Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?

Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?

Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?

“Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—LUKA 12:21.

1, 2. (a) Watu wamekuwa tayari kujidhabihu sana ili kupata nini? (b) Ni lazima Wakristo wakabili hatari na hali gani ngumu?

KUTAFUTA HAZINA si kama mchezo wa kutafuta kitu kilichofichwa ambao watoto wanapenda kucheza. Kwa miaka mingi sana na katika jamii nyingi watu wamekuwa wakitafuta hazina halisi. Kwa mfano, katika karne ya 19 juhudi za kuhamia katika maeneo yenye migodi ya dhahabu huko Australia, Afrika Kusini, Kanada, na Marekani ziliwavutia watu kutoka sehemu za mbali sana. Watu hao walikuwa tayari kuacha wapendwa wao na makao yao ili kutafuta utajiri katika nchi za kigeni ambazo nyakati nyingine zilikuwa na hali ngumu sana. Ndiyo, watu wengi wako tayari kujihatarisha kabisa na kujidhabihu sana ili kupata utajiri ambao mioyo yao inatamani.

2 Ingawa watu wengi leo hawatafuti hazina kihalisi, wanalazimika kujitahidi sana ili kupata mahitaji ya lazima. Kufanya hivyo katika mfumo huu wa mambo kunaweza kuwa jambo gumu, lenye kuchosha, na lenye kulemea sana. Ni rahisi kuhangaikia sana chakula, mavazi, na makao hivi kwamba tunapuuza au hata kusahau mambo yaliyo ya maana zaidi. (Waroma 14:17) Yesu alitoa mfano ambao unaonyesha wazi kabisa mwelekeo huo wa wanadamu. Mfano huo uko katika andiko la Luka 12:16-21.

3. Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu katika Luka 12:16-21.

3 Yesu alitoa mfano huo wakati uleule alipozungumzia uhitaji wa kujilinda na tamaa, ambao tulizungumzia kwa undani katika habari iliyotangulia. Baada ya kutoa onyo kuhusu tamaa, Yesu alitoa mfano wa mtu tajiri ambaye hatosheki na maghala yaliyojaa vitu vyema ambavyo tayari alikuwa amekusanya, badala yake anabomoa maghala hayo na kujenga maghala makubwa zaidi ili akusanye vitu vyema vingi zaidi. Wakati tu anapofikiri kwamba sasa anaweza kupumzika na kujifurahisha, Mungu anamwambia kwamba uhai wake unafikia mwisho, na vitu vyote vyema ambavyo ameweka akiba vitachukuliwa na mwingine. Kisha Yesu anamalizia kwa maneno haya: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:21) Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na mfano huo? Tunaweza kutumia jinsi gani somo hilo katika maisha yetu?

Mtu Mwenye Tatizo

4. Tunaweza kusema mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alikuwa mtu wa aina gani?

4 Watu wengi wanajua mfano huo ambao Yesu alitoa. Tunaona kwamba Yesu alianza kusimulia mfano huo kwa maneno haya: “Shamba la mtu fulani tajiri lilizaa vizuri.” Yesu hakusema kwamba mtu huyo alipata utajiri wake kwa udanganyifu au kwa njia isiyo halali. Kwa maneno mengine, hakusema kwamba mtu huyo alikuwa mbaya. Kwa kweli, kutokana na maneno ya Yesu, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba mtu huyo alikuwa amefanya kazi kwa bidii. Angalau inaweza kuonekana kwamba alikuwa mtu ambaye alifanya mipango na kuweka akiba kwa ajili ya wakati ujao, labda ili familia yake iwe na maisha mazuri. Hivyo, kwa maoni ya watu, anaweza kuonwa kuwa mtu mwenye bidii ambaye alichukua wajibu wake kwa uzito.

5. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alikabili tatizo gani?

5 Kwa vyovyote vile, katika mfano huo Yesu alimwita mtu huyo tajiri, yaani, mtu ambaye tayari alikuwa na vitu vingi vya kimwili. Hata hivyo, kama Yesu alivyoeleza, tajiri huyo alikuwa na tatizo. Shamba lake lilizaa mazao mengi kuliko alivyotazamia, mengi zaidi kuliko kiasi alichohitaji au ambacho angeweza kutunza. Angefanya nini?

