Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu

Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu

Simulizi la Maisha

Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu

Limesimuliwa na Henryk Dornik

NILIZALIWA mwaka wa 1926. Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki wenye bidii. Waliishi huko Ruda Slaska, mji wenye migodi ya mawe ya thamani karibu na Katowice, kusini mwa Poland. Wazazi wetu walitufundisha sisi watoto wao, yaani, mimi, ndugu yangu mkubwa, Bernard; dada zangu wawili wadogo, Róża na Edyta—kusali, kuhudhuria ibada kanisani, na kula sakramenti ya kitubio.

Kweli ya Biblia Inafika Nyumbani Mwetu

Siku moja mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1937, nilipokuwa na umri wa miaka kumi, Baba alirudi nyumbani akiwa mwenye furaha sana. Alikuja na kitabu kikubwa ambacho alikuwa amepewa na Mashahidi wa Yehova. Alisema hivi: “Watoto, tazameni kitabu hiki ambacho nimepata—Maandiko Matakatifu!” Ilikuwa mara yangu ya kwanza kabisa kuona Biblia.

Kwa muda mrefu Kanisa Katoliki lilikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu katika mji wa Ruda Slaska na maeneo ya karibu. Makasisi walikuwa wenye urafiki sana kuelekea watu waliomiliki migodi ya mawe ya thamani na hivyo walitaka watu hao na familia zao ziwatii kabisa. Ikiwa mfanyakazi katika migodi angekosa kuhudhuria Misa au kukataa kuungama, alionwa kuwa mpagani na alifukuzwa katika migodi. Muda si muda, Baba alianza kutishwa kwa njia hiyo kwa sababu alikuwa akishirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, wakati kasisi mmoja alipotutembelea nyumbani, Baba alifunua unafiki wake wa kidini mbele ya watu wote. Kasisi huyo aliyeaibika hakutaka fujo zaidi, kwa hiyo Baba hakufukuzwa kazini.

Niliposikiliza mazungumzo hayo kati ya Baba na kasisi huyo niliazimia hata zaidi kuielewa Biblia. Pole kwa pole, nilimpenda Yehova, nami nikasitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye. Miezi michache baada ya mazungumzo ya Baba pamoja na yule kasisi, tulihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Wakati huo Baba alitambulishwa kwa kikundi cha watu 30 kwa maneno haya, “Huyu ni Myonadabu.” Muda si muda, nilijifunza kwamba “Wayonadabu” walikuwa Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani na kwamba idadi yao ingeongezeka. *2 Wafalme 10:15-17.

“Kijana, Je, Unajua Maana ya Ubatizo?”

Baada ya kukubali kweli, Baba aliacha kuwa mlevi naye akawa mume na baba mzuri. Lakini, Mama hakukubali imani ya Baba, na alikuwa akisema kwamba ni afadhali aishi kama alivyokuwa akiishi na aendelee kuwa Mkatoliki. Hata hivyo, baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza, Mama aliona kwamba makasisi walewale ambao walisali ili Poland iwashinde Wajerumani waliovamia, sasa walikuwa wakitoa sala za kushukuru kwa sababu ya ushindi wa Hitler! Baadaye, mwaka wa 1941, Mama alijiunga nasi katika kumtumikia Yehova.

Kabla ya wakati huo, nilikuwa nimeomba kubatizwa katika maji ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu, lakini wazee wa kutaniko walifikiri kwamba nilikuwa ningali mdogo sana. Waliniambia ningoje. Lakini mwishowe, mnamo Desemba 10, 1940 (10/12/1940), Konrad Grabowy (ndugu ambaye baadaye alikufa akiwa mwaminifu katika kambi ya mateso) aliniuliza maswali kwa busara katika chumba fulani kidogo. Aliniuliza maswali matano, kisha alipotosheka na majibu yangu, akanibatiza. Swali moja ambalo aliniuliza ni, “Kijana, je, unajua maana ya ubatizo?” Swali lingine ambalo aliuliza ni, “Je, unajua kwamba kwa sababu ya vita vilivyopo sasa, hivi karibuni utahitaji kuamua ama kuwa mwaminifu kwa Hitler au kwa Yehova, na huenda utauawa kwa sababu ya uamuzi wako?” Bila kusitasita, nilijibu hivi: “Ninajua.”

