Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Miujiza” Miwili Kwenye Kusanyiko Moja Huko Georgia

“Miujiza” Miwili Kwenye Kusanyiko Moja Huko Georgia

“Miujiza” Miwili Kwenye Kusanyiko Moja Huko Georgia

TUKIO moja lisilosahaulika, ambalo lilitiwa alama kwa “miujiza” miwili, lilitukia katika nchi ya Georgia mwaka wa 2006. Kwa siku tatu, kuanzia Julai 7 mpaka 9, Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la “Ukombozi Unakaribia!” lilifanywa katika maeneo sita nchini kote. Ilikuwa karamu ya kiroho iliyofurahiwa na wahudhuriaji zaidi ya 17,000.

Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 2006, jitihada zilifanywa ili kupata mahali panapofaa kwa ajili ya kusanyiko hilo la maelfu ya watu katika jiji kuu, Tbilisi, mji mkuu wa Georgia. Mahali pengine pa kusanyiko pangeunganishwa kwa simu.

Kwa miaka mingi sasa, watu wamepewa uhuru wa ibada hatua kwa hatua huko Georgia. Hivyo, ingawa kulikuwa na upinzani wakati uliopita, Mashahidi walisonga mbele, wakiwa na uhakika kwamba wangepata mahali ambapo wangefanyia kusanyiko katika mji mkuu. Kwa kawaida, watu wa Georgia ni wachangamfu sana na wakarimu. Hata hivyo, wakuu fulani wa serikali wana ubaguzi mwingi wa kidini. Je, wangebadili maoni yao na hivyo kuwaruhusu Mashahidi wakodi mahali pa kufanyia kusanyiko?

Ndugu wa Halmashauri ya Kusanyiko walitembelea viwanja mbalimbali na majumba makubwa ya michezo. Wasimamizi waliahidi kwamba Mashahidi wangetumia viwanja na majumba yao lakini wakakataa wakati ndugu walipoomba tarehe hususa ya kukodi. Hivyo, halmashauri ilishangaa wakati wasimamizi wa Tbilisi Philharmonic walipokubali Mashahidi wa Yehova wakodi jumba lao. Jumba hilo la maonyesho liko katikati ya jiji, mahali ambapo matukio mengi maarufu sana yanafanyiwa.

Wakiwa wametiwa moyo kwamba mwishowe jitihada zao zilikuwa zimefanikiwa, ndugu wa halmashauri hiyo walianza matayarisho ya kusanyiko la Tbilisi, na pia makusanyiko katika miji na majiji nchini kote, kutia ndani Tsnori, Kutaisi, Zugdidi, Kaspi, na Gori. Kazi kubwa ilifanywa ili kuunganisha kwa njia ya simu maeneo yote hayo ya makusanyiko ili programu iendeshwe wakati uleule. Kila kitu kilikuwa tayari kwa ajili ya kusanyiko. Kisha, kwa ghafula, juma moja tu kabla ya kusanyiko kuanza, wasimamizi wa jumba la maonyesho la Tbilisi Philharmonic wakafutilia mbali mapatano yaliyofanywa. Hawakueleza sababu ya kufanya hivyo.

“Muujiza” wa Kwanza

Ndugu wangefanya nini kwa siku chache tu zilizobaki? Uwezekano pekee ulikuwa kwenda kwenye mji wa Marneuli, eneo la mashambani lililo umbali wa kilomita 40 nje ya jiji la Tbilisi. Makusanyiko mengi yalikuwa yamefanywa huko kwenye uwanja wa familia moja ambayo ni ya Mashahidi wa Yehova. Zamani uwanja huo ulikuwa shamba kubwa. Kwa miaka kumi iliyopita, hapo ndipo mahali pekee ambapo makutaniko ya Tbilisi yalifanyia makusanyiko. Hata hivyo, Marneuli pia ni mahali ambapo Mashahidi wa Yehova wameshambuliwa mara nyingi na umati wa watu wenye hasira.

Shambulio moja lilitukia mnamo Septemba 16, 2000. Polisi kutoka jiji la Marneuli waliweka vizuizi barabarani ili kuzuia Mashahidi wasiende mahali pa kusanyiko. Kisha, mabasi yaliyojaa majambazi yakafika. Mabasi hayo yaliongozwa na Vasili Mkalavishvili aliyeachishwa ukasisi katika kanisa la Othodoksi. Majambazi hao walisimamisha magari na mabasi yaliyoelekea kwenye kusanyiko huko Marneuli, wakawaburuta wajumbe wengi kutoka kwenye magari, na kuwapiga bila huruma. Wasafiri wengine waliibiwa vitu vyao, kutia ndani Biblia na vichapo vya Biblia.

