihi na imani katika yeye na katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (1 Yohana 2:1, 2) Kuwa sehemu ya undugu wa pekee wa kweli wa ulimwenguni pote ni jambo lingine linalotuletea shangwe. (Sefania 3:9; Hagai 2:7) Tumaini letu la Ufalme na pendeleo kubwa ajabu la kutangaza habari njema linatuletea shangwe. (Mathayo 6:9, 10; 24:14) Pia, tarajio la uzima wa milele linatuletea shangwe. (Yohana 17:3) Kwa kuwa tuna tumaini hilo zuri ajabu, tunapaswa kuwa na “shangwe kwelikweli.”—Kumbukumbu la Torati 16:15.

Uwe Mwenye Kufanya Amani na Mstahimilivu

11, 12. (a) Amani ni nini? (b) Amani ya Mungu ina matokeo gani juu yetu?

11 Amani ni sifa nyingine ya matunda ya roho. Amani ni hali ya utulivu na kutokuwa na wasiwasi. Baba yetu wa mbinguni ni Mungu wa amani, na tunahakikishiwa hivi: “Yehova atawabariki kwa amani watu wake.” (Zaburi 29:11; 1 Wakorintho 14:33) Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninawaachia ninyi amani, ninawapa amani yangu.” (Yohana 14:27) Hilo lingewasaidia wafuasi wake jinsi gani?

12 Amani ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake ilituliza mioyo na akili zao na ilipunguza pia woga wao. Walikuwa hasa na amani walipopokea roho takatifu iliyoahidiwa. (Yohana 14:26) Tunapoongozwa na roho na sala zetu zinapojibiwa leo, tunapata “amani ya Mungu” isiyo na kifani, ambayo inatuliza mioyo na akili zetu. (Wafilipi 4:6, 7) Zaidi ya hayo, roho ya Yehova inatusaidia kuwa watulivu na kufanya amani pamoja na waamini wenzetu na pia watu wengine.—Waroma 12:18; 1 Wathesalonike 5:13.

13, 14. Ustahimilivu ni nini, na kwa nini tunapaswa kuonyesha sifa hiyo?

13 Kuna uhusiano kati ya ustahimilivu na kufanya amani, kwa kuwa ustahimilivu ni kuonyesha uvumilivu wenye subira tunapochokozwa huku tukitumaini kwamba hali zitakuwa bora. Mungu ni mstahimilivu. (Waroma 9:22-24) Yesu pia alionyesha sifa hiyo. Tunaweza kufaidika na sifa hiyo, kwa kuwa Paulo aliandika hivi: “Sababu iliyofanya nionyeshwe rehema ilikuwa kwamba kupitia mimi nikiwa ndiye wa kwanza kabisa Kristo Yesu aonyeshe ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaokuwa na imani yao kwake kwa ajili ya uzima wa milele.”—1 Timotheo 1:16.

14 Sifa ya ustahimilivu inatusaidia kuwavumilia wengine wanaposema au kutenda mambo kwa njia isiyo ya fadhili au bila kufikiri. Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Iweni wenye ustahimilivu kuelekea wote.” (1 Wathesalonike 5:14) Kwa kuwa sisi sote si wakamilifu na tunakosea, bila shaka tunataka watu watuonyeshe subira, wawe wastahimilivu tunapokosea wakati tunaposhughulika nao. Acheni basi tujitahidi “kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.”—Wakolosai 1:9-12.

Onyesha Fadhili na Wema

15. Eleza fadhili ni nini, na utoe mifano ya sifa hiyo.

15 Tunaonyesha fadhili kwa kupendezwa na wengine kwa njia yenye urafiki na kuwasaidia kwa maneno na matendo. Yehova ni mwenye fadhili, na pia Mwana wake. (Waroma 2:4; 2 Wakorintho 10:1) Watumishi wa Mungu na wa Kristo wanapaswa kuwa wenye fadhili. (Mika 6:8; Wakolosai 3:12) Hata watu fulani ambao hawana uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu wameonyesha “fadhili za kibinadamu zisizo za kawaida.” (Matendo 27:3; 28:2) Hivyo basi, tuna hakika kwamba tunaweza kuonyesha fadhili ‘tukiendelea kutembea kwa roho.’

