Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuingojea Siku ya Yehova Kwa Uvumilivu

Kuingojea Siku ya Yehova Kwa Uvumilivu

Kuingojea Siku ya Yehova Kwa Uvumilivu

“Ongezeni kwenye imani yenu . . . uvumilivu.”—2 PETRO 1:5, 6.

1, 2. Uvumilivu ni nini, na kwa nini Wakristo wanahitaji sifa hiyo?

SIKU kuu ya Yehova iko karibu sana. (Yoeli 1:15; Sefania 1:14) Tukiwa Wakristo ambao wameazimia kudumisha utimilifu kwa Mungu, tunangojea kwa hamu wakati ambapo enzi kuu ya Yehova itatetewa. Kwa sasa, tunachukiwa, tunashutumiwa, tunateswa, na kuuawa kwa sababu ya imani yetu. (Mathayo 5:10-12; 10:22; Ufunuo 2:10) Hivyo, tunahitaji uvumilivu, yaani, uwezo wa kustahimili hali ngumu. Mtume Petro anatuhimiza hivi: “Ongezeni kwenye imani yenu . . . uvumilivu.” (2 Petro 1:5, 6) Tunahitaji uvumilivu kwa kuwa Yesu alisema: “Yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 24:13.

2 Tunakuwa pia wagonjwa, tunafiwa, na kupata majaribu mengine. Shetani angefurahi sana kuona tukipoteza imani yetu! (Luka 22:31, 32) Tukitegemezwa na Yehova, tunaweza kuvumilia majaribu mbalimbali. (1 Petro 5:6-11) Fikiria masimulizi fulani halisi ambayo yanathibitisha kwamba tunaweza kuingojea siku ya Yehova kwa uvumilivu na imani yenye nguvu.

Ugonjwa Haujawazuia

3, 4. Toa mfano ambao unaonyesha kwamba tunaweza kumtumikia Yehova kwa uaminifu tujapokuwa wagonjwa.

3 Leo, Mungu hatuponyi kimuujiza, lakini anatupa nguvu za kuvumilia magonjwa. (Zaburi 41:1-3) Sharon alisema hivi: “Kwa muda mrefu sana, nimekuwa nikitumia kiti cha magurudumu. Tangu nilipozaliwa, sikufurahia maisha yangu ya utotoni kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza ubongo.” Sharon alipata tumaini alipojifunza kumhusu Yehova na ahadi zake za kuleta afya kamilifu. Ingawa anaongea na kutembea kwa shida, anapata shangwe katika huduma ya Kikristo. Miaka 15 iliyopita, alisema hivi: “Huenda afya yangu ikaendelea kudhoofika, lakini tumaini langu na uhai wangu unategemea uhusiano wangu pamoja na Mungu. Ninafurahi kama nini kuwa kati ya watu wa Yehova na kupata utegemezo wake unaodumu!”

4 Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo huko Thesalonike ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Mambo kama vile kukatishwa tamaa sana yanaweza kumfanya mtu ashuke moyo. Sharon aliandika hivi mwaka wa 1993: ‘Nilishuka moyo kabisa kwa miaka mitatu kwa sababu nilihisi kwamba sifai kamwe. Wazee walinifariji na kunishauri. Kupitia Mnara wa Mlinzi, Yehova alinisaidia kwa upendo kuelewa ugonjwa mbaya wa kushuka moyo. Ndiyo, Yehova anawajali watu wake na anaelewa hisia zetu.’ (1 Petro 5:6, 7) Bado Sharon anamtumikia Mungu kwa uaminifu huku akiingojea siku kuu ya Yehova.

5. Kuna uthibitisho gani kwamba Wakristo wanaweza kuvumilia mfadhaiko mkali?

5 Wakristo fulani wanafadhaika sana kwa sababu ya mambo waliyopitia maishani. Harley aliona mapambano yenye jeuri sana wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu naye aliota ndoto zenye kutisha kuhusu vita. Akiwa katika usingizi, alikuwa akipaaza sauti hivi: “Uwe mwangalifu! Jihadhari!” Alipoamka, mwili wote ulikuwa umejaa jasho. Hata hivyo, aliweza kufuata mwongozo wa Mungu maishani, na pole kwa pole, ndoto zake hazikuwa mbaya sana naye aliota mara chache zaidi.

