Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II

NI DESEMBA (Mwezi wa 12) 609 K.W.K. Mfalme wa Babiloni ameanza jitihada zake za mwisho za kuzingira Yerusalemu. Kufikia sasa, ujumbe wa Ezekieli kwa wahamishwa walio Babiloni umekazia jambo moja: kuanguka na kuharibiwa kwa jiji lao wanalolipenda, Yerusalemu. Hata hivyo, sasa ujumbe wa unabii wa Ezekieli unahusu kuanguka kwa mataifa ya kipagani ambayo yatashangilia msiba utakaowapata watu wa Mungu. Yerusalemu linapoanguka miezi 18 baadaye, ujumbe wa Ezekieli unahusu jambo lingine tofauti: kule kurudishwa kwenye utukufu kwa ibada ya kweli.

Ezekieli 25:1–48:35 ina unabii kuhusu mataifa yaliyozunguka Israeli na pia kuhusu kukombolewa kwa watu wa Mungu. * Isipokuwa Ezekieli 29:17-20, masimulizi mengine yote yamepangwa kulingana na wakati wa matukio na pia ujumbe wake. Hata hivyo, mistari hiyo minne inahusiana na unabii kuhusu Misri. Kikiwa sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho, kitabu cha Ezekieli kina ujumbe ‘ulio hai na ulio na nguvu.’—Waebrania 4:12.

‘ILE NCHI ITAKUWA KAMA BUSTANI YA EDENI’

(Ezekieli 25:1–39:29)

Akiona mapema jinsi mataifa yatakavyotenda kufuatia kuanguka kwa Yerusalemu, Yehova anamfanya Ezekieli atoe unabii juu ya Amoni, Moabu, Edomu, Ufilisti, Tiro, na Sidoni. Misri itaporwa. “Farao mfalme wa Misri na umati wake” wanafananishwa na mwerezi ambao utakatwa kwa “upanga wa mfalme wa Babiloni.”—Ezekieli 31:2, 3, 12; 32:11, 12.

Miezi sita hivi baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K., mtu aliyeponyoka anamjia Ezekieli na kuripoti hivi: “Jiji limepigwa na kuangushwa!” Nabii huyo ‘hawi bubu tena’ kuwaelekea wahamishwa. (Ezekieli 33:21, 22) Ana unabii mbalimbali wa kurudishwa ambao anapaswa kutangaza. Yehova ‘atasimamisha juu yao mchungaji mmoja, mtumishi wake Daudi.’ (Ezekieli 34:23) Edomu itafanywa ukiwa, lakini nchi iliyo kule, yaani, Yuda, itakuwa “kama bustani ya Edeni.” (Ezekieli 36:35) Yehova anaahidi kuwalinda watu wake waliorudishwa kutokana na shambulio la “Gogu.”—Ezekieli 38:2.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

29:8-12—Misri ilifanywa ukiwa kwa miaka 40 wakati gani? Baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mnamo 607 K.W.K., mabaki ya Yuda walikimbilia Misri ingawa walikuwa wameonywa na nabii Yeremia. (Yeremia 24:1, 8-10; 42:7-22) Hiyo haikuwa njia ya kuponyokea kwa kuwa Nebukadneza aliishambulia Misri na kuishinda. Huenda miaka 40 ya ukiwa wa Misri ilianza taifa hilo liliposhindwa. Ingawa historia ya kilimwengu haithibitishi kwamba Misri ilifanywa ukiwa, tunaweza kuwa na hakika kwamba jambo hilo lilitukia kwa sababu Yehova ni Mtimizaji wa unabii.—Isaya 55:11.

29:18—Ni jinsi gani ‘kila kichwa kilitiwa upara, na kila bega likakwaruzwa’? Kazi ya kuzingira jiji la barani la Tiro ilikuwa ngumu sana hivi kwamba askari wa Nebukadneza walitiwa upara na kofia zao na mabega yao yakakwaruzwa kwa sababu ya kubeba vifaa vya kujengea minara na ngome.—Ezekieli 26:7-12.

