Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa mavuno yalianza rasmi wakati wanaume wote Waisraeli walipokuwa wakihudhuria Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, ni nani aliyevuna matunda ya kwanza ya shayiri ambayo yaliletwa katika patakatifu?

Sheria ya Musa iliwaagiza hivi Waisraeli: “Mara tatu katika mwaka kila mwanamume wa kwako ataonekana mbele za Yehova Mungu wako katika mahali ambapo atapachagua: katika sherehe ya keki zisizo na chachu na katika sherehe ya majuma na katika sherehe ya vibanda.” (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kuanzia wakati wa Mfalme Sulemani na kuendelea, hekalu la Yerusalemu lilikuwa mahali ambapo Mungu alichagua.

Sherehe ya kwanza kati ya sherehe hizo tatu ilifanywa mwanzoni mwa majira ya kuchipua. Sherehe hiyo iliitwa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, nayo ilianza siku iliyofuata sherehe ya Pasaka mnamo Nisani 14 na ikaendelea kwa siku saba mpaka Nisani 21. Siku ya pili ya sherehe hiyo, Nisani 16, ilikuwa mwanzo wa mavuno ya kwanza ya mwaka kulingana na kalenda takatifu. Siku hiyo, kuhani mkuu alipaswa kuchukua “mganda wa matunda ya kwanza” ya mavuno ya shayiri na kuutikisa “huku na huku, mbele za Yehova” katika patakatifu. (Mambo ya Walawi 23:5-12) Kwa kuwa wanaume wote walipaswa kuhudhuria Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, ni nani aliyevuna matoleo hayo?

Amri ya kutoa matunda ya kwanza ya mavuno kwa Yehova wakati wa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ilitolewa kwa taifa lote. Kila mtu hakuhitajiwa kuanza kuvuna na kuleta matunda ya kwanza kwa ajili yake mwenyewe katika patakatifu. Badala yake, taifa hilo liliamriwa lifanye hivyo kupitia watu fulani walioliwakilisha taifa lote. Hivyo, mganda wa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ungekatwa na wajumbe waliotumwa katika shamba la karibu la shayiri. Kitabu kimoja (Encyclopaedia Judaica) kinasema hivi kuhusu jambo hilo: “Ikiwa shayiri ilikuwa imekomaa ilichukuliwa kutoka karibu na Yerusalemu; kama sivyo ingeletwa kutoka sehemu yoyote ya Israeli. Ilivunwa na wanaume watatu, kila mmoja wao alikuwa na mundu wake na kikapu.” Kisha, mganda wa shayiri uliletwa kwa kuhani mkuu, ambaye aliutoa kwa Yehova.

Takwa la kutoa matunda ya kwanza ya mavuno liliwapa Waisraeli nafasi nzuri sana ya kuonyesha kwamba walithamini jinsi ambavyo Mungu alibariki nchi yao na mavuno yao. (Kumbukumbu la Torati 8:6-10) Hata hivyo, kwa kuongezea, toleo hilo la sherehe lilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja.” (Waebrania 10:1) Kwa kweli, Yesu Kristo alifufuliwa mnamo Nisani 16 mwaka wa 33 W.K., siku ya kutoa matunda ya kwanza ya mavuno kwa Yehova. Mtume Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo. . . . Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:20-23) Mganda wa matunda ya kwanza ambao kuhani mkuu alitikisa huku na huku mbele za Yehova ulifananisha Yesu Kristo aliyefufuliwa, mtu wa kwanza kabisa kufufuliwa kutoka kwa wafu na kupata uzima wa milele. Hivyo, Yesu alifungua njia ya kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo.

[Picha katika ukurasa wa 26 zimeandaliwa na]

© 2003 BiblePlaces.com