Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Yakobo alikosea alipojifanya kuwa Esau, kama inavyoonyeshwa kwenye Mwanzo 27:18, 19?

Huenda unajua simulizi hilo. Isaka aliyekuwa amezeeka alimwambia Esau aende kuwinda, akisema hivi: “Acha nile, ili kwamba nafsi yangu ipate kukubariki wewe kabla ya kufa kwangu.” Kwa kuwa Rebeka alisikia yale ambayo mume wake alisema, alitayarisha chakula kitamu naye akamwagiza Yakobo hivi: “Ukilete [chakula] kwa baba yako naye apate kula, ili akubariki wewe kabla ya kifo chake.” Kisha, akiwa amevaa mavazi ya Esau na akiwa na manyoya ya mbuzi wachanga kwenye shingo na mikono yake, Yakobo aliingia ndani kwa baba yake akiwa na chakula kitamu. Isaka alipomuuliza, “Wewe ni nani, mwanangu?” Yakobo alijibu: “Mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza.” Isaka aliamini kwamba huyo alikuwa Esau naye akambariki.—Mwanzo 27:1-29.

Biblia haielezi kwa undani kwa nini Rebeka na Yakobo walitenda hivyo, lakini inaonyesha kwamba hali iliyowakabili ilitokea ghafula. Tunapaswa kukumbuka kwamba Neno la Mungu halitetei wala kulaumu yale ambayo Rebeka na Yakobo walifanya. Hivyo, simulizi hilo halituwekei kielelezo cha kusema uwongo au kutenda kwa udanganyifu. Hata hivyo, Biblia inafunua yale yaliyotokea.

Kwanza, simulizi hilo linaonyesha wazi kwamba Yakobo alikuwa na haki ya kubarikiwa na baba yake; Esau hakuwa na haki. Mapema, Yakobo alikuwa amenunua kihalali haki ya mzaliwa wa kwanza kutoka kwa ndugu yake pacha ambaye hakuithamini, na ambaye aliiuza kwa mlo mmoja ili kutuliza njaa yake. Esau “aliidharau haki ya kuzaliwa.” (Mwanzo 25:29-34) Hivyo, kwa kumwendea baba yake, Yakobo alikuwa akitafuta baraka ambayo ilikuwa haki yake.

Pili, Isaka alipotambua kwamba alikuwa amembariki Yakobo, hakujaribu kubadili yale aliyokuwa amefanya. Labda alikumbuka yale ambayo Yehova alikuwa amemwambia Rebeka kabla ya mapacha hao kuzaliwa: “Mkubwa atamtumikia mdogo.” (Mwanzo 25:23) Inapendeza pia kujua kwamba Yakobo alipokuwa karibu kuondoka Harani, Isaka alimbariki tena.—Mwanzo 28:1-4.

Mwishowe, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova alijua kile kilichotendeka na pia alipendezwa na yote yaliyokuwa yakitukia. Baraka ambazo Isaka alitoa zilihusiana na ahadi ya Mungu kwa Abrahamu. (Mwanzo 12:2, 3) Ikiwa Mungu angetaka kwamba Yakobo asipokee baraka hizo, angeingilia kati kwa njia fulani. Badala yake, Yehova alimhakikishia Yakobo jambo hilo kwa kusema: “Kupitia kwa uzao wako familia zote za nchi hakika zitajibariki.”—Mwanzo 28:10-15.