6. Mkristo mmoja alipambana jinsi gani na matatizo ya kihisia?

6 Ilikuwa vigumu sana kwa Mkristo mmoja aliyekuwa na ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, aliendelea kuhubiri kwa sababu alitambua kwamba huduma hiyo itamwokoa yeye na wale wanaokubali ujumbe wake. (1 Timotheo 4:16) Nyakati nyingine, hangeweza kupiga kengele ya mlango, lakini alisema: “Baada ya muda, ningeweza kuzuia hisia zangu, kwenda kwenye nyumba inayofuata, na kujaribu tena. Kwa kuendelea kushiriki katika huduma, nilidumisha afya nzuri ya kiroho.” Pia, haikuwa rahisi kwa ndugu huyo kuhudhuria mikutano, lakini alijua kabisa faida za ushirika wa kiroho. Kwa hiyo, alijitahidi inavyotakikana ili kuhudhuria mikutano.—Waebrania 10:24, 25.

7. Ingawa Wakristo fulani wanaogopa kuzungumza mbele ya watu au kuhudhuria mkutano, wanaonyesha uvumilivu jinsi gani?

7 Wakristo wengine wanaogopa sana hali au vitu fulani. Kwa mfano, wanaweza kuogopa kuzungumza mbele ya watu au hata kuhudhuria mkutano. Wazia jinsi ilivyo vigumu kwao kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo au kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi! Lakini, wanavumilia, na tunathamini sana wanapohudhuria na kushiriki katika mikutano.

8. Ni nini hasa kinachosaidia kupambana na matatizo ya kihisia?

8 Mtu anaweza kupambana na matatizo ya kihisia kwa kupumzika na kulala zaidi. Huenda ikafaa kumwona daktari. Hata hivyo, jambo linalosaidia zaidi ni kumtegemea Mungu kupitia sala. Zaburi 55:22 inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” Basi, jitahidi kabisa ‘kumtegemea Yehova kwa moyo wako wote.’—Methali 3:5, 6.

Kuvumilia Unapofiwa

9-11. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia hali ya huzuni mpendwa wetu anapokufa? (b) Mfano wa Ana unaweza kutusaidia jinsi gani kuvumilia wakati tunapofiwa?

Kifo kinapotenganisha familia, hasara hiyo kubwa inaweza kusababisha huzuni nyingi sana. Abrahamu alilia kwa sababu ya kifo cha mke wake mpendwa, Sara. (Mwanzo 23:2) Hata mwanamume mkamilifu Yesu ‘alitokwa na machozi’ rafiki yake Lazaro alipokufa. (Yohana 11:35) Kwa hivyo, ni jambo la kawaida kuhuzunika wakati mtu fulani unayempenda anapokufa. Hata hivyo, Wakristo wanajua kwamba kutakuwa na ufufuo. (Matendo 24:15) Kwa hiyo, hawawi na “huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.”—1 Wathesalonike 4:13.

10 Tunaweza kukabiliana jinsi gani na kifo cha mpendwa? Huenda mfano unaofuata ukatusaidia kuelewa. Kwa kawaida hatuhuzuniki kwa muda mrefu wakati rafiki yetu anaposafiri kwa sababu tunatazamia kumwona tena anaporudi. Kuwa na maoni kama hayo kuhusu kifo cha Mkristo mwaminifu kunaweza kupunguza huzuni yetu kwa sababu tunajua kwamba atafufuliwa.—Mhubiri 7:1.

11 Kumtegemea kabisa “Mungu wa faraja yote” kutatusaidia kuvumilia kifo cha mpendwa. (2 Wakorintho 1:3, 4) Pia tutafaidika tukitafakari yale ambayo Ana, mjane aliyeishi katika karne ya kwanza alifanya. Alibaki mjane baada tu ya miaka saba ya ndoa. Lakini akiwa na umri wa miaka 84, bado alikuwa akimtolea Yehova utumishi mtakatifu hekaluni. (Luka 2:36-38) Bila shaka, maisha kama hayo ya kujitolea yalimsaidia kukabiliana na huzuni na upweke. Kushiriki kwa ukawaida katika utendaji wa Kikristo, kutia ndani kazi ya kuhubiri Ufalme, kunaweza kutusaidia kuvumilia huzuni ya kufiwa.

Kupambana na Majaribu Mbalimbali

12. Wakristo fulani wamevumilia majaribu gani yanayohusiana na maisha ya familia?

12 Wakristo fulani wanalazimika kuvumilia majaribu yanayohusiana na maisha ya familia. Kwa mfano, familia inaweza kuumia sana mwenzi akifanya uzinzi. Mwenzi wa ndoa aliyekosewa anaweza kukosa usingizi na kulia kupita kiasi kwa sababu ya huzuni na mfadhaiko. Hata kufanya kazi fulani rahisi kunaweza kumlemea sana hivi kwamba anakosea-kosea au kusababisha hasara. Mwenzi wa ndoa asiye na hatia anaweza kushindwa kula, anaweza kukonda, na anaweza kusumbuka sana kihisia. Huenda ikawa vigumu kwake kushiriki katika utendaji wa Kikristo. Nao watoto wanaweza kupatwa na matokeo mabaya sana.

