Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yonathani “Alifanya Kazi na Mungu”

Yonathani “Alifanya Kazi na Mungu”

Yonathani “Alifanya Kazi na Mungu”

MWANA wa mfalme wa kwanza wa Israeli anamtembelea mkimbizi mafichoni. “Usiogope,” anamwambia mkimbizi huyo, “kwa kuwa mkono wa Sauli baba yangu hautakupata, na wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.”—1 Samweli 23:17.

Mwana huyo ni Yonathani, naye mkimbizi ni Daudi. Ikiwa Yonathani hangekufa muda mfupi baadaye, inawezekana kwamba angemtegemeza Daudi kabisa.

Urafiki wa Yonathani na Daudi ulikuwa wa ajabu. Kwa kweli, Yonathani alikuwa mtu wa pekee sana. Wenzake walimwona hivyo pia, kwa kuwa walisema hivi kumhusu: “Alifanya kazi na Mungu.” (1 Samweli 14:45) Kwa nini walisema hivyo? Yonathani alikuwa na sifa gani? Masimulizi ya maisha yake yanakuhusu jinsi gani?

Waisraeli Wako “Katika Shida Kali”

Biblia inapomtaja Yonathani mara ya kwanza, Waisraeli wako “katika shida kali.” Wafilisti walikuwa wamepora nchi yao na kuwazuia wasijilinde.—1 Samweli 13:5, 6, 17-19.

Hata hivyo, Yehova alisema kwamba hangewaacha watu wake, na Yonathani alisadiki maneno hayo. Mungu alikuwa amesema hivi kumhusu Sauli baba yake: “Atawaokoa watu wangu kutoka mkononi mwa Wafilisti.” Yonathani aliamini kabisa maneno hayo. Yeye mwenyewe alikuwa ameongoza Waisraeli 1,000 wenye silaha duni na kuwashinda Wafilisti. Sasa alitaka kumaliza kabisa tishio la Wafilisti.—1 Samweli 9:16; 12:22; 13:2, 3, 22.

Kuvamia kwa Ujasiri

Yonathani alilenga kituo cha Wafilisti kilichokuwa karibu na kipito cha mfereji cha Mikmashi. (1 Samweli 13:23) Ili kukifikia, alihitaji kupanda kwa “mikono yake na miguu yake.” Hilo halikumvunja moyo. Yonathani aliamua kushambulia akiwa na mchukua-silaha wake tu na akamwambia hivi: “Labda Yehova atatenda kwa ajili yetu, kwa maana hakuna kizuizi chochote kwa Yehova kuokoa kwamba ni kwa wengi au ni kwa wachache.”—1 Samweli 14:6, 13.

Waisraeli hao wawili walitafuta ishara kutoka kwa Yehova. Wangejionyesha kwa wanaume waliokuwa kituoni. Ikiwa Wafilisti wangesema: “Simameni tuli mpaka tukutane nanyi!” Yonathani na mchukua-silaha wake hawangewaendea. Lakini ikiwa wangesema: “Njooni juu yetu!” hilo lingemaanisha kwamba Yehova angempa ushindi Yonathani na mchukua-silaha wake. Ikiwa Yonathani alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemtegemeza, alikusudia kupanda kituoni apigane.—1 Samweli 14:8-10.

Je, wanaume wawili tu wangeshinda askari-jeshi wa kituo kizima? Je, Yehova hakumsaidia Mwamuzi Ehudi alipowaongoza Waisraeli kupigana na Moabu? Je, Mungu hakuwa pamoja na Shamgari na kumsaidia kuwapiga na kuwaua Wafilisti 600 kwa mchokoo wa ng’ombe? Na je, Yehova hakumpa Samsoni nguvu za kuwashinda Wafilisti akiwa peke yake? Yonathani alikuwa na uhakika kwamba Mungu angemsaidia pia.—Waamuzi 3:12-31; 15:6-8, 15; 16:29, 30.

Walipowaona Waisraeli hao wawili, Wafilisti walipaaza sauti hivi: “Njooni hapa juu tulipo, na sisi tutawaonyesha jambo fulani!” Yonathani na mchukua-silaha wake wakapanda. Wakashambulia kwa ujasiri na kuwaua askari–jeshi 20 wa maadui, na kusababisha wasiwasi mwingi na mvurugo kituoni. Huenda Wafilisti walidhani kwamba mashujaa wengi Waisraeli walikuwa wakiwafuata wale mashujaa wawili wa kwanza. Baada ya tukio hilo, masimulizi yanasema, ‘tetemeko likatokea katikati ya watu wote wa kile kituo, na dunia ikaanza kutetemeka, nalo likawa ni tetemeko kutoka kwa Mungu.’ Kwa sababu ya tetemeko hilo kutoka kwa Mungu, machafuko yalienea katika kambi ya Wafilisti hivi kwamba ‘upanga wa kila mmoja ukainuka juu ya mtu na mwenzake.’ Askari-jeshi Waisraeli walipoona hayo, wakapata ujasiri. Wakiungwa mkono na Waisraeli waliokuwa wamejificha na wale waliokuwa wamejiunga na Wafilisti, “wakaendelea kuwapiga Wafilisti kutoka Mikmashi mpaka Aiyaloni.”—1 Samweli 14:11-23, 31.

