Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maandishi Yaliyopotea ya John Milton

Maandishi Yaliyopotea ya John Milton

Maandishi Yaliyopotea ya John Milton

NI VIGUMU kumpata mwandishi ambaye alikuwa na uvutano mkubwa sana katika ulimwengu kama John Milton, mtungaji wa shairi maarufu la Kiingereza linaloitwa Paradiso Iliyopotezwa (Paradise Lost). Mwandishi mmoja wa masimulizi ya maisha anasema kwamba Milton “alipendwa na watu wengi, alichukiwa na wengine, lakini alipuuzwa na wachache.” Utamaduni na vitabu vya Kiingereza vinavyotumika hata leo vinategemea sana maandishi yake.

John Milton alianza kuwa na uvutano huo jinsi gani? Kwa nini maandishi yake ya mwisho yanayoitwa Kuhusu Mafundisho ya Kikristo (On Christian Doctrine) yalitokeza ubishi sana hivi kwamba yakakaa kwa muda wa miaka 150 bila kuchapishwa?

Maisha Yake ya Mapema

John Milton alizaliwa mwaka wa 1608 katika familia yenye utajiri iliyoishi huko London. Milton alikumbuka hivi: “Baba yangu alinitayarisha tangu utotoni kujifunza mashairi. Kuanzia umri wa miaka 12 na kuendelea, kwa kawaida sikwenda kulala kabla ya saa sita usiku kwa sababu nilipenda sana kujifunza.” Alifanya vizuri sana katika masomo akapata digrii ya pili katika Chuo Kikuu cha Cambridge mwaka wa 1632. Baada ya hapo, aliendelea kusoma vitabu vya historia na vitabu vya zamani kutoka Ugiriki na Roma.

Milton alitaka kuwa mtungaji wa mashairi, lakini kulikuwa na mapambano makali sana ya kuleta mabadiliko nchini Uingereza. Bunge, ambalo liliongozwa hasa na Oliver Cromwell, lilichagua washiriki wa mahakama ambayo iliamua Mfalme Charles wa Kwanza auawe mwaka wa 1649. Akitumia maandishi yake yenye ushawishi, Milton alitetea hatua hiyo na kuwa msemaji wa serikali ya Cromwell. Kwa kweli, kabla ya kuwa mtungaji wa mashairi anayejulikana sana, tayari John Milton alijulikana sana kwa sababu ya trakti alizoandika kuhusu siasa na maadili.

Baada ya utawala wa mfalme kurudishwa, na Charles wa Pili kutawazwa kuwa mfalme mwaka wa 1660, uhai wa Milton ulikuwa hatarini kwa sababu alishirikiana zamani na Cromwell. Milton alijificha, na aliepuka kuuawa kwa msaada tu wa marafiki fulani wenye mamlaka. Ingawa alikabili mambo hayo yote, aliendelea kupendezwa sana na mambo ya kiroho.

“Biblia Kama Kiwango Kinachofaa”

Milton aliandika hivi kuhusu mapendezi yake ya kiroho katika miaka ya mapema: “Nilianza nikiwa mtoto kujifunza kwa bidii Agano la Kale na Agano Jipya katika lugha za awali.” Milton aliona Maandiko Matakatifu kuwa mwongozo pekee wenye kutegemeka katika mambo ya kimaadili na ya kiroho. Lakini alivunjika moyo sana alipochunguza vitabu vya kidini ambavyo vilikubaliwa katika siku hizo. Baadaye aliandika hivi: “Niliamua kwamba haingefaa kutegemea miongozo hiyo kama msingi wa imani yangu au tumaini langu la wokovu.” Akiwa ameazimia kupima imani yake kwa kutumia tu “Biblia kama kiwango kinachofaa,” Milton alianza kuorodhesha maandiko muhimu chini ya vichwa fulani vikuu naye alinukuu maandiko ya Biblia kutokana na orodha hizo.

Leo, John Milton anajulikana sana kwa sababu ya kutunga shairi linaloitwa Paradiso Iliyopotezwa ambalo linasimulia habari ya Biblia kuhusu jinsi mwanadamu alivyopoteza ukamilifu. (Mwanzo, sura ya 3) Shairi hilo hasa ambalo lilichapishwa mwaka wa 1667, ndilo lililomfanya Milton awe mwandishi mashuhuri, hasa katika nchi zilizozungumza Kiingereza. Baadaye, alichapisha shairi la pili lenye kichwa Paradiso Iliyorudishwa (Paradise Regained). Mashairi hayo yanaonyesha kusudi la kwanza la Mungu kwa ajili ya mwanadamu, yaani, kufurahia uhai mkamilifu katika paradiso duniani, na yanataja jinsi Mungu atakavyorudisha Paradiso duniani kupitia Kristo. Kwa mfano, katika shairi la Paradiso Iliyopotezwa, Mikaeli yule malaika mkuu anatabiri wakati ambapo Kristo “atawathawabisha waaminifu Wake, na kuwapa furaha ya milele, iwe mbinguni au duniani, kwa kuwa wakati huo dunia yote itakuwa paradiso, na itakuwa na furaha zaidi kuliko furaha ya Edeni, na maisha yatakuwa yenye furaha zaidi.”