13, 14. (a) Sala ambayo Sulemani alitoa wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu inakutia moyo jinsi gani? (b) Kwa nini tunasali tupewe roho takatifu?

13 Tunapopatwa na majaribu kama hayo, Yehova anatutolea msaada tunaohitaji. (Zaburi 94:19) Sala ambayo Mfalme Sulemani alitoa wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu la Yehova inaonyesha kwamba Mungu anasikiliza sala za watu wake. Sulemani alisali hivi kwa Mungu: “Sala yoyote, ombi lolote la kutaka kibali ambalo huenda likatolewa na mwanadamu au la watu wako wote Israeli, kwa sababu wanajua kila mmoja wao pigo la moyo wake mwenyewe, nao wanyooshe mikono yao kuelekea nyumba hii, basi na usikie ukiwa mbinguni, makao yako yaliyofanywa imara, nawe usamehe na kutenda na kumpa kila mmoja kulingana na njia zake zote, kwa sababu unaujua moyo wake (kwa maana ni wewe peke yako unayejua vema moyo wa wanadamu wote); kusudi wakuogope siku zote ambazo wako hai juu ya uso wa nchi ambayo uliwapa mababu zetu.”—1 Wafalme 8:38-40.

14 Utafaidika sana ukiendelea kusali upewe roho takatifu. (Mathayo 7:7-11) Matunda ya roho yanatia ndani sifa kama vile shangwe na amani. (Wagalatia 5:22, 23) Tunapata kitulizo kikubwa kama nini wakati Baba yetu wa mbinguni anapojibu sala zetu! Tunakuwa na shangwe badala ya huzuni, na tunakuwa na amani badala ya maumivu makali ya moyoni.

15. Ni maandiko gani yanayoweza kutusaidia kupunguza mahangaiko yetu?

15 Tunaweza kutazamia kuwa na mahangaiko kwa kiasi fulani tunapofadhaika sana. Lakini angalau tunaweza kupunguza mahangaiko hayo tukikumbuka maneno haya ya Yesu: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa . . . . Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:25, 33, 34) Mtume Petro anatuhimiza ‘tutupe mahangaiko yetu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anatujali sisi.’ (1 Petro 5:6, 7) Ni jambo linalofaa kujitahidi kutatua tatizo. Hata hivyo, baada ya kujitahidi kadiri tunavyoweza, kuhangaika juu ya tatizo hilo hakuwezi kutusaidia, lakini sala inaweza kutusaidia. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea, naye mwenyewe atatenda.”—Zaburi 37:5.

16, 17. (a) Kwa nini hatuwezi kuepuka kabisa mahangaiko? (b) Tutapata nini tukifuata andiko la Wafilipi 4:6, 7?

16 Paulo aliandika hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Bila shaka, wazao wasio wakamilifu wa Adamu hawawezi kuepuka kabisa mahangaiko. (Waroma 5:12) Wake Wahiti wa Esau “walikuwa chanzo cha uchungu wa roho” kwa Isaka na Rebeka, wazazi wake waliomwogopa Mungu. (Mwanzo 26:34, 35) Bila shaka, Wakristo kama vile Timotheo na Trofimo walihangaika kwa sababu ya magonjwa. (1 Timotheo 5:23; 2 Timotheo 4:20) Paulo alikuwa na mahangaiko kwa ajili ya waamini wenzake. (2 Wakorintho 11:28) Lakini “Msikiaji wa sala” yuko tayari sikuzote kuwasaidia wale wanaompenda.—Zaburi 65:2.

17 Tunapoingojea siku ya Yehova, tunategemezwa na kufarijiwa na “Mungu wa amani.” (Wafilipi 4:9) Yehova ni “mwenye rehema na neema,” naye ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe,’ na ‘anakumbuka kwamba sisi ni mavumbi.’ (Kutoka 34:6; Zaburi 86:5; 103:13, 14) Kwa hiyo, acheni ‘maombi yetu yajulishwe kwa Mungu,’ kwa sababu tukifanya hivyo tutapata “amani ya Mungu,” yaani, utulivu ambao unazidi fikira zote za wanadamu.

18. Kulingana na Ayubu 42:5, tunaweza ‘kumwona’ Mungu jinsi gani?

18 Sala zetu zinapojibiwa, tunajua kwamba Mungu yupo pamoja nasi. Baada ya Ayubu kuvumilia majaribu yake, alisema hivi: “Nimesikia habari zako [Yehova] kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.” (Ayubu 42:5) Kwa jicho la ufahamu, imani, na shukrani, tunaweza kutafakari mambo ambayo Mungu ametutendea na tunaweza ‘kumwona’ kwa njia ambayo hatujawahi kamwe kumwona. Kwa kweli, uhusiano huo wa karibu unatuletea amani ya moyo na akili!

