Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’

‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’

‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’

“Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.”—LUKA 6:36.

1, 2. Maneno ya Yesu kwa waandishi na Mafarisayo na kwa wafuasi wake yanaonyesha jinsi gani kwamba rehema ni sifa yenye kupendeza?

SHERIA iliyotolewa kupitia Musa ilikuwa na matakwa na masharti 600 hivi. Ingawa lilikuwa jambo la maana kutimiza matakwa ya Sheria ya Musa, lilikuwa pia jambo la maana kuonyesha rehema. Fikiria yale ambayo Yesu aliwaambia Mafarisayo ambao hawakuwaonyesha wengine rehema. Mara mbili, aliwakemea akisema kwamba Mungu alikuwa ametangaza hivi: “Ninataka rehema, wala si dhabihu.” (Mathayo 9:10-13; 12:1-7; Hosea 6:6) Mwishoni mwa huduma yake, Yesu alisema: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu ninyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na bizari, lakini mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.”—Mathayo 23:23.

2 Ni wazi kwamba Yesu aliona rehema kuwa sifa ya maana sana. Aliwaambia wafuasi wake hivi: “Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.” (Luka 6:36) Hata hivyo, ili tuwe “waigaji wa Mungu,” tunahitaji kujua rehema ya kweli ni nini. (Waefeso 5:1) Zaidi ya hayo, kuelewa faida za rehema kutatuchochea kuonyesha sifa hiyo kwa ukamili zaidi katika maisha yetu.

Kuwaonyesha Rehema Wenye Uhitaji

3. Kwa nini tunapaswa kumwendea Yehova ili tujifunze maana ya rehema ya kweli?

3 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova ni mwenye neema na mwenye rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mkuu katika fadhili zenye upendo. Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:8, 9) Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Tunaonyesha rehema kwa kumtendea mtu mwingine kwa huruma. Hiyo ni sehemu muhimu sana ya utu wa Mungu. Tunaweza kujifunza maana ya rehema ya kweli kupitia kielelezo cha Mungu na maagizo anayotupa.

4. Andiko la Isaya 49:15 linatufundisha nini kuhusu rehema?

4 Kama inavyoonyeshwa kwenye Isaya 49:15, Yehova anasema: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake?” Maneno mbalimbali ya Kiebrania yanayohusiana sana na neno linalotafsiriwa hapa kuwa ‘kuhurumia’ yanatumiwa kuhusiana na rehema katika andiko la Zaburi 145:8, 9, linalonukuliwa hapo juu. Hisia zinazomchochea Yehova kuwa mwenye rehema zinalinganishwa na hisia ambazo kwa kawaida mama mwenye kunyonyesha anazo kuelekea mtoto wake. Pengine mtoto ana njaa au ana uhitaji mwingine. Hisia hizo zinamchochea mama kuwa na huruma, na hivyo anatosheleza mahitaji ya mtoto wake. Yehova ana hisia nyororo kama hizo kuelekea wale ambao anawaonyesha rehema.

5. Yehova alionyesha namna gani kwamba alikuwa “tajiri katika rehema” kuwaelekea Waisraeli?

5 Ni jambo zuri kuwahurumia wengine, lakini ni jambo bora hata zaidi kusukumwa na huruma kuchukua hatua ili kuwasaidia wenye uhitaji. Fikiria jinsi Yehova alivyoitikia waabudu wake walipokuwa utumwani huko Misri miaka 3,500 iliyopita. Alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo. Nami ninashuka ili kuwakomboa kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:7, 8) Miaka 500 hivi baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, Yehova aliwakumbusha: “Mimi ndiye niliyewatoa Israeli kutoka Misri nami nikawakomboa ninyi kutoka mkono wa Misri na kutoka mkono wa falme zote zilizokuwa zikiwakandamiza ninyi.” (1 Samweli 10:18) Kwa sababu ya kuacha viwango vya uadilifu vya Mungu, mara kwa mara Waisraeli walikuwa katika hali ngumu. Hata hivyo, Yehova aliwahurumia na aliwaokoa tena na tena. (Waamuzi 2:11-16; 2 Mambo ya Nyakati 36:15) Hilo linaonyesha jinsi Mungu huyo mwenye upendo anavyowatendea wale walio katika uhitaji, hatari, au hali ngumu. Yehova ni “tajiri katika rehema.”—Waefeso 2:4.

