Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hali ya Kiroho ya Kweli Unaweza Kuipata Jinsi Gani?

Hali ya Kiroho ya Kweli Unaweza Kuipata Jinsi Gani?

Hali ya Kiroho ya Kweli Unaweza Kuipata Jinsi Gani?

“KWA maana kukaza akili juu ya mwili humaanisha kifo, bali kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 8:6) Kwa maneno hayo, mtume huyo alikuwa akionyesha kwamba kuwa mtu wa kiroho si suala tu la mapendezi na mtazamo wa kibinafsi wa mtu. Kwa kweli hilo ni suala la uzima na kifo. Hata hivyo, mtu wa kiroho anapata “uzima na amani” jinsi gani? Kulingana na Biblia, mtu kama huyo ana amani moyoni mwake na pamoja na Mungu, naye atapata baraka ya uzima wa milele wakati ujao. (Waroma 6:23; Wafilipi 4:7) Haishangazi kwamba Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Uhakika wa kwamba unasoma gazeti hili unaonyesha kuwa unapendezwa na hali ya kiroho, na hilo ni jambo la hekima. Hata hivyo, kwa kuwa watu wana maoni yanayotofautiana sana kuhusu hali ya kiroho, huenda ukajiuliza: ‘Hali ya kiroho ya kweli ni nini? Mtu anaweza kuipata jinsi gani?’

“Akili ya Kristo”

Zaidi ya kuonyesha umuhimu na faida za kukaza akili juu ya mambo ya kiroho, mtume Paulo alisema mengi kuhusu maana ya hali ya kiroho ya kweli. Paulo aliwaeleza Wakristo katika jiji la kale la Korintho tofauti iliyopo kati ya mtu wa kimwili, yaani, mtu anayefuata tamaa za mwili, na mtu wa kiroho, yule anayethamini mambo ya kiroho. Paulo aliandika: “Mtu wa kimwili hayapokei mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake.” Kwa upande mwingine, Paulo alieleza kwamba mtu wa kiroho ana “akili ya Kristo.”—1 Wakorintho 2:14-16.

Kuwa na “akili ya Kristo” kunamaanisha hasa kuwa na ‘mtazamo wa akili ambao ulikuwa pia ndani ya Kristo Yesu.’ (Waroma 15:5; Wafilipi 2:5) Kwa maneno mengine, mtu wa kiroho ni yule anayefikiri kama Yesu na anayetembea katika hatua Zake. (1 Petro 2:21; 4:1) Kadiri akili ya mtu inavyopatana na ya Kristo, ndivyo anavyozidi kuwa mtu wa kiroho na kukaribia zaidi kupata “uzima na amani.”—Waroma 13:14.

Jinsi ya Kujua “Akili ya Kristo”

Hata hivyo, ili kuwa na akili ya Kristo, mtu anapaswa kwanza kuijua akili hiyo. Hivyo, hatua ya kwanza ya kusitawisha hali ya kiroho ni kujua njia ya Yesu ya kufikiri. Lakini unaweza kujua namna gani njia ya kufikiri ya mtu aliyeishi duniani miaka 2,000 iliyopita? Kwa mfano, ulijifunza jinsi gani kuhusu watu fulani katika historia ya nchi yenu? Inaelekea ulisoma habari kuwahusu. Vivyo hivyo, kusoma historia iliyoandikwa kumhusu Yesu ni njia muhimu ya kujua akili ya Kristo.—Yohana 17:3.

Kuna masimulizi manne yaliyo wazi ya kihistoria kumhusu Yesu, yaani, vitabu vya Injili vilivyoandikwa na Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Kusoma masimulizi hayo kwa makini kutakusaidia ufahamu njia ya Yesu ya kufikiri, hisia zake za ndani, na kilichomchochea kutenda. Unapotafakari kuhusu yale unayojifunza kumhusu Yesu, utaanza kuwazia akilini Yesu alikuwa mtu wa aina gani. Hata ikiwa unajiona kuwa mfuasi wa Kristo, kusoma na kutafakari habari hiyo kutakusaidia ‘uendelee kukua katika fadhili zisizostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.’—2 Petro 3:18.

Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze mafungu fulani ya Injili ili tuone kilichomfanya Yesu awe mtu wa kiroho. Kisha, jiulize unaweza kufanya nini ili kuiga mfano alioweka.—Yohana 13:15.