16. Ni hali gani mbalimbali zinazoweza kutuchochea kuonyesha fadhili?

16 Sifa ya fadhili inaweza kuonyeshwa hata ikiwa tuna sababu ya kukasirika mtu fulani anapotuumiza kwa maneno au anapotenda bila kufikiri. Paulo alisema: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi. . . . Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Waefeso 4:26, 27, 32) Ni jambo linalofaa hasa kuwaonyesha fadhili wale wanaopatwa na majaribu. Bila shaka, halitakuwa jambo la fadhili ikiwa mzee Mkristo atashindwa kutoa shauri la Kimaandiko eti kwa sababu anaepuka kuumiza hisia za mtu fulani aliye katika hatari kubwa ya kuacha njia ya “wema na uadilifu na kweli.”—Waefeso 5:9.

17, 18. Wema ni nini, na sifa hiyo inapaswa kuwa muhimu kadiri gani katika maisha yetu?

17 Wema ni ubora wa kiadili, ni sifa au hali ya kuwa mwema. Mungu ni mwema katika maana kamili. (Zaburi 25:8; Zekaria 9:17) Yesu ni mwema naye ana mwenendo au maadili bora. Hata hivyo, hakukubali kupewa cheo cha kuwa “Mwema” wakati alipoitwa “Mwalimu Mwema.” (Marko 10:17, 18) Kwa wazi, alikataa kwa sababu alitambua kwamba Mungu ndiye mfano bora zaidi wa wema.

18 Uwezo wetu wa kutenda wema unazuiwa na dhambi tuliyorithi. (Waroma 5:12) Hata hivyo, tunaweza kuonyesha sifa hiyo tukimwomba Mungu ‘atufundishe wema.’ (Zaburi 119:66) Paulo aliwaambia hivi waamini wenzake huko Roma: “Mimi mwenyewe pia ninasadikishwa juu yenu, ndugu zangu, kwamba ninyi wenyewe mmejaa wema pia, kwa kuwa mmejawa na ujuzi wote.” (Waroma 15:14) Mwangalizi Mkristo anapaswa kuwa “mpenda-wema.” (Tito 1:7, 8) Tukiongozwa na roho ya Mungu, tutajulikana kwa sifa yetu ya wema, na Yehova ‘atatukumbuka kwa ajili ya wema tunaotenda.’—Nehemia 5:19; 13:31.

“Imani Bila Unafiki”

19. Eleza imani ni nini kulingana na Waebrania 11:1.

19 Imani pia ni moja ya matunda ya roho. Imani “ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Tukiwa na imani, tuna hakika kwamba mambo yote ambayo Yehova ameahidi yatatimia hakika. Uthibitisho wenye kusadikisha wa mambo halisi ambayo hayaonekani ni wenye nguvu hivi kwamba imani inaitwa uthibitisho ulio wazi. Kwa mfano, kuwapo kwa vitu vilivyoumbwa kunatusadikisha kwamba kuna Muumba. Hiyo ndiyo aina ya imani ambayo tutaonyesha tukiendelea kutembea kwa roho.

20. Ni nini “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi,” nasi tunaweza kuiepuka dhambi hiyo na matendo ya mwili jinsi gani?

20 Kukosa imani ni “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Waebrania 12:1) Tunahitaji kutegemea roho ya Mungu ili kuepuka matendo ya mwili, kupenda vitu vya kimwili, na mafundisho ya uwongo ambayo yanaweza kuharibu imani. (Wakolosai 2:8; 1 Timotheo 6:9, 10; 2 Timotheo 4:3-5) Roho ya Mungu inatokeza ndani ya watumishi wa Yehova wa sasa imani kama ile ya mashahidi wa kabla ya Ukristo na wengine wanaotajwa katika Biblia. (Waebrania 11:2-40) Na ‘imani yetu isiyo na unafiki’ inaweza kutia nguvu imani ya wengine.—1 Timotheo 1:5; Waebrania 13:7.

Onyesha Upole na Kujizuia

21, 22. Upole ni nini, na kwa nini tunapaswa kuonyesha sifa hiyo?