Mateso Yanaanza

Kwa nini Konrad Grabowy aliuliza maswali hayo ya moja kwa moja? Jeshi la Ujerumani lilikuwa limevamia Poland mwaka wa 1939, na baada ya hapo, imani na utimilifu wetu ulijaribiwa vikali. Kila siku, mambo yalizidi kuwa mabaya kwa kuwa tulipata habari kwamba ndugu na dada walikuwa wakikamatwa, kuhamishwa, na kupelekwa gerezani au katika kambi za mateso. Muda si muda, sisi pia tungekabili majaribu kama hayo.

Wanazi walitaka kufanya watoto wote kuwa watetezi wenye bidii wa Utawala wa Hitler, kutia ndani watoto wanne wa familia yetu. Kwa kuwa Baba na Mama walikuwa wamekataa mara kadhaa kutia sahihi orodha ya watu ambao walikuwa au ambao walitaka kuwa raia wa Ujerumani (Volkslist), walinyimwa haki ya kutulea sisi watoto. Baba alipelekwa katika kambi ya mateso huko Auschwitz. Mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1944, mimi na ndugu yangu tulipelekwa katika shule ya kuwarekebisha watoto huko Grodków (Grottkau), karibu na Nysa, na dada zetu walipelekwa kwenye makao ya watawa Wakatoliki huko Czarnowąsy (Klosterbrück), karibu na Opole. Walitupeleka huko ili kutufanya tuache yale ambayo wenye mamlaka walisema ni “maoni ya udanganyifu ya wazazi wetu.” Mama alibaki nyumbani peke yake.

Kila asubuhi katika uwanja wa shule ya kuwarekebisha watoto, bendera yenye alama ya Wanazi (swastika) ilipandishwa na tuliamriwa kuinua mikono yetu ya kulia na kuisalimu bendera hiyo huku tukisema “Heil Hitler.” Lilikuwa jaribu kali sana la imani, lakini mimi na Bernard tulibaki imara na tulikataa kulegeza msimamo wetu. Hivyo, tulipigwa vibaya sana kwa sababu ya “kukosa heshima.” Jitihada nyingine za kujaribu kuvunja uaminifu wetu hazikufaulu, kwa hiyo mwishowe askari wa SS walitupa uamuzi wa mwisho: “Mtie sahihi hati inayoonyesha ushikamanifu kwa Serikali ya Ujerumani na kujiunga na Wehrmacht [Jeshi la Ujerumani] kama sivyo, mtapelekwa kwenye kambi ya mateso.”

Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1944, wakati wenye mamlaka walipopendekeza rasmi kwamba tupelekwe kwenye kambi ya mateso, walisema hivi: “Hawawezi kusadikishwa wafanye jambo lolote. Wanapata shangwe wanapokufa kwa ajili ya imani yao. Msimamo wao wa uasi ni tishio kwa shule yote ya kuwarekebisha watoto.” Ingawa sikutaka kufa kwa ajili ya imani yangu, kuteseka kwa ujasiri na heshima kwa ajili ya ushikamanifu wangu kwa Yehova kuliniletea shangwe. (Matendo 5:41) Singefaulu kamwe kwa uwezo wangu mwenyewe kuvumilia mateso ambayo ningekabili. Kwa upande mwingine, sala za kutoka moyoni zilinifanya nimkaribie Yehova zaidi, naye alithibitika kuwa Msaidizi mwenye kutegemeka.—Waebrania 13:6.