19. Ni nini kitakachotukia ‘tukimtupia Yehova mahangaiko yetu yote’?

19 ‘Tukimtupia Yehova mahangaiko yetu yote,’ tunaweza kuvumilia majaribu tukiwa na amani ya ndani ambayo inalinda moyo na uwezo wetu wa kufikiri. Ndani kabisa ya moyo wetu wa mfano, tutahisi tukiwa huru kutokana na wasiwasi, woga, na mahangaiko. Akili yetu haitavurugika wala kulemewa na mahangaiko.

20, 21. (a) Kisa cha Stefano kinaonyesha jinsi gani kwamba mtu anaweza kuwa mtulivu anapokabili mateso? (b) Simulia mfano wa siku zetu wa mtu aliyevumilia majaribu kwa utulivu.

20 Mwanafunzi Stefano alikuwa mtulivu alipokuwa akikabili jaribu kali la imani yake. Kabla hajatoa ushahidi wa mwisho, watu wote waliokuwa katika Sanhedrini ‘waliona kwamba uso wake ulikuwa kama uso wa malaika.’ (Matendo 6:15) Uso wake ulikuwa mtulivu kama uso wa malaika, mjumbe wa Mungu. Baada ya Stefano kufunua kwamba walikuwa na hatia kuhusiana na kifo cha Yesu, waamuzi hao “wakahisi wamechomwa mioyoni mwao na kuanza kumsagia meno yao.” “Akiwa amejaa roho takatifu,” Stefano “akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” Stefano alitiwa nguvu na maono hayo, naye akawa mwaminifu mpaka kifo. (Matendo 7:52-60) Ingawa hatupati maono, tunaweza kuwa na amani ya Mungu tunapoteswa.

21 Fikiria maelezo ya Wakristo fulani ambao waliuawa na Wanazi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mmoja wao alisema hivi alipokuwa akisimulia mambo yaliyompata mahakamani: “Hukumu ya kifo ilipitishwa. Nilisikiliza, na baada ya kusema maneno, ‘Uwe mwaminifu mpaka kifo,’ na maneno mengine machache ya Bwana wetu, mambo yalikwisha. Lakini sasa msiwe na wasiwasi. Nina amani na utulivu ambao hamwezi kamwe kuwazia!” Mkristo mmoja kijana ambaye angeuawa kwa kukatwa kichwa aliwaandikia hivi wazazi wake: “Tayari usiku wa manane umepita. Ningali na wakati wa kubadili msimamo wangu. Aa! je, kweli ninaweza tena kuwa na furaha katika ulimwengu huu baada ya kumkana Bwana wetu? Bila shaka, siwezi! Lakini sasa mna uhakikisho wa kwamba ninauacha ulimwengu huu kwa furaha na amani.” Bila shaka, Yehova anawategemeza watumishi wake washikamanifu.

Unaweza Kuvumilia!

22, 23. Unaweza kuwa na uhakika gani unapoingojea siku ya Yehova kwa uvumilivu?

22 Huenda usipate matatizo fulani ambayo tumezungumzia. Hata hivyo, Ayubu aliyemwogopa Mungu alisema hivi: “Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko.” (Ayubu 14:1) Labda wewe ni mzazi na unajitahidi kabisa kuwapa watoto wako mwongozo wa kiroho. Wanalazimika kuvumilia majaribu shuleni, lakini unafurahi kama nini wakati wanaposhikamana na Yehova na kanuni zake za uadilifu! Labda unapata magumu na vishawishi kazini. Hata hivyo, unaweza kuvumilia hali hizo na nyingine kwa sababu ‘Yehova anakubebea mzigo wako kila siku.’—Zaburi 68:19.

23 Huenda ukajiona kuwa mtu wa kawaida tu, lakini kumbuka kwamba Yehova hatasahau kamwe kazi yako na upendo unaoonyesha kwa ajili ya jina lake takatifu. (Waebrania 6:10) Kwa msaada wake, unaweza kuvumilia majaribu ya imani. Kwa hiyo, sali kuhusu mapenzi ya Mungu na uyatilie maanani unapofanya mipango yako. Ukifanya hivyo unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakubariki na kukutegemeza unapoingojea siku yake kwa uvumilivu.

Ungetoa Jubu Gani?

• Kwa nini Wakristo wanahitaji uvumilivu?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia tunapokuwa wagonjwa au tunapofiwa?

• Sala inatusaidia jinsi gani kuvumilia majaribu?

• Kwa nini tunaweza kuingojea siku ya Yehova kwa uvumilivu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kumtegemea Yehova kunatuwezesha kuvumilia tunapofiwa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Sala ya kutoka moyoni inatusaidia kuvumilia majaribu ya imani