Mambo Tunayojifunza:

29:19, 20. Mfalme Nebukadneza hakupata nyara nyingi huko Tiro kwa sababu Watiro walikimbilia jiji lao la kisiwani wakiwa wamebeba mali nyingi. Hata ingawa Nebukadneza alikuwa mtawala mpagani mwenye ubinafsi na kiburi, Yehova alimthawabisha kwa sababu ya utumishi wake kwa Misri kama “malipo kwa ajili ya jeshi lake.” Je, hatupaswi kumwiga Mungu wa kweli kwa kulipa kodi kwa sababu ya huduma ambazo serikali inatoa kwa ajili yetu? Hata mamlaka za kiserikali zikitenda jinsi gani au kodi zikitumiwa kwa njia gani, bado tuna wajibu wa kulipa kodi.—Waroma 13:4-7.

33:7-9. Jamii ya mlinzi ya leo, yaani, mabaki ya watiwa mafuta, na waandamani wao hawapaswi kuacha kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwaonya watu juu ya “dhiki kuu” inayokuja.—Mathayo 24:21.

33:10-20. Wokovu wetu unategemea kuacha njia mbaya na badala yake kufanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, njia ya Yehova ni “sawa.”

36:20, 21. Kwa sababu hawakuishi kupatana na jina lao, yaani, “watu wa Yehova,” Waisraeli walitia unajisi jina la Mungu kati ya mataifa. Tusiwe kamwe waabudu wa Yehova kwa jina tu.

36:25, 37, 38. Paradiso ya kiroho tunayofurahia leo imejaa “kundi la watu watakatifu.” Hivyo, tunapaswa kujitahidi kuidumisha ikiwa safi.

38:1-23. Ni jambo lenye kutia moyo kama nini kujua kwamba Yehova atawaokoa watu wake watakaposhambuliwa na Gogu wa nchi ya Magogu! Gogu ni jina alilopewa “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi, baada ya kufukuzwa mbinguni. Nchi ya Magogu ni sehemu iliyo karibu na dunia, mahali ambapo Shetani na roho wake waovu wamezuiliwa.—Yohana 12:31; Ufunuo 12:7-12.

“UWEKE MOYO WAKO JUU YA YOTE NINAYOKUONYESHA”

(Ezekieli 40:1–48:35)

Ni mwaka wa 14 tangu jiji la Yerusalemu lilipoangushwa. (Ezekieli 40:1) Bado kuna miaka mingine 56 ya uhamisho. (Yeremia 29:10) Sasa Ezekieli anakaribia umri wa miaka 50. Katika maono, analetwa katika nchi ya Israeli. Anaambiwa hivi: “Mwana wa binadamu, ona kwa macho yako, na kwa masikio yako usikie, na uweke moyo wako juu ya yote ninayokuonyesha.” (Ezekieli 40:2-4) Ezekieli anasisimuka kama nini kupokea maono ya hekalu jipya!

Hekalu tukufu ambalo Ezekieli anaona lina malango 6, vyumba 30 vya kulia chakula, Patakatifu, Patakatifu Zaidi, madhabahu ya mbao, na madhabahu ya matoleo ya kuteketezwa. Maji ‘yaliyokuwa yakitoka’ hekaluni yaliongezeka na kuwa mto. (Ezekieli 47:1) Ezekieli anapewa pia maono ya migawo ya nchi kwa ajili ya makabila—kila kabila likigawiwa sehemu ya nchi kuelekea mashariki au magharibi huku kukiwa na sehemu ya nchi kati ya Yuda na Benyamini iliyotengwa kwa ajili ya shughuli za usimamizi. “Patakatifu pa Yehova” na “jiji” linaloitwa Yehova-Shama liko katika sehemu hiyo iliyotengwa.—Ezekieli 48:9, 10, 15, 35.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

