Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uovu Unaendelea

Kwa Nini Uovu Unaendelea

Kwa Nini Uovu Unaendelea

“YEHOVA [MUNGU] ni mwadilifu katika njia zake zote,” inasema Biblia. (Zaburi 145:17; Ufunuo 15:3) Nabii Musa alisema hivi kumhusu: “Kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Andiko la Yakobo 5:11 linasema: “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” Mungu hasababishi wala hawezi kusababisha uovu.

Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Yehova Mungu hawezi kamwe kutumia uovu kuwajaribu watu wala hawashawishi watende mambo maovu. Basi, ni nani anayepaswa kulaumiwa kwa sababu ya uovu na mateso yanayosababishwa na uovu huo?

Ni Nani Anayepaswa Kulaumiwa?

Yakobo, mwandikaji wa Biblia anawalaumu kwa kiasi fulani wanadamu kwa sababu ya uovu uliopo. Anasema: “Lakini kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Watu mmoja-mmoja wanaweza kutenda kupatana na tamaa zao zisizofaa. Fikiria pia dhambi ambayo wanadamu wamerithi. Nguvu za dhambi zinaweza kufanya tamaa zisizofaa ziongezeke na kuleta matokeo mabaya sana. (Waroma 7:21-23) Kwa kweli, dhambi ambayo wanadamu wamerithi ‘imetawala kama mfalme’ juu yao, na imewafanya kuwa watumwa wa matendo maovu ambayo yanasababisha mateso mabaya sana. (Waroma 5:21) Kwa kuongezea, watu waovu wanaweza kuwafanya wengine wawe wapotovu.—Methali 1:10-16.

Hata hivyo, chanzo kikuu cha uovu ni Shetani Ibilisi. Alileta uovu ulimwenguni. Yesu Kristo alimwita Shetani “yule mwovu” na “mtawala wa ulimwengu,” yaani, jamii ya wanadamu wasio waadilifu. Kwa ujumla, wanadamu wanamtii Shetani anapowashawishi wapuuze njia nzuri za Yehova Mungu. (Mathayo 6:13; Yohana 14:30; 1 Yohana 2:15-17) Andiko la 1 Yohana 5:19 linasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Kwa kweli, Shetani na malaika wake ‘wanaipotosha dunia nzima inayokaliwa,’ na kusababisha tu “ole.” (Ufunuo 12:9, 12) Hivyo, yule hasa anayepaswa kulaumiwa kwa sababu ya uovu uliopo ni Shetani Ibilisi.

Andiko la Mhubiri 9:11 linafunua jambo lingine linalosababisha maumivu au mateso. Linasema hivi: ‘Wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’ Yesu Kristo alizungumza kuhusu msiba fulani uliotukia wakati watu 18 walipokufa baada ya kuangukiwa na mnara. (Luka 13:4) Walikufa kwa sababu walikuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa. Mambo kama hayo yanatukia leo. Kwa mfano, tofali linaweza kutoka kwenye jengo refu na kumwangukia mpita-njia. Je, Mungu ndiye anayepaswa kulaumiwa? Hapana. Ni tukio lisilopangiwa na lisilotazamiwa. Mara nyingi, inakuwa vivyo hivyo wakati ugonjwa unapoikumba familia fulani au kifo cha ghafula kinapoacha watu wakiwa mayatima na wajane.

Hivyo basi, ni wazi kwamba Mungu hasababishi uovu wala mateso. Kinyume chake, Yehova anakusudia kuondoa kabisa uovu na wale wanaosababisha uovu. (Methali 2:22) Kwa kweli, atafanya mengi zaidi ya hayo. Maandiko yanatangaza kwamba kusudi la Mungu kupitia Kristo ni ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Wakati huo, mfumo wa sasa wa mambo, uliojaa pupa, chuki, na matendo maovu, hautakuwapo tena. Mungu hata “atafuta kila chozi kutoka katika macho” yote, na hivyo kukomesha kabisa mateso. (Ufunuo 21:4) Lakini huenda ukauliza: ‘Kwa nini Mungu hajafanya hivyo? Kwa nini ameruhusu uovu na mateso yaendelee mpaka leo?’ Masimulizi ya Biblia kuhusu Adamu na Hawa yanajibu maswali hayo.