21 Upole ni kuwa mwanana katika hali yetu ya moyoni na mwenendo. Mojawapo ya sifa za Mungu ni upole wa tabia. Tunajua hilo kwa sababu Yesu, ambaye alikuwa mwanamume mwenye tabia-pole, alionyesha utu wa Yehova kwa ukamilifu. (Mathayo 11:28-30; Yohana 1:18; 5:19) Hivyo basi, tukiwa watumishi wa Mungu tunatakiwa tufanye nini?

22 Tukiwa Wakristo, tunatazamiwa ‘kuonyesha upole kuelekea watu wote.’ (Tito 3:2) Tunaonyesha upole katika huduma yetu. Wale walio na sifa za kustahili kiroho wanashauriwa kumrekebisha upya “katika roho ya upole” Mkristo aliyetenda dhambi. (Wagalatia 6:1) Sisi sote tunaweza kuendeleza umoja na amani ya Kikristo kwa kuonyesha ‘unyenyekevu wa akili na upole.’ (Waefeso 4:1-3) Tunaweza kuonyesha upole tukitembea daima kwa roho na kwa kujizuia.

23, 24. Kujizuia ni nini, na sifa hiyo inatusaidia jinsi gani?

23 Sifa ya kujizuia inatuwezesha kuyadhibiti au kuyazuia mawazo, usemi, na matendo yetu. Yehova ‘aliendelea kujizuia’ aliposhughulika na Wababiloni walioacha Yerusalemu ukiwa. (Isaya 42:14) Mwana wake ‘alituachia kielelezo’ kwa kujizuia alipokuwa akijaribiwa. Na mtume Petro aliwashauri Wakristo wenzake ‘waongeze kwenye ujuzi wao kujizuia.’—1 Petro 2:21-23; 2 Petro 1:5-8.

24 Wazee Wakristo wanatazamiwa waonyeshe sifa ya kujizuia. (Tito 1:7, 8) Kwa kweli, wote wanaoongozwa na roho takatifu wanaweza kuonyesha sifa ya kujizuia na hivyo kuepuka mwenendo mpotovu, usemi mchafu, au jambo lingine lolote linaloweza kuwafanya wapoteze kibali cha Yehova. Tukiruhusu roho ya Mungu itokeze ndani yetu sifa ya kujizuia, sifa hiyo itaonekana wazi kwa wengine kwa sababu tutakuwa na usemi na mwenendo unaompendeza Mungu.

Endelea Kutembea kwa Roho

25, 26. Kutembea kwa roho kutakuwa na matokeo gani katika mahusiano yetu ya sasa na matarajio yetu ya wakati ujao?

25 Tukitembea kwa roho, tutakuwa watangazaji wenye bidii wa Ufalme. (Matendo 18:24-26) Tutakuwa marafiki wazuri, na hasa watu wenye ujitoaji-kimungu watafurahi kushirikiana nasi. Tukiwa watu wanaoongozwa na roho takatifu, tutawatia moyo kiroho pia waabudu wenzetu wa Yehova. (Wafilipi 2:1-4) Je, si wazi kwamba hivyo ndivyo Wakristo wote wanavyotaka kuwa?

26 Si jambo rahisi kutembea kwa roho katika ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani. (1 Yohana 5:19) Hata hivyo, mamilioni ya watu wanafanya hivyo leo. Tukimtegemea Yehova kwa moyo wetu wote, tutafurahia maisha sasa na hivyo tutaweza kuendelea kutembea milele katika njia za uadilifu za Mtoaji mwenye upendo wa roho takatifu.—Zaburi 128:1; Methali 3:5, 6.

Utatoa Jibu Gani?

• “Kutembea kwa roho” kuna matokeo gani katika uhusiano wetu pamoja na Mungu na Mwana wake?

• Matunda ya roho takatifu yanatia ndani sifa gani?

• Tunaweza kuonyesha matunda ya roho ya Mungu katika njia gani mbalimbali?

• Kutembea kwa roho kutakuwa na matokeo gani katika maisha yetu ya sasa na matarajio yetu ya wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Roho takatifu ya Yehova inatuchochea kuwapenda waamini wenzetu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Onyesha fadhili kwa kuwasaidia wengine kwa maneno na matendo