Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ee Yehova, Unijaribu’

‘Ee Yehova, Unijaribu’

‘Ee Yehova, Unijaribu’

“YEHOVA ndiye mchunguzaji wa mioyo.” (Methali 17:3) Hilo linapaswa kututia moyo sana sisi sote. Kwa nini? Kwa sababu tofauti na wanadamu ambao wanahukumu kwa kutegemea tu sura ya nje, Baba yetu wa mbinguni “huona jinsi moyo ulivyo.”—1 Samweli 16:7.

Kwa kweli, hata sisi wenyewe hatuwezi kuchunguza kwa njia bora nia na mielekeo yetu ya ndani kabisa. Kwa nini? Kwa sababu ‘moyo wetu ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?’ Kwa kweli, Mungu anaujua, kwa sababu anatangaza hivi: “Mimi, Yehova, ninauchunguza moyo, ninazikagua figo.” (Yeremia 17:9, 10) Ndiyo, Yehova anaelewa “moyo,” kutia ndani mielekeo yetu ya ndani, na pia “figo,” yaani, mawazo na hisia zetu za ndani kabisa.

Kwa Nini Tujaribiwe?

Kwa hivyo, haishangazi kwamba Mfalme Daudi wa kale alimwambia Mungu hivi: “Unichunguze, Ee Yehova, na kunijaribu; usafishe figo zangu na moyo wangu.” (Zaburi 26:2) Je, matendo na maneno ya Daudi yalikuwa safi kabisa, hivi kwamba hakuwa na sababu yoyote ya kuogopa kujaribiwa na Yehova? Bila shaka hapana! Daudi alikuwa mtu kama sisi, hakuwa mkamilifu na hangeweza kufuata viwango vya Mungu kwa ukamilifu. Kwa sababu ya udhaifu wake, Daudi alitenda makosa mengi mazito, hata hivyo, ‘alitembea kwa utimilifu wa moyo.’ (1 Wafalme 9:4) Jinsi gani? Kwa kukubali karipio na kurekebisha njia yake. Kwa kufanya hivyo alionyesha kwamba alimpenda Yehova kikweli. Alijitoa kwa Mungu kikamili.

Namna gani sisi leo? Yehova anajua kwamba sisi si wakamilifu na kwamba tunaweza kutenda dhambi kwa maneno na matendo. Hata hivyo, hatumii uwezo wake wa kujua kimbele wakati wetu ujao ili kuongoza maisha yetu. Alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua, naye anaheshimu uhuru wetu wa kuchagua. Uhuru huo ni zawadi ambayo ametupa kwa fadhili.

Hata hivyo, nyakati nyingine Yehova anajaribu utu wetu wa ndani katika mambo fulani, kutia ndani nia zetu. Anaweza kufanya hivyo kwa kutupa nafasi za kuonyesha hali ya moyo wetu. Anaweza pia kuruhusu hali au matatizo mbalimbali yafunue mielekeo yetu ya ndani kabisa. Mambo hayo yanatupa nafasi ya kumwonyesha Yehova ujitoaji na ushikamanifu wetu. Majaribu kama hayo ambayo Yehova anaruhusu yanaweza kuonyesha wazi hali ya imani yetu, kama sisi ni “kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.”—Yakobo 1:2-4.

Jaribu la Kale la Imani

Majaribu ya imani na ya mielekeo si mambo mapya kwa watumishi wa Yehova. Mfikirie mzee wa ukoo Abrahamu. “Mungu wa kweli akamjaribu Abrahamu.” (Mwanzo 22:1) Maneno hayo yaliposemwa, imani ya Abrahamu katika Mungu ilikuwa tayari imejaribiwa. Makumi ya miaka mapema, Yehova alikuwa amemwomba Abrahamu ahame pamoja na familia yake kutoka katika jiji lenye ufanisi la Uru na kwenda katika nchi asiyoijua. (Mwanzo 11:31; Matendo 7:2-4) Abrahamu ambaye huenda alikuwa na nyumba huko Uru, hakununua nyumba yoyote huko Kanaani, ambako aliishi kwa miaka 100 hivi. (Waebrania 11:9) Maisha ya Abrahamu ya kuhama-hama yalimfanya yeye na familia yake wakabili hatari kama vile njaa kali, vikundi vya watu wenye silaha, na watawala wapagani wa eneo hilo. Kupitia yote hayo, imani ya Abrahamu ilithibitika kuwa bora kabisa.