40:3–47:12—Hekalu la maono ya Ezekieli linafananisha nini? Kwa kweli, hekalu hilo kubwa sana ambalo Ezekieli anaona katika maono halikujengwa kamwe. Linafananisha Hekalu la kiroho la Mungu—mpango wake ulio kama hekalu kwa ajili ya ibada safi katika siku zetu. (Ezekieli 40:2; Mika 4:1; Waebrania 8:2; 9:23, 24) Maono ya hekalu yanatimizwa katika “siku za mwisho” wakati ambapo ukuhani unasifishwa. (2 Timotheo 3:1; Ezekieli 44:10-16; Malaki 3:1-3) Hata hivyo, utimizo wa mwisho wa maono hayo utakuwa katika Paradiso. Hekalu la maono ya Ezekieli liliwapa Wayahudi waliohamishwa ahadi ya kwamba ibada safi itarudishwa na kwamba kila familia ya Kiyahudi itapata urithi wake katika nchi.

40:3–43:17—Kupima hekalu kunamaanisha nini? Kupimwa kwa hekalu ni ishara ya kwamba kusudi la Yehova kuhusu ibada safi litatimizwa hakika.

43:2-4, 7, 9—Ni nini iliyokuwa “mizoga ya wafalme wao” ambayo ilipaswa kuondolewa hekaluni? Kwa wazi mizoga hiyo ilifananisha sanamu. Watawala wa Yerusalemu na wakaaji wake walikuwa wamelichafua hekalu la Mungu kwa sanamu, na hivyo wakazifanya kuwa wafalme wao.

43:13-20—Madhabahu ambayo Ezekieli aliona katika maono inafananisha nini? Madhabahu hiyo inafananisha mapenzi ya Mungu kuhusiana na dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Kwa sababu ya uandalizi huo, watiwa-mafuta wanatangazwa kuwa waadilifu, nao “umati mkubwa” una msimamo safi machoni pa Mungu. (Ufunuo 7:9-14; Waroma 5:1, 2) Labda hiyo ndiyo sababu “bahari ya kuyeyushwa” ya hekalu la Sulemani, yaani, beseni kubwa la maji ambalo makuhani walitumia kuoga, haiko katika hekalu hilo la maono.—1 Wafalme 7:23-26.

44:10-16—Ni nani wanaofananishwa na jamii ya kikuhani? Jamii ya kikuhani ilionyesha kimbele kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta katika siku zetu. Walisafishwa mnamo 1918 Yehova alipoketi “kama msafishaji na mtakasaji” katika hekalu la kiroho. (Malaki 3:1-5) Wale waliokuwa safi au waliotubu wangedumisha pendeleo lao la utumishi. Baada ya hilo, walihitaji kujitahidi sana kuendelea kujitunza “bila doa kutokana na ulimwengu,” na hivyo kuuwekea mfano “umati mkubwa,” unaofananishwa na makabila yasiyo ya kikuhani.—Yakobo 1:27; Ufunuo 7:9, 10.

45:1; 47:13–48:29—“Nchi” na kugawanywa kwa nchi kunafananisha nini? Nchi inafananisha eneo la utendaji la watu wa Mungu. Haidhuru anaishi wapi, mwabudu wa Yehova yumo katika nchi iliyorudishwa mradi tu anaunga mkono ibada ya kweli. Kugawanywa kwa nchi kutatimizwa mara ya mwisho katika ulimwengu mpya wakati kila mtu mwaminifu atakapopewa urithi wake.—Isaya 65:17, 21.

Ezekieli 45:7, 16—Ni nini kinachoonyeshwa na mchango ambao watu wanatoa kwa ajili ya jamii ya kikuhani na kwa mkuu? Katika hekalu la kiroho, hilo hasa linaonyesha utegemezo wa kiroho, yaani, kutoa msaada na kuonyesha roho ya ushirikiano.

47:1-5—Ni nini kinachofananishwa na maji ya mto ambao Ezekieli anaona katika maono? Maji hayo yanafananisha uandalizi wa Yehova kwa ajili ya uzima, kutia ndani dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu na ujuzi juu ya Mungu unaopatikana katika Biblia. (Yeremia 2:13; Yohana 4:7-26; Waefeso 5:25-27) Kina cha mto huo kinazidi kuongezeka ili wapya wanaokubali ibada ya kweli wapate nafasi humo. (Isaya 60:22) Maji ya uzima ya mto huo yatatiririka kwa nguvu zaidi wakati wa ile Miaka Elfu, nayo yatatia ndani uelewaji zaidi unaotegemea vile “vitabu vya kukunja” vitakavyofunguliwa wakati huo.—Ufunuo 20:12; 22:1, 2.

