Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maamuzi Ambayo Yanaongoza Kwenye Furaha

Maamuzi Ambayo Yanaongoza Kwenye Furaha

Maamuzi Ambayo Yanaongoza Kwenye Furaha

“LAITI ningefanya uamuzi tofauti!” Umejiambia hivyo mara nyingi kadiri gani? Sote tungependa kufanya maamuzi ambayo hayatatufanya tujute, hasa ikiwa maamuzi hayo yana uvutano juu ya maisha yetu. Hata hivyo, tunaweza jinsi gani kufanya maamuzi yatakayoongoza kwenye furaha?

Kwanza, tunahitaji kuwa na viwango vyenye kutegemeka kabisa. Je, kuna viwango kama hivyo? Watu wengi hawafikiri hivyo. Kulingana na uchunguzi uliofanywa nchini Marekani, asilimia 75 ya wanafunzi wanaokaribia kumaliza masomo yao ya chuo wanaamini kwamba hakuna kiwango cha mema na mabaya na kwamba mema au mabaya yanategemea “viwango vya mtu binafsi na tofauti za kitamaduni.”

Je, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba viwango vya maadili vinategemea tu maoni ya mtu binafsi au maoni yanayopendwa na wengi? Bila shaka hapana. Ikiwa watu wangeruhusiwa kufanya lolote watakalo, kungekuwa na mvurugo. Ni nani angetaka kuishi mahali ambapo hakuna sheria, mahakama, au polisi? Mbali na hayo, nyakati nyingine maoni yanayopendwa na wengi hayatoi mwongozo unaotegemeka. Huenda tukaamua kufanya jambo tunaloamini kuwa sawa lakini baadaye tukagundua kwamba tulikosea. Kwa kweli, historia nzima ya wanadamu inathibitisha ukweli wa kauli hii ya Biblia: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Hivyo basi, tutamwendea nani ili kupata mwongozo tunapofanya maamuzi kuhusu masuala muhimu maishani?

Mtawala kijana aliyetajwa katika habari iliyotangulia alifanya jambo la hekima kumwendea Yesu. Kama tulivyoona, Yesu alipomjibu alirejelea Sheria ya Mungu. Yesu alitambua kwamba Yehova Mungu ndiye Chanzo kikuu zaidi cha ujuzi na hekima na kwamba Yeye anajua mambo yanayowafaa zaidi viumbe Wake. Hivyo, Yesu alisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Kwa kweli, Neno la Mungu ni chanzo kinachotegemeka cha mwongozo ambao utatusaidia kufanya maamuzi ya hekima maishani. Acha tuchunguze kanuni chache katika Neno la Mungu, kanuni ambazo tukizifuata zitazidisha furaha yetu.

Jinsi Tunavyopaswa Kuwatendea Wengine

Katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alifundisha kanuni ya msingi inayoweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima kuhusu mahusiano yetu na wengine. Alisema hivi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

Watu fulani wametumia taarifa kama hiyo kwa njia isiyofaa: “Usiwatendee wengine mambo ambayo hutaki wakutendee wewe.” Ili kuonyesha tofauti iliyopo kati ya taarifa hizo mbili, fikiria mfano wa Yesu wa Msamaria mwema. Myahudi fulani alipigwa na kuachwa kando ya barabara akiwa karibu kufa. Kuhani na Mlawi walimwona lakini wakapita kando yake. Kwa sababu hawakufanya chochote ili kumuumiza zaidi Myahudi huyo, inaweza kusemwa kwamba hawakumtendea jambo ambalo hawakutaka watendewe. Kinyume na hilo, Msamaria aliyekuwa akipita hapo alisimama ili kumsaidia mtu huyo. Alifunga vidonda vyake na kumpeleka kwenye nyumba ya wageni. Alimtendea mtu huyo vile ambavyo yeye angetaka atendewe. Alifuata kanuni ya Yesu, na hivyo, akafanya uamuzi unaofaa.—Luka 10:30-37.