Suala Muhimu Linatokezwa

Sababu inayomfanya Mungu aruhusu uovu uendelee mpaka leo inahusiana na jambo lililotukia mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Jambo hilo lilitokeza suala muhimu kuhusu Muumba mwenyewe, suala ambalo halingeweza kusuluhishwa haraka au kwa urahisi. Acheni tuchunguze kwa undani yale yaliyotukia.

Yehova Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza wakiwa wakamilifu na akawaweka katika Paradiso. Walipewa zawadi ambayo iliwafanya wawe tofauti na wanyama, zawadi ya uhuru wa kuchagua. (Mwanzo 1:28; 2:15, 19) Wakiwa viumbe wenye uhuru wa kuchagua, Adamu na Hawa wangeweza kutumia uwezo wao wa akili kuchagua kumpenda, kumtumikia, na kumtii Muumba wao. Au wangeweza kuchagua kutomtegemea Mungu na kuamua kimakusudi kutomtii.

Ili kumpa Adamu na Hawa nafasi ya kuonyesha kwamba walimpenda, Mungu wa kweli aliwakataza kufanya jambo moja. Alimwamuru Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Ili kuendelea kuwa na kibali cha Mungu, kwa faida yao wenyewe na faida ya familia ambayo wangepata baadaye, Adamu na Hawa hawakupaswa kula matunda ya mti huo mmoja. Je, wangetii?

Biblia inatuambia kile kilichotukia. Shetani Ibilisi alimfikia Hawa na kumwambia hivi kupitia nyoka: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa aliporudia kutaja amri ya Mungu, Shetani akamwambia hivi: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Basi, Hawa akaona mti huo kuwa wenye kutamanika hivi kwamba “akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala.” Masimulizi hayo yanaendelea hivi: “Baadaye akampa mume wake pia alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.” (Mwanzo 3:1-6) Kwa hiyo, Adamu na Hawa walitumia vibaya uhuru wao wa kuchagua nao wakatenda dhambi kwa kutomtii Mungu.

Je, unaona uzito wa yale yaliyotukia? Ibilisi alipinga yale ambayo Mungu alikuwa amemwambia Adamu. Maneno ya Shetani yalimaanisha kwamba Adamu na Hawa hawangemhitaji Yehova awaamulie yaliyo mema na yaliyo mabaya. Kwa hiyo, suala ambalo Shetani alitokeza lilitilia shaka haki na uhalali wa utawala wa Yehova juu ya mwanadamu. Basi, suala muhimu sana ambalo Shetani alitokeza lilihusu haki ya Yehova ya kuwa mwenye enzi kuu. Mungu wa kweli alijibu suala hilo jinsi gani?

Wakati wa Kutosha Ulihitajiwa

Yehova alikuwa na nguvu za kuwaharibu waasi hao watatu, yaani, Shetani, Adamu, na Hawa. Bila shaka, Mungu alikuwa mwenye nguvu kuliko wao. Lakini Shetani hakutilia shaka nguvu za Mungu. Badala yake, alitilia shaka haki ya Yehova ya kutawala. Suala hilo lilihusu viumbe wote wenye uhuru wa kuchagua. Walihitaji kuelewa kwamba ni lazima zawadi ya uhuru wa kuchagua itumiwe vizuri, kulingana na mipaka ya miongozo ya kimwili, kiadili, na kiroho iliyowekwa na Mungu. Kama sivyo, wangepata madhara, kama vile tu mtu anayepuuza sheria ya uvutano na kuruka kutoka kwenye paa la jengo refu atakavyoumia vibaya. (Wagalatia 6:7, 8) Viumbe wote wenye akili wangefaidika kwa kujionea wenyewe matokeo mabaya ya kuchagua kutomtegemea Mungu. Jambo hilo lilihitaji wakati.

Mfano unaofuata unaweza kutusaidia kuelewa kwa nini masuala fulani yanahitaji wakati ili yatatuliwe: Tuseme kwamba baba wa familia fulani anataka kushindana na baba wa familia nyingine ili ijulikane ni nani aliye na nguvu zaidi. Suala hilo linaweza kutatuliwa haraka sana. Nguvu zao zinaweza kupimwa kwa kuinua mawe mazito. Baba anayeinua jiwe zito zaidi ndiye mwenye nguvu zaidi. Lakini tuseme kwamba tunataka kujua ni baba gani anayewapenda kikweli wana na mabinti wake na iwapo wanampenda pia. Au namna gani ikiwa tunataka kujua ni baba gani anayesimamia familia yake kwa njia nzuri zaidi. Kupima nguvu au kusema maneno matupu tu hakungetosha. Wakati wa kutosha na uchunguzi wa makini sana ungehitajiwa, na kauli zinazofaa zingehitaji kukatwa ili suala hilo litatuliwe.