6. Watumishi wengi wa Mungu leo wanakabili maamuzi gani?

6 Watumishi wengi wa Yehova leo wanakabili hali ambayo inalingana sana na ya tajiri huyo. Wakristo wa kweli wanajitahidi kuwa wanyoofu, wenye bidii, na wafanyakazi wenye kutegemeka. (Wakolosai 3:22, 23) Iwe wameajiriwa kazi au wana biashara zao wenyewe, mara nyingi wanafaulu na hata kufanikiwa sana katika kazi yao. Wanahitaji kufanya uamuzi wanapopewa nafasi ya kupandishwa cheo au kupata nafasi mpya za biashara. Je, wakubali vyeo hivyo au nafasi hizo za kupata pesa zaidi? Vivyo hivyo, vijana wengi Mashahidi wanafanya vizuri shuleni. Kwa sababu hiyo, wanaweza kupewa nafasi ya kupata elimu ya juu katika vyuo maarufu. Je, wanapaswa kukubali tu nafasi hizo kama watu wengi wanavyofanya?

7. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alitatua tatizo lake jinsi gani?

7 Tukichunguza tena mfano wa Yesu, yule mtu tajiri alifanya nini wakati shamba lake lilipozaa vizuri hivi kwamba hakuwa na mahali pa kuweka mavuno yake? Aliamua kubomoa maghala ambayo alikuwa nayo na kujenga makubwa zaidi ili aweke akiba nafaka yake yote ya ziada na vitu vyema. Inaonekana alitosheka na mpango huo na kujihisi akiwa salama hivi kwamba akawaza: “Nami nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.’”—Luka 12:19.

Kwa Nini ‘Hakuwa na Akili’?

8. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alipuuza jambo gani la maana?

8 Hata hivyo, kama Yesu alivyoonyesha, mipango ya mtu huyo tajiri ilimfanya ahisi usalama usio wa kweli. Ingawa huenda mipango hiyo ilionekana kuwa mizuri, mtu huyo alipuuza jambo fulani la maana, yaani, mapenzi ya Mungu. Mtu huyo alikuwa akijifikiria mwenyewe tu, jinsi ambavyo angestarehe na kula, kunywa, na kujifurahisha. Alifikiri kwamba kwa sababu alikuwa na ‘vitu vingi vyema’ angeishi pia “miaka mingi.” Lakini inasikitisha kwamba mambo hayakuwa hivyo. Kama tu Yesu alivyosema mapema, “hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Usiku huohuo, jitihada zote za mtu huyo zilifikia mwisho ghafula, kwa sababu Mungu alimwambia hivi: “Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?”—Luka 12:20.

9. Kwa nini yule mtu katika mfano wa Yesu aliitwa asiye na akili?

Sasa tumefikia jambo kuu la mfano wa Yesu. Mungu alisema kwamba mtu huyo hakuwa na akili. Kamusi moja (Exegetical Dictionary of the New Testament) inaeleza kwamba namna mbalimbali za neno la Kigiriki linalotumiwa hapo “sikuzote zinamaanisha kutoelewa.” Kamusi hiyo inasema kwamba katika mfano huo, Mungu anatumia neno hilo ili kuonyesha kwamba “mipango ya wakati ujao ya tajiri haina maana yoyote.” Neno hilo linahusu “mtu ambaye anakataa kumtegemea Mungu” wala si mtu ambaye si mwerevu. Maelezo ya Yesu kumhusu yule mtu tajiri yanatukumbusha yale ambayo aliwaambia baadaye Wakristo wa kutaniko la karne ya kwanza la Laodikia, huko Asia Ndogo: “Unasema: ‘Mimi ni tajiri, nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote hata kidogo,’ lakini hujui kwamba wewe ni mwenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.”—Ufunuo 3:17.

10. Kwa nini kuwa na “vitu vyema vingi” si uhakikisho wa kuishi “miaka mingi”?

10 Tunapaswa kufikiria kwa uzito somo la mfano huo. Je, tunaweza kuwa kama mtu aliye katika mfano huo na kufanya kazi kwa bidii sana ili kuhakikisha kwamba tuna “vitu vyema vingi” lakini tukose kufanya yale tunayohitaji kufanya ili kuwa na tumaini la kuishi “miaka mingi”? (Yohana 3:16; 17:3) Biblia inasema hivi: “Vitu vyenye thamani havitakuwa na faida yoyote siku ya ghadhabu,” na “anayetegemea utajiri wake—yeye mwenyewe ataanguka.” (Methali 11:4, 28) Kwa hiyo, Yesu alimalizia mfano wake kwa himizo hili: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—Luka 12:21.

