Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ubuni Pasipo Mbuni?

Ubuni Pasipo Mbuni?

Ubuni Pasipo Mbuni?

KARIBU miaka 150 imepita tangu Charles Darwin aliposema kwamba uteuzi wa kiasili unaonyesha kwa nini kuna vitu mbalimbali vilivyo tata. Hata hivyo, nadharia yake ya mageuzi na nadharia nyingine leo zinazotegemea nadharia hiyo zimepingwa na wale wanaoamini kwamba muundo wa ajabu wa vitu vilivyo hai unaonyesha kwamba vilibuniwa na mtu mwenye kusudi. Hata wanasayansi kadhaa wanaoheshimika sana hawakubaliani na wazo la kwamba jamii mbalimbali za vitu vilivyo hai duniani zilitokana na mageuzi.

Baadhi ya wanasayansi kama hao wanatoa wazo tofauti la ubuni unaotegemea akili, wakidai kwamba ubuni katika viumbe unaungwa mkono na biolojia, hesabu, na akili. Wanataka wazo hilo litiwe ndani ya masomo ya sayansi na kufundishwa shuleni. Vile ambavyo vinaitwa eti vita vya mageuzi vinapiganwa hasa nchini Marekani, lakini vita hivyo vinaripotiwa pia huko Pakistan, Serbia, Uholanzi, Uingereza, na Uturuki.

Kupuuza Jambo la Maana

Hata hivyo, kwa kawaida kuna jambo linalopuuzwa waziwazi katika hoja za kutetea wazo la ubuni unaotegemea akili. Hoja hizo hazimtaji mbuni hata kidogo. Je, unaamini kwamba inawezekana kuwe na ubuni pasipo mbuni? Gazeti moja (The New York Times Magazine) linaripoti kwamba wale wanaounga mkono wazo la ubuni unaotegemea akili “hawasemi waziwazi mbuni huyo ni nini au ni nani.” Mwandishi Claudia Wallis alisema kwamba watetezi wa wazo la ubuni unaotegemea akili “wanajihadhari sana wasimtaje Mungu popote.” Na gazeti lingine (Newsweek) lilisema kwamba wazo la “ubuni unaotegemea akili halisemi chochote kuhusu kuwapo kwa mbuni wala halimtambulishi.”

Hata hivyo, huenda ukakubali kwamba, ni jambo la ubatili kujaribu kupuuza suala la mbuni. Maelezo kuhusu ubuni katika ulimwengu na uhai wenyewe yangeweza jinsi gani kuwa kamili iwapo habari kumhusu mbuni na kuwapo kwake zingefichwa au hata hazingefikiriwa?

Kwa kadiri fulani, mjadala kuhusu kukubali au kutokubali kwamba kuna mbuni unahusiana sana na maswali haya: Je, kukubali kwamba kuna mbuni aliye na uwezo unaopita ule wa wanadamu kutazuia maendeleo ya kisayansi na kielimu? Je, tunapaswa kukubali kwamba kuna mbuni mwenye akili wakati tu tunapokosa ufafanuzi mwingine wowote? Na je, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba kwa sababu kuna ubuni ni lazima kuwe na mbuni? Habari inayofuata itazungumzia maswali hayo na mengineyo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Charles Darwin aliamini kwamba uteuzi wa kiasili unaonyesha kwa nini kuna vitu hai vilivyo tata

[Hisani]

Darwin: From a photograph by Mrs. J. M. Cameron/U.S. National Archives photo