Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukristo Unaingia Asia Ndogo

Ukristo Unaingia Asia Ndogo

Ukristo Unaingia Asia Ndogo

KATIKA karne ya kwanza W.K., makutaniko mengi ya Kikristo yalisitawi katika Asia Ndogo (sehemu kubwa ya nchi ya Uturuki ya leo). Watu wengi sana, Wayahudi na watu wa mataifa, walikubali ujumbe wa Ukristo. Kamusi moja ya Biblia inasema hivi: “Isipokuwa Siria-Palestina, ni hapa Asia Ndogo ambapo Ukristo ulianza mapema zaidi na kuenea zaidi.”

Tukitumia habari kutoka vyanzo mbalimbali, tunaweza kuelewa vizuri zaidi jinsi Ukristo ulivyoenea katika eneo hilo. Acha tuone jinsi tunavyoweza kufaidika kutokana na habari zilizopo.

Wakristo wa Kwanza Huko Asia Ndogo

Tukio moja muhimu katika kuenea kwa Ukristo huko Asia Ndogo lilitukia katika Pentekoste 33 W.K., umati wa watu kutoka lugha mbalimbali ulipokusanyika Yerusalemu. Umati huo ulitia ndani Wayahudi walioishi nje ya Palestina na watu waliogeuzwa imani na kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi. Mitume wa Yesu waliwahubiria wageni hao habari njema. Rekodi za kihistoria zinasema kwamba wageni hao walitoka Kapadokia, Ponto, wilaya ya Asia, * Frigia, na Pamfilia—maeneo yaliyofanyiza sehemu kubwa ya Asia Ndogo. Karibu wasikilizaji 3,000 walikubali ujumbe wa Ukristo na kubatizwa. Walirudi makwao wakiwa na imani yao mpya.—Matendo 2:5-11, 41.

Tunapata habari nyingine katika masimulizi ya Biblia kuhusu safari za umishonari za mtume Paulo huko Asia Ndogo. Katika safari yake ya kwanza, mwaka wa 47/48 W.K. hivi, Paulo na waandamani wake walisafiri kwa meli kutoka Kipro mpaka Asia Ndogo, nao wakasimama huko Perga, Pamfilia. Katika mji wa bara, yaani, Antiokia ya Pisidia, mafanikio yao katika kazi ya kuhubiri yalitokeza wivu na upinzani wa Wayahudi. Paulo alipoelekea kusini-mashariki huko Ikoniamu, Wayahudi wengine walipanga njama ya kumtendea mmishonari huyo kwa dharau. Mwanzoni, wenyeji wenye msisimko wa eneo la karibu la Listra walitangaza kwamba Paulo ni mungu. Lakini Wayahudi wapinzani kutoka Antiokia na Ikoniamu walipofika, umati wa wenyeji ulimpiga Paulo kwa mawe na kumwacha akiwa karibu kufa! Baada ya tukio hilo, Paulo na Barnaba walisafiri mpaka Derbe katika jimbo la kisiasa la Roma la Galatia, mahali ambapo watu walizungumza lugha ya Likaonia. Makutaniko yalianzishwa, na wazee wakawekwa rasmi. Basi unaweza kuona kwamba karibu miaka 15 baada ya Pentekoste 33 W.K., Ukristo ulikuwa umesitawi kabisa huko Asia Ndogo.—Matendo 13:13–14:26.

Katika safari yake ya pili, karibu mwaka wa 49 mpaka 52 W.K., Paulo na wenzake walielekea kwanza huko Listra, pengine wakipitia eneo la nyumbani kwao la Tarso huko Kilikia. Baada ya kuwatembelea tena akina ndugu huko Listra na kuelekea kaskazini, Paulo alijaribu “kulisema neno” katika majimbo ya Bithinia na Asia. Hata hivyo, roho takatifu iliwazuia. Injili ingehubiriwa katika maeneo hayo baadaye. Badala yake, Mungu alimwongoza Paulo kuelekea maeneo ya kaskazini-magharibi ya Asia Ndogo mpaka Troasi huko pwani. Kisha katika maono, Paulo akaelekezwa kuhubiri habari njema huko Ulaya.—Matendo 16:1-12; 22:3.

