Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kufaidika Kwa Kuvumilia Mateso

Tunaweza Kufaidika Kwa Kuvumilia Mateso

Tunaweza Kufaidika Kwa Kuvumilia Mateso

“Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.”—YAKOBO 5:11.

1, 2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hakukusudia mwanadamu ateseke?

HAKUNA mtu aliye na akili timamu anayetaka kuteseka; wala Muumba wetu, Yehova Mungu, hataki wanadamu wateseke. Tunaweza kuona hilo tunapochunguza Neno lake lililoongozwa na roho na kuona yale yaliyotukia baada ya yeye kumuumba mwanamume na mwanamke. Kwanza, Mungu alimuumba mwanamume. “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Adamu alikuwa mkamilifu kimwili na kiakili, naye hangekuwa mgonjwa wala kufa.

2 Adamu alikuwa na maisha ya namna gani? “Yehova Mungu akapanda bustani katika Edeni, kuelekea mashariki, na hapo akamweka mtu ambaye alikuwa amemfanya. Hivyo Yehova Mungu akachipusha katika nchi kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa ajili ya chakula.” (Mwanzo 2:8, 9) Ndiyo, Adamu alikuwa na makao mazuri sana. Hakukuwa na mateso Edeni.

3. Wenzi wawili wa kwanza walikuwa na matarajio gani?

3 Andiko la Mwanzo 2:18 linatueleza hivi: “Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’” Yehova akamuumbia Adamu mwanamke mkamilifu, na hilo likafanya kuwe na uwezekano wa kutarajia maisha ya familia yenye furaha. (Mwanzo 2:21-23) Zaidi ya hilo, Biblia inatueleza hivi: “Mungu akawabariki na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.’” (Mwanzo 1:28) Wanadamu hao wawili wa kwanza wangekuwa na pendeleo zuri ajabu la kuipanua Paradiso ya Edeni mpaka, mwishowe, ienee duniani, na hivyo kuifanya dunia yote kuwa paradiso. Na wangezaa watoto wenye furaha ambao hawangeteseka. Ungekuwa mwanzo mzuri kama nini!—Mwanzo 1:31.

Mwanzo wa Mateso

4. Historia inaonyesha jambo gani la wazi kuhusu wanadamu?

4 Hata hivyo, tunapotazama hali za wanadamu katika historia yote, ni wazi kwamba jambo fulani lilifanya hali zikawa mbaya sana. Mambo mabaya yametokea, na jamii ya wanadamu imeteseka sana. Kwa karne nyingi, wazao wote wa Adamu na Hawa wamekuwa wagonjwa, wamezeeka, na mwishowe wamekufa. Bila shaka, dunia si paradiso wala haijajaa watu wenye furaha. Hali hiyo inaelezwa kwa usahihi kwenye Waroma 8:22: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.”

5. Wazazi wetu wa kwanza walihusika jinsi gani katika kuiletea mateso jamii ya wanadamu?

5 Yehova hapaswi kulaumiwa kwa sababu ya mateso makubwa ambayo yamekuwapo kwa miaka mingi sana. (2 Samweli 22:31) Kwa kiasi fulani, wanadamu ndio wanaopaswa kulaumiwa. “Wametenda kwa uharibifu, wametenda kwa njia yenye kuchukiza katika shughuli zao.” (Zaburi 14:1) Wazazi wetu wa kwanza walipewa kila kitu kizuri ili waanze maisha vizuri. Walichohitaji kufanya tu ili waendelee na maisha hayo ni kumtii Mungu, lakini Adamu na Hawa walichagua kutomtegemea Yehova. Kwa kuwa wazazi wetu wa kwanza walimkataa Yehova, hangewategemeza tena ili waendelee kuwa wakamilifu. Mwili wao ungeendelea kuharibika mpaka wafe. Tumerithi kutokamilika.—Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12.

