Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hosea

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hosea

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hosea

IBADA ya kweli imetokomea katika ufalme wa kaskazini wa makabila kumi ya Israeli. Chini ya utawala wa Yeroboamu wa Pili, nchi ya Israeli inapata ufanisi, lakini ufanisi huo unadidimia anapokufa. Kisha kunakuwa na kipindi cha ghasia na msukosuko wa kisiasa. Wafalme wanne kati ya wafalme sita wanaotawala baada ya Yeroboamu wa Pili wanauawa. (2 Wafalme 14:29; 15:8-30; 17:1-6) Kipindi cha miaka 59 cha kazi ya Hosea ya kutoa unabii kilichoanza mwaka wa 804 K.W.K., kinaendelea mpaka wakati huu wenye msukosuko.

Hisia za Yehova kuelekea taifa lililoasi la Israeli zinaonyeshwa waziwazi na yale yanayotukia katika ndoa ya Hosea. Ujumbe wa Hosea unahusu kufichuliwa kwa dhambi ya Israeli na hukumu ya kinabii juu ya Israeli na ufalme wa Yuda. Hosea ameandika mambo yote hayo katika kitabu kinachoitwa kwa jina lake akitumia maneno yenye fadhili na hisia, na lugha yenye nguvu na iliyo wazi. Ujumbe wake ambao ni sehemu ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho, ni ujumbe ulio hai na wenye nguvu.—Waebrania 4:12.

“JICHUKULIE MKE WA UASHERATI”

(Hosea 1:1–3:5)

Yehova anamwambia Hosea: “Nenda, jichukulie mke wa uasherati.” (Hosea 1:2) Hosea anatii naye anazaa mwana na Gomeri. Kwa wazi, Gomeri anazaa nje ya ndoa watoto wawili wanaofuata. Maana ya majina yao, Lo-ruhama na Lo-ami, inaonyesha kwamba Yehova hatawaonyesha Waisraeli rehema na atawakataa watu wake wasio washikamanifu.

Kwa kweli, Yehova anahisi namna gani kuhusu watu wake ambao wameasi? Anamwambia Hosea hivi: “Nenda tena, mpende mwanamke anayependwa na rafiki yako na ambaye anafanya uzinzi, kama vile Yehova alivyowapenda wana wa Israeli ingawa wanageukia miungu mingine.”—Hosea 3:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:1—Kwa nini Hosea anawataja wafalme wote wanne waliotawala Yuda wakati wa huduma yake lakini anataja mfalme mmoja tu wa Israeli? Ni kwa sababu wafalme wa familia ya Daudi tu ndio waliotambuliwa kuwa watawala halali wa watu wa Mungu waliochaguliwa. Wafalme wa ufalme wa Yuda walikuwa wa ukoo wa Daudi, lakini wale wa ufalme wa kaskazini hawakuwa wa ukoo huo.

1:2-9—Je, ni kweli kwamba Hosea alioa mke wa uasherati? Ndiyo, kwa kweli Hosea alioa mwanamke ambaye baadaye alikuwa mzinzi. Nabii huyo hasemi chochote kuonyesha kwamba yale aliyoandika kuhusu maisha ya familia yake yalikuwa ndoto au maono.

1:7—Nyumba ya Yuda ilionyeshwa rehema na kuokolewa wakati gani? Hilo lilitukia mwaka wa 732 K.W.K., katika siku za Mfalme Hezekia. Wakati huo, Yehova alikomesha tishio la Waashuru juu ya Yerusalemu alipomtuma malaika aue askari-jeshi 185,000 wa maadui usiku mmoja tu. (2 Wafalme 19:34, 35) Kwa hiyo, Yehova aliokoa nyumba ya Yuda, si “kwa upinde wala kwa upanga wala kwa vita, wala kwa farasi wala kwa wapanda-farasi,” bali kwa malaika.

1:10, 11—Tangu kuanguka kwa ufalme wa kaskazini wa Israeli katika mwaka wa 740 K.W.K., wana wa Israeli ‘walikusanywa pamoja katika umoja’ na wana wa Yuda jinsi gani? Wengi kutoka ufalme wa kaskazini walienda Yuda kabla wenyeji wa nchi ya Yuda hawajapelekwa utekwani huko Babiloni mwaka wa 607 K.W.K. (2 Mambo ya Nyakati 11:13-17; 30:6-12, 18-20, 25) Mateka Wayahudi waliporudi katika nchi yao mnamo 537 K.W.K., watu kutoka ufalme wa kaskazini wa Israeli walikuwa miongoni mwao.—Ezra 2:70.

