Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kumsaidia Mtoto Wako Ampende Mungu Kutoka Moyoni

Jinsi Unavyoweza Kumsaidia Mtoto Wako Ampende Mungu Kutoka Moyoni

Jinsi Unavyoweza Kumsaidia Mtoto Wako Ampende Mungu Kutoka Moyoni

LEO, ni vigumu sana mtu kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu. (Zaburi 16:8) Kulingana na unabii, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watu wengi ‘wanapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Timotheo 3:1-5) Ndiyo, si rahisi kupata watu wanaompenda Mungu kikweli katika ulimwengu wa leo.

Hatuwezi kutazamia kwamba mtoto atampenda Mungu kutoka moyoni tusipofanya jitihada zozote. Ni lazima tuwasaidie watoto wetu kumpenda Yehova Mungu kutoka moyoni. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Mazungumzo ya Kutoka Moyoni

Tunaweza kuwasaidia watoto wetu kumpenda Mungu kutoka moyoni ikiwa moyo wetu wenyewe umejaa upendo kumwelekea Mungu. (Luka 6:40) Biblia inataja hilo inaposema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako.”—Kumbukumbu la Torati 6:4-7.

Tunaweza jinsi gani kumsaidia mtoto wetu ampende Mungu kutoka moyoni? Kwanza, ni lazima tutambue yale yaliyo katika moyo wa mtoto wetu. Pili, ni lazima tufunue yale yaliyo katika moyo wetu wenyewe.

Yesu Kristo alipokuwa njiani kwenda Emau pamoja na wanafunzi wake wawili, kwanza aliwatia moyo waeleze matumaini yao na mambo yaliyowahangaisha. Baada tu ya kuwasikiliza kwa muda fulani ndipo Yesu aliporekebisha maoni yao kwa kuwafafanulia Maandiko. Baadaye walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi?” Huo ni mfano mzuri wa mazungumzo ya kutoka moyoni. (Luka 24:15-32) Tunaweza kutambua namna gani hisia za mtoto wetu?

Hivi karibuni, wazazi fulani ambao watoto wao wamekuwa watu wazima au wanakaribia kuwa watu wazima na ambao ni mifano mizuri kutanikoni waliombwa waeleze kuhusu mazungumzo ya kutoka moyoni. Kwa mfano, Glen kutoka Mexico ana watoto wanne ambao ni watu wazima. * Anasema hivi: “Mazungumzo ya kustarehesha kati ya wazazi na watoto hayatokei bila jitihada zozote. Mimi na mke wangu tuliweka kando mambo yasiyo ya maana sana ili tutumie wakati zaidi pamoja na watoto. Walipokuwa matineja, nyakati nyingine tulikaa nao jioni yote, tukizungumzia mambo yoyote waliyokuwa wakifikiria. Pia, wakati wa chakula tulisikiliza mazungumzo yao na hivyo kutambua matatizo waliyokuwa nayo na kurekebisha kwa upole mwelekeo usiofaa, mara nyingi bila wao kutambua.”

Mazungumzo ya kutoka moyoni yanatia ndani pia kufunua yale yaliyo katika moyo wetu wenyewe. Yesu alisema hivi: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, . . . kwa maana kutokana na wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Toshiki, ambaye ana watoto watatu ambao ni wahudumu wa wakati wote huko Japan, anasema: “Mara nyingi nilikuwa nikiwaambia kwa nini nilimwamini Yehova, jinsi nilivyokuja kuamini kwa moyo wangu wote kwamba yeye yupo, na jinsi ambavyo hali yangu mwenyewe imenisadikisha kwamba Biblia ni ya kweli na ndio mwongozo bora maishani.” Huko Mexico, Cindy anasema hivi: “Mume wangu alisali sikuzote pamoja na watoto. Waliposikia maneno yake ya kutoka moyoni, walijua kwamba Yehova hakuwa mtu wa kuwaziwa tu.”

Mfano Wetu Una Uvutano Wenye Nguvu

Mwenendo wetu una uvutano wenye nguvu zaidi kuliko maneno, kwa kuwa unawaonyesha watoto wetu jinsi tunavyompenda Mungu. Kwa kuona utii wa Yesu Kristo kumwelekea Yehova, watu wangeweza kutambua kina cha upendo wake kumwelekea Mungu. Yesu alisema hivi: “Kusudi ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, kama vile Baba amenipa amri kufanya, ndivyo ninavyofanya.”—Yohana 14:31.

Gareth, ambaye ni Shahidi wa Yehova huko Wales, anasema hivi: “Ni lazima watoto wetu waone kwamba tunampenda Yehova na kwamba tunajitahidi kufanya mambo kwa njia yake. Kwa mfano, watoto wangu wanaona kwamba ninatii yale ambayo Mungu anatuambia kwa kuwa ninakubali makosa yangu. Sasa watoto wangu wanajitahidi kufanya vivyo hivyo.”

Greg, kutoka Australia anasema hivi: “Tulitaka watoto wetu waone kwamba jambo muhimu zaidi katika maisha yetu ni kufuata kweli. Tunapofanya maamuzi kuhusu kazi au michezo, kwanza tunachunguza matokeo yake kwa wajibu wetu wa kiroho. Tunafurahi kuona kwamba binti yetu mwenye umri wa miaka 19 ameiga mtazamo huo katika utumishi wake wa upainia msaidizi.”