6. Shetani alitimiza sehemu gani katika kuleta mateso?

6 Mwingine aliyehusika pia katika kuleta mateso yote haya ni yule kiumbe wa roho ambaye alikuja kuwa Shetani Ibilisi. Alipewa zawadi ya uhuru wa kuchagua. Hata hivyo, alitumia vibaya uwezo huo kwa kujaribu kupata ibada. Lakini, ni Yehova tu ndiye anayepaswa kuabudiwa, wala si uumbaji wake. Shetani ndiye aliyewashawishi Adamu na Hawa wachague kutomtegemea Yehova, kana kwamba kwa kufanya hivyo ‘wangekuwa kama Mungu, wakijua mema na mabaya.’—Mwanzo 3:5.

Yehova Pekee Ndiye Aliye na Haki ya Kutawala

7. Matokeo ya kumwasi Yehova yameonyesha nini?

7 Matokeo mabaya ya uasi yanaonyesha kwamba Yehova peke yake, akiwa Mwenye Enzi Kuu, ndiye aliye na haki ya kutawala na kwamba utawala wake tu ndio wa uadilifu. Maelfu ya miaka iliyopita imeonyesha kwamba Shetani, ambaye alikuja kuwa “mtawala wa ulimwengu huu,” ameendeleza utawala mwovu, usio wa uadilifu, na wenye jeuri ambao hauridhishi watu kamwe. (Yohana 12:31) Utawala wa muda mrefu na wenye taabu wa wanadamu chini ya uongozi wa Shetani, umeonyesha pia kwamba hawana uwezo wa kutawala kwa uadilifu. (Yeremia 10:23) Hivyo, utawala wowote usiotokana na Yehova hauwezi kufanikiwa. Historia imethibitisha jambo hilo kuwa la kweli kabisa.

8. Yehova anakusudia nini kuhusu aina zote za utawala wa wanadamu, naye atatimiza kusudi hilo jinsi gani?

8 Kwa kuwa sasa Yehova ameruhusu maelfu ya miaka ili wanadamu wajaribu kujitawala bila kumtegemea, ana haki ya kuondoa aina zote hizo za utawala duniani na kuweka serikali yake mwenyewe. Unabii mmoja kuhusu serikali hiyo unasema hivi: “Katika siku za wafalme hao [utawala wa wanadamu], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali yake ya kimbingu mikononi mwa Kristo] ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Utawala wa roho waovu na wanadamu utakomeshwa, na Ufalme wa kimbingu wa Mungu ndio tu utakaokuwapo na kuitawala dunia. Kristo atakuwa Mfalme, naye atatawala pamoja na wanadamu waaminifu 144,000 ambao wamechukuliwa kutoka duniani.—Ufunuo 14:1.

Kufaidika Kutokana na Mateso

9, 10. Yesu alifaidika jinsi gani kutokana na mambo aliyoteseka?

9 Ni jambo la maana kuchunguza sifa za kustahili za wale ambao watatawala katika Ufalme wa kimbingu. Kwanza, Kristo Yesu alionyesha jinsi alivyo na sifa za kustahili kutimiza daraka lake la kuwa Mfalme. Aliishi kwa miaka mingi sana isiyojulikana pamoja na Yehova akifanya mapenzi ya Baba yake, huku akiwa ‘stadi Wake wa kazi.’ (Methali 8:22-31) Yehova alipofanya mipango ili Yesu aje duniani, Yesu alikubali kwa kupenda. Akiwa duniani, alijitahidi hasa kuwaambia wengine kuhusu enzi kuu ya Yehova na Ufalme wake. Yesu alituwekea sote kielelezo kwa kujitiisha kabisa kwa enzi kuu hiyo.—Mathayo 4:17; 6:9.

10 Yesu aliteswa na mwishowe akauawa. Wakati wa huduma yake, aliona hali zenye kusikitisha za wanadamu. Je, alifaidika kwa njia yoyote kutokana na mambo aliyoyaona na kuteseka yeye binafsi? Ndiyo. Andiko la Waebrania 5:8 linasema hivi: “Ijapokuwa yeye alikuwa Mwana [wa Mungu], alijifunza kutii kutokana na mambo aliyoteseka.” Mambo yaliyompata Yesu alipokuwa duniani yalimfanya aelewe mambo zaidi na awe mwenye huruma zaidi. Alijionea mwenyewe hali ya jamii ya wanadamu. Aliwasikitikia wale wanaoteseka na hivyo kuelewa vizuri zaidi daraka lake la kuwasaidia. Ona jinsi ambavyo mtume Paulo anaonyesha hilo katika kitabu cha Waebrania: “Alipaswa kuwa kama ‘ndugu’ zake katika mambo yote, ili awe kuhani mkuu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu, kusudi atoe dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi za watu. Kwa kuwa yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akijaribiwa, anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.” “Tuna kuhani mkuu, si mtu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi. Basi na tukikaribie, tukiwa na uhuru wa kusema, kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa, ili tupokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.”—Waebrania 2:17, 18; 4:14-16; Mathayo 9:36; 11:28-30.

