Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani

Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani

Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani

“Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah.”—ZABURI 150:6.

1. Eleza jinsi kijana mmoja alivyotafuta kusudi maishani.

“NILISOMEA udaktari kwa sababu nilitaka kutumia maisha yangu kuwasaidia watu. Pia, nilifikiri kwamba umashuhuri na pesa nyingi ambazo ningepata nikiwa daktari zingeniletea furaha,” anakumbuka Seung Jin, ambaye alilelewa huko Korea. * “Nilivunjika moyo nilipotambua kwamba daktari anaweza kuwasaidia watu kwa kadiri ndogo sana. Kisha niliamua kufuatia kazi ya usanii, lakini jitihada zangu hazikuwafaidi wengine sana, nami nilijiona kuwa mwenye ubinafsi tu. Halafu nikaamua kuwa mwalimu lakini muda si muda niligundua kwamba nilikuwa nikiwapa wengine ujuzi tu wala si mwongozo ambao ungewaletea furaha ya kweli.” Kama watu wengi wanavyofanya, Seung Jin alikuwa akitafuta kusudi lenye maana maishani.

2. (a) Kuwa na kusudi maishani kunamaanisha nini? (b) Tunajua jinsi gani kwamba Muumba alituweka duniani akiwa na kusudi?

2 Kuwa na kusudi la kweli maishani kunamaanisha kuwa na sababu ya kuishi, lengo lililo wazi, kuwa na mradi ambao tunajitahidi kufikia. Je, kweli wanadamu wanaweza kuwa na kusudi kama hilo? Ndiyo! Uhakika wa kwamba tumeumbwa tukiwa na akili, dhamiri, na uwezo wa kufikiri unaonyesha kwamba Muumba alituweka duniani akiwa na kusudi fulani zuri. Hivyo basi, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba tunaweza kupata na kutimiza kusudi la kweli la maisha kwa kuishi tu kupatana na kusudi la Muumba.

3. Kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu linatia ndani nini?

3 Biblia inafunua kwamba kusudi la Mungu kwa ajili yetu linatia ndani mambo mengi. Kwa mfano, tuliumbwa kwa njia nzuri na hilo linaonyesha kwamba kwa kweli Mungu ana upendo usio wa kichoyo. (Zaburi 40:5; 139:14) Kwa hiyo, kuishi kupatana na kusudi la Mungu kunamaanisha kuwapenda wengine bila uchoyo kama Mungu anavyowapenda. (1 Yohana 4:7-11) Kunamaanisha pia kutii maagizo ya Mungu ambayo yanatusaidia kuishi kupatana na kusudi lake lenye upendo.—Mhubiri 12:13; 1 Yohana 5:3.

4. (a) Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa na kusudi la kweli maishani? (b) Ni kusudi gani bora kabisa ambalo mtu yeyote anaweza kufuatia?

4 Pia, Mungu alikusudia kwamba wanadamu waishi pamoja kwa furaha na amani na kuishi hivyo pia na uumbaji mwingine wote. (Mwanzo 1:26; 2:15) Hata hivyo, tunahitaji kufanya nini ili tuwe na furaha, usalama, na amani ya akili? Kama mtoto ambaye anajihisi akiwa salama na mwenye furaha anapojua kwamba wazazi wake wako karibu, tunahitaji kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Baba yetu wa mbinguni ili tupate kusudi la kweli na lenye maana maishani. (Waebrania 12:9) Mungu anatuwezesha kuwa na uhusiano kama huo pamoja naye kwa kuturuhusu tumkaribie na kwa kusikiliza sala zetu. (Yakobo 4:8; 1 Yohana 5:14, 15) ‘Tukitembea pamoja na Mungu’ kwa imani na kuwa marafiki wake, tunaweza kumletea Baba yetu wa mbinguni shangwe na sifa. (Mwanzo 6:9; Methali 23:15, 16; Yakobo 2:23) Hilo ndilo kusudi bora kabisa ambalo mtu yeyote anaweza kufuatia. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah.”—Zaburi 150:6.

Una Kusudi Gani Maishani?

5. Kwa nini si jambo la hekima kutanguliza mapendezi ya kimwili?

5 Kusudi la Mungu kwa ajili yetu linatia ndani kujitunza vizuri sisi wenyewe pamoja na familia zetu. Hilo linatia ndani kutimiza mahitaji yetu ya kimwili na ya kiroho. Lakini, tunahitaji kufanya hivyo kwa usawaziko ili mambo ya kimwili tunayopendezwa nayo na mahangaiko yetu yasifunike mambo ya kiroho ambayo ni ya maana zaidi. (Mathayo 4:4; 6:33) Inasikitisha kwamba jambo kuu katika maisha ya watu wengi ni kutafuta vitu vya kimwili. Hata hivyo, si jambo la hekima kujaribu kutosheleza mahitaji yetu yote kwa kutafuta tu vitu vya kimwili. Uchunguzi wa hivi karibuni wa mamilionea huko Asia unafunua kwamba wengi wao “hawajihisi salama na wanahangaika, hata ingawa wamekuwa maarufu na wametimiza mengi kwa sababu ya utajiri wao.”—Mhubiri 5:11.