Kuwasaidia Watoto Wetu Wamwelewe Mungu

Hatuwezi kumpenda au kumwamini mtu ambaye hatumwelewi. Mtume Paulo alipotaka Wakristo wa Filipi wampende Yehova zaidi, aliandika hivi: “Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na utambuzi kamili.” (Wafilipi 1:9) Falconerio, ambaye anawalea watoto wanne huko Peru, anasema hivi: “Kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja nao kunajenga imani yao. Nyakati nyingine nilipuuza kujifunza nao, na niliona upendo wao kwa Mungu ukidhoofika.” Gary, kutoka Australia anasema: “Kwa kawaida ninawaonyesha watoto wangu uthibitisho wa kwamba unabii wa Biblia unatimizwa. Pia, ninawaeleza faida za kufuata kanuni za Biblia. Funzo la Biblia la kawaida la familia yetu limesaidia sana kujenga imani yao.”

Ujuzi utaingia katika moyo wa mtoto vizuri zaidi katika mazingira yenye kustarehesha lakini yenye heshima ambayo yanamfanya mtu afurahie kujifunza. (Yakobo 3:18) “Wakati wa funzo la Biblia la familia, tulijaribu kutowakaripia watoto wetu kwa hasira, hata walipokuwa watukutu kidogo,” anasema Shawn na Pauline kutoka Uingereza, ambao wana watoto wanne. “Tuliongoza funzo kwa njia mbalimbali. Nyakati nyingi tuliwaomba watoto wachague habari ya kujifunza. Tulitumia video ambazo zimetayarishwa na tengenezo la Yehova. Nyakati nyingine tulirudia kuona sehemu fulani au tuliisimamisha video ili tuweze kuizungumzia.” Pia huko Uingereza, mama mmoja anayeitwa Kim anasema hivi: “Ninatayarisha funzo la familia kwa uangalifu sana ili niweze kuuliza maswali ambayo yatawafanya watoto wangu wafikiri. Tunafurahia kujifunza. Tunacheka sana.”

Kuchagua Marafiki

Watoto wetu watampenda Yehova na kuthamini ibada ya kweli ikiwa watashirikiana na watu ambao ni marafiki wa Mungu. Ni lazima tujitahidi ili tufaulu kupata marafiki ambao wanaweza kucheza na kuzungumza mambo yenye kujenga pamoja na watoto wetu. Lakini kuna faida za kufanya hivyo. Kwa kuongezea, kuna faida za kupanga ili watoto wetu wakutane na Mashahidi wa Yehova ambao huduma ya wakati wote ni kazi yao ya maisha. Wengi ambao walichagua maisha hayo walifanya hivyo kwa sababu ya kushirikiana na watumishi wenye bidii wa Mungu. Dada mmoja ambaye alikuja kuwa mmishonari anasema hivi: “Mara nyingi wazazi wangu waliwaalika mapainia kwa ajili ya chakula. Bila shaka, walifurahia sana huduma yao hivi kwamba nikataka kumtumikia Mungu kwa njia hiyohiyo.”

Bila shaka, mitazamo ya watoto wetu inaweza kuelekezwa kwa njia nzuri au mbaya. Kwa hiyo, ustadi wetu tukiwa wazazi unajaribiwa na hatari za mashirika mabaya. (1 Wakorintho 15:33) Ustadi unahitajiwa ili kuwafundisha watoto jinsi ya kuepuka kushirikiana na wale ambao hawampendi Yehova wala hawamjui. (Methali 13:20) Shawn, aliyetajwa mapema, anasema hivi: “Tuliwafundisha watoto wetu kuwa na mahusiano mazuri na wanashule wenzao lakini kutoendeleza mahusiano hayo nje ya shule. Watoto wetu walielewa kwa nini hawakupaswa kushiriki katika utendaji wa baada ya shule au katika mashindano ya michezo shuleni.”

Umuhimu wa Kuwazoeza

Tunapowazoeza watoto wetu kueleza imani yao, tunawasaidia kufurahia kuonyesha kwamba wanampenda Mungu. Mark anayeishi Marekani anasema hivi: “Tulitaka watoto wetu wa kiume wahisi kwamba wangeweza kufurahia kuwaelezea wengine kuhusu imani yao wakati wowote, si wakati tu wanaposhiriki rasmi katika mahubiri yetu ya hadharani. Kwa hiyo, tunapoenda mahali fulani kwa ajili ya tafrija, kama vile katika bustani, kwenye ufuo, au katika msitu, tunabeba Biblia na vichapo vya Biblia, na tunazungumza na watu walio huko kuhusu imani yetu. Watoto wetu wanafurahia sana kuhubiri isivyo rasmi pamoja nasi katika njia hiyo. Wanashiriki katika mazungumzo na kueleza kuhusu imani yao.”

Mtume Yohana aliyezeeka aliwasaidia watu wengi wakue katika upendo wao kwa Mungu. Aliandika hivi kuwahusu: “Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu [wa kiroho] wanaendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Tukiwasaidia watoto wetu wampende Mungu kutoka moyoni, bila shaka tutakuwa na shangwe kama hiyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mazungumzo ya kutoka moyoni kuhusu mambo ya imani hayatokei kimuujiza tu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazoeze watoto wako kuonyesha kwamba wanampenda Mungu

[Hisani]

Courtesy of Green Chimneys Farm