Katika Kambi ya Mateso

Punde si punde, nilipelekwa katika kambi ya mateso ya Gross-Rosen huko Silesia. Nilipewa namba ya mfungwa na pembetatu ya zambarau ambayo ilinitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova. Askari wa SS walinipa nafasi ya kuchagua jambo moja. Ningeweza kuachiliwa kutoka katika kambi hiyo na hata kuwekwa kuwa ofisa katika jeshi la Nazi kwa sharti moja. “Ni lazima ukatae mawazo ya Wanafunzi wa Biblia ambayo yanapinga Utawala wa Hitler.” Hakuna wafungwa wengine waliopewa nafasi hiyo. Mashahidi wa Yehova tu ndio waliopewa nafasi ya kutoka kambini. Hata hivyo, bado mimi, kama maelfu ya Mashahidi wengine, nilikataa kwa uthabiti “pendeleo” hilo. Kisha, askari hao wakasema hivi: “Tazama kwa makini sana bomba lile la moshi la nyumba ya kuwateketezea watu. Fikiria kwa uzito jambo hilo, kama sivyo utatokea tu kwenye lile bomba la moshi.” Nilikataa tena kwa uthabiti, na wakati huo, nikajaa “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Wafilipi 4:6, 7.

Nilisali ili niweze kukutana na waamini wenzangu kambini, na Yehova alifungua njia. Kati ya Wakristo wenzangu niliokutana nao ni ndugu mwaminifu anayeitwa Gustaw Baumert, ambaye alinitunza kwa wororo na upendo. Bila shaka, Yehova alithibitika kuwa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” kwangu.—2 Wakorintho 1:3.

Baada ya miezi michache, Wanazi walilazimika kukimbia haraka kutoka kambini kwa sababu ya wanajeshi wa Urusi waliokuwa wakikaribia. Tulipokuwa tukijitayarisha kuondoka, sisi akina ndugu—huku tukihatarisha uhai wetu—tuliamua kwenda kwenye kambi za wanawake ili kuona hali ya dada zetu 20 hivi wa kiroho waliokuwamo, kutia ndani Elsa Abt na Gertrud Ott. * Walipotuona, walitukimbilia haraka na baada ya kutiana moyo kidogo pamoja nao, waliimba wimbo wa Ufalme ambao ulikuwa na maneno haya: “Mwaminifu, mshikamanifu, hataruhusu nafsi yake iogope kamwe.” * Macho yetu sote yalijaa machozi!

Tunaenda Kwenye Kambi Nyingine

Wanazi walijaza wafungwa 100 hadi 150 kati yetu katika mabehewa matupu ya gari la moshi la kubeba makaa ya mawe na hawakuwapa chakula wala maji. Tulisafiri kupitia maeneo yenye baridi kali na mvua. Tuliteseka sana kwa sababu ya kiu na homa. Nafasi ilipatikana kwenye mabehewa hayo wakati wafungwa wagonjwa na waliochoka walipoanguka sakafuni na kufa. Miguu na viungo vyangu vilivimba sana hivi kwamba singeweza kusimama. Baada ya kusafiri kwa siku kumi, wafungwa wachache ambao waliokoka walifika katika kambi ya gereza ya Mittelbau-Dora huko Nordhausen, karibu na Weimar huko Thuringia. Jambo la ajabu ni kwamba, hakuna ndugu hata mmoja aliyekufa katika safari hiyo yenye kutisha.

Nilipoanza tu kupata nafuu baada ya safari hiyo, ugonjwa wa kuhara damu ulitokea kambini, na ndugu fulani, kutia ndani mimi tukawa wagonjwa. Tuliambiwa kwa muda fulani tusinywe supu kambini na tule tu mikate iliyokaushwa kwa moto. Nilifanya hivyo na baada ya muda nikapona. Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1945 tulisikia kwamba Andiko la mwaka huo lilikuwa Mathayo 28:19: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Ni wazi kwamba muda si muda, malango ya kambi yangefunguliwa na habari njema ingeendelea kuhubiriwa! Hilo lilituletea shangwe nyingi na tumaini, kwa kuwa tulifikiri kwamba kilele cha Vita vya Pili vya Ulimwengu kingekuwa Har–Magedoni. Yehova alitutia nguvu kama nini katika nyakati hizo ngumu!

