Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatumia neno “kutaniko” katika njia gani nne?

Neno hilo linatumiwa kwanza kuhusu kikundi chenye washiriki wengi cha Wakristo watiwa-mafuta (maandiko fulani yanatia ndani Kristo). Nyakati nyingine, “kutaniko la Mungu” linamaanisha Wakristo wote wanaoishi katika kipindi fulani. Maana ya tatu inawahusu Wakristo wote wanaoishi katika eneo fulani. Mwishowe, neno hilo linaweza kutumiwa kuhusu watu wanaofanyiza kutaniko la mahali fulani.—4/15, ukurasa wa 21-23.

• Wakristo wanaacha kupata mwito wa tumaini la kimbingu wakati gani?

Biblia haitoi jibu kamili kwa swali hilo. Mwito huo ulianza mwaka wa 33 W.K. na uliendelea mpaka nyakati za kisasa. Baada ya mwaka wa 1935, kazi ya kufanya wanafunzi ilihusu hasa kukusanywa kwa umati mkubwa. Wakristo fulani waliobatizwa baada ya mwaka wa 1935 wameshuhudiwa na roho takatifu kwamba wana tumaini la kimbingu, hivyo hatuwezi kuweka tarehe kamili ambayo Wakristo wanaacha kupokea mwito huo. Watiwa-mafuta wa kweli hawana kiasi kikubwa zaidi cha roho ya Mungu kuliko waandamani wao wa kondoo wengine, wala hawatazamii watendewe kwa njia ya pekee. Wakristo wanahitaji kuwa waaminifu na kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu hata iwe wana tumaini gani.—5/1, ukurasa wa 30-31.

• Yeftha alipoweka nadhiri yake, je, alikuwa tayari kumtoa binti yake kuwa toleo la kuteketezwa kwa Mungu?

Hapana. Yeftha alimaanisha kwamba angemtoa yule ambaye angekuja kumpokea ili amtumikie Mungu kikamili, mpango ambao uliruhusiwa na Sheria ya Musa. (1 Samweli 2:22) Binti ya Yeftha alitimiza nadhiri ya baba yake kwa kuendelea kutumika katika maskani. Ilikuwa dhabihu kubwa sana kwa sababu ilimaanisha hangeolewa kamwe.—5/15, ukurasa wa 9-10.

• Kodeksi ilisaidia jinsi gani katika miaka ya mapema ya Ukristo?

Inaonekana kwamba Wakristo walitumia hasa kitabu cha kukunjwa, angalau mpaka mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Katika karne iliyofuata, kulikuwa na ubishi kati ya watu waliopendelea kodeksi na wale waliopendelea kitabu cha kukunjwa. Wataalamu wanaamini kwamba kodeksi ilianza kupendwa na watu wengi kwa sababu Wakristo waliitumia.—6/1, ukurasa wa 14-15.

• Kalenda ya Gezeri ni nini?

Ni bamba dogo la chokaa ambalo liligunduliwa mwaka wa 1908 mahali ambapo jiji la Gezeri lilikuwa. Watu wengi wanafikiri kwamba mvulana wa shule aliandika kwenye bamba hilo kama sehemu ya kazi yake ya shule. Bamba hilo lina maandishi yasiyo na maelezo mengi kuhusu chati ya mwaka au mzunguko wa kilimo, kuanzia mwezi wa kukusanya ambao unalingana na Septemba/Oktoba (Mwezi wa 9/10) na linataja mazao na shughuli mbalimbali za kilimo.—6/15, ukurasa wa 8.

• Ni nini maana ya kuitendea dhambi roho takatifu?

Mtu anaweza kuitendea roho takatifu ya Yehova dhambi ambayo haitasamehewa. (Mathayo 12:31) Mungu ndiye anayeamua kama tumetenda dhambi isiyosamehewa, naye anaweza kutuondolea roho yake. (Zaburi 51:11) Tukihuzunika sana kwa sababu ya dhambi ambayo tumetenda, inaelekea sana kwamba tumetubu kikweli na hivyo hatujaitendea dhambi roho takatifu.—7/15, ukurasa wa 16-17.

• Kwa nini Mfalme Sauli aliuliza Daudi ni mwana wa nani hata ingawa mapema alikuwa ameshirikiana naye? (1 Samweli 16:22; 17:58)

Sauli hakutaka tu kujua jina la baba ya Daudi. Baada ya kuona kwamba Daudi alikuwa mtu mwenye imani na ujasiri ambaye alikuwa ametoka tu kumshinda Goliathi, Sauli alitaka kujua ni mtu wa aina gani aliyemlea mvulana kama huyo. Huenda Sauli alifikiria kumwingiza Yese, au watu wengine wa familia yake katika jeshi.—8/1, ukurasa wa 31.