Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tambua Umuhimu wa Kutoa Pongezi

Tambua Umuhimu wa Kutoa Pongezi

Tambua Umuhimu wa Kutoa Pongezi

JE, UMEWAHI kusikia mtu fulani akilalamika kwamba mwajiri wake wa kazi anampongeza mara chache sana? Je, wewe pia umewahi kulalamika hivyo? Au ikiwa wewe ni kijana, je, umewahi kusema vivyo hivyo kuhusu wazazi wako au walimu wako?

Baadhi ya malalamiko hayo huenda ni ya kweli. Lakini kulingana na mkufunzi mmoja Mjerumani, wafanyakazi wanapotoa malalamiko hayo, kile kinachowasumbua sana si kukosa kupongezwa lakini ni mwajiri wa kazi kukosa kupendezwa nao kibinafsi. Kwa vyovyote vile, ni wazi kwamba kuna jambo ambalo si sawa. Tukitaka kuwa na mahusiano yenye kuridhisha, kuwapongeza watu na kupendezwa nao kibinafsi ni mambo muhimu sana.

Hilo ni kweli pia kuhusiana na ibada. Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanapaswa kupongezana, kuonyeshana uchangamfu, na kupendezwa kibinafsi na wengine. Wanatimiza na kudumisha hali hiyo nzuri kwa kufuata miongozo ya Biblia. Lakini hata kutaniko likiwa na upendo kadiri gani, tunaweza sikuzote kuboresha hali hiyo. Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze mifano mitatu mizuri ya watu waliotoa pongezi: Elihu, mtumishi wa Mungu aliyeishi kabla ya Ukristo, mtume Paulo, na Yesu Kristo mwenyewe.

Kushauri kwa Njia ya Adabu na Heshima

Inaelekea, Elihu, mtu wa ukoo wa mbali wa Abrahamu, alimsaidia sana Ayubu kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu uhusiano wake pamoja na Mungu. Elihu alikuwa mwenye adabu na heshima. Alingoja kwa subira zamu yake ya kusema ifike. Na ingawa wale waliodai kuwa marafiki wa Ayubu waliona tu makosa yake, mbali na kutoa mashauri, Elihu alikuwa tayari kumpongeza Ayubu kwa sababu ya maisha yake manyoofu. Alifanya hivyo kwa uchangamfu na kwa hisia zilizoonyesha wazi kwamba alipendezwa naye akiwa rafiki. Tofauti na wale wengine, Elihu alimwita Ayubu kwa jina. Alimwomba hivi kwa adabu: “Ee Ayubu, tafadhali sikia maneno yangu, nawe tega sikio kwa maneno yangu yote.” Kwa heshima huku akijiweka mwenyewe mahali pa Ayubu, Elihu alikiri hivi: “Tazama! Mimi ni kama wewe tu mbele za Mungu wa kweli; mimi pia niliumbwa kutoka kwenye udongo.” Kisha akampongeza kwa kusema hivi: “Ikiwa kuna maneno yoyote ya kusema, nijibu; sema, kwa maana nimependezwa na uadilifu wako.”—Ayubu 33:1, 6, 32.

Kwa njia fulani, kuwatendea wengine kwa adabu na heshima ni njia moja ya kuwapongeza. Kwa kweli, ni kana kwamba tunamwaambia msikilizaji wetu, ‘Ninavutiwa sana na wewe na unastahili kutendewa kwa heshima.’ Hivyo, tunamfanya awe mchangamfu na kumwonyesha kwamba tunapendezwa naye.

Kuwa mwenye heshima na adabu hakumaanishi kufuata tu kanuni za adabu nzuri. Ili kugusa mioyo ya wengine, tunapaswa kuonyesha adabu na heshima kwa unyoofu na kutoka moyoni. Tunapaswa kufanya hivyo kwa sababu tunawapenda na kuwajali wengine kikweli.

Kupongeza kwa Busara

Mtume Paulo alionyesha jinsi tunavyoweza kuwapongeza wengine kwa busara. Kwa mfano, katika safari yake ya pili ya umishonari alipokuwa akihubiri huko Athene, alitetea Ukristo mbele ya wanafalsafa fulani Wagiriki. Ona jinsi alivyotimiza kwa busara mgawo huo mgumu. “Watu fulani kati ya Waepikurea na wanafalsafa Wastoa pia wakawa wanaongea naye kwa mabishano, na baadhi yao walikuwa wakisema: ‘Mpiga-domo huyu angependa kueleza jambo gani?’ Wengine: ‘Anaonekana kuwa mtangazaji wa miungu migeni.’” (Matendo 17:18) Ingawa alidhihakiwa hivyo, Paulo alibaki akiwa mtulivu na kuwajibu hivi: “Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuogopa miungu kuliko wengine.” Badala ya kuwashutumu kuwa waabudu-sanamu, Paulo aliwapongeza kwa ujitoaji wao kwa mambo ya kidini.—Matendo 17:22.

