Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtawala Tajiri Anafanya Uamuzi Usiofaa

Mtawala Tajiri Anafanya Uamuzi Usiofaa

Mtawala Tajiri Anafanya Uamuzi Usiofaa

MTAWALA fulani kijana aliyekuwa tajiri, alikuwa mnyoofu, alitii sheria, na alipenda mambo ya kidini. Alimwendea Yesu, akaanguka miguuni pake na kumuuliza: “Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”

Katika jibu lake, Yesu alionyesha kwamba ili mtu huyo apate uzima alipaswa kutii amri za Mungu. Alipoulizwa atoe jibu hususa, Yesu alisema: “Usiue, Usifanye uzinzi, Usiibe, Usitoe ushahidi wa uwongo, Mheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Hizo zilikuwa amri za msingi zilizokuwa katika Sheria ya Musa. Kisha mtu huyo akasema: “Nimeyashika yote hayo; ni nini bado ninachokosa?”—Mathayo 19:16-20.

Yesu “akampenda” na kusema: “Umekosa jambo moja: Nenda, ukauze vitu ulivyo navyo uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje uwe mfuasi wangu.”—Marko 10:17-21.

Kwa ghafula, mtawala huyo kijana alihitaji kufanya uamuzi mzito. Angefanya nini? Je, angekubali kuacha utajiri wake wa kimwili na kuwa mfuasi wa Yesu, au angeendelea kushikamana na mali zake? Je, angefuatilia hazina zilizo duniani, au angetafuta hazina zilizo mbinguni? Hapana shaka kwamba alikabili uamuzi mgumu. Kwa wazi alipendezwa na viwango vya kiroho, kwa kuwa alishika Sheria na alitaka kujua jambo lingine alilohitaji kufanya ili apate kibali cha Mungu. Alifanya uamuzi gani? ‘Alikwenda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.’—Marko 10:22.

Uamuzi wa mtawala huyo kijana haukuwa wa hekima. Ikiwa angekuwa mfuasi mwaminifu wa Yesu, angepata kile alichokuwa akitafuta, yaani, uzima wa milele. Hatuambiwi kilichompata kijana huyo. Hata hivyo, tunajua kwamba miaka 40 hivi baadaye, majeshi ya Roma yaliharibu Yerusalemu na sehemu kubwa ya Yudea. Wayahudi wengi walipoteza mali zao na uhai wao pia.

Tofauti na mtawala huyo kijana, mtume Petro na wanafunzi wengine walifanya uamuzi mzuri. Waliacha “vitu vyote” na kumfuata Yesu. Uamuzi huo uliwafaidi kama nini! Yesu aliwaambia kwamba wangepokea mara nyingi zaidi kuliko vitu walivyokuwa wameacha. Zaidi ya hilo, wangepata uzima wa milele. Hawangejuta kamwe kwa kufanya uamuzi huo.—Mathayo 19:27-29.

Sote tunakabili maamuzi maishani—yawe madogo au makubwa. Yesu alisema nini kuhusu maamuzi hayo? Je, utakubali mashauri yake? Ukiamua kufanya hivyo, utapata thawabu kubwa sana. Sasa acha tuzungumzie jinsi tunavyoweza kumfuata Yesu na kufaidika na yale aliyosema.