Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtumikia Yehova—Ni Heshima na Pendeleo Lisilo na Kifani

Kumtumikia Yehova—Ni Heshima na Pendeleo Lisilo na Kifani

Simulizi la Maisha

Kumtumikia Yehova—Ni Heshima na Pendeleo Lisilo na Kifani

LIMESIMULIWA NA ZERAH STIGERS

Mume wangu, ambaye alikuwa mwandamani wangu mwaminifu katika huduma ya wakati wote, alikufa mwaka wa 1938. Kwa sababu hiyo, nikawa na daraka la kumlea mtoto wetu mchanga sana na mvulana wetu mwenye umri wa miaka kumi. Ingawa bado nilitamani kufanya huduma ya wakati wote, ningeweza kufanya hivyo jinsi gani? Acheni niwaeleze kidogo kuhusu maisha yangu ya mapema kabla ya kuwaambia jinsi nilivyoweza kufanya huduma ya wakati wote.

MUDA mfupi baada ya mimi kuzaliwa mnamo Julai 27, 1907, huko Alabama, Marekani, wazazi wangu walihama pamoja nami na dada na ndugu zangu kwenda Georgia. Muda mfupi baadaye tulihamia Tennessee na kisha tukahamia karibu na jiji la Tampa, Florida. Tukiwa huko, mwaka wa 1916, niliona sinema yenye sauti inayoitwa “Photo-Drama of Creation.” Biashara ya sinema ilikuwa tu imeanza, na kila mtu alifurahia sana sinema ya “Photo-Drama”!

Wazazi wangu walikuwa wasomaji wenye bidii wa gazeti la Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Biblia. Ingawa Baba alipenda kusoma vichapo hivyo, wakati huo hakushirikiana kwa bidii na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Hata hivyo, tukiwa watoto, tulienda na mama katika mikutano. Kwa kweli, muda mfupi baada ya kuhamia Niles, Michigan, kwa ukawaida tulisafiri zaidi ya kilomita 16 kwa garimoshi kwenda South Bend, Indiana, ili kuhudhuria mikutano.

Mwishowe, mnamo Julai 22, 1924, nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova. Muda mfupi baadaye, Mama alipanga mambo yake ili kuwa kolpota, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Mfano wake mzuri na wa makolpota wengine ulichochea tamaa yangu ya kuanza kazi hiyo.

Ninapata Mwenzi

Tulipokuwa tukihudhuria kusanyiko kubwa huko Indianapolis, Indiana, mwaka wa 1925, nilikutana na James Stigers, ambaye alikuwa ametoka Chicago. Papo hapo James alinivutia kwa sababu alikuwa mtumishi wa Yehova mwenye bidii. Niliishi umbali wa kilomita 160 hivi kutoka Chicago, hivyo haikuwa rahisi kwetu kutembeleana. Wakati huo, kulikuwa na kutaniko moja tu katika jiji hilo kubwa, na mikutano ilifanywa kwenye ghorofa ya pili katika chumba kimoja kilichokodiwa. James aliniandikia mara nyingi ili kunitia moyo kiroho. Tulifunga ndoa Desemba 1926, na mwaka mmoja hivi baadaye, nilizaa mwana wetu wa kwanza, Eddie.

Muda mfupi baadaye, mimi na James tulianza pamoja huduma ya upainia. Tulitumika katika majimbo manane, yaani, Michigan, Louisiana, Mississippi, South Dakota, Iowa, Nebraska, California, na Illinois, na tulifurahia miaka yenye kupendeza zaidi ya maisha yetu. Lakini siku hizo zenye furaha katika familia yetu zilikatizwa wakati James alipoanza kuwa mgonjwa.

Matatizo ya kiuchumi yaliyosababishwa na ugonjwa wa James yalitulazimisha kurudi Chicago mwaka wa 1936 ili kuishi pamoja na mama mkwe wangu, ambaye pia alikuwa Shahidi. Wakati wa ugonjwa wa James, huku nikiwa na mimba ya mtoto wetu wa pili, nilifanya kazi katika hoteli moja na nililipwa mshahara wa dola 1 kwa siku. Mama mkwe wangu mpendwa alihakikisha kwamba tulikuwa na chakula kingi, na alifanya hivyo bila kutazamia malipo yoyote. Alitutunza vizuri sana.

James alikuwa na ugonjwa wa uvimbe wa ubongo kwa miaka miwili hivi kabla ya kifo chake. Alikufa mnamo Julai 1938. Alipokuwa mgonjwa, hangeweza kuendesha gari au kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, lakini alitumia kila nafasi ili kuwahubiria wengine. Ili kusaidia kulipia gharama za familia yetu, niliacha huduma ya wakati wote. Niliweza kupata kazi mbalimbali, ambazo zilikuwa za muda mfupi tu.