47:12—Miti ya matunda inafananisha nini? Miti hiyo ya mfano inafananisha maandalizi ya kiroho ya Mungu ya kuwarudisha wanadamu kwenye ukamilifu.

48:15-19, 30-35—Jiji katika maono ya Ezekieli linafananisha nini? Jiji la “Yehova-Shama” liko katika nchi “najisi,” na hilo linaonyesha kwamba linafananisha jambo fulani la kidunia. Inaelekea kwamba jiji hilo linafananisha usimamizi wa kidunia ambao unawafaidi wote watakaofanyiza “dunia mpya” yenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Kuwa na malango kila upande kunaonyesha kwamba linaweza kuingiwa kwa urahisi. Waangalizi miongoni mwa watu wa Mungu wanapaswa kuwa wenye kufikika.

Mambo Tunayojifunza:

40:14, 16, 22, 26. Michongo ya miti ya mitende iliyokuwa kwenye miingilio ya hekalu hilo inaonyesha kwamba wale tu walio wanyoofu kiadili ndio wanaoruhusiwa kuingia. (Zaburi 92:12) Hilo linatufundisha kwamba ibada yetu inakubalika kwa Yehova ikiwa tu sisi ni wanyoofu.

44:23. Tunashukuru kama nini kwa ajili ya utumishi unaotolewa na jamii ya kikuhani leo! “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anaongoza katika kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa, chakula ambacho kinatusaidia kutambua tofauti kati ya kitu safi na kisicho safi machoni pa Yehova.—Mathayo 24:45.

47:9, 11. Ujuzi, ambao ni sehemu muhimu ya maji ya mfano, umekuwa ukiponya kwa njia ya ajabu katika siku zetu. Ujuzi huo unawapa uhai wa kiroho watu wanaoupata. (Yohana 17:3) Kwa upande mwingine, wale wasiokubali maji yanayoleta uzima ‘wataachwa kwenye chumvi,’ yaani, wataharibiwa milele. Ni muhimu kama nini ‘tufanye kabisa yote tunayoweza ili tulitumie sawasawa neno la kweli’!—2 Timotheo 2:15.

“Hakika Nitalitakasa Jina Langu Kuu”

Baada ya kumwondoa mfalme wa mwisho wa ukoo wa Daudi, Mungu wa kweli aliacha muda mrefu upite kabla ya kuja kwa Yule “aliye na haki ya kisheria” ya kuwa Mfalme. Hata hivyo, Mungu hakusahau agano lake pamoja na Daudi. (Ezekieli 21:27; 2 Samweli 7:11-16) Unabii wa Ezekieli unazungumza kumhusu “mtumishi wangu Daudi,” ambaye angekuja kuwa “mchungaji” na “mfalme.” (Ezekieli 34:23, 24; 37:22, 24, 25) Huyo si mwingine ila Yesu Kristo akiwa na nguvu za Ufalme. (Ufunuo 11:15) Yehova ‘atalitakasa jina lake kuu” kupitia Ufalme wa Kimasihi.—Ezekieli 36:23.

Hivi karibuni sana, wote wanaonajisi jina takatifu la Mungu wataharibiwa. Lakini wale wanaolitakasa jina hilo katika maisha yao kwa kumwabudu Yehova kwa njia inayokubalika watapata uzima wa milele. Basi acheni tufaidike kabisa na maji ya uzima yanayotiririka kwa wingi katika siku zetu na tuifanye ibada ya kweli iwe jambo kuu maishani mwetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa mazungumzo kuhusu Ezekieli 1:1–24:27, ona “Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—I,” katika toleo la Julai 1, 2007 (1/7/2007), la Mnara wa Mlinzi.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Hekalu tukufu la maono ya Ezekieli

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mto wa uzima katika maono ya Ezekieli unafananisha nini?

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.