11. Kwa nini ni ubatili kuweka tumaini na usalama katika vitu vya kimwili?

11 Yesu aliposema “hivyo ndivyo huwa,” alikuwa akimaanisha kwamba mambo yaliyompata yule tajiri katika mfano huo yatawapata pia wale ambao wanajenga maisha yao, yaani, wanaweka tumaini lao na usalama wao katika vitu vya kimwili. Kosa si ‘kujikusanyia mwenyewe hazina’ lakini ni kutokuwa “tajiri kwa Mungu.” Mwanafunzi Yakobo alitoa onyo kama hilo alipoandika hivi: “Haya, basi, ninyi ambao husema: ‘Leo au kesho tutasafiri kwenda jiji fulani nasi tutakaa mwaka mmoja huko, tutafanya biashara na kupata faida,’ ingawa hamjui uzima wenu utakuwa namna gani kesho.” Wanapaswa kufanya nini? “Badala yake, mnapaswa kusema: ‘Yehova akipenda, tutaishi na pia kufanya hili au lile.’” (Yakobo 4:13-15) Hata mtu awe tajiri namna gani au awe na vitu vingi kadiri gani, vyote vitakuwa ubatili ikiwa yeye si tajiri kwa Mungu. Basi, ni nini maana ya kuwa tajiri kwa Mungu?

Kuwa Tajiri kwa Mungu

12. Tutakuwa matajiri kwa Mungu tukifanya nini?

12 Yesu alisema kwamba kuwa tajiri kwa Mungu ni tofauti kabisa na kujiwekea hazina za vitu vya kimwili, au kujitafutia utajiri wa kimwili. Hivyo, Yesu alikuwa akisema kwamba hangaiko letu kuu maishani halipaswi kuwa kukusanya utajiri wa kimwili au kufurahia vitu tulivyo navyo. Badala yake, tunapaswa kutumia mali zetu kwa njia ambayo itaboresha, au kujenga, uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tukifanya hivyo, bila shaka tutakuwa matajiri kwa Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tutaweza kupata baraka nyingi kutoka kwake. Biblia inatuambia hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.

13. Baraka ya Yehova “hutajirisha” namna gani?

13 Yehova anapowabariki watu wake, sikuzote anawapa vitu vilivyo bora. (Yakobo 1:17) Kwa mfano, Yehova alipowapa Waisraeli nchi, “ilikuwa nchi inayotiririka maziwa na asali.” Ingawa nchi ya Misri pia ilisemwa kuwa hivyo, nchi ambayo Yehova aliwapa Waisraeli ilikuwa tofauti angalau katika njia moja muhimu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: Ni “nchi ambayo Yehova Mungu wako anaitunza.” Kwa maneno mengine, wangefanikiwa kwa sababu Yehova angewatunza. Maadamu Waisraeli waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, aliwabariki sana na ni wazi kwamba waliishi kwa njia bora kuliko mataifa yote yaliyowazunguka. Ndiyo, baraka ya Yehova ndiyo “hutajirisha”!—Hesabu 16:13; Kumbukumbu la Torati 4:5-8; 11:8-15.

14. Wale walio matajiri kwa Mungu wanapata nini?

14 Maneno “tajiri kwa Mungu” yanatafsiriwa pia kuwa “tajiri mbele ya Mungu” (Biblia Habari Njema) au “tajiri machoni pa Mungu.” (The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Wale ambao ni matajiri kimwili kwa ujumla wanahangaikia jinsi ambavyo wanaonwa na wengine. Mara nyingi njia yao ya maisha inaonyesha hivyo. Wanataka kuwapendeza watu kwa ‘kujionyesha mali yao maishani’ kama Biblia inavyosema. (1 Yohana 2:16) Kinyume chake, wale ambao ni matajiri kwa Mungu wanapata kibali, upendeleo, na fadhili nyingi zisizostahiliwa kutoka kwa Mungu, na wana uhusiano wa karibu pamoja naye. Bila shaka, kuwa katika hali hiyo nzuri sana kunawaletea furaha na usalama, baraka nyingi ambazo utajiri wa kimwili hauwezi kuleta. (Isaya 40:11) Swali linalobaki ni, Ni lazima tufanye nini ili tuwe matajiri machoni pa Mungu?