Je, Paulo alikuwa mnafiki? Hapana. Alijua kwamba halikuwa daraka lake kuwahukumu wasikilizaji wake; kwa kuwa alijua vizuri kwamba wakati mmoja yeye mwenyewe hakuijua kweli. Kazi yake ilikuwa kutangaza ujumbe wa Mungu, na si kuwahukumu wengine. Alijua kutokana na mambo yaliyompata jambo hili ambalo Mashahidi wa Yehova wengi wametambua leo: Watetezi fulani wanyoofu wa dini ya uwongo mwishowe wanageuka na kuwa watetezi thabiti zaidi wa dini ya kweli.

Paulo alikuwa na maoni mazuri, nayo yalitokeza mafanikio. “Wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini, kati yao pia wakiwa ni Dionisio, mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke mmoja aliyeitwa Damari, na wengine mbali na hao.” (Matendo 17:34) Badala ya kuwashutumu kwa sababu ya kukosa ujuzi sahihi, ni jambo la hekima kama nini kwamba Paulo aliwapongeza Waathene kwa ajili ya mambo waliyoamini kwa unyoofu hata ingawa mambo hayo hayakuwa ya kweli! Inaelekea kwamba watu wanaopotoshwa na habari za uwongo mara nyingi wana mioyo mizuri.

Alipoitwa ili kujitetea mbele ya Herode Agripa wa Pili, Paulo alishughulikia pia hali hiyo kwa busara. Ilijulikana kwamba Herode alikuwa na uhusiano wa kingono na dada yake Bernike, jambo ambalo linashutumiwa waziwazi na Neno la Mungu. Hata hivyo, Paulo hakumshutumu Herode. Badala yake, alipata jambo fulani la kumpongeza. “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi, Mfalme Agripa, ninajihesabu mwenyewe kuwa mwenye furaha kwamba ninajitetea mbele yako leo, hasa kwa kuwa wewe una ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi.”—Matendo 26:1-3.

Litakuwa jambo la hekima kama nini kwetu kutenda kwa njia kama hiyo ya busara tunaposhughulika na wengine! Kumpongeza jirani, mwanafunzi mwenzetu, au mfanyakazi mwenzetu kunaweza kusitawisha uhusiano wenye amani na kuwafanya wajiendeshe vizuri. Tukigusa mioyo ya watu kwa kuwapongeza inavyostahili, huenda nyakati nyingine tukawachochea wale walio wanyoofu wabadili matendo na mawazo yao ya uwongo na kutenda kupatana na ujuzi sahihi.

Yesu ni Kielelezo Kikamilifu Katika Kuwapongeza Wengine

Yesu aliwapongeza wengine. Kwa mfano, baada ya kufufuliwa na kupanda mbinguni, Yesu akiongozwa na Mungu, alimtumia mtume Yohana kuyaandikia makutaniko saba huko Asia Ndogo. Hakukosa kamwe kuwapongeza wale ambao walistahili kupongezwa. Katika ujumbe wake kwa makutaniko ya Efeso, Pergamamu, na Thiatira, alitumia maneno kama vile: “Mimi nayajua matendo yako, na kazi yako ya jasho na uvumilivu, na kwamba huwavumilii watu wabaya”; “bado unaendelea kulishika sana jina langu, nawe hukukana imani yako katika mimi”; na “mimi nayajua matendo yako, na upendo wako na imani na huduma na uvumilivu wako, na kwamba matendo yako ya hivi karibuni yanazidi yale ya zamani.” Hata katika kutaniko la Sardi ambalo lilihitaji shauri kali, Yesu alitambua kwamba lilikuwa na watu ambao walistahili kupongezwa. Alisema hivi: “Hata hivyo, una majina machache katika Sardi ambayo hayakutia unajisi mavazi yao ya nje, nao watatembea pamoja nami wakiwa na mavazi meupe, kwa sababu wanastahili.” (Ufunuo 2:2, 13, 19; 3:4) Yesu aliweka kielelezo kizuri kama nini!