Hali ya Kiroho na “Matunda ya Roho”

Luka, mwandikaji wa Injili, alisema kwamba Yesu alipobatizwa, alimiminiwa roho ya Mungu na kwamba Yesu alikuwa “amejaa roho takatifu.” (Luka 3:21, 22; 4:1) Naye Yesu alikazia akilini mwa wafuasi wake umuhimu wa kuongozwa na roho takatifu ya Mungu, au ‘nguvu zake za utendaji.’ (Mwanzo 1:2; Luka 11:9-13) Kwa nini hilo ni jambo la maana? Ni kwa sababu roho ya Mungu ina nguvu ya kubadili akili ya mtu, ili ianze kufanana na akili ya Kristo. (Waroma 12:1, 2) Roho takatifu inatokeza ndani ya mtu sifa kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” Sifa hizo, ambazo Biblia inaziita “matunda ya roho,” zinaonyesha kwamba mtu fulani ni mtu wa kiroho kikweli. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa ufupi, mtu aliye makini kiroho ni yule anayeongozwa na roho ya Mungu.

Yesu alionyesha matunda ya roho wakati wote wa huduma yake. Sifa kama vile upendo, fadhili, na wema zilionekana wazi aliposhughulika na wale ambao walionwa kuwa watu wa hali ya chini katika jamii. (Mathayo 9:36) Kwa mfano, fikiria kisa kinachosimuliwa na mtume Yohana. Tunasoma hivi: “[Yesu] alipokuwa akipita alimwona mtu aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa.” Wanafunzi wa Yesu pia walimwona lakini walimwona kuwa mtenda dhambi. “Ni nani aliyetenda dhambi,” wakauliza, “ni mtu huyu au wazazi wake?” Majirani wake pia walimwona, lakini machoni pao alikuwa mwombaji tu. “Je, huyu siye yule mtu aliyekuwa akiketi na kuombaomba?” walisema. Hata hivyo, Yesu alimwona kipofu huyo kuwa mtu aliyehitaji msaada. Alizungumza naye na kumponya.—Yohana 9:1-8.

Kisa hicho kinakufundisha nini kuhusu akili ya Kristo? Kwanza, Yesu hakuwapuuza watu wa hali ya chini bali aliwatendea kwa huruma nyororo. Pili, alichukua hatua ya kuwasaidia wengine. Je, unafikiri kwamba unafuata mfano wa Yesu? Je, unawaona watu jinsi Yesu alivyowaona, ukiwapa msaada wanaohitaji ili kuboresha maisha yao na kuwa na tumaini zuri la wakati ujao? Au unapendelea wale walio mashuhuri na kuwapuuza watu wa hali ya chini? Ikiwa unawaona watu jinsi Yesu alivyowaona, unafuata mfano wake.—Zaburi 72:12-14.

Hali ya Kiroho na Sala

Masimulizi ya Injili yanaonyesha kwamba Yesu alisali kwa Mungu kwa ukawaida. (Marko 1:35; Luka 5:16; 22:41) Katika huduma yake hapa duniani, Yesu alitenga wakati wa kusali. Mwanafunzi Mathayo aliandika: “Baada ya kuwaruhusu umati waende zao, [Yesu] akapanda mlimani akiwa peke yake ili kusali.” (Mathayo 14:23) Yesu alipata nguvu kutokana na pindi hizo tulivu ambazo alitumia kuzungumza na Baba yake wa mbinguni. (Mathayo 26:36-44) Vivyo hivyo leo, watu walio makini kiroho wanatafuta nafasi za kuzungumza na Mungu, wakijua kwamba hilo litaimarisha uhusiano wao na Muumba na kuwawezesha kuwa na akili kama ya Kristo.

Mara nyingi Yesu alisali kwa muda mrefu. (Yohana 17:1-26) Kwa mfano, kabla ya kuwachagua wanaume 12 waliokuja kuwa mitume wake, Yesu “alienda mlimani kusali, naye akaendelea kusali kwa Mungu usiku wote.” (Luka 6:12) Ingawa si lazima wasali usiku wote, wale walio makini kiroho wanafuata mfano wa Yesu. Kabla ya kufanya maamuzi makubwa maishani, wanatumia muda wa kutosha kusali kwa Mungu, wakiomba roho takatifu iwaongoze kufanya maamuzi yatakayoboresha hali yao ya kiroho.