Watu Wanamkomboa Yonathani

Bila hekima, Mfalme Sauli alikuwa ameweka laana juu ya askari-jeshi yeyote ambaye angekula kabla ya ushindi kupatikana. Kwa sababu fulani, Yonathani hakujua jambo hilo. Yonathani alikula. Alichovya fimbo yake ndani ya sega la asali na kula asali kidogo. Inaonekana kwamba, hilo lilimfanya awe na nguvu mpya ya kupigana mpaka mwisho.—1 Samweli 14:24-27.

Alipojua kwamba Yonathani alikuwa amekula, Sauli aliamuru Yonathani afe. Yonathani hakuogopa kufa. “Mimi hapa! Na nife!” akasema. “Lakini watu wakamwambia Sauli: ‘Je, Yonathani afe, ambaye ametimiza wokovu huu mkubwa katika Israeli? Ni jambo lisilowaziwa! Kama anavyoishi Yehova, hakuna hata unywele mmoja wa kichwa chake utakaoanguka chini; kwa maana alifanya kazi na Mungu leo.’ Hivyo watu wakamkomboa Yonathani, naye hakufa.”—1 Samweli 14:38-45.

Mtumishi wa Mungu hahitaji kupigana katika vita halisi leo, lakini huenda kukawa na pindi fulani katika maisha unapohitaji imani na ujasiri. Inaweza kuwa vigumu kufanya yaliyo sawa huku wenzako wakifanya yasiyo sawa. Hata hivyo, Yehova ataimarisha na kubariki tamaa yako ya kushikamana na viwango vyake vya uadilifu. Huenda ukahitaji ujasiri ili kukubali pendeleo fulani la utumishi katika tengenezo la Yehova, kama vile kupanua utumishi wako, kukubali pendeleo jipya, au kuhama ili kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme. Huenda ukajiuliza ikiwa kwa kweli unastahili kupata pendeleo hilo. Hata hivyo, uwe na uhakika kwamba unafanya jambo jema unapojitoa ili Yehova akutumie katika njia anayoona inafaa. Mkumbuke Yonathani! “Alifanya kazi na Mungu.”

Yonathani na Daudi

Miaka 20 hivi baadaye, Goliathi, shujaa Mfilisti alidhihaki jeshi la Waisraeli, lakini Daudi akamuua. Ingawa Yonathani alimzidi Daudi umri kwa miaka 30, wanaume hao wawili walilingana sana. * Ujasiri ambao Yonathani alionyesha huko Mikmashi ulionyeshwa pia na Daudi. Ulinganisho mkubwa zaidi kati yao ni kwamba, Daudi alikuwa na imani ileile katika nguvu za Yehova za kuokoa, imani iliyomwezesha kupambana na Goliathi bila woga wakati Waisraeli wengine wote walipojikunyata kwa woga. Kwa sababu hiyo, “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi, na Yonathani akaanza kumpenda kama nafsi yake mwenyewe.”—1 Samweli 17:1–18:4.

Ujasiri wa Daudi ulimfanya Mfalme Sauli amwone kuwa mpinzani, hata hivyo, Yonathani hakumwonea Daudi wivu hata kidogo. Yonathani na Daudi walikuja kuwa marafiki wakubwa sana, na inaelekea kwamba kupitia mazungumzo yao ya siri, Yonathani alipata kujua kuwa Daudi alikuwa ametiwa mafuta awe mfalme wa Israeli ambaye angefuata. Yonathani aliheshimu uamuzi wa Mungu.

Mfalme Sauli alipozungumza na mwana wake na watumishi wake kuhusu kumuua Daudi, Yonathani alimwonya Daudi. Yonathani alimsadikisha Sauli kwamba hakuwa na sababu ya kumwogopa Daudi. Daudi hakuwa amemtendea mfalme dhambi hata kidogo! Je, Daudi hakuhatarisha uhai wake kwa kumkabili Goliathi? Ombi la kutoka moyoni la Yonathani kwa ajili ya rafiki yake aliyekuwa amekosewa lilimtuliza Sauli. Hata hivyo, muda si muda mfalme alipanga tena njama ya kumuua Daudi naye alijaribu tena na tena kumuua, na hivyo Daudi akalazimika kukimbia.—1 Samweli 19:1-18.

Yonathani alimuunga Daudi mkono kwa ushikamanifu. Marafiki hao wawili walikutana ili kupanga watakalofanya. Akiwa mshikamanifu kwa rafiki yake, huku akijitahidi kuwa mshikamanifu kwa baba yake, Yonathani alimwambia Daudi hivi: “Ni jambo lisilowaziwa! Hutakufa.” Hata hivyo, Daudi akamwambia Yonathani: “Kuna kama hatua moja tu kati yangu na kifo!”—1 Samweli 20:1-3.