Kuhusu Mafunsisho ya Kikristo

Kwa miaka mingi, Milton alitaka pia kuandika kitabu ambacho kinazungumzia mambo mbalimbali kuhusu maisha na mafundisho ya Kikristo. Ijapokuwa alikuwa amepofuka kabisa kufikia mwaka wa 1652, aliandika kitabu hicho kwa msaada wa waandishi mpaka alipokufa mwaka wa 1674. Milton alikiita kitabu chake hicho cha mwisho Uchanganuzi wa Mafundisho ya Kikristo Unaotegemea Maandiko Matakatifu Peke Yake (A Treatise on Christian Doctrine Compiled From the Holy Scriptures Alone). Aliandika hivi katika utangulizi wa kitabu hicho: “Watungaji wengi wa vitabu ambao wameshughulikia habari hii . . . wameandika maelezo machache tu ya pambizoni kuhusu sura na mistari ya Biblia ambayo ni msingi wa mafundisho yao. Lakini mimi, nimejitahidi kujaza kurasa zangu kabisa na manukuu kutoka katika sehemu zote za Biblia.” Milton alisema ukweli kwa sababu kitabu hicho kinataja au kurejelea Maandiko zaidi ya mara 9,000.

Ingawa hapo zamani Milton hakusitasita kutoa maoni yake, alikataa kuchapisha kitabu hicho. Kwa nini? Kwanza, alijua kwamba maelezo yake ya Kimaandiko yalitofautiana sana na mafundisho yaliyokubaliwa na kanisa. Kwa kuongezea, Mfalme wa Uingereza alipoanza kutawala tena nchi hiyo, Milton hakupendwa tena na serikali. Kwa hiyo, huenda alikuwa akingoja nyakati zenye utulivu zaidi. Kwa vyovyote vile, baada ya kifo cha Milton, mwandishi wake alipeleka hati yake ya Kilatini kwa kampuni fulani ya kuchapisha, lakini ilikataa kuichapisha. Kisha, waziri wa mambo ya nje wa Uingereza aliichukua kwa nguvu hati hiyo na kuiweka. Kitabu hicho cha Milton kiligunduliwa baada ya karne moja na nusu kupita.

Mwaka wa 1823, karani mmoja aligundua hati iliyofunikwa ya mtungaji huyo maarufu wa mashairi. Mfalme George wa Nne ambaye alikuwa akitawala Uingereza wakati huo aliagiza kwamba hati hiyo itafsiriwe kutoka katika lugha ya Kilatini na kusambazwa kwa watu. Hati hiyo ilipochapishwa katika Kiingereza miaka miwili baadaye, ilitokeza ubishi mkali sana miongoni mwa wanadini na waandishi wa vitabu. Askofu mmoja alitangaza papo hapo kwamba hati hiyo ni ya uwongo. Alikataa kuamini kwamba Milton ambaye alionwa na watu wengi kuwa mtungaji bora zaidi wa mashairi ya kidini nchini Uingereza angeweza kukataa kabisa mafundisho ambayo yalionwa na kanisa kuwa matakatifu. Huku akitambua kimbele kwamba ubishi ungetokea na ili kuthibitisha kwamba Milton ndiye mtungaji, mtafsiri wa kitabu hicho aliandika katika chapa hiyo maelezo ya chini yakitaja mambo 500 yanayolingana katika kitabu Kuhusu Mafundisho ya Kikristo na shairi Paradiso Iliyopotezwa. *

Mambo Ambayo Milton Aliamini

Kufikia wakati wa Milton, Uingereza ilikuwa imekubali Mabadiliko ya Kiprotestanti na ilikuwa imevunja uhusiano na Kanisa Katoliki. Kwa ujumla, Waprotestanti waliamini kwamba Maandiko Matakatifu ndiyo yaliyokuwa na mamlaka ya kuamua masuala ya imani na maadili wala si papa. Hata hivyo, katika kitabu Kuhusu Mafundisho ya Kikristo, Milton alionyesha kwamba mafundisho na mazoea mengi ya Waprotestanti pia hayakupatana na Maandiko. Akitegemea Biblia, alikataa mafundisho ya Calvin ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine na badala yake akaunga mkono uhuru wa kuchagua. Aliwafundisha watu kulitumia kwa heshima jina la Mungu, Yehova, naye alilitumia sana katika maandishi yake.