6. Yesu Kristo alimwiga Baba yake jinsi gani katika kuonyesha rehema?

6 Alipokuwa duniani, Yesu Kristo alimwiga Baba yake kikamilifu katika kuonyesha rehema. Yesu alitenda namna gani wanaume wawili vipofu walipomsihi hivi: “Bwana, uturehemu, Mwana wa Daudi”? Walikuwa wakimsihi Yesu awarudishie kimuujiza uwezo wa kuona. Yesu alifanya hivyo, lakini hakufanya muujiza bila hisia. ‘Akiwasikitikia,’ inasema Biblia, “[Yesu] akayagusa macho yao, na mara moja wakapata kuona.” (Mathayo 20:30-34) Sikitiko lilimchochea Yesu kufanya miujiza mingi ambayo iliwaletea kitulizo vipofu, watu waliokuwa na roho waovu, wenye ukoma, na wazazi wenye watoto waliokuwa wakiteseka.—Mathayo 9:27; 15:22; 17:15; Marko 5:18, 19; Luka 17:12, 13.

7. Mfano wa Yehova Mungu na Mwana wake unatufundisha nini kuhusu rehema?

7 Mfano wa Yehova Mungu na Yesu Kristo unaonyesha kwamba rehema inahusisha mambo mawili—hisia za huruma, au sikitiko kuelekea wenye uhitaji na matendo yanayoleta kitulizo kwa wale walio katika uhitaji. Ili kuwa mwenye rehema ni lazima mtu awe na hisia na atende. Katika Maandiko, mara nyingi rehema inarejelea tendo la fadhili kuelekea wale walio katika uhitaji. Hata hivyo, rehema inaonyeshwa jinsi gani katika hukumu? Je, rehema inahusu pia kutofanya jambo fulani kama vile kujizuia kutoa adhabu?

Kuwaonyesha Rehema Wakosaji

8, 9. Rehema ambayo Daudi alionyeshwa baada ya dhambi yake pamoja na Bath-sheba ilitia ndani nini?

8 Fikiria yale yaliyotukia baada ya nabii Nathani kuzungumza na Mfalme Daudi wa Israeli la kale kuhusu uzinzi wa Daudi pamoja na Bath-sheba. Daudi aliyetubu alisali hivi: “Ee Mungu, unionyeshe kibali kulingana na fadhili zako zenye upendo. Ufutilie mbali makosa yangu kulingana na wingi wa rehema zako. Unioshe kabisa kutokana na kosa langu, na kunitakasa kutokana na dhambi yangu. Kwa maana mimi mwenyewe nayajua makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi, nami nimefanya lililo baya machoni pako.”—Zaburi 51:1-4.

9 Daudi alisikitika sana. Yehova alimsamehe dhambi yake na alijizuia kuwahukumu vikali Daudi na Bath-sheba. Kulingana na Sheria ya Musa, Daudi na Bath-sheba walipaswa kuuawa. (Kumbukumbu la Torati 22:22) Ingawa hawakuuawa, hawakuepuka matokeo mabaya ya dhambi yao. (2 Samweli 12:13) Rehema ya Mungu inatia ndani kusamehe makosa. Hata hivyo, hajizuii kutoa adhabu inayostahili.

10. Ingawa Yehova ni mwenye rehema anapotekeleza hukumu, kwa nini hatupaswi kuchezea rehema zake?

10 Kwa kuwa “kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu,” na “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” wanadamu wote wanastahili kifo. (Waroma 5:12; 6:23) Tunashukuru kama nini kwamba Yehova anaonyesha rehema anapotekeleza hukumu! Hata hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusichezee rehema za Mungu. ‘Njia zote za Yehova ni haki,’ linasema andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4. Anapoamua kuonyesha rehema, Mungu hapuuzi viwango vyake vikamilifu vya haki.

11. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba hakupuuza haki aliposhughulikia dhambi ya Daudi pamoja na Bath-sheba?

11 Daudi na Bath-sheba walipaswa kwanza kusamehewa kabla ya hukumu ya kifo kupunguzwa. Waamuzi wa Israeli hawakuruhusiwa kusamehe dhambi. Ikiwa wangeruhusiwa kushughulikia kisa hicho, wangelazimika tu kutoa hukumu ya kifo. Sheria ilitaka watoe hukumu hiyo. Hata hivyo, kwa sababu ya agano lake pamoja na Daudi, Yehova alitaka kuona ikiwa kulikuwa na msingi wa kusamehe dhambi ya Daudi. (2 Samweli 7:12-16) Hivyo, Yehova Mungu, yule “Mwamuzi wa dunia yote,” ambaye ni “mchunguzaji wa moyo,” aliamua kushughulikia kisa hicho yeye mwenyewe. (Mwanzo 18:25; 1 Mambo ya Nyakati 29:17) Mungu aliweza kusoma kwa usahihi moyo wa Daudi, akaona kwamba alikuwa ametubu kikweli, na hivyo akamsamehe.

12. Wanadamu wenye dhambi wanaweza kufaidika jinsi gani na rehema ya Mungu?

12 Rehema ambayo Yehova anatuonyesha kwa kutuwezesha kuwekwa huru kutokana na adhabu ya kifo kwa sababu ya dhambi tuliyorithi inapatana na haki yake. Ili asamehe dhambi bila kuvunja haki yake, Yehova ameandaa dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo, ambalo ndilo tendo kubwa zaidi la rehema. (Mathayo 20:28; Waroma 6:22, 23) Ili tufaidike kutokana na rehema ya Mungu, ambayo inaweza kutuokoa tusipatwe na adhabu ya kifo kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, tunapaswa ‘kumwamini Mwana.’—Yohana 3:16, 36.

Mungu wa Rehema na Haki

13, 14. Je, rehema ya Mungu inapunguza uzito wa haki yake? Eleza.

13 Ingawa rehema ya Yehova haivunji kiwango chake cha haki, je, kwa kadiri fulani rehema inabadili haki yake? Je, rehema inapunguza uzito wa haki ya Mungu? Hapana.

14 Kupitia nabii Hosea, Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Nitakuchumbia mpaka wakati usio na kipimo, nitakuchumbia uwe wangu katika uadilifu na katika haki na katika fadhili zenye upendo na katika rehema.” (Hosea 2:19) Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba rehema ya Yehova sikuzote inapatana na sifa zake nyingine, kutia ndani haki. Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, . . . anayesamehe kosa na ubaya na dhambi, lakini kwa vyovyote hatakosa kuadhibu.” (Kutoka 34:6, 7) Yehova ni Mungu wa rehema na haki. Biblia inasema hivi kumhusu: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Haki ya Mungu ni kamilifu, kama ilivyo rehema yake. Hakuna iliyo kubwa kuliko nyingine, wala hakuna ile inayohitaji kupunguza uzito wa nyingine. Badala yake, sifa hizo mbili zinafanya kazi pamoja kwa upatano.

15, 16. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba haki ya Mungu si yenye ukatili? (b) Waabudu wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika gani wakati Yehova atakapotekeleza hukumu yake juu ya mfumo huu mbovu wa mambo?

15 Haki ya Yehova si yenye ukatili. Sikuzote haki inahusiana na sheria, na kwa kawaida hukumu inatolewa kwa wakosaji ambao wanastahili adhabu. Hata hivyo, haki ya Mungu inaweza pia kutia ndani wokovu kwa ajili ya wale wanaostahili. Kwa mfano, watu waovu katika majiji ya Sodoma na Gomora walipoharibiwa, mzee wa ukoo Loti na mabinti wake wawili waliokolewa.—Mwanzo 19:12-26.

16 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakapotekeleza hukumu juu ya mfumo huu mbovu wa mambo, ule “umati mkubwa” wa waabudu wa kweli, ambao “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” utaokolewa. Kwa hiyo, waabudu hao ‘watatoka katika ile dhiki kuu.’—Ufunuo 7:9-14.