Katika safari yake ya tatu ya umishonari, karibu mwaka wa 52 mpaka 56 W.K., Paulo alipitia Asia Ndogo, akafika Efeso, jiji muhimu la bandari huko Asia. Tayari alikuwa ametua hapo aliporudi kutoka katika safari yake ya pili. Kulikuwa na kikundi cha Wakristo wenye bidii katika jiji hilo, na Paulo na wenzake walijiunga nao kwa miaka mitatu hivi. Katika kipindi hicho walikabili hali mbalimbali ngumu na hatari, kama vile ule mchafuko uliosababishwa na Waefeso fulani waliokuwa mafundi wa fedha ili kutetea biashara yao kubwa ya kidini.—Matendo 18:19-26; 19:1, 8-41; 20:31.

Kazi ya umishonari iliyowekewa msingi huko Efeso ilikuwa na matokeo makubwa. Andiko la Matendo 19:10 linasema: “Wale wote waliokuwa wakikaa katika wilaya ya Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.”

Matukio Huko Asia Ndogo

Paulo aliwaandikia hivi Wakorintho katika siku zake za mwisho-mwisho huko Efeso: “Makutaniko ya Asia yanawatumia ninyi salamu zao.” (1 Wakorintho 16:19) Paulo alikuwa akizungumza kuhusu makutaniko gani? Inaelekea kwamba alitia ndani makutaniko yaliyokuwa Kolosai, Laodikia, na Hierapolisi. (Wakolosai 4:12-16) Kitabu kimoja (Paul—His Story) kinasema hivi: “Kupatana na akili inaelekea kwamba jamii huko Smirna, Pergamamu, Sardi, na Filadelfia, zilitokana na jitihada ya umishonari huko Efeso. . . . Maeneo hayo yalikuwa maili 120 (kilomita 192) kuzunguka Efeso na yaliunganishwa na barabara nzuri sana.”

Hivyo, miaka 20 hivi baada ya Pentekoste 33 W.K., makutaniko kadhaa ya Kikristo yalikuwako kusini na magharibi mwa Asia Ndogo. Namna gani sehemu nyingine za eneo hilo?

Waliopokea Barua za Petro

Mtume Petro aliandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho miaka kadhaa baadaye, karibu mwaka wa 62 mpaka 64 W.K. Aliwaandikia Wakristo huko Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia. Barua ya Petro inaonyesha kwamba huenda kulikuwa na makutaniko ya Kikristo katika maeneo hayo, nao wazee walihimizwa ‘walichunge kundi.’ Makutaniko hayo yalianzishwa wakati gani?—1 Petro 1:1; 5:1-3.

Baadhi ya maeneo ambamo watu walioandikiwa na Petro waliishi, kama vile Asia na Galatia, yalikuwa yamehubiriwa na Paulo. Hata hivyo, hakuwa ameingia katika maeneo ya Kapadokia au Bithinia. Biblia haituelezi jinsi Ukristo ulivyoenea katika maeneo hayo, lakini huenda ulienezwa na Wayahudi au wageuzwa-imani waliokuwa Yerusalemu katika Pentekoste 33 W.K. ambao baadaye walirudi makwao. Kwa vyovyote vile, karibu miaka 30 baada ya Pentekoste, Petro alipoandika barua zake, ni wazi kwamba, kama msomi mmoja anavyosema, makutaniko “yalikuwako kotekote katika Asia Ndogo.”

Makutaniko Saba ya Ufunuo

Uasi wa Wayahudi kuelekea Waroma ulisababisha uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Inawezekana kwamba mwishowe Wakristo fulani wa Yudea walihamia Asia Ndogo. *

Karibu mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Yesu Kristo alimtumia mtume Yohana kuyaandikia barua makutaniko saba ya Asia Ndogo. Barua hizo, kwa makutaniko huko Efeso, Smirna, Pergamamu, Thiatira, Sardi, Filadelfia, na Laodikia, zinafunua kwamba Wakristo katika sehemu fulani za Asia Ndogo walikuwa wakikabili hatari mbalimbali, kama vile upotovu wa maadili, migawanyiko, na uasi-imani.—Ufunuo 1:9, 11; 2:14, 15, 20.

