Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vutiwa na Ubuni Jifunze Kumhusu Mbuni

Vutiwa na Ubuni Jifunze Kumhusu Mbuni

Vutiwa na Ubuni Jifunze Kumhusu Mbuni

PENGINE umesikia kuhusu Michelangelo, mchoraji picha na mchongaji sanamu Mwitaliano. Huenda hujawahi kamwe kuona mojawapo ya kazi zake binafsi zilizo bora za sanaa. Hata hivyo, inaelekea sana kwamba unakubaliana na mwanahistoria wa sanaa ambaye alimwita Mwitaliano huyo mwenye kipawa, “msanii wa ajabu na asiye na kifani.” Uhakika wa kwamba Michelangelo alikuwa na kipawa hauwezi kupingwa. Ni nani anayeweza kukubali kwamba kazi za sanaa za Michelangelo ni bora sana na wakati huohuo akane kwamba alikuwa msanii mwenye kipawa?

Sasa fikiria vitu hai vya ajabu vilivyo tata na tofauti sana ambavyo vimejaa duniani. Kwa kufaa, gazeti moja (The New York Times) lilimnukuu profesa wa sayansi ya biolojia aliyesema hivi: “Uthibitisho halisi wa ubuni unaonekana katika maeneo yote ya biolojia.” Aliongeza hivi: “Tuna uthibitisho mwingi wa ubuni katika vitu hai.” Je, ni jambo linalopatana na akili kuvutiwa na ubuni na kutokubali kwamba kuna mbuni?

Mtume Paulo, ambaye alichunguza kwa makini vitu vilivyomzunguka, alizungumza kuhusu watu fulani ambao “walikiheshimu na kukitumikia kiumbe kuliko yule aliyekiumba.” (Waroma 1:25, Darby) Kwa sababu wamepotoshwa na mawazo ya kimageuzi yaliyoenea sana, watu fulani wanakataa au hawakubali kwamba ubuni unathibitisha kwamba kuna mbuni. Lakini je, nadharia ya mageuzi inapatana kabisa na sayansi ya kweli? Ona kauli hii ya Christoph Schönborn askofu Mkatoliki wa Vienna, iliyo katika gazeti moja (The New York Times): “Kila wazo linalopinga au kujaribu kupuuza uthibitisho mwingi wa ubuni katika biolojia ni nadharia tu, wala si sayansi.”

Je, Tunakataa Sayansi?

Hata hivyo, kuna wale wanaoona kwamba kukubali kuwa kuna uthibitisho wa kwamba kuna Muumba “kutazuia utafiti.” Makala katika gazeti moja (New Scientist) ilizungumzia woga huo, ikidai kwamba “sayansi haingekuwa tena mradi unaotoa nafasi ya kuendelea kugundua mambo mapya, kwa kuwa ungesimamishwa na kizuizi kisichoweza kupenywa kinachoitwa ‘mbuni alibuni.’” Je, woga huo una msingi? Hapana. Kwa hakika, woga huo hauna msingi hata kidogo. Kwa nini?

Kwa kweli, kukubali kwamba ulimwengu wetu na vitu vyote vilivyomo duniani vilijitokeza vyenyewe tu kupitia mageuzi ni kutupilia mbali jitihada zozote za kupata jibu lenye maana. Kwa upande mwingine, tukikubali kwamba Muumba mwenye akili ndiye aliyetokeza vitu vyote tunavyoona, tutachunguza vitu vya asili na kuona jinsi ambavyo Muumba ametumia akili yake kutokeza ulimwengu unaoonekana. Fikiria hili: Kujua kwamba Leonardo da Vinci alichora picha ya “Mona Lisa” hakujawazuia wanahistoria wa sanaa wasichunguze ufundi wake wa kuchora na vitu alivyotumia. Vivyo hivyo, kukubali kwamba kuna Mbuni hakupaswi kutuzuia tusichunguze mambo mengi na utata wa vitu alivyobuni na kuumba.