Yonathani na Daudi walipanga jinsi ya kujaribu nia ya Sauli. Ikiwa ingegunduliwa kwamba Daudi hayupo mezani pa mfalme, Yonathani angemwambia baba yake kwamba Daudi aliomba ruhusa ya kutokuwepo ili aende akashiriki kutoa dhabihu kwa ajili ya familia. Iwapo Sauli angekasirika, hiyo ingekuwa ishara ya kwamba alikusudia kumuumiza Daudi. Yonathani alimbariki Daudi na kwa njia isiyo ya moja kwa moja akamkubali kuwa mfalme atakayefuata, akisema hivi: “Yehova na awe pamoja nawe, kama vile alivyokuwa pamoja na baba yangu.” Marafiki hao wawili waliapa kuwa washikamanifu kwa mmoja na mwenzake na wakaamua jinsi ambavyo Yonathani angemjulisha Daudi kuhusu matokeo ya mpango wao.—1 Samweli 20:5-24.

Sauli alipogundua kwamba Daudi hayupo, Yonathani alieleza kwamba Daudi alikuwa amemsihi hivi: “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, acha niende kisirisiri, ili niwaone ndugu zangu.” Yonathani hakuogopa kusema kwamba Daudi alipata kibali chake. Mfalme alikasirika sana! Alimtukana Yonathani na kufoka kwamba Daudi angemzuia mwanawe asiwe mfalme baada yake. Sauli alimwamuru Yonathani amlete Daudi kwake ili auawe. Yonathani akajibu hivi: “Kwa nini auawe? Amefanya nini?” Kwa hasira, Sauli akamrushia mkuki mwana wake. Yonathani aliponyoka bila jeraha lakini aliumizwa sana moyoni kuhusiana na Daudi.—1 Samweli 20:25-34.

Yonathani alionyesha ushikamanifu kama nini! Kwa maoni ya wanadamu, urafiki wake na Daudi haungemfaidi sana, badala yake ungemletea hasara kubwa sana. Lakini, Yehova alikuwa ameagiza Daudi awe mfalme baada ya Sauli, na kusudi la Mungu lingemfaidi Yonathani na watu wengine pia.

Kuagana kwa Machozi

Yonathani alikutana na Daudi kisiri ili kumpasha habari. Ilikuwa wazi kwamba Daudi hangeweza tena kuingia kwenye makao ya Sauli. Wanaume hao wawili walilia na kukumbatiana. Kisha Daudi akakimbia mafichoni.—1 Samweli 20:35-42.

Yonathani alikutana na mkimbizi huyo kwa mara ya mwisho, Daudi alipomkimbia Sauli na kujificha “katika nyika ya Zifu kule Horeshi.” Huo ndio wakati Yonathani alimtia moyo Daudi kwa maneno haya: “Usiogope; kwa kuwa mkono wa Sauli baba yangu hautakupata, na wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako; na Sauli baba yangu pia anajua jambo hilo.” (1 Samweli 23:15-18) Muda mfupi baadaye, Yonathani na Sauli wakafa katika vita walipokuwa wakipigana na Wafilisti.—1 Samweli 31:1-4.

Wote wanaompenda Mungu wanapaswa kutafakari mwenendo wa Yonathani. Je, unahitaji kuwa mshikamanifu kwa pande mbili tofauti? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba Sauli alimhimiza Yonathani afuatie faida zake mwenyewe. Hata hivyo, Yonathani alimheshimu Yehova na akajitiisha kwake kutoka moyoni na kushangilia kwamba Mungu alikuwa amemchagua mfalme wa Israeli ambaye angefuata. Ndiyo, Yonathani alimuunga Daudi mkono, naye alikuwa mshikamanifu kwa Yehova.

Yonathani alikuwa na sifa zenye kuvutia. Iga sifa hizo! Kisha watu watasema hivi kukuhusu sawa na walivyosema kumhusu Yonathani: “Alifanya kazi na Mungu.”—1 Samweli 14:45.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Yonathani alikuwa na miaka 20 hivi alipotajwa mara ya kwanza akiwa kiongozi wa kijeshi mwanzoni mwa utawala wa miaka 40 wa Sauli. (Hesabu 1:3; 1 Samweli 13:2) Hivyo, haikosi kwamba Yonathani alikuwa akikaribia miaka 60 alipokufa karibu mwaka wa 1078 K.W.K. Kwa kuwa wakati huo Daudi alikuwa na umri wa miaka 30, ni wazi kwamba Yonathani alimzidi Daudi umri kwa miaka 30 hivi.—1 Samweli 31:2; 2 Samweli 5:4.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Yonathani hakumwonea Daudi wivu