Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Jilinde na Kila Namna ya Tamaa’

‘Jilinde na Kila Namna ya Tamaa’

‘Jilinde na Kila Namna ya Tamaa’

“Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—LUKA 12:15.

1, 2. (a) Umeona watu leo wanapendezwa na wanafuatia nini? (b) Mitazamo hiyo inaweza kuwa na matokeo gani mabaya kwetu?

PESA, mali, sifa, kazi yenye mshahara mnono, na familia, ni kati ya mambo ambayo watu wengi wanafikiri yanaonyesha kwamba mtu amefanikiwa au yanamhamkikishia wakati ujao ulio salama. Ni wazi kwamba katika nchi tajiri na maskini, watu wengi wanapendezwa na wanafuatia vitu vya kimwili na mafanikio maishani. Kwa upande mwingine, ikiwa wanapendezwa na mambo ya kiroho kwa kadiri fulani, upendezi huo unazidi kupungua.

2 Hivyo ndivyo Biblia ilivyotabiri hasa. Inasema: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kuwa wanaishi kati ya watu hao kila siku, Wakristo wa kweli wanasukumwa kuwa na mtazamo na mtindo wa maisha kama wa watu hao. Ni nini kinachoweza kutusaidia kupinga jitihada za ulimwengu za ‘kutufinyanga katika muundo wake wenyewe’?—Waroma 12:2, The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips.

3. Sasa tutazungumzia shauri gani lililotolewa na Yesu?

3 Akiwa “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu,” Yesu Kristo alitufundisha mambo muhimu sana kuhusiana na hilo. (Waebrania 12:2) Pindi moja, Yesu alipokuwa akiufundisha umati wa watu mambo fulani ya kiroho yenye kuelimisha, mtu fulani alikatiza mazungumzo hayo alipoomba hivi: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” Yesu alimjibu mtu huyo kwa kumpa yeye na wote waliokuwa wakisikiliza shauri zito. Alitoa onyo kali sana kuhusu kuepuka tamaa na akakazia onyo hilo kwa kutumia mfano wenye kuchochea fikira. Tunapaswa kutii shauri ambalo Yesu alitoa wakati huo na kuona jinsi tunavyoweza kufaidika kwa kulitumia katika maisha yetu.—Luka 12:13-21.

Ombi Lisilofaa

4. Kwa nini haikufaa mtu huyo kumkatiza Yesu?

4 Kabla ya mtu huyo kukatiza mazungumzo, Yesu alikuwa akizungumza na wanafunzi wake na watu wengine kuhusu kujihadhari na unafiki, kuwa na ujasiri wa kukiri kuwa na muungano pamoja na Mwana wa binadamu, na kuhusu kupata msaada wa roho takatifu. (Luka 12:1-12) Bila shaka, wanafunzi walipaswa kutia moyoni mambo hayo muhimu. Hata hivyo, alipokuwa akiendelea kutoa hotuba hiyo yenye kuchochea fikira, mtu huyo alikatiza mazungumzo ghafula na kumwomba Yesu asuluhishe mgogoro ambao ulionekana kuwa wa kifamilia kuhusu vitu vya kimwili. Hata hivyo, kuna jambo la maana ambalo tunaweza kujifunza kutokana na tukio hilo.

5. Ombi la mtu huyo lilionyesha nini kumhusu?

5 Inasemekana kwamba “kwa kawaida mambo ambayo mtu anafikiria wakati anaposikiliza mafundisho ya kidini yanaonyesha mwelekeo wake.” Wakati Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu mambo mazito ya kiroho, inaelekea mtu huyo alikuwa akifikiria jambo ambalo angefanya ili apate faida fulani za kifedha. Hatuambiwi ikiwa mtu huyo alikuwa na sababu halali ya kulalamika kuhusu urithi huo. Labda alikuwa akijaribu kufaidika kutokana na mamlaka na sifa ya Yesu akiwa mwamuzi mwenye hekima katika shughuli za wanadamu. (Isaya 11:3, 4; Mathayo 22:16) Kwa vyovyote vile, swali lake lilionyesha kwamba alikuwa na tatizo ndani kabisa ya moyo wake, tatizo kubwa sana la kutothamini mambo ya kiroho. Je, hiyo si sababu nzuri ya kutufanya tujichunguze wenyewe? Kwa mfano, ni rahisi kuruhusu akili zetu zitangetange tunapokuwa katika mikutano ya Kikristo au kufikiria mambo tutakayofanya baadaye. Badala yake, tunapaswa kusikiliza kwa makini yale yanayosemwa na kufikiria njia za kutumia habari hiyo maishani ili tuboreshe uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu, na pamoja na Wakristo wenzetu.—Zaburi 22:22; Marko 4:24.