Tunaweza kutumia kanuni hiyo ya mwenendo katika hali nyingi na hivyo kupata furaha. Tuseme familia fulani imehamia kwenye ujirani wenu. Mbona usiwatembelee na kuwakaribisha? Huenda ukawasaidia kufahamiana na eneo hilo jipya, ukajibu baadhi ya maswali yao, na kuwatimizia mahitaji fulani. Ukiwakaribisha kama jirani mwema, utajenga uhusiano mzuri na majirani wako wapya. Pia utapata uradhi kujua kwamba umefanya jambo linalompendeza Mungu. Je, huo si uamuzi wa hekima?

Maamuzi Yanayotegemea Kuwapenda Wengine

Mbali na kanuni ambayo tumetoka kuzungumzia, Yesu alitoa mwelekezo mwingine utakaokusaidia kufanya maamuzi ya hekima. Alipoulizwa ni amri gani iliyo kuu katika Sheria ya Musa, Yesu alijibu hivi: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.”—Mathayo 22:36-40.

Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwapa wanafunzi wake “amri mpya,” kwamba wapendane. (Yohana 13:34) Kwa nini alisema hiyo ni amri mpya? Je, hakuwa amesema kwamba kumpenda jirani ni moja kati ya amri mbili ambazo Sheria yote hutegemea? Chini ya Sheria ya Musa, Waisraeli waliamriwa hivi: “Mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” (Mambo ya Walawi 19:18) Hata hivyo, sasa Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wafanye mengi zaidi. Usiku huohuo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba angetoa uhai wake kwa ajili yao. Kisha akawaambia: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:12, 13) Ndiyo, amri hiyo ilikuwa mpya kwa kuwa ilitaka mtu atangulize faida za wengine.

Tunaweza kuonyesha upendo usio na uchoyo katika njia nyingi, na hivyo kutohangaikia tu mambo yetu wenyewe. Kwa mfano, tuseme unaishi katika jengo moja na wapangaji wengine na unataka kusikiliza muziki kwa sauti inayokusisimua, lakini sauti hiyo inamsumbua jirani yako. Je, ungekubali kujinyima raha ili jirani yako apate utulivu? Kwa maneno mengine je, ungetanguliza mapendezi ya jirani yako?

Fikiria hali nyingine. Asubuhi moja yenye baridi kali na theluji huko Kanada, mwanamume mmoja mzee alitembelewa na Mashahidi wawili wa Yehova. Walipokuwa wakizungumza, mwanamume huyo alisema kwamba alikuwa na ugonjwa wa moyo ambao ulimzuia kuondoa theluji iliyokuwa mbele ya nyumba yake. Saa moja hivi baadaye, alisikia sauti kubwa ya vyombo vya kuondoa theluji. Wale Mashahidi wawili walikuwa wamerudi ili kuondoa theluji kwenye njia na ngazi zilizoelekea kwenye mlango wa mbele wa nyumba yake. “Leo nimejionea upendo wa kweli wa Kikristo ukitenda kazi,” akasema mzee huyo katika barua aliyoandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kanada. “Jambo hilo lilibadili kabisa maoni yangu mabaya kuhusu ulimwengu wa leo. Limenifanya niheshimu hata zaidi kazi mnayofanya ulimwenguni pote.” Ndiyo, kuamua kuwasaidia wengine, hata kwa kadiri ndogo, kunaweza kuwa na matokeo mazuri juu yao. Kufanya maamuzi hayo yanayohusisha kujidhabihu kunaleta furaha kubwa kama nini!

Maamuzi Yanayotegemea Kumpenda Mungu

Jambo lingine tunalopaswa kufikiria tunapofanya maamuzi ni lile ambalo Yesu alisema kuwa ni amri kuu—kwamba tumpende Mungu. Yesu alikuwa akizungumza na Wayahudi waliokuwa taifa lililo wakfu kwa Yehova. Hata hivyo, kila Mwisraeli alipaswa kuamua ikiwa angemtumikia Mungu kwa nafsi yote na kumpenda kwa moyo wote.—Kumbukumbu la Torati 30:15, 16.