Kuwekwa Huru Kutoka Kwenye Kambi

Mnamo Aprili 1, 1945 (1/4/1945), majeshi ya Muungano yaliangusha mabomu kwenye kambi ya askari wa SS na kambi yetu iliyokuwa karibu. Watu wengi waliuawa au kuumizwa. Siku iliyofuata, tuliangushiwa mabomu mengi sana, na wakati wa shambulio hilo, mlipuko wenye nguvu ulinirusha hewani.

Ndugu mmoja, Fritz Ulrich, alinisaidia. Aliondoa marundo ya vitu vilivyokuwa juu yangu akitumaini kwamba bado nilikuwa hai. Mwishowe, alinipata na kunitoa katika marundo hayo. Niliporudiwa na fahamu, niligundua kwamba nilikuwa nimeumia vibaya sana usoni na mwilini na singeweza kusikia chochote. Mlipuko huo ulikuwa umeharibu masikio yangu. Kwa miaka mingi masikio yangu yalinitatiza sana lakini mwishowe yakapona.

Wafungwa wachache tu kati ya maelfu ndio waliookoka mabomu hayo. Ndugu zetu wengine walikufa, kutia ndani ndugu mpendwa Gustaw Baumert. Majeraha ambayo nilipata yalisababisha maambukizo pamoja na homa kali. Hata hivyo, baada ya muda, tulipatikana na kuwekwa huru na wanajeshi wa Muungano. Wakati huo, miili iliyokuwa ikioza ya wafungwa waliokufa au kuuawa ilisababisha homa kali inayoletwa na chawa. Mimi pia nilipata homa hiyo. Nilipelekwa hospitalini pamoja na wagonjwa wengine. Madaktari walijitahidi sana lakini ni watatu tu kati yetu tuliookoka! Nilimshukuru Yehova kama nini kwamba alinitia nguvu kubaki mwaminifu katika nyakati hizo ngumu. Nilishukuru pia kwamba Yehova aliniokoa kutoka katika “kivuli kizito” cha kifo.—Zaburi 23:4.

Mwishowe Ninarudi Nyumbani!

Baada ya Wajerumani kujisalimisha, nilitumaini kurudi nyumbani haraka iwezekanavyo, lakini haikuwa rahisi kama nilivyotazamia. Watu fulani tuliokuwa tumefungwa pamoja nao waliniona. Watu hao walikuwa washiriki wa Harakati ya Katoliki. Walisema hivi kwa sauti: “Muueni!” kisha wakaniangusha chini na kunikanyaga-kanyaga. Mtu fulani alikuja na kuniokoa kutokana na ukatili wao, lakini sikupona haraka kwa sababu nilikuwa nimeumia sana na nilikuwa dhaifu kwa sababu ya homa inayoletwa na chawa. Hata hivyo, mwishowe niliweza kwenda nyumbani. Nilifurahi kama nini kuungana tena na familia yangu! Wote walisisimuka sana kuniona, kwa kuwa walifikiri nilikuwa nimekufa.

Muda si muda, tulianza tena kazi ya kuhubiri, na watu wengi waliotafuta kweli kwa unyoofu waliitikia vizuri. Nilipewa mgawo wa kuyapelekea makutaniko vichapo vya Biblia. Pamoja na ndugu wengine, nilikuwa na pendeleo la kwenda Weimar ili kukutana na wawakilishi wa ofisi ya tawi ya Ujerumani, na kutoka huko tulileta nchini Poland matoleo ya kwanza kabisa ya Mnara wa Mlinzi ya baada ya vita. Yalitafsiriwa mara moja, mabamba ya kuchapa yakatayarishwa na nakala zikakatolewa. Ofisi yetu huko Lodz ilipoanza kusimamia kikamili kazi nchini Poland, makutaniko yalianza kupokea kwa ukawaida vichapo vya Biblia. Nilianza kutumika nikiwa painia wa pekee, au mweneza-injili wa wakati wote, na nilihubiri eneo kubwa la Silesia, ambalo sehemu yake kubwa ilikuwa sehemu ya Poland.

Hata hivyo, baada ya muda Mashahidi wa Yehova waliteswa tena, lakini sasa walikuwa wakiteswa na serikali mpya ya Kikomunisti nchini Poland. Kwa sababu ya msimamo wangu wa Kikristo wa kutokuwamo, nilifungwa gerezani mnamo 1948 kwa miaka miwili. Nikiwa gerezani, niliweza kuwasaidia wafungwa wengine wengi kumkaribia Mungu. Mmoja wao alikubali kweli na baadaye akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Mwaka wa 1952, nilifungwa tena gerezani, wakati huu kwa madai ya kwamba nilikuwa mpelelezi wa Marekani! Nilipokuwa nikingoja kesi yangu isikilizwe, nilitiwa katika kifungo cha upweke na kuhojiwa usiku na mchana. Hata hivyo, Yehova alinikomboa tena kutoka mikononi mwa wale waliokuwa wakinitesa, na miaka iliyofuata, sikuteswa tena kwa njia hiyo.

Kilichonisaidia Kuvumilia

Ninapotazama miaka hiyo yote ya majaribu na magumu, ninaweza kutaja mambo muhimu yaliyonitia moyo. Kwanza kabisa, nguvu za kuvumilia zilitoka kwa Yehova na Neno lake, Biblia. Kusali kwa “Mungu wa faraja yote” kutoka moyoni na kwa ukawaida, na kujifunza kila siku Neno lake kulinisaidia mimi na wengine kudumisha hali yetu ya kiroho. Pia, nakala za Mnara wa Mlinzi zilizoandikwa kwa mkono zilituandalia chakula cha kiroho tulichohitaji sana. Katika kambi za mateso, nilitiwa nguvu sana na waamini wenzangu wenye kujali ambao walikuwa tayari na walijitolea kusaidia.

Baraka nyingine ambayo Yehova alinipa ni mke wangu, Maria. Tulifunga ndoa mnamo Oktoba 1950 na baadaye tukamzaa binti, Halina, ambaye alimpenda na kumtumikia Yehova hata alipokuwa mtu mzima. Mimi na Maria tulikaa pamoja kwa miaka 35 kabla ya kifo chake baada ya kuwa mgonjwa kwa muda mrefu. Kifo chake kiliniletea huzuni kubwa na uchungu mwingi sana. Hata ingawa nilihisi kwamba kwa muda fulani ‘nimeangushwa chini, sikuangamizwa.’ (2 Wakorintho 4:9) Katika nyakati hizo ngumu, nilitegemezwa na binti yangu mpendwa, mume wake na watoto wao, yaani, wajukuu wangu, ambao wote wanamtumikia Yehova kwa uaminifu.

Tangu 1990, nimekuwa nikitumika katika ofisi ya tawi ya Poland. Ni baraka kubwa sana kushirikiana kila siku na familia nzuri sana ya Betheli. Nyakati nyingine afya yangu inayozorota inanifanya nijione kama tai aliye dhaifu ambaye anaweza tu kuelea hewani. Hata hivyo, ninatazamia wakati ujao nikiwa na uhakika, nami ‘ninamwimbia Yehova, kwa maana amenitendea kwa njia ya kunipa thawabu’ mpaka leo. (Zaburi 13:6) Ninatazamia wakati ambapo Yehova, Msaidizi wangu, ataondoa madhara yote ambayo yamesababishwa na utawala wa Shetani wenye kuonea.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Januari 1, 1998, ukurasa wa 13, fungu la 6.

^ fu. 20 Ona simulizi la maisha la Elsa Abt katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Oktoba 15, 1980, ukurasa wa 5-9.

^ fu. 20 Ni wimbo namba 101 katika kitabu cha nyimbo cha 1928 chenye kichwa Nyimbo za Kumsifu Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Katika kitabu cha sasa cha nyimbo, ni wimbo namba 56.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nilipewa namba hii na pembetatu ya zambarau katika kambi ya mateso

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa na mke wangu, Maria, mwaka wa 1980