6. Kwa nini Yesu alikataa kutimiza ombi la mtu huyo?

6 Hata iwe mtu huyo alichochewa na nini kutoa ombi hilo, Yesu alikataa kulitimiza. Badala yake, Yesu alimwambia hivi: “Wewe mtu, nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawaji juu yenu?” (Luka 12:14) Kwa kusema hivyo, Yesu alikuwa akizungumzia jambo fulani ambalo watu walijua vizuri, kwa sababu kulingana na Sheria ya Musa, waamuzi wa miji waliwekwa ili kuamua mambo hayo. (Kumbukumbu la Torati 16:18-20; 21:15-17; Ruthu 4:1, 2) Kwa upande mwingine, Yesu alihangaikia mambo ya maana zaidi, yaani, kutoa ushahidi kuhusu kweli ya Ufalme na kuwafundisha watu mapenzi ya Mungu. (Yohana 18:37) Tunafuata mfano wa Yesu kwa kutumia wakati na nguvu zetu kuhubiri habari njema na kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,” badala ya kukengeushwa na mambo yasiyo na maana.—Mathayo 24:14; 28:19.

Jihadhari na Tamaa

7. Yesu alitambua jambo gani lililokuwa moyoni mwa mtu huyo?

7 Kwa kuwa alikuwa na uwezo wa kutambua mielekeo iliyo ndani kabisa ya moyo, Yesu alijua kwamba jambo lingine zito zaidi lilihusika katika ombi la mtu huyo la kumtaka aingilie jambo la kibinafsi. Kwa hiyo, badala ya kukataa tu kulitimiza , Yesu alitaja sababu kuu ya ombi hilo aliposema hivi: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.

8. Tamaa ni nini, na inaweza kuongoza kwenye nini?

8 Tamaa inatia ndani mengi zaidi ya kutaka kuwa na pesa au vitu fulani tu, ambavyo vinaweza kutumiwa kwa njia na kusudi linalofaa. Inatia ndani kutamani kupita kiasi utajiri, mali, au vitu vya mtu mwingine. Inaweza kutia ndani hamu isiyoweza kutoshelezwa, pupa ya kupata vitu, labda vitu vya mtu mwingine, ili tu kuwa navyo bila uhitaji wowote au bila kujali matokeo kwa wengine. Mtu mwenye tamaa anaruhusu kitu anachokitamani kitawale fikira na matendo yake hivi kwamba kinakuwa mungu wake. Kumbuka kwamba mtume Paulo anamlinganisha mtu mwenye pupa na mwabudu-sanamu, ambaye hana urithi katika Ufalme wa Mungu.—Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5.

9. Tamaa inaweza kuonyeshwa kwa njia gani? Toa mifano.

9 Kwa kweli, Yesu alionya kuhusu “kila namna ya tamaa.” Tamaa inaonyeshwa kwa njia mbalimbali. Amri ya mwisho kati ya zile Amri Kumi inataja njia fulani kati ya hizo. Inasema hivi: “Usiitamani nyumba ya mwenzako. Usimtamani mke wa mwenzako, wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe-dume wake wala punda wake wala chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Biblia ina mifano mingi ya watu ambao wametenda dhambi nzito kwa sababu ya kuongozwa na tamaa fulani. Shetani alikuwa wa kwanza kutamani kitu ambacho kilikuwa cha mwingine, yaani, alitamani utukufu, heshima, na mamlaka ambayo ni ya Yehova peke yake. (Ufunuo 4:11) Hawa alitamani kupata haki ya kujiongoza, na alipodanganywa na tamaa hiyo aliwatumbukiza wanadamu katika dhambi na kifo. (Mwanzo 3:4-7) Roho waovu ni malaika ambao hawakutosheka na ‘mahali pao pa kwanza bali waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa’ na kufanya jambo ambalo hawakustahili kufanya. (Yuda 6; Mwanzo 6:2) Mfikirie pia Balaamu, Akani, Gehazi, na Yuda. Badala ya kutosheka na sehemu yao maishani, walitumia vibaya mapendeleo yao kwa sababu waliruhusu tamaa isiyotoshelezwa ya vitu vya kimwili iwaongoze katika maangamizo na uharibifu.