Badala ya kuzuia utafiti zaidi, Biblia inawatia moyo watu watafute majibu kwa maswali ya kisayansi na ya kiroho. Mfalme Daudi wa zamani alitafakari kuhusu jinsi mwili wake ulivyoumbwa kwa ustadi. Kwa sababu hiyo alisema hivi: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, Biblia inasema kwamba Muumba alimuuliza hivi mzee wa ukoo, Ayubu: “Je, umezifikiria kwa akili nafasi pana za dunia?” (Ayubu 38:18) Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Muumba hataki watu waulize maswali au wachunguze mambo. Badala yake, katika andiko hilo yule Mbuni Stadi aliwahimiza watu wachunguze kazi ya mikono yake. Ona pia, mwaliko ulioandikwa na nabii Isaya unaotuhimiza tuongeze ujuzi wetu kumhusu Yule aliyeumba vitu tunavyoona: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi?” Kwa kweli, andiko la Isaya 40:26 linafunua jambo hakika linalopatana na kanuni maarufu ya Einstein inayosema kwamba nishati ni sawa na uzito kuzidisha na mwendo wa nuru mara mbili (E=mc2). Jambo hilo la hakika ni kwamba ulimwengu wote ulitokana na chanzo cha nguvu zenye msukumo.

Kwa kweli, nyakati nyingine majibu ya maswali kuhusu uumbaji hayapatikani kwa urahisi. Sababu moja ni kwamba hatuna uwezo mkubwa wa kuelewa na hatujui mambo yote kuhusu ulimwengu. Ayubu alielewa jambo hilo. Alimsifu Muumba, ambaye anaiwezesha dunia yetu kuning’inia pasipo kitu kinachoonekana angani na mawingu mazito ya maji kuning’inia juu ya dunia. (Ayubu 26:7-9) Hata hivyo, Ayubu alitambua kwamba maajabu kama hayo ‘ni kingo tu za njia za Muumba.’ (Ayubu 26:14) Bila shaka, Ayubu alitaka kujifunza mengi zaidi kuhusu ulimwengu uliomzunguka. Naye Daudi alikubali kwamba hakuwa na ujuzi kamili alipoandika hivi: “Ujuzi wa namna hiyo ni wa ajabu mno kwangu. Ni wa juu sana hivi kwamba siwezi kuufikia.”—Zaburi 139:6.

Kukubali kwamba kuna Muumba hakuzuii maendeleo ya kisayansi. Jitihada za kutafuta ujuzi mwingi zaidi kuhusu mambo ya kimwili na ya kiroho hazina mwisho. Mfalme mmoja wa zamani aliyejulikana kwa sababu ya ujuzi wake mwingi aliandika hivi kwa unyenyekevu: “Ameweka mawazo ya umilele katika akili ya mwanadamu, lakini mwanadamu hawezi kuelewa kazi ambayo Mungu amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”—Mhubiri 3:11, Holy Bible—New Life Version.

Je, Yeye Ni “Mungu wa Kuzibia Mapengo”?

Watu fulani wanadai kwamba, wakati wowote kunapokosekana uthibitisho wa kisayansi, Mungu anaonwa pasipo msingi kuwa “suluhisho.” Kwa maneno mengine, wanadai kwamba Mungu kama huyo ambaye ni Mbuni anakuwa “Mungu wa kuzibia mapengo,” na ndiyo sababu watu wamezoea kusema “Mungu” alifanya, wakati wowote wanaposhindwa kueleza jambo kupatana na akili na sayansi. Lakini ni mapengo gani tunayozungumzia? Je, ni mapengo madogo na yasiyo na maana katika ujuzi wetu? Hapana, ni mapengo makubwa sana na ya maana sana yaliyo katika nadharia ya Darwin ya mageuzi. Ni mapengo makubwa sana na yaliyo muhimu katika biolojia hivi kwamba nadharia ya mageuzi imeshindwa kuyaziba. Kusema kweli, wanamageuzi wanaotegemea dhana zisizo na msingi ndio wanaofanya nadharia ya Darwin iwe kwao “Mungu wa kuzibia mapengo.”

Muumba anayetajwa katika Biblia si “Mungu wa kuzibia mapengo.” Badala yake, kazi zake zinatia ndani hatua zote, mambo yote, na tofauti zote katika viumbe. Mtunga-zaburi alikazia kazi za Yehova za uumbaji zinazohusu mambo yote: “Wewe ndiwe chanzo cha uhai wote, na kwa sababu ya nuru yako tunaona nuru.” (Zaburi 36:9, Today’s English Version) Yehova anaelezwa vema kuwa Ndiye ‘aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.’ (Matendo 4:24; 14:15; 17:24) Mwalimu fulani wa karne ya kwanza alikuwa na sababu nzuri ya kuandika kwamba Mungu ‘aliviumba vitu vyote.’—Waefeso 3:9.