Kwa Nini Tuwe Wenye Rehema?

17. Ni nini sababu ya msingi ya kuwa wenye rehema?

17 Kwa kweli, mfano wa Yehova na wa Yesu Kristo unatufundisha maana ya rehema ya kweli. Likitupa sababu ya msingi ya kuwa wenye rehema, andiko la Methali 19:17 linasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” Yehova anafurahi tunapomwiga yeye na Mwana wake kwa kuwa wenye rehema tunaposhughulika na wenzetu. (1 Wakorintho 11:1) Wengine pia wanatiwa moyo kuwa wenye rehema, kwa kuwa tunapowaonyesha wengine rehema wao pia wanatuonyesha rehema.—Luka 6:38.

18. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuwa wenye rehema?

18 Rehema ni mchanganyiko wa sifa nyingi nzuri. Inatia ndani neema, upendo, fadhili, na wema. Hisia nyororo za huruma ndizo zinazotuchochea kutenda kwa rehema. Ingawa rehema ya Mungu haipunguzi uzito wa haki yake, Yehova si mwepesi wa hasira na kwa subira anawapa wakosaji wakati wa kutosha ili watubu. (2 Petro 3:9, 10) Kwa hiyo, rehema inahusiana na subira na ustahimilivu. Kwa kuwa rehema ni mchanganyiko wa sifa nyingi nzuri, kutia ndani sifa mbalimbali za matunda ya roho ya Mungu, rehema inaweza kutusaidia kusitawisha sifa hizo. (Wagalatia 5:22, 23) Ni jambo la maana kama nini tujitahidi kuwa wenye rehema!

“Wenye Furaha ni Wale Walio na Rehema”

19, 20. Ni katika maana gani rehema inafurahi juu ya hukumu?

19 Mwanafunzi Yakobo anatuambia kwa nini rehema inapaswa kuwa sifa muhimu katika maisha yetu. Aliandika hivi: “Rehema hufurahi kwa njia ya ushindi juu ya hukumu.” (Yakobo 2:13b) Yakobo alikuwa akisema kuhusu rehema ambayo mwabudu wa Yehova anawaonyesha wengine. Rehema inafurahi kwa njia ya ushindi juu ya hukumu katika maana ya kwamba wakati unapofika wa mtu ‘kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe,’ Yehova anafikiria matendo ya rehema ya mtu huyo naye anamsamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Mwana Wake. (Waroma 14:12) Bila shaka, sababu moja iliyofanya Daudi aonyeshwe rehema kuhusiana na dhambi yake pamoja na Bath-sheba ni kwamba Daudi mwenyewe alikuwa mtu mwenye rehema. (1 Samweli 24:4-7) Kwa upande mwingine, “yeye asiye na mazoea ya kuonyesha rehema atapata hukumu yake bila rehema.” (Yakobo 2:13a) Haishangazi kwamba wale “wasio na rehema” wanaorodheshwa kati ya watu ambao Mungu anaona kuwa “wanastahili kifo”!—Waroma 1:31, 32.

20 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7) Maneno hayo yanaonyesha kwa mkazo kama nini kwamba wale wanaotafuta rehema ya Mungu wanapaswa wao wenyewe kuwa wenye rehema! Habari inayofuata itazungumzia jinsi tunavyoweza kuonyesha rehema katika maisha yetu ya kila siku.

Umejifunza Nini?

• Rehema ni nini?

• Rehema inaonyeshwa katika njia gani?

• Yehova ni Mungu wa rehema na haki katika njia gani?

• Kwa nini tunapaswa kuwa wenye rehema?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Hisia nyororo za Yehova kwa wale walio katika uhitaji ni kama za mama kumwelekea mtoto wake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunajifunza nini kuhusu rehema kutokana na miujiza ya Yesu?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, Yehova alivunja haki yake kwa kumwonyesha Daudi rehema?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Rehema ya Mungu kuwaelekea wanadamu wenye dhambi inapatana na haki yake