10. Kupatana na himizo la Yesu, tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu’ jinsi gani?

10 Inafaa kama nini kwamba kabla ya Yesu kutoa onyo kuhusu tamaa alisema maneno haya: “Endeleeni kufungua macho yenu”! Kwa nini? Kwa sababu ni rahisi sana kwa watu kuona kwamba mtu mwingine ana pupa au anatamani, lakini si rahisi wao wenyewe kukubali kwamba wana tatizo hilo. Hata hivyo, mtume Paulo anasema kwamba “kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” (1 Timotheo 6:9, 10) Mwanafunzi Yakobo anaeleza kwamba tamaa isiyofaa, “wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.” (Yakobo 1:15) Kupatana na himizo la Yesu, tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu,’ si kuangalia wengine kuona kama wana tamaa lakini kujichunguza wenyewe ili kuona mambo tunayotamani mioyoni mwetu kisha ‘tujilinde na kila namna ya tamaa.’

Kuwa na Vitu Vingi Maishani

11, 12. (a) Yesu alitoa onyo gani kuhusu tamaa? (b) Kwa nini tunahitaji kutii onyo la Yesu?

11 Tunapaswa kujilinda na tamaa kwa sababu nyingine. Angalia yale ambayo Yesu alisema baadaye: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Bila shaka, hilo ni jambo linalohitaji kufikiriwa kwa uzito katika nyakati zetu ambazo watu wanapenda mali na wanafikiri kwamba utajiri na ufanisi unaleta furaha na mafanikio. Yesu aliposema maneno hayo alikuwa akionyesha kwamba maisha yenye kusudi la kweli na yenye kuridhisha hayatokani au hayategemei vitu vya kimwili hata viwe vingi kadiri gani.

12 Hata hivyo, huenda watu fulani wakapinga hilo. Pengine wanaweza kudai kwamba vitu vya kimwili vinafanya maisha yawe yenye kustarehesha zaidi na kufurahisha, na hivyo yanakuwa yenye kusudi zaidi. Kwa hiyo, wanakazana kufuatia mambo ambayo yatawawezesha kupata vitu vya kimwili na vifaa vyote ambavyo wanatamani. Wanafikiri kwamba vitu hivyo vitawawezesha kuwa na maisha mazuri. Lakini kwa kufikiri hivyo, wanakosa kuelewa jambo ambalo Yesu alikuwa anakazia.

13. Tunapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu uhai na vitu tulivyo navyo?

13 Badala ya kuzungumza kuhusu ikiwa kuwa na vitu vingi ni sawa au si sawa, Yesu alikuwa akikazia kwamba uzima wa mtu hautokani na “vitu alivyo navyo,” yaani, vitu ambavyo tayari anavyo. Kuhusiana na hilo, sote tunajua kwamba kwa kweli hatuhitaji vitu vingi ili kuishi au kuendelea kuwa hai. Tunahitaji tu chakula kidogo, mavazi, na mahali pa kulala. Matajiri wana vitu hivyo vingi, nao maskini huenda wakalazimika kujitahidi sana ili kupata vitu wanavyohitaji. Hata hivyo, matajiri na maskini wanakuwa sawa wakati wanapokufa kwa sababu mambo yote yanaishia hapo. (Mhubiri 9:5, 6) Kwa hiyo, ili maisha yawe yenye kusudi na maana, hayawezi na hayapaswi kutegemea tu vitu ambavyo mtu anaweza kupata au kuwa navyo. Wazo hilo linaeleweka wazi zaidi tunapochunguza aina ya uzima ambao Yesu alikuwa akizungumzia.

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na neno linalotafsiriwa “uzima” katika Biblia?

14 Yesu alisema, ‘Uzima wa mtu hautokani na vitu alivyo navyo.’ Neno linalotafsiriwa “uzima” katika Injili ya Luka (Kigiriki, zo·eʹ) halimaanishi namna au mtindo wa maisha, bali uzima wenyewe, yaani, uhai. * Yesu alikuwa akisema kwamba tuwe matajiri au maskini, tuwe tunaishi maisha ya raha au tunapata riziki yetu kwa shida, hatuwezi kuamua urefu wa maisha yetu au hata hatuwezi kujua ikiwa kesho tutakuwa hai. Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” (Mathayo 6:27) Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova peke yake ndiye “chemchemi ya uzima,” na ndiye peke yake anayeweza kuwapa wale walio waaminifu “uzima ulio wa kweli,” au “uzima wa milele,” uhai usio na mwisho, iwe mbinguni au duniani.—Zaburi 36:9; 1 Timotheo 6:12, 19.