6. Yesu alitoa shauri gani kuhusu kufuatia utajiri?

6 Yesu alizungumza kuhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Utajiri unadanganya kwa njia gani? Unamfanya mtu aonekane kuwa na furaha, ijapokuwa hana furaha. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha.” (Mhubiri 5:10) Lakini je, mtu anaweza kufuatia miradi ya kimwili na wakati uleule amtumikie Mungu kwa nafsi yake yote? Bila shaka hawezi. Yesu alieleza hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” Yesu aliwahimiza wafuasi wake wajiwekee “hazina mbinguni,” wala si vitu vya kimwili duniani, yaani, wajifanyie jina zuri pamoja na Mungu, ambaye ‘anajua ni vitu gani wanavyohitaji hata kabla hawajamwomba.’—Mathayo 6:8, 19-25.

7. Tunaweza jinsi gani ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli’?

7 Mtume Paulo alitoa shauri zito kuhusu jambo hilo alipomwandikia Timotheo, mfanyakazi mwenzake. Alimwambia Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri . . . waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie . . . , wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.”—1 Timotheo 6:17-19.

“Uzima Ulio wa Kweli” Ni Nini?

8. (a) Kwa nini watu wengi wanajitahidi kutafuta utajiri na umaarufu? (b) Watu hao hawatambui nini?

8 Watu wengi wanafikiri kwamba maneno “uzima ulio wa kweli” yanamaanisha maisha ya raha na starehe. Gazeti moja la Asia linasema hivi: “Wale wanaotazama sinema au televisheni wanaanza kutamani yale wanayoona na kuota kuhusu vitu ambavyo wanaweza kuwa navyo.” Wengi wanafanya kutafuta utajiri na umaarufu kuwe kusudi kuu maishani mwao. Wengi wanapoteza maisha yao ya ujana, wanaacha kufuatia viwango vya kiroho, na afya yao na maisha yao ya familia yanaharibika kwa sababu ya kufuatia vitu hivyo. Ni watu wachache sana wanaotambua kwamba maisha ya raha na starehe yanayotangazwa na vyombo vya habari yanaonyesha tu “roho ya ulimwengu,” yaani, njia ya kufikiri ambayo ina uvutano juu ya mabilioni ya watu duniani na ambayo inawasukuma watende kinyume cha kusudi la Mungu kwa ajili yetu. (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2) Haishangazi kwamba kuna watu wengi sana ambao hawana furaha leo!—Methali 18:11; 23:4, 5.

9. Wanadamu hawawezi kutimiza nini, na kwa nini?

9 Namna gani wale wanaojitahidi sana kuwasaidia wengine bila uchoyo, kumaliza njaa, magonjwa, na ukosefu wa haki? Kwa kawaida, jitihada zao nzuri na za kujitolea zinawafaidi watu wengi. Lakini, hata wakijitahidi kadiri gani, hawawezi kamwe kubadili mfumo huu wa mambo uwe mzuri na wenye haki. Kwa nini? Kwa sababu ukweli ni kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani, naye hataki ubadilike.—1 Yohana 5:19.

10. Watu waaminifu watapata “uzima ulio wa kweli” wakati gani?

10 Inahuzunisha sana mtu kuweka tumaini lake lote katika ulimwengu huu! Paulo aliandika hivi: “Ikiwa ni katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi kati ya watu wote.” Watu wengi wanaoamini kwamba maisha ndiyo haya tu, wana mtazamo huu: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:19, 32) Lakini kuna ahadi ya wakati ujao, yaani, ‘mbingu mpya na dunia mpya, ambazo tunangojea kulingana na ahadi ya Mungu, na humo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:13) Wakati huo, Wakristo watafurahia “uzima ulio wa kweli,” yaani, “uzima wa milele” kwa ukamilifu, ama mbinguni au chini ya utawala wenye upendo wa serikali ya Ufalme wa Mungu!—1 Timotheo 6:12.

11. Kwa nini kujitahidi kuendeleza mambo ya Ufalme wa Mungu ni jambo lenye kusudi?

11 Ufalme wa Mungu tu ndio utakaosuluhisha kabisa matatizo ya wanadamu. Kwa hiyo, kujitahidi kuendeleza mambo ya Ufalme wa Mungu ndilo jambo lenye kusudi zaidi ambalo mtu anaweza kufuatia. (Yohana 4:34) Tunaposhiriki katika kazi hiyo, tunakuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Pia, tunafurahia kutumika pamoja na mamilioni ya ndugu na dada zetu wa kiroho ambao wanafuatia kusudi kama letu maishani.

Kujidhabihu kwa Njia Inayofaa

12. Eleza tofauti iliyopo kati ya maisha katika mfumo wa sasa na “uzima ulio wa kweli.”

12 Biblia inasema kwamba ulimwengu huu “unapitilia mbali na pia tamaa yake.” Kila sehemu ya ulimwengu wa Shetani itaharibiwa, kutia ndani umaarufu na utajiri wake, “lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Tofauti na utajiri usio hakika, utukufu wa muda, na raha zisizoridhisha za mfumo huu, “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele chini ya Ufalme wa Mungu, utadumu na tunapaswa kujidhabihu kwa ajili yake, maadamu tunajidhabihu kwa njia inayofaa.

13. Mume na mke fulani walijidhabihu kwa njia gani inayofaa?

13 Wafikirie Henry na Suzanne. Wanaamini kabisa ahadi ya Mungu ya kwamba atawasaidia wote wanaotanguliza Ufalme maishani mwao. (Mathayo 6:33) Kwa hivyo, badala ya wote wawili kufanya kazi ya kuajiriwa, waliamua kuishi katika nyumba ya hali ya chini ili wawe na wakati zaidi wa kufuatia mambo ya kiroho pamoja na mabinti wao wawili. (Waebrania 13:15, 16) Rafiki yao mmoja mwenye nia nzuri hakuelewa kwa nini waliamua hivyo. Alimwambia Suzanne hivi: “Mpendwa, ikiwa unataka kuishi katika nyumba nzuri zaidi, ni lazima ujinyime kitu fulani.” Hata hivyo, Henry na Suzanne walijua kwamba kumtanguliza Yehova ‘kuna ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.’ (1 Timotheo 4:8; Tito 2:12) Mabinti wao walikuja kuwa waeneza-injili wenye bidii sana. Wakiwa familia wanahisi kwamba hawakukosa kitu chochote; badala yake walifaidika sana kwa kufanya mradi wa kufuatia “uzima ulio wa kweli” uwe kusudi lao.—Wafilipi 3:8; 1 Timotheo 6:6-8.

‘Usiutumie Ulimwengu kwa Ukamili’

14. Kuacha kukazia fikira kusudi la kweli kunaweza kuongoza kwenye misiba gani?

14 Hata hivyo, kuna hatari kubwa tukiacha kukazia fikira kusudi la kweli na kuacha kushika imara “uzima ulio wa kweli.” Tunakabili hatari ya “kuchukuliwa na mahangaiko na utajiri na raha za maisha haya.” (Luka 8:14) Tamaa zisizozuiwa na pia “mahangaiko ya maisha” yanaweza kutufanya tujihusishe kupita kiasi katika mfumo huu wa mambo. (Luka 21:34) Inahuzunisha kwamba watu fulani wamenaswa na tamaa inayoenea sasa ya kuwa matajiri na “wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi,” hata wamepoteza uhusiano wao wenye thamani pamoja na Yehova. Wamepata hasara kubwa kama nini kwa sababu ya ‘kutoshika imara uzima wa milele!’—1 Timotheo 6:9, 10, 12; Methali 28:20.

15. Familia moja ilipata faida gani kwa sababu ya ‘kutoutumia ulimwengu kwa ukamili’?

15 Paulo aliwashauri “wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili.” (1 Wakorintho 7:31) Keith na Bonnie walitii shauri hilo. Keith anasema hivi: “Niliamua kuwa Shahidi wa Yehova nilipokuwa nikikamilisha masomo yangu katika chuo cha udaktari wa meno. Nilihitaji kufanya uamuzi. Ningeweza kuwatibu wagonjwa wengi na kupata pesa nyingi, lakini kufanya hivyo kungeharibu hali yetu ya kiroho. Niliamua kutibu wagonjwa wachache ili nipate wakati zaidi wa kushughulikia mahitaji ya kiroho na ya kihisia ya familia yangu ambayo baadaye ilikuwa na mabinti watano. Ingawa mara nyingi hatukuwa na pesa nyingi, tulijifunza kupunguza gharama, na sikuzote tulikuwa na vitu tulivyohitaji. Familia yetu ilikuwa na uhusiano wa karibu, wenye uchangamfu, na ilikuwa yenye furaha sana. Mwishowe, sisi sote tuliingia katika huduma ya wakati wote. Sasa mabinti wetu wana ndoa zenye furaha, na watatu kati yao wana watoto. Familia zao pia zina furaha zinapoendelea kutanguliza kusudi la Yehova maishani.”