2:21-23—Maneno haya ya Yehova yalitabiri nini: “Hakika nitampanda [Yezreeli] duniani kama mbegu kwa ajili yangu, nami nitamwonyesha rehema”? Jina la mwana wa kwanza wa Hosea na Gomeri lilikuwa Yezreeli. (Hosea 1:2-4) Jina hilo linalomaanisha “Mungu Atapanda Mbegu,” ni unabii wa kuonyesha jinsi Yehova angewakusanya mabaki waaminifu mwaka wa 537 K.W.K. na kuwapanda kama mbegu katika nchi ya Yuda. Nchi iliyokuwa ukiwa kwa miaka 70 sasa ingehitaji kutoa nafaka, divai tamu, na mafuta. Kwa lugha ya kishairi, unabii huo unasema kwamba mambo hayo mazuri yangeisihi dunia itoe chakula, nayo dunia ingeiomba mbingu mvua. Nazo mbingu zingemwomba Mungu alete mawingu ya mvua. Mambo hayo yote yangefanywa kwa kusudi la kutosheleza mahitaji ya mabaki waliokuwa wakirudi. Mtume Paulo na Petro walitumia Hosea 2:23 kuhusiana na kukusanywa kwa mabaki ya Israeli wa kiroho.—Waroma 9:25, 26; 1 Petro 2:10.

Mambo Tunayojifunza:

1:2-9; 3:1, 2Hebu fikiria jinsi Hosea alivyojidhabihu kwa kubaki katika ndoa kupatana na mapenzi ya Mungu! Inapohusu kufanya mapenzi ya Mungu, tunadhabihu mapendezi yetu kadiri gani?

1:6-9. Yehova anachukia uzinzi wa kiroho kama anavyochukia uzinzi wa kimwili.

1:7, 10, 11; 2:14-23. Kile ambacho Yehova alitabiri kuhusu Israeli na Yuda kilitimia. Sikuzote Neno la Yehova linatimia.

2:16, 19, 21-23; 3:1-4. Yehova yuko tayari kuwasamehe wote wanaoonyesha toba kutoka moyoni. (Nehemia 9:17) Kama Yehova, sisi pia tunapaswa kuwa wenye huruma na rehema tunaposhughulika na wengine.

“YEHOVA ANA KESI”

(Hosea 4:1–13:16)

“Yehova ana kesi na wakaaji wa nchi.” Kwa nini? Kwa sababu “hakuna kweli wala fadhili zenye upendo wala kumjua Mungu katika nchi.” (Hosea 4:1) Waisraeli walioasi wamewapunja watu, wamemwaga damu, na kufanya uasherati wa kimwili na wa kiroho. Badala ya kumwomba Mungu awasaidie, “wameita Misri; wameenda Ashuru.”—Hosea 7:11.

Yehova anatangaza hukumu yake, akisema: “Israeli watamezwa.” (Hosea 8:8) Ufalme wa Yuda pia una hatia. “Yehova ana kesi na Yuda,” Hosea 12:2 linasema, “kumtoza Yakobo hesabu kulingana na njia zake; atamlipa kulingana na matendo yake.” Lakini bila shaka watarudishwa, kwa kuwa Mungu anaahidi hivi: “Nitawakomboa wao kutoka katika mkono wa Kaburi; nitawaokoa wao kutoka kwenye kifo.”—Hosea 13:14.

Maswali ya Kimaandilo Yajibiwa:

6:1-3—Ni nani aliyekuwa akisema: “Njooni, turudi kwa Yehova”? Labda Waisraeli wasio waaminifu walikuwa wakitiana moyo wamrudie Yehova. Ikiwa ndivyo ilivyo, walikuwa tu wakijifanya kwamba wanatubu. Fadhili zao zenye upendo zilitoweka haraka kama “mawingu ya asubuhi na . . . umande ambao hutoweka mapema.” (Hosea 6:4) Kwa upande mwingine, huenda Hosea ndiye aliyesema maneno hayo akiwasihi watu wamrudie Yehova. Kwa vyovyote vile, wenyeji walioasi wa ufalme wa makabila kumi ya Israeli walihitaji kuonyesha toba ya kweli na kumrudia Yehova kikweli.

7:4—Waisraeli wazinzi walikuwa kama ‘tanuru ambalo limewashwa’ katika njia gani? Ulinganisho huo unaonyesha jinsi tamaa za uovu zilivyokuwa zimetia mizizi moyoni mwao.

Mambo Tunayojifunza:

4:1, 6Tukitaka kuendelea kuwa na kibali cha Yehova, ni lazima tuendelee kujifunza kumhusu na kuishi kupatana na yale tunayojifunza.

4:9-13. Yehova atawahukumu wale wanaozoea mwenendo mchafu kingono na wale wanaofuatia ibada isiyo safi.—Hosea 1:4.

5:1. Wale wanaoongoza kati ya watu wa Mungu wanapaswa kukataa kabisa uasi-imani. Wasipofanya hivyo, wanaweza kuwashawishi wengine wajihusishe katika ibada ya uwongo, na hivyo kuwa ‘mtego na wavu’ kwao.