15. Kwa nini watu wengi wanategemea vitu vya kimwili?

15 Maneno ya Yesu yanaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa watu kuwa na maoni yaliyopotoka au yasiyo sawa kuhusu maisha. Iwe ni matajiri au maskini, wanadamu wote si wakamilifu nao wana mwisho mmoja. Musa aliyeishi zamani alisema hivi: “Kwa maana siku za miaka yetu ni miaka 70; na ikiwa kwa sababu ya nguvu za pekee ni miaka 80, hata hivyo hizo husisitiza kuleta taabu na mambo yenye kuumiza; kwa maana lazima zipite upesi, nasi huruka na kwenda zetu.” (Zaburi 90:10; Ayubu 14:1, 2; 1 Petro 1:24) Kwa sababu hiyo, mara nyingi watu ambao hawajasitawisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu wanakuwa na mtazamo ambao unatajwa na mtume Paulo wa kwamba “tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Wengine wanapotambua kwamba maisha ni mafupi sana na hayategemeki, wanajaribu kutafuta usalama na maisha marefu kutokana na vitu vya kimwili. Labda wanafikiri kwamba wakiwa na vitu vingi vya kimwili, kwa njia fulani watakuwa na maisha salama zaidi. Hivyo, wanajikakamua kabisa kukusanya mali na utajiri, wakifikiri kimakosa kwamba vitu hivyo vinaleta usalama na furaha.—Zaburi 49:6, 11, 12.

Wakati Ujao Ulio Salama

16. Kusudi la kweli maishani halitegemei nini?

16 Huenda ni kweli kwamba mtu anayeishi maisha ya hali ya juu akiwa na chakula cha kutosha, mavazi, makao na vitu vingine vya kujifurahisha anaweza kuishi maisha yenye starehe zaidi au anaweza kupata matibabu mazuri zaidi na hivyo kurefusha maisha yake kwa miaka michache. Hata hivyo, je, kweli maisha ya aina hiyo yako salama zaidi na ni yenye kusudi zaidi? Kusudi la kweli maishani halitegemei miaka ambayo mtu anaweza kuishi au wingi wa vitu vya kimwili ambavyo anaweza kuwa navyo au kutumia. Mtume Paulo alionyesha hatari ya kutegemea sana vitu kama hivyo. Alimwandikia Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.”—1 Timotheo 6:17.

17, 18. (a) Tunapaswa kuiga mifano gani bora kuhusiana na vitu vya kimwili? (b) Ni mfano gani wa Yesu utakaozungumziwa katika habari inayofuata?

17 Si jambo la hekima kwa mtu kuweka tumaini lake katika utajiri kwa sababu ‘si hakika.’ Mzee wa ukoo Ayubu alikuwa tajiri sana, lakini msiba ulipotokea ghafula, utajiri wake haungeweza kumsaidia; utajiri wake ulipotea ghafula. Uhusiano wake mzuri sana pamoja na Mungu ndio uliomwezesha kuvumilia majaribu na mateso yote. (Ayubu 1:1, 3, 20-22) Abrahamu hakuruhusu utajiri wake umzuie kukubali mgawo mgumu kutoka kwa Yehova, naye alibarikiwa na kuwa “baba ya umati wa mataifa.” (Mwanzo 12:1, 4; 17:4-6) Tunapaswa kuiga mifano hiyo na mifano mingine. Sisi sote vijana kwa wazee, tunahitaji kujichunguza ili tuone ni nini kilicho cha maana zaidi katika maisha yetu na tumaini letu linategemea nini.—Waefeso 5:10; Wafilipi 1:10.

18 Maneno machache ambayo Yesu alisema kuhusu tamaa na maoni yanayofaa kuhusu uhai ni muhimu na kwa kweli yanafundisha. Hata hivyo, Yesu alikuwa na mambo mengine akilini, naye alisimulia mfano wenye kuchochea fikira kuhusu mtu tajiri ambaye hakutumia akili yake. Mfano huo unahusu maisha yetu leo jinsi gani, na tunaweza kujifunza nini kutokana nao? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Neno lingine la Kigiriki linalotafsiriwa “uhai” ni biʹos, ambalo linatokeza maneno ya Kiswahili kama vile “biografia” na “biolojia.” Kulingana na kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words), neno biʹos linamaanisha “kipindi au urefu wa maisha,” “namna ya maisha,” na “riziki ya maisha.”

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunaweza kujifunza nini kutokana na uamuzi wa Yesu wa kukataa kutimiza ombi la mtu fulani aliyekuwa kati ya umati wa watu?

• Kwa nini ni lazima tujilinde na tamaa, nasi tunaweza kujilinda jinsi gani?

• Kwa nini uhai hautokani na vitu vya kimwili?

• Ni nini kinachoweza kufanya maisha yawe salama na yenye kusudi la kweli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa nini Yesu alikataa kutimiza ombi la mtu fulani?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kutamani kunaweza kuongoza kwenye msiba

[Picha katika ukurasa wa 25]

Abrahamu alionyesha namna gani kwamba alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili?