Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Danieli

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Danieli

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Danieli

“KITABU cha Danieli ni kimoja kati ya vitabu vyenye kuvutia sana vya Biblia,” kinasema kitabu kimoja (Holman Illustrated Bible Dictionary). “Kurasa za kitabu cha Danieli zimejaa kweli zisizobadilika.” Masimulizi ya Danieli yanaanza mwaka wa 618 K.W.K. Mfalme Nebukadneza wa Babiloni anapokuja Yerusalemu na kulizingira jiji hilo, kisha kuwapeleka utekwani huko Babiloni “baadhi ya wana wa Israeli.” (Danieli 1:1-3) Kijana Danieli ni mmoja wao, na huenda bado ni mvulana tu. Kitabu hicho kinamalizia huku Danieli akiwa bado Babiloni. Sasa akiwa na umri wa karibu miaka 100, Danieli anapokea ahadi ya Mungu: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.”—Danieli 12:13.

Ingawa sehemu ya kwanza ya kitabu cha Danieli imeandikwa kulingana na wakati wa matukio kwa maoni ya mtazamaji, sehemu ya mwisho imeandikwa kwa maoni ya mhusika. Kitabu hicho ambacho kiliandikwa na Danieli mwenyewe kina unabii mbalimbali kuhusu kuinuka na kuanguka kwa serikali za ulimwengu, wakati wa kufika kwa Masihi, na matukio ya siku zetu. * Pia, nabii huyo aliyezeeka anakumbuka maisha yake marefu na anaeleza matukio ambayo yanatutia moyo kuwa wanaume na wanawake wanaomwogopa Mungu na kushika utimilifu. Ujumbe wa Danieli uko hai na una nguvu.—Waebrania 4:12.

TUNAJIFUNZA NINI KUTOKANA NA MFUATANO WA MATUKIO?

(Danieli 1:1–6:28)

Ni mwaka wa 617 K.W.K. Danieli na marafiki wake watatu, Shadraki, Meshaki, na Abednego, wako katika makao ya mfalme wa Babiloni. Wakati wa miaka mitatu ya mazoezi katika makao ya mfalme, vijana hao wanadumisha utimilifu wao kwa Mungu. Miaka minane hivi baadaye, Mfalme Nebukadneza anaota ndoto ambayo inamfadhaisha. Danieli anafunua ndoto hiyo na kisha anatafsiri maana yake. Mfalme anakiri kwamba Yehova ni “Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme na Mfunuaji wa siri.” (Danieli 2:47) Hata hivyo, punde si punde, inaonekana Nebukadneza anasahau somo hilo. Marafiki watatu wa Danieli wanapokataa kuabudu sanamu kubwa, mfalme anaamuru watupwe ndani ya tanuru ya moto. Mungu wa kweli anawaokoa wanaume hao watatu, na Nebukadneza analazimika kutambua kwamba “hakuna mungu mwingine yeyote anayeweza kuokoa kama huyu.”—Danieli 3:29.

Nebukadneza anaota ndoto nyingine ya maana sana. Anaona mti mrefu sana, ambao unakatwa na kufungwa pingu ili usikue. Danieli anatafsiri maana ya ndoto hiyo. Ndoto hiyo inatimia kwa sehemu Nebukadneza anapopatwa na wazimu na kisha kupata nafuu. Miaka mingi baadaye, Mfalme Belshaza anafanya karamu kubwa kwa ajili ya wakuu wake na bila heshima anatumia vyombo ambavyo vilikuwa vimechukuliwa kutoka katika hekalu la Yehova. Usiku huohuo, Belshaza anauawa na Dario Mmedi anaupokea ufalme. (Danieli 5:30, 31) Katika siku za Dario, Danieli akiwa na umri wa miaka zaidi ya 90, wakuu wa serikali wenye wivu wanapanga njama ya kumuua nabii huyo aliyezeeka. Lakini Yehova anamwokoa “kutoka katika makucha ya simba.”—Danieli 6:27.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:11-15—Je, sura za vijana wanne wa Yudea zilikuwa nzuri sana kwa sababu ya chakula cha mboga za majani? Hapana. Hakuna chakula kinachoweza kutokeza mabadiliko hayo kwa siku kumi tu. Yehova ndiye aliyesababisha mabadiliko hayo ya sura za vijana hao Waebrania. Aliwabariki kwa sababu walimtumaini.—Methali 10:22.

2:1—Nebukadneza aliota ndoto kuhusu sanamu kubwa sana wakati gani? Masimulizi yanasema kwamba hilo lilitukia “katika mwaka wa pili wa ufalme wa Nebukadneza.” Nebukadneza alikuwa mfalme mwaka wa 624 K.W.K. Hivyo, mwaka wa pili wa utawala wake ulianza mwaka wa 623 K.W.K., miaka mingi kabla ya kuivamia Yuda. Wakati huo, Danieli hangekuwa Babiloni ili kutafsiri ndoto hiyo. Inaelekea “mwaka wa pili” unahesabiwa kuanzia mwaka wa 607 K.W.K., mfalme wa Babiloni alipoharibu Yerusalemu na kuwa mtawala wa ulimwengu.

2:32, 39—Ni katika njia gani ufalme wa fedha ulikuwa mdogo kuliko ule wa kichwa cha dhahabu, na ufalme wa shaba ulikuwa mdogo jinsi gani kuliko ule wa fedha? Milki ya Umedi na Uajemi, iliyowakilishwa na sehemu ya fedha ya sanamu hiyo, ilikuwa ndogo kuliko Babiloni, kichwa cha dhahabu, katika maana ya kwamba haikupata pendeleo la pekee la kuiangusha Yuda. Serikali ya ulimwengu iliyofuata ilikuwa Ugiriki, iliyowakilishwa na shaba. Bado serikali ya Ugiriki ilikuwa ndogo, kama vile shaba ilivyo na thamani ndogo ikilinganishwa na fedha. Ingawa Milki ya Ugiriki ilimiliki eneo kubwa zaidi, milki hiyo haikupata pendeleo la pekee la kuwaweka huru watu wa Mungu kutoka uhamishoni kama ilivyofanya milki ya Umedi na Uajemi.

4:8, 9—Je, Danieli mwenyewe alikuwa kuhani mwenye kufanya uchawi? Hapana. Usemi “mkuu wa makuhani wenye kufanya uchawi” unaeleza tu cheo cha Danieli akiwa “mkuu wa manaibu wa maliwali juu ya watu wote wenye hekima wa Babiloni.”—Danieli 2:48.

4:10, 11, 20-22—Ni nini kilichowakilishwa, au kufananishwa, na ule mti mrefu sana katika ndoto ya Nebukadneza? Kwanza, mti huo uliwakilisha Nebukadneza akiwa mtawala wa serikali ya ulimwengu. Hata hivyo, kwa kuwa utawala huo ulienea na ‘kufika mpaka sehemu za mwisho za dunia,’ lazima mti huo uwe unafananisha kitu fulani kilicho kikubwa hata zaidi. Andiko la Danieli 4:17 linahusianisha ndoto hiyo na utawala wa “Aliye Juu Zaidi” juu ya wanadamu. Hivyo basi, mti huo, ulifananisha pia enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote, hasa kuhusiana na dunia. Kwa hiyo, ndoto hiyo ya mti ina utimizo wenye sehemu mbili, yaani, utawala wa Nebukadneza na enzi kuu ya Yehova.

4:16, 23, 25, 32, 33—Zile “nyakati saba” zilikuwa na urefu gani? Mabadiliko yote yaliyohusika katika kutokea kwa Mfalme Nebukadneza yalihitaji “nyakati saba” zilizo ndefu zaidi kuliko siku saba halisi. Katika kisa chake, nyakati hizo zilimaanisha miaka saba ya siku 360 kila mmoja, au siku 2,520. Katika utimizo mkubwa zaidi, “nyakati saba” ni miaka 2,520. (Ezekieli 4:6, 7) Miaka hiyo ilianza na uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. nayo ilimalizika Yesu alipowekwa rasmi kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914 W.K.—Luka 21:24.

6:6-10—Kwa kuwa kusali kwa Yehova hakuhitaji kikao chochote hususa, je, halingekuwa jambo la hekima kwa Danieli kusali faraghani kwa kile kipindi cha siku 30? Ni jambo lililojulikana kwamba Danieli alikuwa akisali mara tatu kila siku. Ndiyo sababu wale waliopanga njama hiyo walitokeza wazo la kutunga sheria iliyokataza kusali. Ikiwa Danieli angebadili kwa vyovyote kawaida yake ya kusali, huenda wengine wangeona kwamba amelegeza msimamo wake na hilo lingeonyesha kwamba ameshindwa kujitoa kikamili kwa Yehova.

Mambo Tunayojifunza:

1:3-8. Azimio la Danieli na la wenzake la kubaki washikamanifu kwa Yehova linakazia thamani ya mazoezi waliyopata kutoka kwa wazazi wao. Wazazi wanaomwogopa Mungu wanapotanguliza mambo ya kiroho maishani mwao na kufundisha wazao wao kufanya vivyo hivyo, inaelekea watoto wao watashinda vishawishi na mikazo yoyote ile ambayo huenda ikatokea shuleni au mahali pengine.

1:10-12. Danieli alielewa kwa nini “ofisa mkuu wa makao ya mfalme” alimwogopa mfalme naye akaacha kutoa ombi lake kwa ofisa huyo. Hata hivyo, baadaye Danieli alimwendea “mlinzi,” ambaye angeweza kukubali kwa urahisi ombi lake. Tunaposhughulika na hali ngumu, tunapaswa kutenda kwa ufahamu, uelewaji, na hekima kama hiyo.

2:29, 30. Kama Danieli, tunapaswa kumtukuza Yehova kwa ajili ya ujuzi, sifa, na uwezo mbalimbali ambao huenda tukawa nao kwa sababu ya maandalizi yake ya kiroho.

3:16-18. Inaelekea kwamba wale Waebrania watatu hawangejibu kwa uthabiti hivyo ikiwa tayari walikuwa wameshindwa na jaribu la chakula. Sisi pia tunapaswa kujitahidi kuwa “waaminifu katika mambo yote.”—1 Timotheo 3:11.

4:24-27. Kutangaza ujumbe wa Ufalme, ambao unatia ndani hukumu kali za Mungu, kunahitaji imani na ujasiri kama ule ambao Danieli alionyesha alipomwambia Nebukadneza yale ambayo yangempata na yale ambayo mfalme alipaswa kufanya ili ‘mafanikio yake yarefushwe.’

5:30, 31. ‘Neno la kimethali juu ya mfalme wa Babiloni’ lilitimia. (Isaya 14:3, 4, 12-15) Shetani Ibilisi, ambaye ni mwenye kiburi kama wafalme wa ukoo wa Kibabiloni, pia atapatwa na mwisho wenye aibu.—Danieli 4:30; 5:2-4, 23.

MAONO YA DANIELI YANAFUNUA NINI?

(Danieli 7:1–12:13)

Danieli anapopokea maono ya ndoto yake ya kwanza katika mwaka wa 553 K.W.K., ana umri wa zaidi ya miaka 70. Danieli anaona wanyama mwitu wanne wakubwa ambao wanawakilisha mfuatano wa serikali za ulimwengu kuanzia siku zake mpaka siku zetu. Katika maono ya mambo yanayotendeka mbinguni, anaona “mtu fulani kama mwana wa binadamu” akipewa “utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 7:13, 14) Miaka miwili baadaye, Danieli anaona maono yanayohusu Umedi na Uajemi, Ugiriki, na kikundi ambacho kinakuwa “mfalme mwenye sura kali.”—Danieli 8:23.

Sasa tuko katika mwaka wa 539 K.W.K. Jiji la Babiloni limeanguka, na Dario Mmedi amekuwa mtawala juu ya ufalme wa Wakaldayo. Danieli anasali kwa Yehova kuhusu kurudishwa kwa nchi yake. Huku akiwa bado anasali, Yehova anamtuma malaika Gabrieli ili kumfanya Danieli ‘apate ufahamu kwa kuelewa’ kuhusu kuja kwa Masihi. (Danieli 9:20-25) Wakati unasonga mpaka mwaka wa 536/535 K.W.K. Mabaki ya Waisraeli wamerudi Yerusalemu. Lakini kuna upinzani kuelekea kazi ya ujenzi wa hekalu. Jambo hilo linamsumbua sana Danieli. Anasali sana kulihusu, na Yehova anamtuma malaika wa cheo cha juu kwa Danieli. Baada ya kumwimarisha na kumtia moyo Danieli, malaika huyo anaeleza unabii unaoonyesha mapambano ya kupata mamlaka kubwa kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Mapambano kati ya wafalme hao wawili yanaanza wakati ufalme wa Aleksanda Mkuu unapogawanyika kati ya majemadari wake wanne mpaka wakati ambapo Mikaeli yule Mkuu “atasimama.”—Danieli 12:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

8:9—“Pambo” linafananisha nini? Katika kisa hiki, “Pambo” linafananisha hali ya kidunia ya Wakristo watiwa-mafuta wakati wa utawala wa Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani.

8:25—“Mkuu wa wakuu” ni nani? Neno la Kiebrania sar, linalotafsiriwa “mkuu,” kimsingi linamaanisha “mkuu,” au “kichwa.” Cheo “Mkuu wa wakuu” kinamhusu tu Yehova Mungu ambaye ni Mkuu wa malaika wote wakuu, kutia ndani “Mikaeli, aliye mmoja wa hao wakuu wa mbele.”—Danieli 10:13.

9:21—Kwa nini Danieli anamwita malaika Gabrieli “mwanamume”? Ni kwa sababu Gabrieli alimjia katika umbo la kibinadamu, kama alivyomtokea Danieli katika maono ya mapema.—Danieli 8:15-17.

9:27—Ni agano gani lililoendelea ‘kutendeshwa kwa ajili ya wengi’ mpaka mwishoni mwa juma la 70 la miaka, au mwaka wa 36 W.K.? Agano la Sheria liliondolewa mwaka wa 33 W.K. Yesu alipotundikwa. Lakini, kwa kuendelea kutendesha agano la Kiabrahamu kwa ajili ya Waisraeli wa asili mpaka mwaka wa 36 W.K., Yehova aliongeza kipindi cha pendeleo la pekee kwa Wayahudi kwa sababu walikuwa wazao wa Abrahamu. Agano la Kiabrahamu linaendelea kutendeshwa kwa ajili ya “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 3:7-9, 14-18, 29; 6:16.

Mambo Tunayojifunza:

9:1-23; 10:11. Danieli alikuwa “mtu mwenye kutamanika sana” kwa sababu ya unyenyekevu wake, ujitoaji-kimungu, bidii yake ya kujifunza, na kudumu kwake katika sala. Sifa hizo zilimsaidia pia kubaki mwaminifu kwa Mungu mpaka mwisho wa maisha yake. Acheni tuazimie kufuata mfano wa Danieli.

9:17-19. Hata tunaposali kwa ajili ya kuja kwa ulimwengu mpya wa Mungu, ambamo “uadilifu utakaa,” je, hatupaswi kukazia fikira kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi yake kuu badala ya kukomeshwa kwa mateso na matatizo yetu?—2 Petro 3:13.

10:9-11, 18, 19. Kwa kumwiga malaika aliyemtembelea Danieli, tunapaswa kutiana moyo na kutiana nguvu kwa kusaidiana kwa matendo na maneno yenye kufariji.

12:3. Katika siku hizi za mwisho, “wale walio na ufahamu,” yaani, Wakristo watiwa-mafuta, ‘wameangaza kama mianga’ na wamewaleta “wengi kwenye uadilifu,” kutia ndani “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.” (Wafilipi 2:15; Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Watiwa-mafuta ‘wataangaza kama nyota’ katika maana kamili wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, watakaposhirikiana naye kutumia kwa ukamili faida za fidia kwa ajili ya wanadamu watiifu duniani. “Kondoo wengine” wanapaswa kubaki washikamanifu kwa watiwa-mafuta na kuwategemeza kwa moyo wote katika kila njia.

Yehova ‘Anawabariki Wale Wanaomwogopa’

Kitabu cha Danieli kinatufundisha nini kuhusu Mungu tunayemwabudu? Fikiria unabii mbalimbali ulio katika kitabu hicho, ule ambao tayari umetimia na ule ambao haujatimia bado. Unamwonyesha Yehova kuwa Mtimizaji wa neno lake.—Isaya 55:11.

Sehemu ya masimulizi ya kitabu cha Danieli inaonyesha nini kumhusu Mungu wetu? Wale vijana wanne Waebrania ambao walikataa kujiingiza katika maisha ya makao ya mfalme wa Babiloni walipokea ‘ujuzi, ufahamu, na hekima.’ (Danieli 1:17) Mungu wa kweli alimtuma malaika wake naye akawaokoa Shadraki, Meshaki, na Abednego kutoka katika tanuru ya moto. Danieli aliokolewa kutoka katika tundu la simba. Yehova ‘anawasaidia na kuwalinda wale wanaomtegemea’ na ‘anawabariki wale wanaomwogopa.’—Zaburi 115:9, 13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kuhusu uchunguzi wa mstari kwa mstari wa kitabu cha Danieli, ona kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kwa nini Danieli alikuwa “mtu mwenye kutamanika sana”?