Kupitia sala zake, Yesu alionyesha bidii ambayo tunapaswa kuwa nayo tunaposali. Ona yale ambayo Luka aliandika kuhusu jinsi Yesu alivyosali jioni iliyotangulia kifo chake. “Akaingia katika maumivu makali, akaendelea kusali kwa bidii zaidi; na jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka chini.” (Luka 22:44) Yesu aliwahi kusali kwa bidii, lakini pindi hii, akikabili jaribu kali zaidi katika maisha yake hapa duniani, alisali “kwa bidii zaidi” na sala yake ikajibiwa. (Waebrania 5:7) Watu walio makini kiroho wanafuata mfano wa Yesu. Wanapokabili majaribu makali zaidi, wanasali “kwa bidii zaidi” kwa Mungu ili awape roho takatifu, mwongozo, na utegemezo.

Kwa kuwa ni wazi kwamba Yesu alisali mara nyingi, haishangazi kwamba wanafunzi wake walitaka kumwiga. Hivyo, walimwomba hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Vivyo hivyo leo, wale wanaothamini mambo ya kiroho na wanataka kuongozwa na roho takatifu ya Mungu wanafuata mfano wa Yesu wanaposali kwa Mungu. Hali ya kiroho ya kweli inahusiana sana na sala.

Hali ya Kiroho na Kuhubiri Habari Njema

Katika Injili ya Marko, tunapata masimulizi ya Yesu akiwaponya wagonjwa wengi, kazi ambayo alifanya mpaka usiku sana. Asubuhi na mapema siku iliyofuata, alipokuwa peke yake akisali, mitume wake walimjia na kumwambia kwamba watu wengi walikuwa wakimtafuta, labda wakitaka kuponywa. Hata hivyo, Yesu aliwaambia: “Twendeni mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia.” Kisha Yesu akaeleza kwa nini: “Kwa maana nilitoka kwa kusudi hilo.” (Marko 1:32-38; Luka 4:43) Ijapokuwa Yesu aliona kuponya watu kuwa jambo la maana, kazi yake kuu ilikuwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Marko 1:14, 15.

Leo, bado kazi ya kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu inawatambulisha wale walio na akili ya Kristo. Yesu aliwapa amri hii watu wote wanaotaka kuwa wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kwa kuongezea, Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kwa kuwa Neno la Mungu linaonyesha kwamba kazi ya kuhubiri inafanywa kwa nguvu za roho takatifu, kushiriki kwa bidii katika kazi hiyo kunaonyesha kwamba mtu ana hali ya kiroho ya kweli.—Matendo 1:8.

Jitihada za mamilioni ya watu zinahitajiwa ili kuwahubiria watu ulimwenguni pote ujumbe wa Ufalme. (Yohana 17:20, 21) Wale wanaofanya kazi hii hawahitaji tu kuwa makini kiroho bali pia wanahitaji kufuata utaratibu mzuri ulimwenguni pote. Je, unaweza kuwatambua watu wanaofuata hatua za Kristo na kuhubiri habari njema ya Ufalme ulimwenguni pote?

Je, Unatimiza Matakwa Hayo?

Bila shaka, kuna mambo mengine yanayomtambulisha yule ambaye kwa kweli ni mtu wa kiroho, lakini je, unatimiza matakwa ambayo tumezungumzia? Ili kujibu swali hilo, jiulize: ‘Je, ninasoma Neno la Mungu, Biblia, na kutafakari mambo ninayosoma? Je, ninaonyesha matunda ya roho katika maisha yangu? Je, ninasali kwa ukawaida? Je, ninataka kushirikiana na watu wanaohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote?’

Kujichunguza kwa unyoofu kunaweza kukusaidia kujua kina cha hali yako ya kiroho. Tunakuhimiza uchukue sasa hatua zinazohitajiwa ili upate “uzima na amani.”—Waroma 8:6; Mathayo 7:13, 14; 2 Petro 1:5-11.

[Picha/Sanduku katika ukurasa wa 7]

ALAMA ZA HALI YA KIROHO

◆ Kupenda Neno la Mungu

◆ Kuonyesha matunda ya roho

◆ Kusali kwa Mungu kwa ukawaida na kwa bidii

◆ Kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 5]

Biblia inakusaidia kujua “akili ya Kristo”