Kwa kumwiga Yesu, hatupaswi kamwe kushutumu kikundi chote cha watu kwa sababu ya makosa ya washiriki wachache au kutoa mashauri yanayohitajiwa pasipo pia kutoa pongezi zinazostahili. Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba tukitoa pongezi wakati tu tunapopanga kutoa mashauri, huenda pongezi zetu zikapuuzwa. Uwe mkarimu katika kutoa pongezi inapowezekana! Ukifanya hivyo, pindi fulani mashauri yatakapohitajiwa, itakuwa rahisi zaidi kwa wengine kuyakubali.

Wazee Wanaotoa Pongezi Zinazofaa

Cornelia, mwanamke Mkristo anayetumika sasa katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ulaya, anakumbuka kwamba mapema katika miaka ya 1970, mwangalizi anayesafiri alimuuliza jinsi alivyokuwa akifanya funzo lake la kibinafsi na kusoma magazeti. “Niliona aibu,” anasema. Lakini alikubali kwamba hakuwa akisoma makala zote za gazeti. “Badala ya kunishutumu kwa sababu hiyo,” anakumbuka, “alinipongeza kwa kujitahidi kusoma kadiri nilivyoweza. Nilihisi amenitia moyo sana kwa kunipongeza na tangu hapo, niliazimia kusoma kila makala.”

Ray, anayetumika katika ofisi moja ya tawi huko Ulaya, anakumbuka siku aliyoanza utumishi wa upainia. Mwangalizi-msimamizi wa kutaniko lao, ambaye ni mfanyakazi aliye na wajibu wa familia na pia madaraka mengi kutanikoni, aliingia katika Jumba la Ufalme jioni hiyo na kwenda moja kwa moja kwa Ray na kumuuliza: “Siku yako ya kwanza katika utumishi wa upainia ilikuwa namna gani?” Sasa, miaka 60 hivi imepita, na bado Ray anakumbuka jinsi mzee huyo alivyomjali sana.

Kama mambo hayo mawili yaliyoonwa yanavyoonyesha, shauku ya unyoofu, kupendezwa kikweli na wengine, na kupenda yale ambayo wengine wamefanya kunaweza kufaidi sana. Maneno matupu tu au kuwasifu-sifu watu hakuwezi kuwafaidi. Katika kutaniko la Kikristo, tuna sababu nyingi nzuri za kuwapongeza waamini wenzetu. Tunaweza kuwapongeza kwa sababu ya tamaa yao ya kumtumikia Yehova, maelezo yao yaliyotayarishwa vizuri, maendeleo yao katika kushinda woga ili kutoa hotuba au kushiriki katika sehemu za mikutano, bidii yao katika kuhubiri na kufundisha, na jitihada zao za kutanguliza mambo ya Ufalme na miradi ya kiroho. Tunapowapongeza wengine, tunathawabishwa sana. Tunakuwa wenye furaha na hilo linatusaidia kuona mambo kwa njia nzuri.—Matendo 20:35.

Ni vizuri wazee wa kutaniko wawapongeze washiriki wa kutaniko kwa sababu ya kazi yao nzuri. Na shauri linapohitajiwa, watalitoa kwa roho ya upendo. Kwa upande mwingine, hawatadai mambo yote yafanywe kwa ukamilifu na kuona kila jambo lisilofanywa kikamilifu kuwa kosa zito.

Wazee Wakristo wanaomwiga Elihu katika kuonyesha heshima na adabu, wanaomwiga Paulo katika kutumia busara, na wanaomwiga Yesu katika kuwahangaikia wengine kwa upendo watawatia moyo kwelikweli ndugu zao. Pongezi zitawatia wengine moyo kutimiza mengi zaidi na zitafanya kuwe na mahusiano mazuri na yenye shangwe. Yesu alipobatizwa alishangilia kama nini kumsikia Baba yake wa mbinguni akimpongeza kwa maneno haya: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe”! (Marko 1:11) Basi na tufanye mioyo ya ndugu zetu ishangilie kwa kuwapongeza kikweli na kwa unyoofu.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutumia busara kulimletea Paulo matokeo mazuri, inaweza kuwa vivyo hivyo kutuhusu

[Picha katika ukurasa wa 16]

Pongezi inayotolewa kwa shauku na unyoofu inaweza kuwa na matokeo mazuri sana