Kwa kuongezea, Mungu aliweka “sheria za mbingu,” sheria za asili zinazoongoza vitu na nguvu, sheria ambazo wanasayansi bado wanachunguza. (Ayubu 38:33) Ubuni wake ni mkamilifu na wenye kusudi, nao unatimiza lengo lake la kuifanya dunia iwe makao ya viumbe vingi sana vilivyo hai vya aina tofauti-tofauti.

Ubuni na Akili

Mwishowe, tunahitaji kufikiria suala la akili. Akizungumza kwa ujumla kuhusu kukubalika kwa nadharia mbalimbali za kisayansi, John Horgan, mwandikaji wa mambo ya sayansi alisema hivi: “Uthibitisho unapokosa kuwa hakika, hatupaswi kuona haya kuacha akili yetu ituongoze.”

Je, kweli ni jambo linalopatana na akili kudai kwamba uhai ulijitokeza wenyewe kupitia nguvu zisizo na akili? Ingawa nadharia ya mageuzi inapendwa sana, watu wengi wenye akili, kutia ndani wanasayansi fulani, wanasadiki kwamba kuna Muumba mwenye akili. Profesa mmoja wa sayansi anasema kwamba kwa ujumla watu “wengi wanafikiri kupatana na akili kwamba uhai ulibuniwa.” Kwa nini? Kwa sababu watu wengi watakubali kwa urahisi maneno haya ya mtume Paulo: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani.” (Waebrania 3:4) Kisha, Paulo anakata kauli hii inayopatana na akili: “Yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” Kulingana na maoni ya Biblia, si jambo linalopatana na akili kukubali kwamba nyumba inahitaji mbuni na mjenzi na wakati huohuo kudai kwamba chembe iliyo tata ilijitokeza yenyewe tu.

Biblia inasema hivi kuwahusu wale wanaokana kwamba kuna Mbuni na Muumba: “Asiye na akili amesema katika moyo wake: ‘Hakuna Yehova.’” (Zaburi 14:1) Hapa, mtunga-zaburi anawashutumu wale ambao bado hawajasadikishwa. Mtu anaweza kuongozwa na maoni yake ya kibinafsi badala ya kufuata mambo ya hakika. Kwa upande mwingine, mtu mwenye hekima, aliye na utambuzi, anakubali kwa unyenyekevu kwamba kuna Muumba.—Isaya 45:18.

Watu wengi wenye kufikiri wanakubali kuwa kuna uthibitisho ulio wazi kabisa wa kwamba kuna Mbuni Mkuu.

Unaweza Kumjua Mbuni

Ikiwa tulibuniwa, tulibuniwa kwa kusudi gani? Ni nini lililo kusudi la uhai wetu? Sayansi peke yake imeshindwa kutoa majibu yenye kuridhisha ya maswali kama hayo. Hata hivyo, masuala hayo ya msingi yanahitaji majibu yenye kusadikisha na kuridhisha. Biblia inaweza kutusaidia sana kupata majibu. Inamtambulisha Yehova kuwa Muumba na pia Mkusudiaji aliye na sababu nzuri za kutenda atendavyo. Maandiko yanafunua kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu, nayo yanatupa tumaini la wakati ujao.

Lakini, Yehova ni nani? Yeye ni Mungu wa aina gani? Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha umjue Mbuni wetu Stadi ambaye ni mtu halisi. Unaweza kujifunza kuhusu jina, sifa, na shughuli zake pamoja na wanadamu. Ukisoma Neno lake, Biblia, utaona kwa nini hatupaswi tu kuvutiwa na ubuni wake wa ajabu bali pia kumtukuza akiwa Mbuni.—Zaburi 86:12; Ufunuo 4:11.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Michelangelo

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kuamini kwamba kuna Mbuni ni jambo linalopatana na sayansi ya kweli

[Picha katika ukurasa wa 6]

Tofauti za viumbe na jinsi ambavyo vinabadilika kulingana na hali ni uthibitisho wa kwamba vimebuniwa kwa ustadi sana

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ubuni unahitaji mbuni