Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Elekea Mahali Ilipo Nuru

Elekea Mahali Ilipo Nuru

Elekea Mahali Ilipo Nuru

MINARA YA TAA ya kuongozea meli imeokoa watu wengi sana. Hata hivyo, mbali na kumwonya baharia aliyechoka kuhusu miamba hatari iliyo baharini, nuru inayoonekana kutoka mbali inamsaidia kwa njia nyingine. Anapoiona anajua kwamba anakaribia mwisho wa safari yake. Vivyo hivyo, Wakristo leo wanakaribia mwisho wa safari ndefu katika ulimwengu wenye giza na ulio hatari kiroho. Katika Biblia, wanadamu kwa ujumla ambao wametengwa mbali na Mungu, wanalinganishwa na “bahari inayorushwa-rushwa, wakati ambapo haiwezi kutulia, ambayo maji yake yanaendelea kurusha juu magugu-maji na matope.” (Isaya 57:20) Watu wa Mungu wanaishi katika mazingira hayo. Hata hivyo, wana tumaini zuri sana la wokovu, ambalo ni kama nuru yenye kutegemeka. (Mika 7:8) Kwa msaada wa Yehova na Neno lake, “nuru imemwangazia mwadilifu, na shangwe kwa ajili ya walio wanyoofu moyoni.”—Zaburi 97:11. *

Hata hivyo, Wakristo fulani wameruhusu vikengeusha-fikira viwaondoe katika nuru ya Yehova na hivyo imani yao imevunjika kama meli kwenye miamba iliyofichika. Tunaweza kulinganisha miamba hiyo na hali ya kupenda vitu vya kimwili, mwenendo mpotovu kiadili, au hata uasi-imani. Ndiyo, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, “imani [ya watu fulani leo] imevunjika.” (1 Timotheo 1:19; 2 Petro 2:13-15, 20-22) Ulimwengu mpya unaweza kulinganishwa na bandari ambako tunaelekea. Kwa kuwa tunakaribia sana bandari hiyo, ungekuwa msiba mkubwa kama nini kwa mtu kupoteza kibali cha Yehova!

Epuka ‘Kuvunjikiwa na Imani’

Katika karne zilizopita, meli ingeweza kusafiri kwa usalama baharini lakini ivunjike ikikaribia bandari. Mara nyingi meli ilikabili hatari kubwa zaidi ilipokuwa ikikaribia nchi kavu. Vivyo hivyo, kwa watu wengi kipindi chenye hatari zaidi katika historia ya wanadamu ni “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. Biblia inaeleza kwa usahihi kwamba hizi ni siku “ngumu kushughulika nazo,” hasa kwa Wakristo walio wakfu.—2 Timotheo 3:1-5.

Kwa nini siku hizi za mwisho ni ngumu sana? Shetani anajua kwamba ana “kipindi kifupi [tu] cha wakati” cha kupigana na watu wa Mungu. Hivyo, ameimarisha zaidi kampeni yake kali ya kuvunja imani yao. (Ufunuo 12:12, 17) Hata hivyo, hatujaachwa bila msaada wala mwongozo. Yehova anaendelea kuwa kimbilio kwa wale ambao wanatii mashauri yake. (2 Samweli 22:31) Ametupatia vielelezo vya kutuonya ambavyo vinafunua mbinu za werevu na zenye uovu za Shetani. Acheni sasa tuzungumzie mifano miwili kama hiyo inayohusisha taifa la Israeli wakati lilipokuwa likikaribia Nchi ya Ahadi.—1 Wakorintho 10:11; 2 Wakorintho 2:11.

Karibu na Nchi ya Ahadi

Chini ya uongozi wa Musa, Waisraeli waliweza kukimbia kutoka Misri. Muda si muda, walikaribia mpaka wa kusini wa Nchi ya Ahadi. Musa akawatuma wanaume 12 ili waipeleleze nchi. Wapelelezi kumi ambao hawakuwa na imani walileta ripoti mbaya, wakisema kwamba Waisraeli hawangeweza kuwashinda Wakanaani kwa sababu walikuwa “wenye ukubwa usio wa kawaida” na wenye nguvu zaidi kijeshi. Hilo lilikuwa na matokeo gani kwa Waisraeli? Masimulizi hayo yanatuambia kwamba walianza kunung’unika juu ya Musa na Haruni, wakisema: “Kwa nini Yehova anatuleta kwenye nchi hii ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu wadogo watakuwa nyara. . . . Na tuchague kiongozi, nasi turudi Misri!”—Hesabu 13:1, 2, 28-32; 14:1-4.