11. Mambo yaliyowapata wafalme na makuhani hao wakiwa duniani yatawasaidia jinsi gani watakapotawala?

11 Mengi pia yanaweza kusemwa kuhusu wale 144,000 ambao “walinunuliwa” kutoka duniani ili watawale pamoja na Kristo Yesu katika Ufalme wa kimbingu. (Ufunuo 14:4) Wote walizaliwa wakiwa wanadamu duniani, wakalelewa katika ulimwengu uliojaa mateso, na wakateseka pia. Wengi wao waliteswa, na wengine hata waliuawa kwa sababu ya kuwa watimilifu kwa Yehova na kuwa tayari kumfuata Yesu. Lakini ‘hawakuona aibu juu ya ule ushahidi kumhusu Bwana wao, wakishiriki sehemu yao katika kuvumilia uovu kwa ajili ya habari njema.’ (2 Timotheo 1:8) Mambo yaliyowapata duniani yanawafanya wawe na sifa za kustahili ili kuihukumu jamii ya wanadamu kutoka mbinguni. Wamejifunza kuwa wenye huruma na wenye fadhili zaidi, na tayari kuwasaidia watu.—Ufunuo 5:10; 14:2-5; 20:6.

Furaha kwa Wale Walio na Tumaini la Kuishi Duniani

12, 13. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kufaidika jinsi gani kutokana na mateso?

12 Je, mateso ya sasa yanaweza kuwafaidi wale wanaotumaini kuishi milele katika paradiso duniani bila magonjwa, huzuni, na kifo? Kwa kweli maumivu na taabu zinazotokana na mateso hazipendezi hata kidogo. Lakini tunapovumilia mateso kama hayo, sifa zetu nzuri zinaweza kuboreshwa na hivyo tunapata furaha.

13 Ona yale ambayo Neno la Mungu lililoongozwa na roho linasema kuhusu hilo: “Hata mkiteseka kwa ajili ya uadilifu, ninyi ni wenye furaha.” “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha.” (1 Petro 3:14; 4:14) “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mathayo 5:11, 12) “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.”—Yakobo 1:12.

14. Ni katika maana gani mateso yanawafanya waabudu wa Yehova wawe wenye furaha?

14 Bila shaka, si mateso tunayovumilia sasa yanayotufanya tuwe wenye furaha. Furaha na kuridhika kunatokana na kujua kwamba tunateseka kwa sababu tunafanya mapenzi ya Yehova na kufuata kielelezo cha Yesu. Kwa mfano, katika karne ya kwanza, mitume fulani walifungwa gerezani, wakapelekwa mbele ya mahakama kuu ya Wayahudi, na kushtakiwa kwa sababu ya kuhubiri kuhusu Yesu Kristo. Walipigwa viboko na baadaye wakaachiliwa huru. Walikuwa na mtazamo gani? Masimulizi ya Biblia yanasema kwamba ‘walitoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 5:17-41) Hawakufurahia kupigwa viboko na maumivu ya kimwili yaliyotokana na kupigwa huko. Walifurahi kwa kuwa walielewa kwamba walipigwa kwa sababu walishika utimilifu wao kwa Yehova na kufuata hatua za Yesu.—Matendo 16:25; 2 Wakorintho 12:10; 1 Petro 4:13.