Mwana wetu Bobby alizaliwa Julai 30, 1938, siku nane tu baada ya kifo cha baba yake. Hata hivyo, mama mkwe wangu alikataa kuniruhusu kwenda katika hospitali ya mkoa. Badala yake, alinifanyia mipango ya kwenda katika hospitali bora na kutibiwa na daktari wake. Zaidi ya hilo, alilipia gharama zote. Huo ulikuwa wonyesho wa upendo wa Kikristo ambao nilithamini sana.

Ninarudi Tena Katika Huduma ya Wakati Wote

Tuliendelea kuishi pamoja na mama mkwe wangu mpaka Bobby alipokuwa na umri wa zaidi ya miaka 2, na Eddie akiwa na miaka 12. Ingawa nililazimika kubadili maisha yangu, bado nilikuwa na tamaa kubwa ya kumtumikia Yehova wakati wote. Tulipokuwa kwenye kusanyiko la mwaka wa 1940 huko Detroit, Michigan, nilikutana na wenzi wawili wa ndoa mapainia ambao walinitia moyo kuhamia South Carolina ili kufanya upainia. Hivyo, nilinunua gari kwa dola 150 na nikajitayarisha kuhamia huko. Katika mwaka wa 1941, mwaka ambao Marekani iliingia katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, mimi na watoto wangu wawili wa kiume tulisafiri kusini mwa Marekani, na kwa mara nyingine tena nikaanza huduma ya wakati wote.

Tulipohamia South Carolina, tulienda kwanza Camden, karibu na mji wa Little River, na kisha tukaenda Conway. Huko Conway, nilipata nyumba ndogo ya kukokotwa na gari. Mtu mmoja mwenye fadhili aliyekuwa na kituo cha mafuta aliniruhusu kuegesha gari langu karibu na kituo chake. Nilitumia umeme na mafuta ya kituo hicho, na hata nilitumia choo chao. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, kwa sababu ya uhaba watu hawakuruhusiwa kununua mafuta mengi, na singeweza kamwe kupata mafuta. Hivyo, nikanunua baiskeli iliyokuwa tayari imetumika. Kisha, mwaka wa 1943, ilipoonekana haiwezekani kuendelea na upainia kwa sababu hatukuwa na pesa zozote, niliombwa kuwa painia wa pekee; hivyo kila mwezi nilipokea kiasi kidogo cha pesa ili kunisaidia kulipia gharama. Kwa miaka yote hiyo, Yehova amenisaidia sana!

Wakati huo, hakukuwa na Mashahidi wengine huko Conway, na ilikuwa vigumu kwangu na watoto kwenda peke yetu katika huduma. Hivyo, niliandika na kuomba painia wa pekee wa kuhubiri naye, na mwaka wa 1944, nilibarikiwa nilipopewa painia wa pekee mzuri sana wa kushirikiana naye! Painia huyo aliitwa Edith Walker. Tulitumika pamoja katika migawo mbalimbali kwa miaka 16. Kisha, kwa kusikitisha, alirudi Ohio kwa sababu ya matatizo ya afya.

Baraka Zisizosahauliwa

Kati ya mambo mengi yenye kupendeza ambayo ninakumbuka kwa miaka yote hiyo, siwezi kamwe kumsahau Albertha, msichana mwenye umri wa miaka 13 aliyeishi huko Conway na ambaye alimtunza nyanya yake kiwete na ndugu zake wawili wachanga. Alipenda kweli za Biblia ambazo nilimfundisha na alitaka kuwaambia wengine kuzihusu. Yeye pia alithamini sana utumishi wa upainia na akaanza upainia baada ya kumaliza shule ya sekondari mwaka wa 1950. Zaidi ya miaka 57 baadaye, bado anaendelea katika huduma ya wakati wote!

Katika mwaka wa 1951, mimi na Edith tulitumwa kwa muda mfupi huko Rock Hill, South Carolina, ambako kulikuwa na Mashahidi wachache sana. Kisha tulihamishwa kwenda Elberton, Georgia, kwa miaka mitatu. Halafu nilirudi tena South Carolina, ambako nilikaa tangu 1954 mpaka 1962. Nikiwa huko Walhalla, nilikutana na mwanamke mzee aliyekuwa na matatizo ya kusikia aliyeitwa Nettie, ambaye aliishi peke yake katika eneo la mashambani. Ili tujifunze Biblia, alisoma fungu katika kichapo, kisha nikamwonyesha kwa kidole swali la fungu chini ya ukurasa, halafu akaonyesha jibu katika fungu.

Alipokosa kuelewa jambo fulani, aliandika swali lake kwenye karatasi, kisha nikaandika jibu kando ya swali hilo. Baada ya muda, Nettie alipendezwa sana na kweli ya Biblia hivi kwamba akaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Alihubiri peke yake nyumba kwa nyumba, lakini kila mara sikuwa mbali sana naye. Kwa kawaida, nilikuwa ng’ambo ya barabara, nikiwa tayari kumsaidia iwapo alihitaji msaada.