Tajiri Machoni pa Mungu

15. Tunapaswa kufanya nini ili tuwe matajiri kwa Mungu?

15 Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alipanga na kufanya kazi ngumu ili ajitajirishe, naye aliitwa asiye na akili. Kwa hiyo, ili tuwe matajiri kwa Mungu, tunapaswa kujitahidi kabisa kushiriki kikamili katika utendaji ambao ni wa maana na wenye thamani kikweli machoni pa Mungu. Utendaji huo unatia ndani amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19) Kutumia wakati, nguvu, na vipawa vyetu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi wala si kuboresha maisha yetu kunaweza kulinganishwa na kuwekeza pesa katika biashara. Wale ambao wamefanya hivyo wamepata baraka nyingi sana za kiroho, kama mambo yafuatayo yanavyoonyesha.—Methali 19:17.

16, 17. Unaweza kusimulia mambo gani yaliyoonwa ili kuonyesha njia ya maisha ambayo inamfanya mtu awe tajiri machoni pa Mungu?

16 Mfikirie mwanamume mmoja Mkristo katika nchi fulani ya Asia. Alikuwa fundi wa kompyuta naye alipata mshahara mnono. Hata hivyo, kazi yake ilichukua wakati wake wote na hivyo akadhoofika kabisa kiroho. Mwishowe, badala ya kujaribu kufanya maendeleo katika kazi hiyo, aliiacha na kuanza kutengeneza aiskrimu (glace) na kuiuza mitaani, ili awe na wakati zaidi wa kushughulikia mahitaji na wajibu wake wa kiroho. Wafanyakazi wenzake wa zamani walimdhihaki, lakini matokeo yalikuwa nini? Alisema hivi: “Kwa kweli, nilipata pesa nyingi zaidi kuliko nilizopata nilipokuwa nikifanya kazi ya kompyuta. Nimepata furaha zaidi kwa sababu sina mfadhaiko wala wasiwasi kama niliokuwa nao katika kazi yangu ya zamani. Jambo la maana zaidi ni kwamba sasa ninajihisi nikiwa karibu zaidi na Yehova.” Kubadili kazi kulimwezesha Mkristo huyo kuanza huduma ya wakati wote, na hivi sasa anatumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi yake. Kwa kweli, baraka ya Yehova ‘inatajirisha.’

17 Mfano mwingine ni wa mwanamke ambaye alilelewa katika familia ambayo ilithamini sana elimu. Alipata elimu katika vyuo vikuu nchini Ufaransa, Mexico, na Uswisi, naye alitumaini kupata kazi nzuri. Alisema hivi: “Nilifanikiwa; niliheshimiwa na kupewa mapendeleo ya pekee, lakini moyoni nilihisi kwamba maisha yangu hayana maana yoyote, nami sikutosheka hata kidogo.” Kisha alijifunza kumhusu Yehova. Anasema hivi: “Kadiri nilivyofanya maendeleo ya kiroho, tamaa yangu ya kumpendeza Yehova na kumshukuru angalau kidogo kwa ajili ya mambo aliyonipa ilinisaidia kuelewa wazi jambo nililopaswa kufanya, yaani, kumtumikia kwa wakati wote.” Aliacha kazi yake na muda si muda akabatizwa. Kwa miaka 20 iliyopita, amefurahi kutumika katika huduma ya wakati wote. Anasema: “Watu fulani wanafikiri kwamba nimepoteza vipawa vyangu, lakini wanatambua kwamba nina furaha, nao wanavutiwa na kanuni ambazo ninafuata maishani. Kila siku ninamwomba Yehova anisaidie kuwa mnyenyekevu ili nipate kibali chake.”

18. Kama Paulo, tunaweza kuwa matajiri kwa Mungu jinsi gani?

18 Sauli, ambaye alikuja kuwa mtume Paulo, alikuwa na nafasi ya kupata kazi nzuri sana. Hata hivyo, aliandika hivi baadaye: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu.” (Wafilipi 3:7, 8) Paulo aliona kwamba utajiri ambao alipata kupitia Kristo ulikuwa wenye thamani zaidi kuliko kitu chochote ambacho ulimwengu ungempa. Vivyo hivyo, tukiacha miradi ya kichoyo na kufuatia maisha ya ujitoaji-kimungu, sisi pia tunaweza kuwa matajiri machoni pa Mungu. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

Je, Unaweza Kueleza?

• Mtu aliyetajwa katika mfano wa Yesu alikuwa na tatizo gani?

• Kwa nini mtu huyo aliitwa asiye na akili?

• Ni nini maana ya kuwa tajiri kwa Mungu?

• Tunaweza kuwa matajiri kwa Mungu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa nini yule mtu tajiri aliitwa asiye na akili?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nafasi za kuboresha maisha yetu zinaweza jinsi gani kuwa jaribu kubwa?

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

“Baraka ya Yehova —hiyo ndiyo hutajirisha”