Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Zawadi Kubwa” Kwa Watu wa Poland

“Zawadi Kubwa” Kwa Watu wa Poland

“Zawadi Kubwa” Kwa Watu wa Poland

MNAMO Julai 6, 1525, Mtawala Albrecht wa Hohenzollern alitangaza dini ya Kilutheri kuwa dini ya Taifa. Hivyo, Prussia, ambayo wakati huo ilikuwa chini ya ufalme wa Poland, ikawa taifa la kwanza huko Ulaya kufuata rasmi mafundisho ya Martin Luther.

Albrecht alitaka kufanya Königsberg, mji mkuu wa Prussia Mashariki, kuwa kitovu cha utamaduni wa Waprotestanti. Alianzisha chuo kikuu katika mji huo na kutegemeza uchapishaji wa vichapo vya Walutheri katika lugha nyingi. Mwaka wa 1544, mtawala huyo pia aliagiza kwamba watu wa Poland walio katika nchi zake wanapaswa kusomewa Maandiko Matakatifu katika lugha yao. Hata hivyo, Biblia haikuwa imetafsiriwa katika lugha ya Kipolishi.

Tafsiri Katika “Lugha ya Kawaida”

Ili kubadili hali hiyo, Albrecht alianza kumtafuta mtu mwenye uwezo wa kutafsiri Biblia ya Kipolishi ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Karibu mwaka wa 1550, alimwomba Jan Seklucjan afanye kazi hiyo. Seklucjan alikuwa mwandishi, muuzaji wa vitabu, na mchapishaji. Seklucjan alikuwa amehitimu katika Chuo Kikuu cha Leipzig naye alijulikana kwa sababu ya kuchokoza Kanisa Katoliki kwa kueneza mafundisho ya Kiprotestanti. Kabla ya hapo, alikuwa amekimbilia Königsberg ili asishtakiwe kwa kueneza mafundisho yake ya kidini.

Jan Seklucjan alikuwa mwenye bidii katika kazi ya kutafsiri Maandiko katika lugha ya Kipolishi. Mwaka mmoja tu baada ya Seklucjan kupewa kazi hiyo, nakala za kwanza za Injili ya Mathayo zilichapishwa. Tafsiri hiyo ilitia ndani maelezo mengi na habari muhimu za pambizoni ambazo zilionyesha tafsiri nyingine za maandiko fulani. Muda mfupi baadaye, Seklucjan alisimamia kazi ya kuchapisha tafsiri yenye vitabu vyote vinne vya Injili. Katika muda wa miaka mitatu tu, alikuwa amechapisha Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo.

Ili kutokeza tafsiri iliyo sahihi, mtafsiri huyo alichunguza maandishi ya Kigiriki. Kwa kuongezea, utangulizi wa tafsiri ya mwaka wa 1551 ulisema kwamba tafsiri za Kilatini na “tafsiri za lugha nyingine zilichunguzwa.” Stanisław Rospond, mtungaji wa kitabu kimoja (Studies on the Polish Language of the 16th Century) anaeleza kwamba tafsiri hiyo ilitafsiriwa “kwa njia maridadi na yenye mtiririko.” Mtafsiri hakufuata kiholela “lugha ya vitabu,” anasema Rospond. Badala yake, alijitahidi kutumia maneno ya Kipolishi ambayo “yalikaribiana sana na lugha ya kawaida.”

Ingawa Seklucjan alisimamia kazi hiyo, ushuhuda unaonyesha kwamba si yeye aliyetafsiri Biblia hiyo. Basi ni msomi gani aliyeitafsiri? Ni Stanisław Murzynowski, ambaye alikuwa na umri wa miaka 20 hivi wakati Seklucjan alipompa kazi hiyo ngumu.

Murzynowski alizaliwa katika kijiji fulani, lakini alipokuwa na umri wa kutosha, baba yake alimtuma huko Königsberg ili aanze kujifunza Kigiriki na Kiebrania. Baadaye, Murzynowski alijiandikisha katika Chuo Kikuu cha Wittenberg, Ujerumani, ambako huenda alikutana na Martin Luther. Mwanafunzi huyo kijana alifundishwa na Philipp Melanchthon, ambaye bila shaka alimsaidia kujua vizuri Kigiriki na Kiebrania. Baada ya kuongeza masomo yake huko Italia, Murzynowski alirudi Königsberg na kumwomba Mtawala Albrecht amwajiri kazi.

Maria Kossowska anaandika hivi katika kitabu chake (The Bible in the Polish Language): “Murzynowski alifanya kazi kwa bidii na kwa matokeo, lakini hakujitafutia sifa, umaarufu, wala kuomba jina lake liwekwe kwenye ukurasa wa kwanza wa tafsiri hiyo.” Kijana huyo anaandika hivi kuhusu uwezo wake mwenyewe: “Sijui kuandika vizuri ama Kilatini au Kipolishi.” Ingawa alikuwa na shaka, Murzynowski alisaidia sana kutafsiri Neno la Mungu kwa ajili ya Wapolishi. Seklucjan ambaye alishirikiana naye, alisema kwamba tafsiri yao ilikuwa “zawadi kubwa” kwa watu wa Poland.

Mojawapo ya Zawadi Kubwa Zaidi

Tangu tafsiri ya kwanza ya Kipolishi ya Biblia itolewe, kumekuwa na tafsiri nyingine nyingi. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa mwaka wa 1994, na mwaka wa 1997, chapa nzima ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikatolewa katika Kipolishi. Watafsiri, ambao hawajitafutii sifa, walijitahidi kutafsiri Neno la Mungu kwa njia ambayo ni sahihi na pia kwa lugha ambayo inakaribiana na lugha inayotumiwa kwa kawaida leo, wala si ile ya karne ya 16.

Leo, Biblia inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 2,400 hivi. Ikiwa unaweza kupata tafsiri sahihi ya Neno la Mungu katika lugha yenu, hiyo ni mojawapo ya zawadi kubwa zaidi ambazo unaweza kupata. Ni zawadi kutoka kwa Yehova Mungu ya kukuongoza.—2 Timotheo 3:15-17.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jiwe la ukumbusho wa Stanisław Murzynowski, mtafsiri wa “Agano Jipya” katika Kipolishi

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sura ya 3 ya kitabu cha Mathayo ambayo ilitafsiriwa na Stanisław Murzynowski

[Hisani]

Dziȩki uprzejmości Towarzystwa Naukowego Płockiego