Mambo Ambayo Kupita kwa Wakati Kumeonyesha

Miaka 6,000 hivi imepita tangu Shetani alipotilia shaka haki ya Mungu ya kutawala. Historia imefunua nini? Fikiria madai mawili ya Shetani kumhusu Mungu. Shetani alimwambia Hawa kwa ujasiri hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4) Kwa kusema kwamba Adamu na Hawa hawangekufa ikiwa wangekula tunda lililokatazwa, kwa kweli, Shetani alikuwa akimwita Yehova mwongo. Hilo ni shtaka zito sana! Ikiwa Mungu hakusema kweli katika jambo hilo, angeweza jinsi gani kuaminiwa katika jambo lingine lolote? Hata hivyo, wakati umeonyesha nini?

Adamu na Hawa walipata magonjwa, maumivu, walizeeka, na mwishowe wakafa. Biblia inasema hivi: “Siku zote ambazo Adamu aliishi zikajumlika kuwa miaka 930, naye akafa.” (Mwanzo 3:19; 5:5) Wanadamu wote wamerithi matokeo hayo yenye kuhuzunisha kutoka kwa Adamu. (Waroma 5:12) Kupita kwa wakati kumethibitisha kwamba Shetani ni “mwongo na ndiye baba ya uwongo” na kumeonyesha kwamba Yehova ni “Mungu wa ukweli.”—Yohana 8:44; Zaburi 31:5.

Shetani alimwambia Hawa hivi pia: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake [mti uliokatazwa] macho yenu [ya Hawa na Adamu] yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:5) Kwa maneno hayo ya ujanja, Shetani aliwadanganya wanadamu kwamba wanaweza kujiongoza. Kwa udanganyifu, Shetani alidokeza kwamba wanadamu wangekuwa na maisha mazuri bila kumtegemea Mungu. Je, hilo limethibitika kuwa kweli?

Katika historia yote, milki mbalimbali zimetokea na kutoweka. Wanadamu wamejaribu serikali za kila aina. Hata hivyo, familia ya wanadamu imekumbwa tena na tena na mambo yenye kuogopesha. Kwa hekima, mwandishi mmoja wa Biblia alikata kauli hii miaka 3,000 hivi iliyopita: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Nabii Yeremia aliandika hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Hata maendeleo ya kisayansi na ya kiteknolojia ya miaka ya karibuni hayajapinga ukweli wa maneno hayo. Kupita kwa wakati kumethibitisha tu kwamba maneno hayo ni ya kweli.

Utafanya Nini?

Wakati ambao Mungu ameruhusu upite umethibitisha kwamba dai la Shetani kuhusu suala la haki ya enzi kuu ya Yehova ni la uwongo. Yehova Mungu ndiye mwenye haki kamili ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Ana haki ya kutawala viumbe wake, na njia yake ya kutawala ndiyo bora. Viumbe wa mbinguni ambao wameishi chini ya utawala wa Mungu wanakiri jambo hilo kwa kutangaza hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

Unaunga mkono upande gani wa suala la utawala wa Mungu? Je, unakubali kwamba Mungu anastahili kukutawala? Ikiwa unakubali, ni lazima utambue enzi kuu ya Yehova. Unaweza kufanya hivyo kwa kufuata kweli na mashauri mazuri ajabu yaliyo katika Neno lake, Biblia, katika kila sehemu ya maisha yako. “Mungu ni upendo,” naye anawawekea viumbe wake sheria na amri kwa sababu anawapenda. (1 Yohana 4:8) Yehova hamnyimi yeyote kati yetu jambo lenye faida. Kwa hiyo, unaweza kufuata himizo hili la Biblia: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaweza kuchagua utawala wa Mungu kwa kujifunza Biblia na kufuata mafundisho yake maishani mwako

[Picha katika ukurasa wa 4]

© Jeroen Oerlemans/Panos Pictures