Nilipokuwa Walhalla, gari langu zee liliharibika. Nafasi ilijitokeza ya kununua gari fulani kwa dola 100, lakini sikuwa na pesa. Nilimwendea Shahidi mmoja aliyekuwa mfanyabiashara, naye akanikopesha dola 100. Muda mfupi baadaye, bila kutarajia nikapokea barua kutoka kwa dada yangu mdogo iliyosema kwamba ndugu na dada zangu wa kimwili waligundua kwamba baba alipokufa, aliacha pesa fulani katika benki. Walizungumza kuhusu kile wangefanya na pesa hizo, na wote wakakubaliana kunitumia pesa hizo. Zilikuwa dola 100!

Ninafanya Upainia Pamoja na Wana Wangu

Wakiwa wachanga, Eddie na Bobby walikuwa kila mara pamoja nami katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Katika siku hizo, watu kwa ujumla hawakuwa na matatizo ya dawa za kulevya, na uvutano wa mwenendo mbaya haukuwa mkubwa kama ilivyo leo. Kuwa na maisha rahisi na kukazia akili kazi ya kuhubiri kulinisaidia kuepuka matatizo mengi ambayo wazazi leo wanakabili katika kuwalea watoto wao ili wamtumikie Yehova.

Eddie alienda shule huko Camden mpaka alipomaliza darasa la nane, na baadaye alitaka kufanya upainia pamoja nami. Tulifurahia pamoja utumishi wetu wa upainia kwa miaka fulani. Kisha, akasitawisha tamaa ya kutumika kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, ambako alitumika tangu 1947 mpaka 1957. Mwaka wa 1958 alimuoa Albertha, mwanafunzi wangu wa zamani wa Biblia, na wote wawili wakawa mapainia. Ilikuwa shangwe kama nini mwaka wa 2004, wakati sisi watatu tulipohudhuria pamoja Shule ya Utumishi wa Painia!

Ninakumbuka siku moja miaka mingi iliyopita, nilimsikia Bobby mchanga akimwomba Yehova katika sala anisaidie nipate mafuta ya kutosha ili nitumie gari langu kwenda kuwaona wanafunzi wangu wa kawaida wa Biblia. Katika maisha yake yote, Bobby ameonyesha kwamba anapenda huduma naye amefurahia huduma ya upainia kwa miaka mingi. Kwa kusikitisha, Bobby pia alipatwa na msiba wa familia. Mwaka wa 1970, baada ya kuishi katika ndoa kwa miezi 22 tu, mke wake alikufa alipokuwa akizaa mapacha ambao pia walikufa. Sikuzote nimeishi karibu na Bobby na tumekuwa na uhusiano wa karibu sana.

Bado Ninaendelea Kupainia!

Mwaka wa 1962, nilipewa mgawo wa kutumika katika kutaniko langu la sasa huko Lumberton, North Carolina, na nimetumika katika kutaniko hili kwa zaidi ya miaka 45. Niliendelea kuendesha gari langu mpaka nilipokuwa na umri wa miaka 84 hivi. Ninapelekwa kwenye mikutano ya kutaniko na pia katika kazi ya kuhubiri na familia moja ya Mashahidi inayoishi karibu nami.

Nina kifaa cha kunisaidia kutembea na kiti cha magurudumu, lakini sihitaji kuvitumia kwa kuwa ninaweza kutembea bila msaada wowote. Ninamshukuru Yehova kwa sababu nimekuwa na afya bora, lakini hivi karibuni tu ndipo nimepata matatizo fulani ya macho. Sikosi kamwe mikutano ya kutaniko isipokuwa niwe mgonjwa sana nami ninaendelea kutumika nikiwa painia wa kawaida anayeruhusiwa kutotimiza saa za utumishi.

Baada ya kutumika kwa shangwe katika huduma ya upainia kwa zaidi ya miaka 70, ninaweza kusema kwa unyoofu kwamba Yehova amenisaidia katika maisha yangu yote. * Ninatambua kwamba kiasili mimi si mtu mwenye akili sana au mwenye kufanya kazi haraka, lakini Yehova anajua kile ninachoweza na nisichoweza kufanya. Ninashukuru sana kwamba Yehova anajua kuwa ninajitahidi na kwamba amenitumia.

Ninahisi kwamba kumtumikia Yehova kadiri tunavyoweza ni muhimu kwa sababu kila kitu tulicho nacho kimetoka kwake. Maadamu nina uwezo, singechagua kazi nyingine yoyote ila ya upainia. Nimekuwa na pendeleo kubwa kama nini! Ninasali kwamba Yehova aendelee kunitumia kwa umilele wote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Dada Stigers alikufa mnamo Aprili 20, 2007 (20/4/2007) akiwa na tumaini la kwenda mbinguni. Alikuwa na umri wa miaka 99 na miezi 9. Tunatiwa moyo na utumishi wake wa uaminifu wa miaka na tunafurahi kwamba alipokea thawabu ya kimbingu.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mimi na mume wangu tulitumia gari hili katika kazi ya ukolpota

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikiwa na wana wangu mwaka wa 1941

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Eddie na Bobby hivi karibuni