Mahali pa kusanyiko huko Marneuli palivamiwa pia na umati wa watu 60 hivi. Mashahidi 40 hivi waliumizwa. Ndugu mmoja alidungwa kisu kifuani. Washambuliaji wengine walitikisa bunduki zao, na kufyatua risasi hewani kwa hasira. Mmoja wao alimwelekezea dada mwenye uwanja huo bunduki na kumwomba pesa na vito. Umati huo ulipekua-pekua nyumba yake ambayo ilikuwa pembeni mwa uwanja, na wakaiba vitu vyake vyenye thamani. Baada ya kuvunja madirisha yote ya nyumba hiyo, walichoma moto vichapo vya Biblia na viti ambavyo vilitengenezwa hasa kwa ajili ya kusanyiko. Tani moja na nusu ya vichapo iliharibiwa. Badala ya kusimamisha uhalifu huo, polisi waliokuja mahali hapo walishiriki katika kuwatendea Mashahidi jeuri. *

Halmashauri ya Kusanyiko ilipaswa kukabiliana si tu na tishio la jeuri bali pia ugumu wa kufanyia kusanyiko la watu 5,000 mahali ambapo kwa kawaida panatoshea watu 2,500 hivi. Tatizo hilo lingetatuliwa jinsi gani kwa muda huo mfupi? Ilionekana kama muujiza wakati wamiliki wa mashamba mawili yaliyokuwa karibu na mahali hapo walipowaendea akina ndugu na kupendekeza kwamba wakodi mashamba yao.

Kugeuza mashamba hayo yawe mahali panapofaa kufanyia kusanyiko ilikuwa kazi ngumu. Hali ya hewa ilifanya mambo yawe magumu sana, kwa kuwa mvua ilinyesha juma zima kabla ya kusanyiko. Viazi vilikuwa vimepandwa katika mashamba hayo, navyo vilipaswa kuvunwa. Kwanza, wajitoleaji walichimbua viazi huku mvua ikinyesha. Kisha, nyua ziliondolewa na paa zikajengwa za kuwakinga wasikilizaji na jua na mvua. Viti zaidi vya mbao vilihitaji kutengenezwa, na vifaa vya sauti vya ziada kuwekwa. Wajitoleaji walikata na kutoboa mbao, nao wakapigilia misumari. Walifanya kazi hiyo usiku na mchana, na wengine hata walijinyima usingizi.

Kila mtu alijiuliza, “Itakuwa namna gani ikiwa mvua itaendelea wakati wa kusanyiko? Je, wajumbe watazama na kutoweka ndani ya matope ya eneo hili?” Majani makavu yalinunuliwa ili kufunika udongo uliolowa. Mwishowe, jua liliangaza! Kwa siku zote tatu za kusanyiko, udongo ulipigwa na joto la jua jangavu.

Wajumbe walipofika, mazingira yalikuwa mazuri sana. Mazingira hayo yenye utulivu yalionekana kama yale ya ulimwengu mpya. Wakiwa wameketi kwa starehe, wajumbe walizungukwa na mitini, miti mingine ya matunda, mashamba ya mahindi, na nyanya. Sehemu ya nyuma ya jukwaa ilipambwa kwa mizabibu. Pindi kwa pindi wakati wa programu, wasikilizaji walisikia majogoo yakiwika na sauti za kuku wakati mayai yao yalipokuwa yakikusanywa. Kulikuwa na sauti nyingine zinazosikika tu mashambani, lakini kwa wahudhuriaji, sauti hizo zote zilikuwa zenye kuburudisha. Wasikilizaji hawakukengeushwa na sauti hizo kwa sababu walitaka kusikiliza kwa makini programu bora iliyotegemea Biblia. Hata hivyo, hizo hazikuwa pindi pekee zisizosahauliwa za kusanyiko hilo.

“Muujiza” wa Pili

Mwishoni mwa kipindi cha Ijumaa (Siku ya 5) asubuhi, wajumbe walishangaa sana wakati mshiriki mmoja wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, Geoffrey Jackson, alipotangaza kutolewa kwa chapa nzima ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kigeorgia. * Wengi walijawa na machozi, na walistaajabu sana. Familia moja ilisema hivi kwa msisimko: “Hatuwezi kuacha kushukuru kwa ajili ya muujiza huu, muujiza wa Yehova. Kazi kubwa kama hiyo kwa muda mfupi sana!”