15. Kuvumilia mateso sasa kunaweza kutusaidia jinsi gani wakati ujao?

15 Tukivumilia upinzani na mateso tukiwa na mtazamo mzuri, mateso hayo yanaweza kujenga ndani yetu sifa ya uvumilivu. Hilo litatusaidia kuvumilia mateso wakati ujao. Tunasoma hivi: “Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapokutana na majaribu ya namna mbalimbali, mkijua kwamba sifa iliyojaribiwa ya imani yenu hutokeza uvumilivu.” (Yakobo 1:2, 3) Vivyo hivyo, andiko la Waroma 5:3-5 linatueleza hivi: “Na tufurahi tukiwa katika dhiki, kwa kuwa tunajua kwamba dhiki hutokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini, nalo tumaini halikatishi tamaa.” Kwa hivyo, kadiri tunavyovumilia sasa majaribu kwa sababu ya maisha yetu ya Kikristo, ndivyo tutakavyopata nguvu za kuvumilia majaribu zaidi katika mfumo huu mbovu wa mambo.

Yehova Atatulipa

16. Yehova atawathawabisha kwa njia gani wafalme na makuhani wa wakati ujao kwa sababu ya kuteseka kwao?

16 Hata tukipoteza vitu vya kimwili kwa sababu ya upinzani au mateso kwa kuwa tunashikamana na njia ya Kikristo, tunaweza kufurahi kujua kwamba Yehova atatuthawabisha kikamili. Kwa mfano, mtume Paulo aliwaandikia hivi watu fulani ambao walikuwa na tumaini la kwenda mbinguni: “Kwa shangwe mkavumilia kuporwa mali zenu, mkijua ninyi wenyewe mna miliki bora na yenye kudumu” mkiwa watawala katika Ufalme wa Mungu. (Waebrania 10:34) Wazia shangwe watakayokuwa nayo watakapokuwa chini ya uongozi wa Yehova na Kristo wakishiriki katika kuwamiminia baraka za ajabu wakaaji wa dunia katika ulimwengu mpya. Maneno haya ya mtume Paulo kwa Wakristo waaminifu ni ya kweli kabisa: “Nahesabu kwamba mateso ya majira haya si kitu kwa kulinganisha na utukufu utakaofunuliwa ndani yetu.”—Waroma 8:18.

17. Yehova atafanya nini kwa ajili ya wale walio na tumaini la kuishi duniani ambao wanamtumikia kwa ushikamanifu leo?

17 Vivyo hivyo, hata wale walio na tumaini la kuishi duniani wakipoteza au kujinyima nini kwa sababu ya kumtumikia Yehova, atawathawabisha kwa njia kubwa zaidi kwa yale atakayofanya wakati ujao. Atawapa uhai mkamilifu na usio na mwisho katika paradiso duniani. Katika ulimwengu huo mpya, Yehova “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Ni ahadi nzuri kama nini! Hakuna kitu chochote ambacho huenda tukajinyima kwa kupenda au kutopenda katika ulimwengu huu kwa ajili ya Yehova kinachoweza kulinganishwa na maisha mazuri ajabu yanayokuja, ambayo Yehova atawapa watumishi wake waaminifu wanaovumilia mateso.

18. Yehova anatupa ahadi gani yenye kufariji katika Neno lake?

18 Mateso yoyote ambayo huenda tutavumilia hayatavuruga uzima wa milele tutakaopata katika ulimwengu mpya wa Mungu. Mateso yote hayo yatasahauliwa kabisa kwa sababu ya hali nzuri ajabu zitakazokuwa katika ulimwengu mpya. Andiko la Isaya 65:17, 18 linatueleza hivi: “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, na muwe na shangwe milele katika hivi ninavyoumba.” Kwa sababu hiyo, ilifaa kabisa kwa Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, kusema hivi: “Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.” (Yakobo 5:11) Ndiyo, tukivumilia kwa uaminifu mateso ya sasa, tunaweza kufaidika sasa na wakati ujao.

Ungetoa Jibu Gani?

• Wanadamu walianza kuteseka jinsi gani?

• Mateso yanaweza kuwaletea faida gani wale watakaotawala dunia wakati ujao na pia wale watakaoishi duniani?

• Kwa nini tunaweza kuwa wenye furaha hata tukiteseka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wazazi wetu wa kwanza walikuwa na wakati ujao mzuri sana mbele yao

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kuona watu wakiteseka kulimsaidia na kumtayarisha Yesu kuwa Mfalme na Kuhani Mkuu mzuri

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mitume ‘walishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima’ kwa sababu ya imani yao