Milton alitumia Maandiko kuthibitisha kwamba nafsi ya mwanadamu inaweza kufa. Aliandika hivi kuhusu Mwanzo 2:7: “Mtu alipoumbwa kwa njia hiyo, mwishowe andiko hilo linasema hivi: naye mtu akawa nafsi hai. . . . Mtu hana sehemu mbili au hawezi kugawanywa: si kama vile wengi wanavyofikiri, ya kwamba mtu ameumbwa kutokana na sehemu mbili naye ana vitu viwili vilivyo tofauti kabisa, nafsi na mwili. Kinyume chake, mtu ni nafsi, na nafsi ni mtu.” Basi Milton akauliza swali: “Je, kila sehemu inayofanyiza mtu inakufa, au ni mwili tu unaokufa?” Baada ya kutaja maandiko mbalimbali ya Biblia yanayoonyesha kwamba kila sehemu ya mtu inakufa, aliongeza hivi: “Lakini maelezo yenye kusadikisha kabisa ninayoweza kupata kuhusu kufa kwa nafsi ni maelezo ya Mungu mwenyewe, Ezek[ieli 18:]20: Nafsi inayotenda dhambi hiyo yenyewe itakufa.” Milton pia alitaja maandiko kama vile Luka 20:37 na Yohana 11:25 yanayoonyesha kwamba tumaini la wanadamu waliokufa linategemea ufufuo wa wakati ujao kutoka katika usingizi wa kifo.

Ni nini kilichoanzisha ubishi mkali zaidi kuhusiana na kitabu Kuhusu Mafundisho ya Kikristo? Ni uthibitisho rahisi lakini wenye nguvu wa Milton kwamba Kristo, Mwana wa Mungu, yuko chini ya Mungu, Baba. Baada ya kutaja Yohana 17:3 na Yohana 20:17, Milton anauliza hivi: “Ikiwa Baba ni Mungu wa Kristo na Mungu wetu, na ikiwa kuna Mungu mmoja tu, ni nani anayeweza kuwa Mungu isipokuwa Baba?”

Kwa kuongezea, Milton anasema hivi: “Mwana mwenyewe na mitume wake wanakubali katika kila jambo wanalosema na kuandika kwamba Baba ni mkuu kuliko Mwana katika mambo yote.” (Yohana 14:28) “Kwa kweli ni Kristo anayesema, katika Mathayo 26:39: Ee Baba yangu, ikiwezekana, acha kikombe hiki kipitilie mbali kutoka kwangu; lakini, si kulingana na mapenzi yangu, bali kulingana na mapenzi yako. . . . Kwa nini anasali kwa Baba peke yake, badala ya kusali kwake mwenyewe, ikiwa yeye mwenyewe ni Mungu kikweli? Ikiwa yeye ni mwanadamu na Mungu mkuu, mbona anasali afanyiwe jambo ambalo yeye mwenyewe anaweza kufanya? . . . Kama vile Mwana anavyomheshimu na kumwabudu Baba peke yake kila mahali, anatufundisha tufanye vivyo hivyo.”

Udhaifu wa Milton

John Milton alitafuta kweli. Hata hivyo, bado alikuwa na udhaifu wa kibinadamu, na huenda baadhi ya maoni yake yalitegemea mambo mabaya yaliyompata. Kwa mfano, mara tu baada ya kuoa, mke wake ambaye alikuwa binti mdogo wa tajiri fulani Mwingereza mwenye mashamba alimwacha na kurudi kwa familia yao kwa miaka mitatu hivi. Wakati huo, Milton aliandika trakti zilizounga mkono talaka kwa sababu ya kutopatana, bali si kwa msingi wa uzinzi tu ambao ndio msingi pekee uliotajwa na Yesu. (Mathayo 19:9) Milton alifundisha wazo hilo katika kitabu Kuhusu Mafundisho ya Kikristo.

Hata ingawa Milton alikuwa na kasoro zake, kitabu hicho kinaonyesha waziwazi maoni ya Biblia kuhusu mafundisho mengi sana muhimu. Kufikia leo, kitabu chake kinawahimiza wasomaji wapime mafundisho yao kwa kiwango kikamilifu cha Maandiko Matakatifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Tafsiri mpya ya kitabu Kuhusu Mafundisho ya Kikristo, iliyochapishwa na Chuo Kikuu cha Yale mwaka wa 1973, inalingana hata zaidi na hati ya kwanza ya Kilatini ya Milton.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Milton alijifunza Biblia kwa makini sana

[Hisani]

Courtesy of The Early Modern Web at Oxford

[Picha katika ukurasa wa 12]

Shairi “Paradiso Iliyopotezwa” lilimfanya Milton awe mtu maarufu

[Hisani]

Courtesy of The Early Modern Web at Oxford

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kitabu cha mwisho cha Milton kilitoweka kwa miaka 150

[Hisani]

Image courtesy of Rare Books and Special Collections, Thomas Cooper Library, University of South Carolina

[Picha katika ukurasa wa 11]

Image courtesy of Rare Books and Special Collections, Thomas Cooper Library, University of South Carolina