Dada mmoja kutoka mji wa Tsalendjikha ambaye alisikiliza programu kwa simu alisema hivi: “Siwezi kueleza shangwe ambayo nilihisi tulipopokea Biblia nzima. Ninawashukuru kwa kusanyiko hili nzuri sana la siku tatu. Kwa kweli, lilikuwa tukio la kihistoria.” Familia fulani katika kutaniko moja lililo kwenye mpaka wa Bahari Nyeusi, magharibi mwa Georgia, ilisema hivi: “Kufikia sasa, tulikuwa tu na Biblia moja katika familia yetu, lakini sasa kila mmoja kati yetu wanne ana nakala yake ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Sasa kila mmoja wetu anaweza kujifunza Biblia kibinafsi.”

Hata hivyo, wahudhuriaji hawakujua kwamba mambo yote hayakwenda sawa. Kwa mfano, ingawa Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilichapishwa na kutumwa Georgia kwa wakati kwa ajili ya kusanyiko, wakuu wa Idara ya Forodha hawakuruhusu Biblia hizo kuingizwa Georgia. Akina ndugu walizungumza na Ofisi ya Mchunguzi wa Malalamiko ya Wananchi wa Georgia. Mchunguzi huyo aliruhusu Biblia hizo kuingizwa nchini kwa wakati unaofaa kabisa kwa ajili ya kusanyiko la wilaya. Hata alimtuma msaidizi wake kwenye kusanyiko la Marneuli ili achukue nakala kadhaa za Biblia mpya kwa ajili ya ofisi yao.

Kukaribishwa kwa Uchangamfu, Kulingana na Utamaduni wa Georgia

Kuna sababu nyingine iliyofanya kusanyiko la wilaya la Marneuli liwe la pekee sana kwa Mashahidi wa Yehova wa Georgia. Mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alishiriki kwenye programu. Wahudhuriaji wote walisisimka sana hivi kwamba kila mtu alitaka kumkaribisha kwa uchangamfu kulingana na utamaduni wao. Ndugu Jackson alilazimika kusimama na kusalimu ndugu na dada kwa saa nyingi kabla, wakati, na baada ya kusanyiko, lakini alikubali kwa furaha kufanya hivyo.

Mapema mwaka wa 1903 mwishoni mwa kusanyiko moja, ndugu mmoja alisema hivi: “Singekubali kupewa dola elfu moja badala ya faida zote ambazo nimepokea kwenye kusanyiko hili, ingawa mimi ni maskini.” Zaidi ya karne moja baadaye, hizo hasa ndizo hisia za Mashahidi ambao walihudhuria makusanyiko ya pekee sana yaliyofanywa mwaka wa 2006 nchini Georgia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa habari zaidi kuhusu mateso ya Mashahidi wa Yehova huko Georgia, ona gazeti la Amkeni! la Januari 22, 2002, ukurasa wa 18-24.

^ fu. 16 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya Kigeorgia ilitolewa mwaka wa 2004.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

“Mdogo” Ameongezeka

Maneno ya Isaya 60:22 yamethibitika kuwa ya kweli huko Georgia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” Katika muda usiozidi miaka 20, hesabu ya wahubiri wa Ufalme huko Georgia imeongezeka kutoka wahubiri wasiozidi 100 mpaka 16,000 hivi. Wahudumu hao wenye bidii wa Neno la Mungu wanaongoza karibu mafunzo ya Biblia 8,000 kila juma. Hilo linaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa ongezeko zaidi huko Georgia.

[Picha katika ukurasa wa 16]

 

MUUNGANO WA URUSI

GEORGIA

⇨ Zugdidi

⇨ Kutaisi

Marneuli ⇨ Gori

⇨ Kaspi

⇨ Tsnori

TBILISI

UTURUKI

ARMENIA

AZERBAIJAN

[Hisani]

Globe: Based on NASA/Visible Earth imagery

[Picha katika ukurasa wa 16]

Sanamu huko Tbilisi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kusanyiko la Marneuli liliunganishwa kwa simu ya mkononi na maeneo mengine tano

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wajumbe walishangaa kwa furaha wakati chapa nzima ya “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” ya Kigeorgia ilipotolewa