Utumishi Wenye Kiasi wa Nafsi Yote

Kwa wazi, kuenea kwa Ukristo katika karne ya kwanza kulitia ndani mengi zaidi ya yale tunayosoma katika kitabu cha Matendo ya Mitume. Mitume Petro na Paulo, wanaojulikana sana, walihusika katika matukio yanayosimuliwa katika kitabu cha Matendo, lakini watu wengine wengi wasiojulikana walikuwa wakihubiri kwingineko. Matukio huko Asia Ndogo yanathibitisha kwamba Wakristo wa mapema walichukua kwa uzito amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mathayo 28:19, 20.

Vivyo hivyo leo, akina ndugu ulimwenguni pote wanajua shughuli za idadi ndogo tu ya Mashahidi waaminifu wa Yehova ulimwenguni pote. Katika karne ya kwanza huko Asia Ndogo, waeneza-injili wengi waaminifu hawakujulikana sana. Leo pia wahubiri wengi wa habari njema hawajulikani sana. Hata hivyo, wao pia wana maisha yenye shughuli nyingi, yenye kuthawabisha, na yenye kuridhisha sana wakijua kwamba wanatii kwa kujitoa ili kuwaokoa wengine.—1 Timotheo 2:3-6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na pia makala hii, “Asia” inarejelea jimbo la Roma lililokuwa magharibi mwa Asia Ndogo, wala si bara la Asia.

^ fu. 17 Mwanahistoria Eusebio (260-340 W.K.) anasema kwamba muda fulani kabla ya mwaka wa 66 W.K., “mitume, ambao walikabili hatari ya kuuawa, walifukuzwa Yudea. Lakini ili kueneza ujumbe wao walisafiri katika kila nchi kwa nguvu za Kristo.”

[Picha katika ukurasa wa 11]

UKRISTO WA MAPEMA HUKO BITHINIA NA PONTO

Jimbo la Bithinia na Ponto lilikuwa katika Pwani ya Bahari Nyeusi ya Asia Ndogo. Tunajua mengi kuhusu maisha katika jimbo hilo kutokana na yale ambayo Plini Mdogo, mmoja wa maofisa wa jimbo hilo, alimwandikia Trajani, Maliki Mroma.

Miaka 50 baada ya barua za Petro kusambazwa katika makutaniko ya eneo hilo, Plini alimwomba Trajani shauri kuhusu kuwashughulikia Wakristo. “Sijawahi kamwe kuhudhuria kesi inayowahusu Wakristo. Kwa hiyo, sijui aina wala kiwango cha adhabu wanayopewa kwa ukawaida,” akaandika Plini. “Watu wengi sana, wa umri na tabaka mbalimbali, wanaume kwa wanawake, wanaletwa mahakamani, na inaelekea hali hiyo itaendelea. Hilo halitukii mijini tu bali pia vijijini na katika wilaya za mashambani ambako kuna madhehebu hayo yanayodharauliwa.”

[Ramani/ Picha katika ukurasa wa 9]

 

SAFARI ZA PAULO

Safari ya Kwanza ya Umishonari

SAIPRASI

PAMFILIA

Perga

Antiokia (ya Pisidia)

Ikoniamu

Listra

Derbe

Safari ya Pili ya Umishonari

KILIKIA

Tarso

Derbe

Listra

Ikoniamu

Antiokia (ya Pisidia)

FRIGIA

GALATIA

Troasi

Safari ya Tatu ya Umishonari

KILIKIA

Tarso

Derbe

Listra

Ikoniamu

Antiokia (ya Pisidia)

Efeso

ASIA

Troasi

[Makutaniko Saba]

Pergammum

Thiatira

Sardi

Smirna

Efeso

Filadelfia

Laodikia

 

Hierapolisi

Kolosai

LYKIA

BITHINIA

PONTO

KAPADOKIA

[Picha katika ukurasa wa 9]

Antiokia

[Picha katika ukurasa wa 9]

Troasi

[Hisani]

© 2003 BiblePlaces.com

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jumba la maonyesho huko Efeso. —Matendo 19:29

[Picha katika ukurasa wa 10]

Msingi wa madhabahu ya Zeu huko Pergamamu. Wakristo katika jiji hilo walikaa ‘mahali kilipokuwa kiti cha ufalme cha Shetani.’—Ufunuo 2:13

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.