Kisha Yehova akamjaribu Abrahamu kwa njia kubwa zaidi. “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana, Isaka, . . . umtoe kama toleo la kuteketezwa.” (Mwanzo 22:2) Isaka hakuwa mwana yeyote tu kwa Abrahamu. Alikuwa mtoto pekee wa Abrahamu na mke wake, Sara. Isaka alikuwa mwana aliyeahidiwa, mwana ambaye Abrahamu alitumaini kwamba kupitia kwake “uzao” wake ungerithi nchi ya Kanaani na kuwaletea wengi baraka, kama Mungu alivyoahidi. Kwa kweli, Isaka alikuwa mwana ambaye Abrahamu alitazamiwa kupata na ambaye alizaliwa kimuujiza kwa uwezo wa Mungu.—Mwanzo 15:2-4, 7.

Unaweza kuwazia jinsi ilivyokuwa vigumu kwa Abrahamu kuelewa amri hiyo. Je, Yehova angetaka mwanadamu atolewe kuwa dhabihu? Kwa nini Yehova amruhusu Abrahamu aonje kwa muda mfupi tu shangwe ya pekee ya kupata mwana katika miaka ya mwisho ya maisha yake, kisha amwambie amtoe mwana huyo kuwa dhabihu? *

Abrahamu alitii mara moja bila kujua vizuri majibu ya maswali hayo. Alisafiri siku tatu ili kufika kwenye mlima uliochaguliwa. Alijenga madhabahu kwenye mlima huo na kuweka kuni juu yake. Sasa kilele cha jaribu hilo kikafika. Abrahamu alichukua kisu cha kuchinjia, lakini alipokuwa akijitayarisha kumuua mwana wake, Yehova alimtumia malaika kumzuia na kumwambia: “Sasa mimi najua kwamba wewe unamwogopa Mungu kwa kuwa hukunizuilia mwana wako, mwana wako wa pekee.” (Mwanzo 22:3, 11, 12) Hebu fikiria jinsi Abrahamu alivyofurahi aliposikia maneno hayo! Makadirio ya Yehova kuhusu imani ya Abrahamu yalikuwa sahihi. (Mwanzo 15:5, 6) Hivyo, Abrahamu alimdhabihu kondoo-dume badala ya Isaka. Kisha, Yehova akathibitisha ahadi za agano kuhusu uzao wa Abrahamu. Hiyo ndiyo sababu Abrahamu alikuja kuitwa rafiki ya Yehova.—Mwanzo 22:13-18; Yakobo 2:21-23.

Imani Yetu Inajaribiwa Pia

Sote tunatambua kwamba watumishi wa Mungu leo hawawezi kuepuka majaribu. Hata hivyo, huenda tukajaribiwa na yale ambayo Yehova anaruhusu yatukie badala ya yale anayotuambia tufanye.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Mateso hayo yanaweza kutokana na wanashule wenzetu, marafiki, watu wa jamaa yetu, majirani, au wenye mamlaka wa serikali walio na habari za uwongo kutuhusu. Mateso hayo yanaweza kutia ndani Mkristo kutukanwa, kutendewa vibaya au hata kuzuiwa kupata riziki. Wakristo wa kweli pia wanapata matatizo ambayo yanawapata wanadamu kwa kawaida kama vile magonjwa, kukatishwa tamaa, na kutendewa isivyo haki. Mateso hayo yote yanajaribu imani ya mtu.

Mtume Petro alikazia faida za kujaribiwa kwa imani yetu: “Mmehuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali, ili sifa iliyojaribiwa ya imani yenu, iliyo na thamani kubwa zaidi kuliko dhahabu ambayo huharibika ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, ipatikane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.” (1 Petro 1:6, 7) Ndiyo, matokeo ya majaribu yanalinganishwa na kusafisha dhahabu kwa moto. Kazi hiyo ya kusafisha inaondoa uchafu na kuacha dhahabu safi. Imani yetu inasafishwa kwa njia kama hiyo.