Hebu wazia! Watu hao walikuwa wameona Yehova akiiaibisha serikali yenye nguvu ya Misri, ambayo ilikuwa serikali kuu ya ulimwengu wakati huo, alipoleta mapigo kumi yenye uharibifu na kufanya muujiza wenye kutisha katika Bahari Nyekundu. Nchi ya Ahadi ilikuwa mbele yao, kwa hiyo walihitaji tu kuelekea katika nchi hiyo kama meli inavyoelekea mahali ilipo nuru inayoonyesha mwisho wa safari yake. Hata hivyo, waliamini kwamba Yehova hangeweza kushinda falme ndogo zilizogawanyika za Kanaani. Bila shaka, itikio lao lisilo la imani lilimhuzunisha sana Mungu na pia wale wapelelezi wawili jasiri, Yoshua na Kalebu, ambao walihisi kwamba watu wa Kanaani walikuwa kama “mkate [kwa Waisraeli]”! Wapelelezi hao wawili walielewa vizuri hali hiyo kwa sababu walikuwa wametembea katika nchi yote ya Kanaani. Watu walipokosa kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yoshua na Kalebu pia walilazimika kutembea nyikani kwa makumi ya miaka, lakini hawakufa nyikani pamoja na wale ambao hawakuwa na imani. Kwa kweli, Yoshua na Kalebu walisaidia sana kuongoza kizazi kilichofuata kutoka nyikani kuelekea katika Nchi ya Ahadi. (Hesabu 14:9, 30) Katika safari hii ya pili, Waisraeli wangepata jaribu tofauti. Wangetenda jinsi gani?

Mfalme Balaki wa Moabu alijaribu kuwalaani Waisraeli kupitia nabii wa uwongo aliyeitwa Balaamu. Hata hivyo, Yehova alizuia njama hiyo kwa kumfanya Balaamu awabariki badala ya kuwalaani. (Hesabu 22:1-7; 24:10) Akiwa ameazimia, Balaamu alipanga njama nyingine mbovu, ambayo ilikusudiwa kuwafanya watu wa Mungu wasistahili kurithi ile nchi. Njama gani? Njama ya kuwashawishi wafanye uasherati na kushiriki katika ibada ya Baali. Ingawa kwa ujumla njama hiyo haikufaulu, Waisraeli 24,000 walishawishiwa. Walifanya uasherati na wanawake Wamoabu na wakajishikamanisha na Baali wa Peori.—Hesabu 25:1-9.

Fikiria hilo! Wengi kati ya Waisraeli hao walikuwa wameona Yehova akiwaongoza kwa usalama kupitia “nyika yote hiyo iliyo kuu na yenye kutia woga.” (Kumbukumbu la Torati 1:19) Hata hivyo, walipokuwa karibu sana kupata urithi wao, watu 24,000 kati ya watu wa Mungu walishindwa na tamaa za mwili na Yehova akawaua. Hilo ni onyo kubwa kama nini kwa watumishi wa Mungu leo wanapokaribia kupata urithi ulio bora zaidi!

Katika jitihada zake za mwisho za kujaribu kuwazuia watumishi wa leo wa Yehova wasipate thawabu yao, Shetani hahitaji mbinu mpya. Akitumia mbinu inayotukumbusha yaliyotukia wakati Waisraeli walipokaribia Nchi ya Ahadi kwa mara ya kwanza, mara nyingi Shetani anajaribu kutufanya tuogope na kuwa na shaka, iwe ni kupitia vitisho, mateso, au dhihaka. Wakristo fulani wameshindwa na vitisho hivyo. (Mathayo 13:20, 21) Mbinu nyingine ya ujanja ambayo ametumia kwa muda mrefu ni kumchafua mtu mmoja-mmoja kiadili. Pindi fulani, watu wenye nia mbaya ambao wamejiunga na kutaniko la Kikristo wamejaribu kuwachafua wale ambao ni dhaifu kiroho na wasiotembea kwa uhakika kupatana na nuru inayotoka kwa Mungu.—Yuda 8, 12-16.

Watu wakomavu ambao wanakesha wanaona kwamba maadili ya ulimwengu yanayozidi kuzorota yanaonyesha wazi kabisa kuwa Shetani anajitahidi kadiri anavyoweza. Ndiyo, Shetani anajua kwamba hivi karibuni hataweza tena kuwajaribu watumishi washikamanifu wa Mungu. Kwa hivyo, hapana shaka kwamba huu ndio wakati ambao tunapaswa kujihadhari kiroho ili kutambua jitihada za Shetani.