Vivyo hivyo, maamuzi unayofanya yanaonyesha jinsi unavyohisi kumwelekea Mungu. Kwa mfano, unapozidi kuelewa na kutambua thamani ya Biblia maishani, wewe pia utahitaji kufanya uamuzi. Je, utakubali kujifunza Biblia hatua kwa hatua, ukiwa na lengo la kuwa mfuasi wa Yesu? Bila shaka, ukichagua kufanya hivyo utapata furaha, kwa kuwa Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Hatujui ikiwa yule mtawala kijana alijuta kwa sababu ya uamuzi wake. Lakini tunajua jinsi mtume Petro alivyohisi baada ya kumfuata Yesu Kristo kwa miaka mingi. Karibu mwaka wa 64 W.K., alipokuwa akikaribia mwisho wa maisha yake, Petro aliwatia moyo waamini wenzake kwa maneno haya: “Fanyeni yote mnayoweza ili mwishowe [Mungu] awapate ninyi mkiwa bila doa na bila dosari na mkiwa katika amani.” (2 Petro 1:14; 3:14) Kwa wazi, Petro hakujuta kwa sababu ya uamuzi aliofanya zaidi ya miaka 30 mapema, naye aliwatia moyo wengine washikamane na uamuzi waliokuwa wamefanya.

Kufuata shauri la Petro kunamaanisha kuamua kukubali wajibu wa kuwa mwanafunzi wa Yesu na kushika amri za Mungu. (Luka 9:23; 1 Yohana 5:3) Huenda hilo likaonekana kuwa jambo gumu, lakini tuna ahadi hii yenye kutia moyo kutoka kwa Yesu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

Fikiria kisa cha Arthur. Akiwa na umri wa miaka kumi, Arthur alianza kujifunza kupiga fidla (violon), akitazamia kuwa mwanamuziki mashuhuri. Alipokuwa na umri wa miaka 14, alikuwa mwanamuziki mashuhuri wa kupiga fidla. Hata hivyo, bado hakuwa na furaha. Nyakati zote baba yake alikuwa na maswali mengi kuhusu kusudi la maisha na aliwaalika walimu wa dini nyumbani; lakini, hakuridhika na majibu yao. Wakiwa familia, walizungumzia ikiwa kweli kuna Mungu na kwa nini ameruhusu uovu. Kisha baba ya Arthur akaanza kuzungumza na Mashahidi wa Yehova. Mazungumzo hayo yalimpendeza sana baba yake Arthur, na familia nzima ikaanza kujifunza Biblia.

Baada ya muda, Arthur akaelewa kutokana na Maandiko kwa nini Mungu anaruhusu mateso na akatambua waziwazi kusudi la maisha. Arthur pamoja na washiriki watatu wa familia yake wakafanya uamuzi ambao hajajuta kamwe kuufanya, yaani, uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova. “Ninafurahi sana kwamba Yehova amenibariki kwa kuniwezesha kujua kweli na kunikomboa kutoka katika ushindani wa wanamuziki. Watu watafanya chochote ili wafanikiwe.”

Bado Arthur anapenda kupiga fidla ili kuwafurahisha marafiki wake, lakini hilo silo jambo kuu maishani mwake. Badala yake, kumtumikia Mungu ndilo jambo kuu maishani mwake. Amekuwa akitumika katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Tofauti na yule mtawala kijana aliyekuwa tajiri, wewe pia unaweza kufanya uamuzi kama wa Arthur na kama wa mamilioni ya watu wengine ambao utakuletea furaha kubwa zaidi, uamuzi wa kukubali mwaliko wa Yesu wa kuwa mfuasi wake.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Uamuzi wako unaweza kuwa na uvutano juu ya maisha ya wengine

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, utajifunza Biblia na kuwa mfuasi wa Yesu?