6:1-4; 7:14, 16. Toba ya maneno tu ni ya unafiki na ya ubatili. Ili mtenda-dhambi apate rehema ya Mungu, lazima aonyeshe toba kutoka moyoni, inayoonyeshwa kwa kurudia “ibada ya kweli” iliyoinuliwa. Matendo yake yanapaswa kupatana na viwango vya juu vya Mungu.—Hosea 7:16.

6:6. Kuzoea dhambi kunaonyesha kwamba mtu hana upendo mshikamanifu kumwelekea Mungu. Hakuna dhabihu za kiroho zinazoweza kulipia kasoro hiyo.

8:7, 13; 10:13. Ile kanuni inayosema “lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia” ilithibitika kuwa ya kweli katika kisa cha Waisraeli walioabudu sanamu.—Wagalatia 6:7.

8:8; 9:17; 13:16. Unabii kuhusu ufalme wa kaskazini ulitimia wakati jiji lake kuu, Samaria, lilipochukuliwa na Ashuru. (2 Wafalme 17:3-6) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatenda yale anayosema na kutimiza yale aliyonena.—Hesabu 23:19.

8:14. Yehova alipeleka ‘moto katika majiji yote ya Yuda’ mnamo 607 K.W.K. kupitia mkono wa Wababiloni, na hivyo akaleta ukiwa uliotabiriwa juu ya Yerusalemu na nchi ya Yuda. (2 Mambo ya Nyakati 36:19) Neno la Mungu haliwezi kamwe kukosa kutimia.—Joshua 23:14.

9:10. Ingawa walikuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu wa kweli, Waisraeli “waliingia kwa Baali wa Peori, nao wakajiweka wakfu kwa kitu kile cha aibu.” Tunatenda kwa hekima tunapokubali kuonywa kutokana na kielelezo chao kibaya na kujilinda tusivunje wakfu wetu kwa Yehova.—1 Wakorintho 10:11.

10:1, 2, 12. Tunapaswa kumwabudu Mungu kwa moyo usio na unafiki. ‘Tunapojipandia mbegu kwa uadilifu, tunavuna kulingana na fadhili zenye upendo za Mungu.’

10:5. Beth-aveni (linalomaanisha “Nyumba ya Madhara”) ni jina la dharau la Betheli (linalomaanisha “Nyumba ya Mungu”). Sanamu ya ndama ya Beth-aveni ilipopelekwa uhamishoni, wakaaji wa Samaria waliomboleza kwa sababu ya kupoteza kitu ambacho walikuwa wakitumikia. Ni jambo la upumbavu kama nini kutegemea sanamu isiyo na uhai na ambayo hata haiwezi kujilinda yenyewe!—Zaburi 135:15-18; Yeremia 10:3-5.

11:1-4. Nyakati zote Yehova anawatendea watu wake kwa upendo. Kujitiisha chini ya Mungu si jambo lenye kukandamiza hata kidogo.

11:8-11; 13:14. Neno la Yehova kuhusu kurudishwa kwa watu wake kwenye ibada ya kweli ‘halikurudi kwake bila matokeo.’ (Isaya 55:11) Kipindi cha uhamisho huko Babiloni kilimalizika mwaka wa 537 K.W.K., na mabaki wakarudi Yerusalemu. (Ezra 2:1; 3:1-3) Jambo lolote ambalo Yehova amesema kupitia manabii wake litatimia hakika.

12:6. Tunapaswa kuazimia kabisa kuonyesha fadhili zenye upendo, kutenda haki, na kumtumaini Yehova sikuzote.

13:6. Waisraeli ‘walishiba, kisha moyo wao ukaanza kujiinua. Ndiyo sababu walimsahau Yehova.’ Tunahitaji kujihadhari ili tusiwe na mwelekeo wowote wa kujiinua.

“NJIA ZA YEHOVA ZIMENYOOKA”

(Hosea 14:1-9)

Hosea anasihi hivi: “Ee Israeli, rudi kwa Yehova Mungu wako, kwa maana umejikwaa katika kosa lako.” Anawahimiza watu wamwambie Yehova hivi: “Samehe kosa letu; na ukubali lililo jema, nasi tutatoa ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu.”—Hosea 14:1, 2.

Mkosaji anayetubu anapaswa kumrudia Yehova, kukubali njia zake, na kumtolea dhabihu za sifa. Kwa nini? Kwa sababu “njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo.” (Hosea 14:9) Tunashangilia kama nini kwamba bado wengi “watakuja kwa Yehova na kwa wema wake wakitetemeka katika siku za mwisho”!—Hosea 3:5.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Maisha ya familia ya Hosea yalionyesha jinsi Yehova alivyokuwa akishughulika na Waisraeli

[Picha katika ukurasa wa 17]

Samaria lilipoanguka mwaka wa 740 K.W.K., ufalme wa makabila kumi ya Israeli ulikoma