Kwa mfano, aksidenti au msiba wa kiasili unaweza kusababisha hali ngumu. Hata hivyo, wale walio na imani ya kweli hawashindwi na mahangaiko yasiyo ya lazima. Wanafarijiwa na uhakikisho huu wa Yehova: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Wanaendelea kutanguliza mambo ya kiroho, wakiwa na hakika kwamba Yehova Mungu atabariki jitihada zao za kupata mahitaji yao ya lazima. Imani yao inawasaidia kuvumilia nyakati ngumu na kuwazuia wasifanye maisha yao yawe magumu bila sababu kwa kuhangaika isivyo lazima.

Uhakika wa kwamba majaribu yanaweza kufunua udhaifu wa imani yetu unaweza pia kutufaidi ikiwa tutaona uhitaji wa kuchukua hatua za kurekebisha udhaifu huo. Mtu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninaweza jinsi gani kuitia nguvu imani yangu? Je, ninahitaji kutumia wakati zaidi kusali na kutafakari kuhusu Neno la Mungu? Je, ninafaidika kabisa na mpango wa kuhudhuria mikutano pamoja na waamini wenzangu? Je, ninajitegemea badala ya kumjulisha Yehova Mungu mahangaiko yangu katika sala?’ Hata hivyo, kujichunguza kibinafsi kwa njia hiyo ni mwanzo tu.

Ili mtu aitie nguvu imani yake, anahitaji kuongeza hamu yake ya kiroho na kuonyesha kwamba ana “tamaa kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno.” (1 Petro 2:2; Waebrania 5:12-14) Tunapaswa kujitahidi kuwa kama mtu ambaye alifafanuliwa na mtunga-zaburi: “Mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.”—Zaburi 1:2.

Hilo linatia ndani mengi zaidi ya kusoma tu Biblia. Ni jambo la maana tufikirie yale ambayo tunasoma katika Neno la Mungu na kufuata mashauri yake. (Yakobo 1:22-25) Tukifanya hivyo, upendo wetu kwa Mungu utaongezeka, tutatoa sala zilizo wazi na za kutoka moyoni, na imani yetu katika Mungu itakuwa na nguvu zaidi.

Thamani ya Imani Iliyojaribiwa

Kujua kwamba imani ni ya maana kabisa ili tukubaliwe na Mungu kunatuchochea ili tuitie nguvu. Biblia inatukumbusha hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Kwa hiyo, tunapaswa kuhisi kama yule mtu aliyemsihi Yesu hivi: “Unisaidie mahali ambapo ninahitaji imani!”—Marko 9:24.

Majaribu ya imani yetu yanaweza pia kuwasaidia wengine. Kwa mfano, Mkristo anapofiwa na mpendwa wake, imani yake yenye nguvu katika ahadi ya Mungu ya ufufuo inamsaidia kuvumilia. Anaomboleza, lakini ‘hawi na huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.’ (1 Wathesalonike 4:13, 14) Watu wengine ambao wanaona nguvu zenye kuimarisha za imani ya Mkristo huyo, wanaweza kutambua kwamba ana kitu chenye thamani kubwa sana. Huenda hilo likaamsha katika mioyo yao tamaa ya kuwa na imani kama hiyo. Tamaa hiyo inaweza kuwachochea wajifunze Neno la Mungu na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.

Yehova anajua kwamba imani iliyojaribiwa ina thamani kubwa. Kwa kuongezea, majaribu ya imani yanatuwezesha kuona ikiwa imani yetu kwa kweli ina nguvu za kutusaidia kuvumilia. Majaribu yanatusaidia kutambua udhaifu katika imani yetu, na hivyo kutuwezesha kurekebisha mambo. Mwishowe, tunapopambana na majaribu kwa mafanikio tunaweza kuwasaidia wengine kuwa wanafunzi wa Yesu. Kwa hivyo, na tufanye yote tunayoweza ili kudumisha imani yenye nguvu, imani ambayo baada ya kukabili jaribu moja baada ya lingine ‘itapatikana kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.’—1 Petro 1:7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kuhusu maana ya mfano ya “dhabihu” ya Isaka, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1989 (1/7/1989), ukurasa wa 22.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Matendo ya Abrahamu ya imani yalimfanya awe rafiki ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 15]

Majaribu yanaweza kuthibitisha kwamba imani yetu ina nguvu zinazotusaidia kabisa kuvumilia

[Picha katika ukurasa wa 12]

From the Illustrated Edition of the Holy Scriptures, by Cassell, Petter, & Galpin