Kutanguliza Kusudi la Mungu Maishani Mwako

16, 17. Biblia inataja mifano gani ya watu ambao walikuwa na vipawa, na kwa nini wanakumbukwa?

16 Biblia inataja mifano ya watu ambao waliishi kupatana na kusudi la Mungu na wale ambao hawakufanya hivyo. Mambo tunayojifunza kutokana na mifano hiyo yanawafaa watu wa kila umri, utamaduni, na hali. (Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:6, 11) Nimrodi alijenga majiji makubwa, lakini alifanya hivyo kwa kumpinga Yehova. (Mwanzo 10:8, 9) Hata hivyo, watu wengine wengi waliweka mifano mizuri. Kwa mfano, Musa hakufanya kusudi lake maishani liwe kudumisha cheo chake akiwa Mmisri mwenye kuheshimiwa. Badala yake, alithamini sana mapendeleo yake ya kiroho na kuyaona “kuwa ni utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri.” (Waebrania 11:26) Inaelekea kwamba daktari Luka alimsaidia Paulo na wengine katika magonjwa yao. Lakini Luka aliwafaidi wengine sana kwa kuwa mweneza-injili na mwandikaji wa Biblia. Naye Paulo, hakujulikani kuwa mtaalamu wa Sheria, bali mmishonari, “mtume kwa mataifa.”—Waroma 11:13.

17 Daudi anakumbukwa hasa kwa sababu ya kuwa ‘mtu aliyekubalika kwa moyo wa Mungu,’ wala si kama kiongozi wa jeshi au mwimbaji na mtungaji wa muziki. (1 Samweli 13:14) Tunamjua Danieli kwa sababu ya utumishi wake akiwa nabii mshikamanifu wa Yehova wala si ofisa wa serikali ya Babiloni; tunamkumbuka Esta kwa sababu ya mfano wake wa ujasiri na imani wala si kwa sababu alikuwa malkia wa Uajemi; tunawakumbuka Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana kama mitume wa Yesu wala si wavuvi hodari. Na mwishowe, tunamkumbuka Yesu akiwa “Kristo” wala si “seremala.” (Marko 6:3; Mathayo 16:16) Wote hao walielewa wazi kwamba hata iwe walikuwa na vipawa, mali, au cheo gani, walipaswa kutanguliza utumishi wa Mungu maishani mwao wala si kazi za kimwili. Walijua kwamba kusudi bora zaidi na lenye kuthawabisha zaidi ambalo wangeweza kuwa nalo ni kuwa wanaume au wanawake wanaomwogopa Mungu.

18. Kijana mmoja Mkristo aliamua kutumia maisha yake kwa njia gani, na mwishowe alitambua nini?

18 Mwishowe Seung Jin, aliyetajwa mwanzoni, alielewa jambo hilo pia. Anasema hivi: “Badala ya kutumia nguvu zangu zote katika udaktari, usanii, au ualimu, niliazimia kutumia maisha yangu kupatana na wakfu wangu kwa Mungu. Sasa ninatumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa walimu wa Biblia, nikiwasaidia watu watembee katika njia ya uzima wa milele. Mwanzoni nilifikiri kwamba huduma ya wakati wote haisisimui sana. Sasa maisha yangu yanasisimua sana kuliko wakati mwingine wowote kadiri ninavyojitahidi kuboresha utu wangu na uwezo wangu wa kuwafundisha watu wenye utamaduni mbalimbali. Ninaona kwamba kufanya kusudi la Yehova liwe kusudi letu ndiyo njia pekee ya maisha yenye maana.”

19. Tunaweza kupata jinsi gani kusudi la kweli maishani?

19 Tukiwa Wakristo, tumebarikiwa kuwa na ujuzi wenye kuokoa uhai na tumepata tumaini la wokovu. (Yohana 17:3) Basi acheni ‘tusipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha tukose kusudi lake.’ (2 Wakorintho 6:1) Badala yake, acheni tutumie siku zetu na miaka yetu ambayo ni yenye thamani kumsifu Yehova. Acheni tueneze ujuzi unaoleta furaha ya kweli sasa na unaoongoza kwenye uzima wa milele. Tukifanya hivyo, tutaona maneno haya ya Yesu yakitimia katika maisha yetu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Na tutapata kusudi la kweli maishani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni kusudi gani bora kabisa ambalo tunaweza kuwa nalo maishani?

• Kwa nini si jambo la hekima kufuatia vitu vya kimwili maishani?

• “Uzima ulio wa kweli” ambao Mungu anaahidi ni nini?

• Tunaweza kutumia maisha yetu jinsi gani kwa ajili ya kusudi la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo wanahitaji kujidhabihu kwa njia inayofaa