Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani ya Mama Mmoja Inashinda Msiba

Imani ya Mama Mmoja Inashinda Msiba

Imani ya Mama Mmoja Inashinda Msiba

“Ikiwa mnasoma barua hii, hilo linamaanisha kwamba sikuendelea kuishi baada ya upasuaji na kwamba sipo tena pamoja nanyi.”

HAYO ni maneno ya utangulizi ya barua ambayo mama mmoja Mkristo, Carmen, aliwaandikia mabinti wake watatu wenye umri wa miaka 25, 19, na 16. Kwa kweli, upasuaji huo haukufanikiwa, na inasikitisha kwamba Carmen alikufa.

Kwa kweli, inasikitisha sana kuacha mabinti watatu katika hali yenye kuhuzunisha kama hiyo. Hata hivyo, ni wazi kwamba imani yenye nguvu ya mama huyo katika Yehova na ahadi zake ilishinda msiba huo. Imani hiyo ilimwezesha kuwa na amani ya ndani ambayo inaonekana wazi katika barua yake yenye kugusa moyo. Ona yale aliyowaambia mabinti wake.

“Kwanza kabisa, ninataka kuwaambia kwamba ninawapenda kwa moyo wangu wote. . . . Ninyi ni mabinti wazuri sana ambao mama yeyote anaweza kupata, nami najivunia kuwa nanyi.

“Ningependa kuendelea kuishi pamoja nanyi mpaka ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa . . . , lakini kwa kuwa hilo haliwezekani, nimemwomba Mungu awasaidie ili muwe waaminifu, kama vile ambavyo mmekuwa. Tumevumilia majaribu mengi pamoja, na Yehova hajawahi kamwe kutuacha. . . . Kwa hiyo, endeleeni kutegemea mwongozo ambao anaandaa kupitia tengenezo lake na endeleeni kuunga mkono kutaniko na wazee. Mhubiri mara nyingi kadiri mnavyoweza na muwapende ndugu wote.

“Kutengana kwetu ni kwa muda tu. . . . Ninawaomba mnisamehe kwa makosa yote niliyofanya na kwa wakati wote ambao sikuwaelewa au sikuwaambia ni kwa kadiri gani niliwapenda sana. . . . Ninajua kwamba kila mmoja wenu ana mahitaji yake mwenyewe. Yehova anajua mahitaji yenu kuliko mnavyoyajua, naye atawapa kila kitu mnachohitaji na atawathawabisha kwa yote ambayo mmevumilia.

“Msisahau kamwe mradi wenu, yaani, uzima katika ulimwengu mpya. Endeleeni kujitahidi kuufikia. Yehova na awabariki na kuwatia nguvu ili muwe waaminifu mpaka mwisho. . . . Msihuzunike, mabinti wangu wenye thamani. Ninawapenda!”

Msiba unaweza kumpata mtu yeyote wakati wowote. “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote,” akaandika Mfalme Sulemani wa kale. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, wale walio na imani yenye nguvu katika Mungu, wanaweza kuwa na uhakikisho uleule kama wa mtume Paulo, aliyesema hivi: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima . . . wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 8:38, 39; Waebrania 6:10.