Mambo ya Kutusaidia Kuendelea Kukesha Kiroho

Mtume Petro alisema kwamba neno la Mungu la kinabii ni kama “taa inayoangaza mahali penye giza,” kwa kuwa linawasaidia Wakristo kuona na kuelewa jinsi kusudi la Mungu linavyotimizwa. (2 Petro 1:19-21) Wale wanaositawisha upendo kwa ajili ya Neno la Mungu na kuendelea kuongozwa nalo, wanatambua kwamba Yehova atanyoosha mapito yao. (Methali 3:5, 6) Wakiwa wamejaa tumaini, watu hao wenye uthamini ‘wanapiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo,’ lakini wale ambao hawamjui Yehova au wale wanaoacha njia yake, mwishowe wanakuwa na “maumivu ya moyo” na “mvunjiko wa roho.” (Isaya 65:13, 14) Kwa hiyo, kwa kujifunza Biblia kwa bidii na kutumia yale tunayojifunza, tunaweza kukazia macho tumaini letu hakika badala ya raha za muda tu za mfumo huu wa mambo.

Pia, sala inatusaidia kuendelea kukesha kiroho. Yesu alisema hivi alipozungumza kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo: “Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Ona kwamba Yesu alitumia neno “dua,” ambalo linamaanisha sala nzito sana ya kutoka moyoni. Yesu alijua kwamba tungekabili hatari ya kupoteza uzima wa milele wakati huu wa hatari. Je, sala zako zinaonyesha kuwa unatamani sana kuendelea kukesha kiroho?

Tusisahau kwamba mkondo wa mwisho wa safari yetu ya kupata urithi ndio mkondo ulio hatari zaidi. Hivyo, ni muhimu sana kuendelea kuona nuru ambayo inaweza kutuongoza kwenye wokovu.

Jihadhari na Taa Zinazopotosha

Zamani meli zilikabili hatari ya kushambuliwa na watu waovu ambao walipendelea usiku usio na mwezi wakati ambapo ilikuwa vigumu kwa mabaharia kuona ufuo. Watu hao waliweka taa katika sehemu za pwani zilizo hatari ili kuwadanganya manahodha wa meli na kuwafanya wabadili mwelekeo wa meli. Meli za waliodanganyika zilivunjika, mizigo yao ikaibiwa, na watu wakauawa.

Vivyo hivyo, Shetani, yule anayejifanya kuwa “malaika wa nuru,” anataka kuwanyang’anya watu wa Mungu uhusiano wao pamoja Naye. Ibilisi anaweza kutumia “mitume wa uwongo” na waasi-imani wanaojifanya “wahudumu wa uadilifu” ili kuwadanganya wasiojihadhari. (2 Wakorintho 11:13-15) Lakini kama vile nahodha na mabaharia walio macho na wenye uzoefu hawangeweza kudanganywa kwa urahisi na taa zinazopotosha, ndivyo Wakristo “ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia” wasivyoweza kupotoshwa na wale wanaoendeleza mafundisho ya uwongo na falsafa zenye kuumiza.—Waebrania 5:14; Ufunuo 2:2.

Mabaharia walibeba orodha ya minara ya taa ambayo walitazamia kuona walipokuwa safarini. Orodha hiyo ilieleza muundo wa kila mnara wa taa, kutia ndani ishara ya pekee ya kila mnara. Kitabu kimoja (The World Book Encyclopedia) kinasema hivi: “Mabaharia wanatambua mnara wa taa ambao wanaona na hivyo wanajua walipo kwa kuangalia muundo wa kila mnara wa taa na kuchunguza orodha ya minara ya taa.” Vivyo hivyo, Neno la Mungu linawasaidia watu wanyoofu kutambua ibada ya kweli na wale wanaoifuata, hasa katika siku hizi za mwisho wakati ambapo Yehova ameiinua ibada hiyo juu ya dini ya uwongo. (Isaya 2:2, 3; Malaki 3:18) Ili kuonyesha tofauti kubwa iliyopo kati ya ibada ya kweli na ibada ya uwongo, andiko la Isaya 60:2, 3 linasema hivi: “Giza litaifunika dunia, na weusi mzito utavifunika vikundi vya mataifa; lakini Yehova ataangaza juu yako, na utukufu wake utaonekana juu yako. Na hakika mataifa yataenda kwenye nuru yako, na wafalme kwenye mwangaza wa mwanga wako.”

Mamilioni ya watu kutoka katika mataifa yote wanapoendelea kuongozwa na nuru ya Yehova, hawataona imani yao ikivunjika katika mkondo huu wa mwisho wa safari yao. Badala yake, watasafiri kwa usalama katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo na kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani na usalama.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Maandiko yanatumia neno “nuru” kwa njia mbalimbali za mfano. Kwa mfano, Biblia inamhusianisha Mungu na nuru. (Zaburi 104:1, 2; 1 Yohana 1:5) Mafundisho ya kiroho kutoka katika Neno la Mungu yanafananishwa na nuru. (Isaya 2:3-5; 2 Wakorintho 4:6) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alikuwa nuru. (Yohana 8:12; 9:5; 12:35) Wafuasi wa Yesu waliamriwa waache nuru yao iangaze.—Mathayo 5:14, 16.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama mabaharia, Wakristo wanajihadhari ili wasidanganywe na taa zinazopotosha