Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Hali ya Kiroho

Kutafuta Hali ya Kiroho

Kutafuta Hali ya Kiroho

KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani ambayo yanajulikana sana, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Pengine unakubaliana na maneno hayo. Watu kila mahali wanatambua umuhimu wa hali ya kiroho katika maisha yao, nao wanafikiri kwamba wakitimiza uhitaji huo watapata furaha. Hata hivyo, maneno “hali ya kiroho” yanamaanisha nini?

Kamusi moja inafafanua hali ya kiroho kuwa “kutambua uhitaji wa au kushikamana na viwango vya kidini” na pia “sifa au hali ya kuwa mtu wa kiroho.” Hivyo, maneno kama vile “hali ya kiroho,” “kuwa mtu wa kiroho,” na “kuwa makini kiroho” yanaonwa kuwa yanamaanisha jambo lilelile. Ili kufafanua zaidi maneno “hali ya kiroho,” fikiria ulinganisho huu: Mtu aliye stadi katika biashara anasemwa kuwa makini kibiashara. Vivyo hivyo, mtu anayethamini sana mambo ya kiroho au ya kidini anasemwa kuwa makini kiroho.

Hivyo basi, unaweza jinsi gani kuwa mtu wa kiroho kikweli? Ingawa karibu kila dini inadai kwamba inajua jinsi mtu anavyoweza kutimiza uhitaji wake wa kiroho, njia zinazotolewa ni nyingi kama dini hizo zilivyo nyingi. Mprotestanti anadai kuwa ameokoka akiwa katika mkutano wa kuwaamsha watu kiroho. Mkatoliki anajitahidi kuwa na ushirika na Mungu wakati wa Misa. Mbudha anatafakari ili apate ujuzi. Mhindu anajinyima ili afaulu kujiweka huru kutoka katika mzunguko wa kuzaliwa upya. Je, wote hao wamo katika njia itakayowawezesha kuwa watu wa kiroho kikweli? Je, kila moja ya njia hizo itamwezesha mtu kuwa na hali ya kiroho?

Wengi wanaamini kwamba majibu ya maswali hayo ni hapana. Wanadai kwamba kuwa mtu wa kiroho kunamaanisha, “kuamini bila kuwa mshiriki,” yaani, kuamini kwamba kuna mungu bila kujiunga na kanisa lolote. Wengine wanaona kwamba kuwa mtu wa kiroho, si kuwa mwanadini, bali ni kutamani kuwa na amani ya ndani na kusudi maishani. Wanadai kwamba wale wanaojitahidi kuwa watu wa kiroho hawahitaji dini hata kidogo. Badala ya kumwendea Mungu au dini wanahitaji tu kufuata hisia zao za ndani ili kuwa watu wa kiroho. Mwandikaji mmoja anasema hivi: “Hali ya kiroho ya kweli ni hali inayopatikana ndani sana ya mtu. Ni jinsi unavyopenda, unavyokubali, na unavyochangamana na ulimwengu na watu walio karibu nawe. Haiwezi kupatikana kanisani au kwa kufuata imani fulani.”

Kwa wazi, watu wana maoni yanayotofautiana sana kuhusu hali ya kiroho. Maelfu ya vitabu vinadai kwamba vinaonyesha jinsi ya kuwa mtu wa kiroho, lakini mara nyingi sana wasomaji wa vitabu hivyo wanavurugika na hawatosheki. Hata hivyo, kuna kitabu kimoja ambacho kina mwongozo unaotegemeka kuhusu mambo ya kiroho. Ni kitabu ambacho kina uthibitisho wa kwamba kimeongozwa na roho ya Mungu. (2 Timotheo 3:16) Acha tuone yale ambayo kitabu hicho, Biblia, kinasema kuhusu maana ya hali ya kiroho na faida zake.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

COVER: Background: © Mark Hamblin/age fotostock